Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Fadhili Zenye Upendo na Utunzaji wa Yehova

Kupata Fadhili Zenye Upendo na Utunzaji wa Yehova

Simulizi la Maisha

Kupata Fadhili Zenye Upendo na Utunzaji wa Yehova

LIMESIMULIWA NA FAY KING

Wazazi wangu walikuwa wenye fadhili, lakini kama watu wengine wengi, walichukia sana dini. Mama yangu alikuwa akisema: “Lazima kuna Mungu, la sivyo, ni nani aliyefanya maua na miti?” Lakini hakutaka kujua mengi zaidi.

BABA yangu alikufa mwaka wa 1939 nikiwa na umri wa miaka 11, nami niliishi na mama yangu huko Stockport, kusini ya Manchester, Uingereza. Sikuzote nilitamani kujua mengi zaidi kumhusu Muumba wangu na niliiheshimu Biblia, ingawa sikujua lolote kuihusu. Hivyo, nikaamua kwenda katika Kanisa la Anglikana ili kusikia mafundisho yao.

Ibada ya kanisa hilo haikunisaidia, lakini vitabu vya Injili viliposomwa, kwa njia fulani maneno ya Yesu yalinisadikisha kwamba lazima Biblia iwe ya kweli. Ninapofikiria jambo hilo, mimi hushangaa kwamba sikuisoma Biblia. Hata baadaye nilipopewa tafsiri ya kisasa ya “Agano Jipya” na rafiki fulani wa familia yetu, sikuisoma.

Kuanza kwa Vita vya Korea mwaka wa 1950 kulifanya nifikiri sana. Je, vita hivyo vingeenea kama vile Vita vya Pili vya Ulimwengu? Kama vingeenea, ningewezaje kutii amri ya Yesu ya kuwapenda adui zangu? Lakini je, ningekaa tu bila kufanya lolote na kutazama watu wakivamia nchi yangu? Kama ningefanya hivyo, bila shaka ningekuwa nikipuuza daraka langu. Ijapokuwa nilikuwa nimechanganyikiwa, nilikuwa na hakika kwamba ningepata majibu kwa maswali yangu yote katika Biblia, ingawa sikujua ningeyapata wapi au namna gani.

Kutafuta Kweli Huko Australia

Mnamo 1954 mimi na mama yangu tuliamua kuhamia Australia, ambako dada yangu, Jean, alikuwa akiishi. Miaka michache baadaye, Jean aliniambia kwamba alikuwa amewaomba Mashahidi wa Yehova wanitembelee kwa sababu alijua nilipendezwa na Biblia na nilienda kanisani. Alitaka kujua maoni yangu kuwahusu. Aliniambia, “Sijui kama maelezo yao ni sahihi ama sivyo, lakini angalau wanaeleza mambo mengi zaidi kuliko makanisa mengine.”

Bill na Linda Schneider, wenzi walionitembelea, walikuwa watu wazuri. Umri wao ulikuwa unakaribia miaka 70 na walikuwa Mashahidi kwa miaka mingi. Walikuwa wamefanya kazi kwenye kituo cha redio kilichosimamiwa na Mashahidi wa Yehova huko Adelaide, na kazi ya kuhubiri ilipopigwa marufuku huko Australia wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, walianza huduma ya wakati wote ya kueneza injili. Ingawa Bill na Linda walinisaidia sana, bado nilikuwa nikichunguza dini mbalimbali.

Mfanyakazi mwenzangu alinipeleka kwenye mkutano wa mhubiri Billy Graham. Baada ya mkutano huo, baadhi yetu tulikutana na kasisi fulani aliyekubali kuulizwa maswali. Nilimwuliza swali hili ambalo bado lilikuwa likinisumbua: “Unawezaje kuwa Mkristo na kuwapenda adui zako na bado uende vitani na kuwaua?” Wote waliokuwa katika kikundi hicho walipiga kelele kuonyesha kwamba hata wao walikuwa wamesumbuliwa na swali hilo! Mwishowe, kasisi huyo alisema: “Sijui jibu la swali hilo. Bado ninalifikiria.”

