Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tamasha ya Ulimwengu Huu Inabadilika”

“Tamasha ya Ulimwengu Huu Inabadilika”

“Tamasha ya Ulimwengu Huu Inabadilika”

“Nasema hili, akina ndugu, wakati uliobaki umepungua.”—1 WAKORINTHO 7:29.

1, 2. Ni mabadiliko gani ambayo umejionea maishani mwako?

NI MABADILIKO gani ambayo umejionea maishani mwako? Je, unaweza kutaja baadhi yake? Kwa mfano, kuna maendeleo ambayo yamefanywa katika sayansi ya kitiba. Katika nchi fulani leo, muda ambao mtu anatarajiwa kuishi umeongezeka kutoka miaka inayopungua 50 mwanzoni mwa karne ya 20, hadi miaka zaidi ya 70 kwa sababu ya utafiti ambao umefanywa katika sayansi ya kitiba! Fikiria pia jinsi ambavyo tumenufaika kwa kutumia redio, televisheni, simu za mkononi, na mashini za faksi kwa njia inayofaa. Maisha ya watu wengi yameboreka kwa sababu ya hatua muhimu ambazo zimepigwa katika nyanja za elimu, usafiri, na katika kulinda haki za binadamu.

2 Bila shaka, si mabadiliko yote ambayo yamewanufaisha wanadamu. Hatuwezi kupuuza matokeo mabaya ya kuongezeka kwa uhalifu, kuzorota kwa maadili, kuongezeka kwa matumizi ya dawa za kulevya, ongezeko la haraka la talaka, mfumuko wa bei, na kuongezeka kwa tisho la ugaidi. Vyovyote vile, yaelekea utakubaliana na mtume Paulo aliyeandika hivi zamani: “Tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.”—1 Wakorintho 7:31.

3. Paulo alimaanisha nini alipoandika kwamba “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika”?

3 Paulo aliposema maneno hayo, alikuwa akiulinganisha ulimwengu na jukwaa la waigizaji. Waigizaji kwenye jukwaa hilo, yaani, wanasiasa, wanadini, na watu mashuhuri, hutokea na kufanya tamasha zao, kisha wanawaachia wengine jukwaa hilo. Hilo limekuwa likiendelea kwa muda mrefu. Zamani, familia ya kifalme ingeweza kutawala kwa muda mrefu sana na mabadiliko yalitokea polepole. Sivyo ilivyo leo, kwa kuwa historia inaweza kubadilika kwa ghafula kiongozi mashuhuri anapouawa! Naam, katika nyakati hizi zenye misukosuko, hatujui kesho itakuwaje.

4. (a) Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani yaliyosawazika kuhusu matukio ya ulimwengu? (b) Ni mambo gani mawili yanayotoa uthibitisho tutakayochunguza?

4 Ikiwa ulimwengu ni jukwaa na viongozi wake ni waigizaji, basi Wakristo ni watazamaji. * Hata hivyo, kwa kuwa Wakristo “si sehemu ya ulimwengu” hawajishughulishi sana na uigizaji huo au hata kuwajua waigizaji wenyewe. (Yohana 17:16) Badala yake, wanatafuta kwa hamu mambo yanayoonyesha kwamba drama hiyo inaelekea kufikia kilele chake, yaani mwisho wenye maafa, kwa kuwa wanajua kwamba lazima mfumo huu uishe kabla Yehova hajaleta ulimwengu mpya wenye uadilifu ambao umengojewa kwa muda mrefu. * Kwa hiyo, na tuchunguze mambo mawili yanayothibitisha kwamba tunaishi wakati wa mwisho na kwamba ulimwengu mpya unakaribia. Mambo hayo ni (1) Kronolojia ya Biblia na (2) kuzorota kwa hali duniani.—Mathayo 24:21; 2 Petro 3:13.

Mwishowe Fumbo Lafumbuliwa!

5. “Nyakati zilizowekwa za mataifa,” ni zipi, na kwa nini tupendezwe nazo?

