Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dhamiri Nyoofu

Dhamiri Nyoofu

Dhamiri Nyoofu

IKU moja, Charles, ambaye ni mfanyakazi katika chuo kikuu fulani nchini Kenya, alipoteza simu yake ya mkononi alipokuwa akisafiri kutoka kazini kwenda nyumbani. Nchini Kenya, simu hizo bado ni vifaa ghali vya anasa.

Charles alisema, “Sikutarajia mtu yeyote airudishe.” Hata hivyo, baada ya siku chache alishangaa alipopigiwa simu kutoka ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Kenya. Hakuamini masikio yake alipoombwa aje na kuchukua simu yake! Alipata habari kwamba mhudumu mmoja wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova aliyesafiri katika gari moja naye alikuwa ameiokota simu hiyo. Katika jitihada za kumtafuta aliyeipoteza simu hiyo, mhudumu huyo aliipeleka kwenye ofisi ya tawi, na mwishowe wafanyakazi wa kujitolea wa ofisi hiyo wakampata Charles kwa kumpigia simu wakitumia namba iliyokuwa kwenye simu hiyo.

“Ninashukuru sana kwa jitihada zilizofanywa ili kunitafuta japo magumu yaliyohusika,” akasema Charles katika barua aliyoandikia ofisi hiyo ya tawi. “Ninawashukuru kutoka moyoni washiriki wa tengenezo lenu walioipata simu hiyo, wakanitafuta, na kunirudishia. Leo si rahisi kupata mtu mnyoofu, lakini inatia moyo kwamba kuna watu wachache wanaojitokeza kuwa Mashahidi wa kweli wa Yehova Mungu.”

Mashahidi wa Yehova wanajulikana kila mahali kwa unyoofu wao. Wanamwiga mtume Paulo aliyesema: “Tuna uhakika kwamba tuna dhamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18; 1 Wakorintho 11:1) Wanaelewa kwamba mwenendo huo humtukuza Yehova Mungu kama vile Yesu alivyosema: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.”—Mathayo 5:16.