Wakati huohuo nilikuwa ninaendelea kujifunza Biblia na Bill na Linda, na mnamo Septemba 1958 nikabatizwa. Niliamua kufuata kielelezo cha walimu wangu, kwa hiyo, mwezi wa Agosti mwaka uliofuata nikawa painia wa kawaida, yaani, mweneza-injili wa wakati wote. Miezi minane baadaye, nilitiwa moyo niwe painia wa pekee. Nilifurahi sana kujua kwamba pia dada yangu Jean, alifanya maendeleo na kubatizwa.

Mlango wa Utendaji Wafunguliwa

Nilikuwa nikiongoza mafunzo kadhaa ya Biblia ya nyumbani nilipokuwa nikishirikiana na kutaniko moja la Sydney. Siku moja nilikutana na kasisi mstaafu wa Kanisa la Anglikana na kumuuliza kanisa hilo lilifundisha nini kuhusu mwisho wa ulimwengu. Ingawa aliniambia kwamba alikuwa amefundisha imani ya kanisa hilo kwa miaka 50, nilishangazwa na jibu lake: “Nitahitaji wakati wa kufanya utafiti kwa sababu siijui Biblia vizuri kama Mashahidi wa Yehova.”

Baada ya hapo, mwito ulitolewa ili wahubiri wajitolee kwenda kutumika huko Pakistan. Nilituma maombi bila kujua kwamba dada waseja hawakuwa wakitumwa, ila tu ndugu waseja au wenzi wa ndoa. Yaonekana maombi yalipelekwa makao makuu ya Brooklyn kwa sababu baada ya muda nilipokea barua iliyonieleza kwamba kulikuwa na uhitaji huko Bombay (sasa linaitwa Mumbai), India, na kama ningekubali kwenda huko. Ilikuwa mwaka wa 1962. Nilikubali kwenda Bombay na nikakaa huko kwa miezi 18 kabla ya kwenda Allahabad.

Upesi niliamua kujifunza Kihindi. Kwa ujumla, lugha hiyo inatamkwa jinsi inavyoandikwa, hivyo si vigumu sana kuijua. Hata hivyo, mara nyingi nilivunjika moyo wakati wenye-nyumba waliponiomba nizungumze Kiingereza badala ya kung’ang’ana kuzungumza lugha yao! Lakini katika nchi hii kulikuwa na magumu yasiyo ya kawaida na yenye kusisimua, nami nilifurahia kushirikiana na Mashahidi wenzangu kutoka Australia.

Nilipokuwa mchanga, nilifikiria ndoa, lakini kufikia wakati nilipobatizwa, nilikuwa na mengi sana katika utumishi wa Yehova hivi kwamba sikuendelea kuifikiria. Hata hivyo, nilianza kuhisi tena kwamba ninahitaji mwenzi maishani. Bila shaka, sikutaka kuacha mgawo wangu katika nchi ya kigeni, hivyo nikasali kwa Yehova kuhusu jambo hilo na nikaacha kulifikiria.

Baraka Zisizotarajiwa

Wakati huo, Edwin Skinner ndiye aliyesimamia kazi katika ofisi ya tawi ya India. Alihudhuria darasa la nane la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower mwaka wa 1946 akiwa na ndugu wengine wengi waaminifu, kutia ndani Harold King na Stanley Jones, waliopewa mgawo wa kwenda China. * Mnamo 1958, Harold na Stanley walifungwa kifungo cha upweke kwa sababu ya kuhubiri huko Shanghai. Harold alipoachiliwa 1963, Edwin alimwandikia barua. Harold alijibu barua hiyo aliporudi Hong Kong baada ya kusafiri Marekani na Uingereza na kutaja kwamba alitaka kuoa. Alimwambia Edwin kwamba alikuwa amesali kuhusu jambo hilo akiwa gerezani na kumuuliza kama alijua Shahidi ambaye angeweza kuwa mke mzuri.