5 Kronolojia ni utafiti kuhusu uhusiano kati ya wakati na matukio. Yesu alitaja wakati ambapo viongozi wa ulimwengu wangekuwa waigizaji wakuu bila kuingiliwa na Ufalme wa Mungu. Yesu alikiita kipindi hicho “nyakati zilizowekwa za mataifa.” (Luka 21:24) Mwishoni mwa ‘nyakati hizo zilizowekwa,’ Ufalme wa mbinguni wa Mungu ungeanza kutawala, Yesu akiwa Mtawala wake anayefaa. Mwanzoni, Yesu angetawala “katikati ya adui [zake].” (Zaburi 110:2) Kisha, kulingana na Danieli 2:44, Ufalme huo ‘ungezivunja na kuzikomesha’ serikali zote za wanadamu, nao ungesimama milele.

6. “Nyakati zilizowekwa za mataifa” zilianza lini, zilidumu kwa muda gani, nazo zilimalizika lini?

6 “Nyakati zilizowekwa za mataifa” zingeisha lini nao Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala lini? Jibu ambalo lilikuwa ‘limefungwa kwa muhuri mpaka wakati wa mwisho,’ linatia ndani kronolojia ya Biblia. (Danieli 12:9) ‘Wakati’ huo ulipokaribia, Yehova alichukua hatua ya kufunua jibu hilo kwa kikundi fulani cha wanafunzi wa Biblia wanyenyekevu. Kwa msaada wa roho ya Mungu walifahamu kwamba “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilianza Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. na kwamba “nyakati” hizo zilikuwa na urefu wa miaka 2,520. Kutokana na ufahamu huo, walipiga hesabu na kutambua kwamba “nyakati zilizowekwa za mataifa” ziliisha mwaka wa 1914. Pia walitambua kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo ulianza mwaka wa 1914. Ukiwa mwanafunzi wa Biblia, je, unaweza kueleza kwa kutumia Maandiko jinsi ya kupiga hesabu na kupata mwaka wa 1914? *

7. Ni maandiko gani yanayotusaidia kujua mwanzo, urefu, na mwisho wa nyakati saba zinazotajwa katika kitabu cha Danieli?

7 Dokezo moja la kupiga hesabu hiyo limefichwa katika kitabu cha Danieli. Kwa kuwa Yehova alimtumia Mfalme Nebukadneza wa Babiloni kuharibu Yerusalemu katika mwaka wa 607 K.W.K., mwanzoni mwa “nyakati zilizowekwa,” Alifunua kupitia mtawala huyo kwamba mataifa yangeendelea kutawala kwa jumla ya nyakati saba za mfano bila yeye kuyaingilia. (Ezekieli 21:26, 27; Danieli 4:16, 23-25) Nyakati hizo saba zina urefu gani? Kulingana na Ufunuo 11:2, 3, na 12:6, 14, nyakati tatu na nusu ni siku 1,260. Hivyo, bila shaka nyakati saba ni siku 1,260 mara mbili au siku 2,520. Je, zina urefu wa siku 2,520 pekee? La, kwa kuwa Yehova alimpa nabii Ezekieli, aliyeishi wakati mmoja na Danieli, kanuni hii ya kutusaidia kuhesabu nyakati hizo za mfano: “Nimekupa wewe siku moja kwa mwaka mmoja, siku moja kwa mwaka mmoja.” (Ezekieli 4:6) Kwa hiyo, nyakati saba zingekuwa na urefu wa miaka 2,520. Tukitumia mwaka wa 607 K.W.K. kuwa mwanzo, na miaka 2,520 kuwa urefu wa nyakati hizo, tunaweza kusema kwamba nyakati zilizowekwa zingeisha mwaka wa 1914.

“Wakati wa Mwisho” Wathibitishwa

8. Unaweza kutoa uthibitisho gani kwamba hali za ulimwengu zimezorota tangu mwaka wa 1914?

8 Matukio ya ulimwengu kuanzia mwaka wa 1914 na kuendelea huthibitisha kwamba ufahamu uliotajwa hapo juu ambao unategemea kronolojia ya Biblia ni sahihi. Yesu mwenyewe alisema kwamba katika “umalizio wa mfumo wa mambo” kungekuwa na vita, njaa kali, na tauni. (Mathayo 24:3-8; Ufunuo 6:2-8) Bila shaka, hali imekuwa hivyo tangu mwaka wa 1914. Mtume Paulo alitoa habari zaidi, akisema kwamba mitazamo kati ya mtu na mwenzake ingekuwa tofauti sana. Ufafanuzi wake kuhusu mabadiliko hayo ambayo sote tumeyaona ulikuwa sahihi.—2 Timotheo 3:1-5.

