Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hali ya Kiroho na Hali Yako Njema

Hali ya Kiroho na Hali Yako Njema

Hali ya Kiroho na Hali Yako Njema

YAELEKEA unatumia wakati mwingi kutunza afya yako. Huenda kila siku unatumia muda wa saa nane kulala, saa kadhaa kupika na kula, na saa nane au zaidi kufanya kazi ili kugharimia nyumba na chakula. Unapokuwa mgonjwa, huenda ukatumia wakati na pesa kumwona daktari au kutayarisha dawa ya kienyeji. Unasafisha nyumba yako, unaoga, na hata pengine kufanya mazoezi kwa ukawaida ili uwe na afya njema.

Hata hivyo, kudumisha afya njema, huhusisha mengi zaidi ya kutosheleza mahitaji yako ya kimwili. Kuna jambo jingine linalochangia sana hali yako njema. Utafiti wa kitiba umeonyesha kwamba afya ya kimwili inahusiana sana na ya kiroho kwa kuwa hali yako ya kiroho inaweza kuathiri afya yako.

Uhusiano wa Moja kwa Moja

“Makala nyingi za kwanza kabisa za utafiti kuhusu jambo hilo zinaonyesha kwamba kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya afya bora na hali nzuri ya kiroho,” asema Profesa Hedley G. Peach wa Chuo Kikuu cha Melbourne, Australia. Likieleza juu ya matokeo ya utafiti huo, jarida The Medical Journal of Australia (MJA) linasema: ‘Watu wa dini wana shinikizo la damu la chini, kiwango cha chini cha kolesteroli, na si rahisi wapatwe na kansa ya utumbo mpana.’

Vivyo hivyo, nchini Marekani uchunguzi uliofanywa na Chuo Kikuu cha California (UC), Berkeley mwaka wa 2002, ambao ulihusisha watu 6,545, ulionyesha kwamba “watu waliohudhuria ibada za dini mara moja kila juma waliishi muda mrefu kuliko wale waliohudhuria mara chache au wasiohudhuria kabisa.” Doug Oman, aliyeongoza uchunguzi huo ambaye pia ni mhadhiri wa Chuo cha Afya ya Umma cha UC Berkeley, alisema: “Tuliona tofauti hiyo hata baada ya kufikiria mambo kama vile mahusiano ya kijamii na yale yanayohusiana na afya ambayo yanatia ndani kuvuta sigara na kufanya mazoezi.”

Likitaja manufaa nyingine ambazo watu walio na mtazamo wa kiroho hupata, jarida MJA linasema: “Uchunguzi uliofanywa huko Australia unaonyesha kwamba watu wanaofuata dini wana ndoa thabiti zaidi, wengi hawatumii kileo au dawa za kulevya, si wengi wanaojiua au kufikiria kujiua, hawana mahangaiko mengi, hawashuki moyo, na hawana ubinafsi.” Isitoshe, jarida BMJ (ambalo zamani liliitwa The British Medical Journal) linaripoti: “Inaonekana baada ya kufiwa na mpendwa, watu walio na imani ya kidini yenye nguvu zaidi hushinda hisia za huzuni kabisa na haraka zaidi kuliko watu wasio na imani.”

Watu wana maoni mbalimbali kuhusu hali ya kweli ya kiroho. Hata hivyo, hali yako ya kiroho huathiri sana afya yako ya kimwili na kiakili. Jambo hilo la hakika linapatana na maneno yaliyosemwa na Yesu Kristo miaka 2,000 hivi iliyopita. Alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Kwa kuwa afya na furaha yako huathiriwa na hali yako ya kiroho, ni jambo la busara kuuliza: ‘Ni wapi ninapoweza kupata mwongozo wa kiroho wenye kutegemeka? Kuwa mtu wa kiroho kunahusisha nini?’

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

Photo Credits: Page 18: Mao Tse-tung and Golda Meir: Hulton/Archive by Getty Images; Francis Ferdinand: From the book The War of the Nations; Hirohito, Lindbergh, & Einstein: U.S. National Archives photo; Stalin: U.S. Army photo; Roosevelt: Franklin D. Roosevelt Library; Churchill: The Trustees of the Imperial War Museum (MH 26392)