Huko India, ndoa nyingi hupangwa, na ingawa sikuzote Edwin alikuwa akiombwa afanye mipango hiyo, yeye alikuwa akikataa. Hivyo, akampa Ruth McKay barua hiyo ya Harold. Ruth alikuwa mke wa mwangalizi asafiriye aitwaye Homer. Mwishowe, Ruth aliniandikia barua kusema kwamba mishonari fulani ambaye alikuwa katika kweli kwa miaka mingi alikuwa akitafuta mke, naye akaniuliza kama ningependa kumwandikia barua. Hakuniambia ndugu huyo alikuwa nani wala habari zaidi kumhusu.

Bila shaka, Yehova tu ndiye aliyejua kwamba nilikuwa nimesali nipate mwenzi, hivyo mwanzoni nilitaka kukataa wazo hilo. Lakini kadiri nilivyofikiria jambo hilo ndivyo nilivyoona kwamba mara nyingi Yehova hajibu sala kwa njia tunayotazamia. Kwa hiyo, nikamwandikia Ruth barua na kumwambia kwamba maadamu sitalazimika kuolewa na ndugu huyo, angeweza kumwambia aandike tena. Barua ya pili ambayo Harold King aliandika ilikuwa yangu.

Picha za Harold na mambo yaliyompata yalichapishwa katika magazeti mbalimbali baada ya kuachiliwa kutoka gerezani huko China. Kufikia wakati huo, alijulikana sana duniani, lakini nilivutiwa na utumishi wake wa uaminifu katika tengenezo. Hivyo, tuliwasiliana kupitia barua kwa miezi mitano, kisha nikaenda Hong Kong. Tulioana Oktoba 5, 1965.

Sote tulitaka kufunga ndoa na kuendelea na utumishi wa wakati wote, na kwa kuwa tulikuwa tunaendelea kuzeeka, tulihisi kwamba tamaa ya kuwa na mwenzi ilikuwa kubwa sana. Nilianza kumpenda Harold na kumheshimu sana nilipoona jinsi alivyotendea watu kwa fadhili na huruma, na jinsi alivyoshughulika na matatizo yaliyohusu utumishi wetu. Tulifurahia ndoa yetu kwa miaka 27 na kupata baraka nyingi kutoka kwa Yehova.

Wachina ni watu wenye bidii na ninawapenda sana. Huko Hong Kong wanazungumza Canton, lahaja ya Kichina ambayo ni ngumu sana kujifunza kwa kuwa matamshi yake hunyambulika zaidi ya lugha ya Mandarin. Mimi na Harold tulianza maisha yetu ya ndoa katika makao ya mishonari kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, kisha tukatumikia katika sehemu mbalimbali za eneo hilo. Naam, tulikuwa wenye furaha sana lakini, mnamo 1976 nikawa na tatizo baya la afya.

Kukabiliana na Matatizo ya Afya

Nilikuwa ninatokwa na damu kwa miezi michache, na damu yangu ikapungua sana. Nilihitaji kufanyiwa upasuaji, lakini madaktari kwenye hospitali wakaniambia kwamba hawangefanya upasuaji huo bila damu kwa kuwa kama wangefanya hivyo, ningekufa kwa sababu ya mshtuko. Siku moja madaktari walipokuwa wakizungumzia hali yangu, wauguzi walijaribu kunifanya nibadili nia yangu, wakisema kwamba haikufaa nife bure. Watu 12 walikuwa wafanyiwe upasuaji siku hiyo, na 10 kati yao walikuwa watolewe mimba, lakini nikatambua kwamba hakuna yeyote aliyepinga hatua ya wanawake hao ya kutoa mimba.