9. Watazamaji wanasema nini kuhusu hali za ulimwengu tangu mwaka wa 1914?

9 Je, kweli “tamasha ya ulimwengu huu” imebadilika sana tangu mwaka wa 1914? Kitabu The Generation of 1914 cha Profesa Robert Wohl kinasema: “Wale walioishi wakati wa vita wanaamini kabisa kwamba ulimwengu mmoja uliisha na mwingine ukaanza Agosti 1914.” Akithibitisha hilo, Dakt. Jorge A. Costa e Silva, akiwa mkurugenzi wa magonjwa ya akili wa Shirika la Afya Ulimwenguni, aliandika hivi: “Tunaishi wakati ambapo mambo yanabadilika haraka sana, na hali hiyo inaleta wasiwasi na mkazo ambao haujawahi kuonekana katika historia ya mwanadamu.” Je, umejionea mambo hayo?

10. Biblia hutufunuliaje yule anayesababisha kuzorota kwa hali za ulimwengu tangu mwaka wa 1914?

10 Ni nani anayesababisha kuzorota kwa hali za ulimwengu? Andiko la Ufunuo 12:7-9 linamfunua: “Vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli [Yesu Kristo] na malaika zake wakapigana na yule joka [Shetani Ibilisi] mkubwa, naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana lakini hakushinda, wala mahali hapakupatikana mbinguni kwa ajili yao tena. Kwa hiyo yule joka mkubwa akatupwa chini, . . . yule anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” Kwa hiyo, Shetani Ibilisi ndiye anayesababisha hali hizo, na kufukuzwa kwake kutoka mbinguni mwaka wa 1914 kumemaanisha “ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:10, 12.

Jinsi Igizo la Mwisho Litakavyokuwa

11. (a) Shetani hutumia njia gani kupotosha “dunia nzima inayokaliwa”? (b) Mtume Paulo alikazia jitihada gani ya kipekee ya Shetani?

11 Tangu mwaka wa 1914 Shetani amezidisha jitihada zake za kupotosha “dunia nzima inayokaliwa” kwa kuwa anajua kwamba mwisho wake unakaribia. Kwa kuwa sikuzote Shetani amekuwa mdanganyaji mkuu, yeye hufanya kazi bila kuonekana, akitumia viongozi wa ulimwengu na watu wanaoanzisha mitindo mipya. (2 Timotheo 3:13; 1 Yohana 5:19) Mojawapo ya malengo yake ni kudanganya wanadamu wafikiri kwamba njia yake ya kutawala inaweza kuwaletea amani ya kweli. Kwa ujumla, propaganda yake imefanikiwa kwa kuwa watu bado wanatazamia mema ingawa kuna uthibitisho unaoongezeka kwamba hali zinazidi kuzorota. Mtume Paulo alitabiri kwamba kabla tu ya mfumo huu wa mambo kuharibiwa, kutakuwa na jambo moja lenye kutokeza kuhusu propaganda ya Shetani. Aliandika hivi: “Wakati watakapokuwa wakisema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao mara moja kama vile maumivu ya taabu juu ya mwanamke mwenye mimba.”—1 Wathesalonike 5:3; Ufunuo 16:13.

12. Kumekuwa na jitihada gani zenye kuendelea za kuleta amani wakati wetu?

12 Katika miaka ya hivi karibuni, mara nyingi wanasiasa wametumia maneno “amani na usalama” kuelezea mipango mbalimbali ya wanadamu. Waliuita mwaka wa 1986 Mwaka wa Amani ya Kimataifa, ingawa katika mwaka huo hakukuwa na amani ya kimataifa. Je, jitihada hizo za viongozi wa ulimwengu zinaonyesha utimizo kamili wa andiko la 1 Wathesalonike 5:3, au je, Paulo alikuwa akizungumzia tukio hususa na lenye kutokeza sana hivi kwamba lingetambuliwa ulimwenguni?