Mwishowe, Harold akaandika barua ya kuiondolea hospitali hiyo lawama iwapo ningekufa, nao madaktari wakakubali kunifanyia upasuaji huo muhimu. Nilipelekwa kwenye chumba cha upasuaji na kutayarishwa kupewa dawa inayomaliza hisia wakati wa upasuaji. Hata hivyo, wakati huo mtaalamu aliyepaswa kunipa dawa hiyo alikataa, hivyo hospitali ikalazimika kuniacha niende nyumbani.

Ndipo tukaenda kumwona mtaalamu wa magonjwa ya akina mama ambaye hakufanya kazi katika hospitali hiyo. Alipoona kwamba hali yangu ilikuwa mbaya, alisema atafanya upasuaji huo kwa malipo ya chini, maadamu tu tusingemwambia yeyote pesa alizotulipisha. Alifanikiwa kunipasua bila kutumia damu yoyote. Wakati huo, mimi na Harold tuliona wazi utunzaji na fadhili zenye upendo za Yehova.

Mnamo 1992, Harold aliugua ugonjwa usioweza kupona. Sote tulihamia ofisi ya tawi ambako tulitunzwa kwa upendo. Mume wangu mpendwa aliyekuwa na tumaini la kwenda mbinguni alikufa 1993 akiwa na umri wa miaka 81.

Narudi Uingereza

Nilifurahia kuwa mmoja wa familia ya Betheli ya Hong Kong, lakini ikazidi kuwa vigumu kwangu kukaa huko kwa sababu ya joto na unyevunyevu. Ndipo nikapata barua kutoka makao makuu ya Brooklyn, iliyoniuliza kama ningependa kuhamia ofisi yenye vifaa zaidi kwa sababu ya afya yangu. Kwa hiyo, mnamo 2000, nikarudi Uingereza na kujiunga na familia ya Betheli ya London. Huo umekuwa mpango wenye upendo kama nini! Nilikaribishwa kwa shauku, na ninafurahia sana migawo mbalimbali ninayopewa huko, ambayo inatia ndani kusaidia kutunza maktaba ya familia ya Betheli yenye mabuku 2,000.

Pia ninashirikiana na kutaniko la Kichina linalokutana London, ingawa hapa mambo yamebadilika. Siku hizi, ni watu wachache sana wanaokuja kutoka Hong Kong, badala yake wanakuja kutoka China. Wanazungumza lugha ya Mandarin, na hiyo hutokeza hali ngumu katika kazi ya kuhubiri. Nchini mwote kuna ripoti nyingi kuhusu mafunzo ya Biblia yenye kupendeza yanayoongozwa pamoja na wanafunzi wa chuo kikuu kutoka China ambao wanasomea digrii ya pili. Wana bidii nao wanafurahia kweli ya Biblia wanayojifunza. Inafurahisha kuwasaidia.

Mara nyingi nikiwa katika makao yangu mapya yenye utulivu, mimi hufikiria maisha yangu yenye furaha na ninaendelea kustaajabia fadhili zenye upendo za Yehova. Zinaonekana katika mambo yote yanayohusiana na kusudi lake, na ni wazi kwamba anawajali watumishi wake mmoja-mmoja. Nina kila sababu ya kumshukuru kwa jinsi ambavyo amenitunza kwa upendo.—1 Petro 5:6, 7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Masimulizi ya maisha ya mishonari hao wawili yalichapishwa katika gazeti la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 1963, ukurasa wa 437-442, na Desemba 15, 1965, ukurasa wa 756-767.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikitumika huko India

[Picha katika ukurasa wa 25]

Harold King mnamo 1963 na akitumika huko China miaka ya 1950

[Picha katika ukurasa wa 26]

Siku ya arusi yetu huko Hong Kong, Oktoba 5, 1965

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tukiwa na Wanabetheli wa Hong Kong, Liang na mke wake wako katikati, naye Gannaway na mke wake wako kulia