13. Paulo alipotabiri kuhusu tangazo la “Amani na usalama!,” aliulinganisha uharibifu ambao ungefuata na jambo gani, na tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

13 Kwa kuwa mara nyingi unabii wa Biblia hueleweka kikamili tu baada ya kutimia au wakati unapotimia, itatubidi tungoje tuone itakuwaje. Hata hivyo, ni jambo lenye kupendeza kwamba Paulo alilinganisha uharibifu wa ghafula baada ya tangazo la “Amani na usalama!” na utungu wa mwanamke mwenye mimba. Kwa muda wa miezi tisa hivi, mama mjamzito huzidi kutambua kwamba kuna mtoto anayekua ndani yake. Huenda akasikia moyo wa mtoto wake ukipiga-piga au akamsikia akicheza-cheza tumboni. Huenda hata akampiga teke. Mara nyingi ishara hizo huzidi kuwa wazi hadi, siku moja, anahisi maumivu makali, utungu unaoonyesha kwamba tukio lililokuwa likitazamiwa, yaani, kuzaliwa kwa mtoto, limefika. Hivyo, hata tangazo lililotabiriwa la “Amani na usalama!” liwe litatimizwaje, utimizo huo utatokeza jambo fulani la ghafula, lenye maumivu, lakini litakaloleta furaha, kwa kuwa uovu utaondolewa na mfumo mpya wa ulimwengu kuanza.

14. Matukio ya wakati ujao yatafuatanaje, yakiongoza kwenye nini?

14 Uharibifu unaokuja utakuwa wenye kuogopesha kwa Wakristo waaminifu watakaokuwa watazamaji. Kwanza, wafalme wa dunia (sehemu ya kisiasa ya tengenezo la Shetani) watawashambulia wale wanaounga mkono Babiloni Mkuu (sehemu ya kidini) na kuwaharibu. (Ufunuo 17:1, 15-18) Hivyo, hali zitabadilika ghafula na ufalme wa Shetani ugawanyike, huku sehemu moja ikishambulia ile nyingine, naye Shetani atashindwa kuzuia mambo hayo. (Mathayo 12:25, 26) Yehova atatia jambo hilo ndani ya mioyo ya wafalme wa dunia “ili kutekeleza wazo lake,” yaani, kuwaondoa duniani maadui wake wa kidini. Baada ya dini za uwongo kuharibiwa, Yesu Kristo ataongoza majeshi yake ya kimbingu kuharibu kabisa sehemu ya tengenezo la Shetani itakayokuwa imebaki, yaani, mfumo wa kibiashara na kisiasa. Mwishowe, Shetani mwenyewe atazuiwa. Baada ya hayo, pazia litateremshwa na drama ambayo imeendelea kwa muda mrefu iishe.—Ufunuo 16:14-16; 19:11-21; 20:1-3.

15, 16. Maisha yetu yanapaswa kuathiriwaje na kikumbusho kwamba “wakati uliobaki umepungua”?

15 Mambo hayo yote yatatukia lini? Hatujui siku wala saa. (Mathayo 24:36) Hata hivyo, tunajua kwamba “wakati uliobaki umepungua.” (1 Wakorintho 7:29) Basi, ni muhimu kutumia kwa hekima wakati unaobaki. Jinsi gani? Kama mtume Paulo anavyoeleza, tunapaswa ‘kununua wakati unaofaa’ kwa ajili ya mambo yaliyo muhimu zaidi na hivyo kufanya kila siku iwe yenye thamani, badala ya kutumia wakati kwa mambo yasiyo ya lazima. Kwa nini? “Kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” Kwa “kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova,” hatutaharibu wakati mfupi wenye thamani unaobaki.—Waefeso 5:15-17; 1 Petro 4:1-4.

16 Tunapaswa kuathiriwaje kwa kujua kwamba mfumo wote wa mambo wa ulimwengu utaangamizwa? Mtume Petro aliandika hivi kwa manufaa yetu: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu!” (2 Petro 3:11) Naam, tunapaswa kuwa watu wa namna hiyo! Kupatana na shauri la hekima la Petro tunapaswa (1) kuangalia sana mwenendo wetu ili kuhakikisha kwamba ni mtakatifu na (2) kuhakikisha kwamba sikuzote tunamtumikia Yehova kwa bidii kwa sababu tunampenda sana.

17. Wakristo waaminifu wanapaswa kuendelea kujilinda na mitego gani ya Shetani?

17 Kumpenda Mungu kutatuzuia tusishikamane na ulimwengu huu kwa sababu ya vivutio vyake. Kwa kufikiria mambo yatakayoupata mfumo huu wa mambo, ni hatari kupumbazwa na vivutio na maisha ya anasa ya ulimwengu. Ingawa tunaishi na kufanya kazi katika ulimwengu, tunapaswa kutii shauri la hekima la kutoutumia ulimwengu kikamili. (1 Wakorintho 7:31) Kwa kweli, tunapaswa kujitahidi kadiri tuwezavyo kujilinda ili tusipotoshwe na propaganda ya ulimwengu. Ulimwengu huu hautafanikiwa kutatua matatizo yake wala hautaendelea kujitegemeza milele. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika hivyo? Kwa sababu Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake linasema: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17.

Tunatazamia Hali Bora Zaidi!

18, 19. Unatazamia mabadiliko gani katika ulimwengu mpya, na kwa nini hutakuwa umengoja bure?

18 Hivi karibuni, Yehova atateremsha pazia kwa kumwondoa Shetani na wale wanaomwunga mkono. Baada ya hapo, kwa baraka za Mungu, watu waaminifu watakaookoka mwisho wa mfumo huu wataanza kufanya mabadiliko kwenye “jukwaa” la ulimwengu ambayo yatadumu milele. Vita havitaharibu ulimwengu tena kwa kuwa Mungu ‘atakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9) Badala ya upungufu wa chakula, “kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; . . . kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Magereza, vituo vya polisi, magonjwa yanayoambukizwa kingono, wafanyabiashara mashuhuri wa dawa za kulevya, mahakama za talaka, kesi za kufilisika, na ugaidi havitakuwako.—Zaburi 37:29; Isaya 33:24; Ufunuo 21:3-5.

19 Mabilioni watafufuliwa kutoka katika makaburi ya ukumbusho, na hivyo waigizaji wataongezeka duniani. Kutakuwa na shangwe iliyoje kizazi kimoja kinapoungana na kingine, na wapendwa waliotenganishwa kwa muda mrefu wanapokumbatiana kwa shauku nyingi! Mwishowe, kila aliye hai atamwabudu Yehova. (Ufunuo 5:13) Mabadiliko hayo yatakapomalizika, pazia litainuliwa na kuonyesha dunia nzima ikiwa paradiso. Utahisije unapotazama dunia hiyo? Bila shaka utachochewa kusema, ‘Nilingojea dunia hii kwa muda mrefu, lakini sikungoja bure!’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika muktadha tofauti, Paulo alitaja Wakristo watiwa-mafuta kuwa “tamasha kwa ulimwengu, na kwa malaika, na kwa wanadamu.”—1 Wakorintho 4:9.

^ fu. 4 Kwa mfano, kuhusu utambulisho wa “mfalme wa kaskazini” anayetajwa katika Danieli 11:40, 44, 45, ona kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli, ukurasa wa 280-281.

^ fu. 6 Biblia yenyewe inaonyesha kwamba Yerusalemu lilianguka miaka 70 kabla ya wahamishwa Wayahudi kurudi mwaka wa 537 K.W.K. (Yeremia 25:11, 12; Danieli 9:1-3) Kwa habari kamili kuhusu “nyakati zilizowekwa za mataifa,” ona kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, ukurasa wa 308-310, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungejibuje?

• Maneno ya mtume Paulo kwamba “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika” yamethibitikaje kuwa kweli wakati wetu?

• Kronolojia ya Biblia inaonyeshaje mwisho wa “nyakati zilizowekwa za mataifa”?

• Hali zinazobadilika za ulimwengu zinathibitishaje kwamba “wakati wa mwisho” ulianza mwaka wa 1914?

• Tunapaswa kuathiriwaje na uhakika kwamba “wakati uliobaki umepungua”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mwishowe, fumbo lafumbuliwa!