Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kukabiliana na Shaka

Unaweza Kukabiliana na Shaka

Unaweza Kukabiliana na Shaka

“HAKIKA!” “Ni kweli kabisa!” “Hakuna shaka!” Yaelekea umeyasikia maneno hayo mara nyingi. Lakini katika maisha yetu ya kila siku, kuna mambo mengi ambayo hatuna uhakika nayo. Maisha yamekuwa yasiyotabirika hivi kwamba mara nyingi tunajiuliza kama kuna jambo lolote tunaloweza kuwa na uhakika kabisa nalo. Shaka na kutokuwa na uhakika huonwa kuwa mambo ya kawaida maishani.

Haishangazi kwamba watu wengi hutamani usalama na furaha kwao wenyewe na familia zao. Wao hufanya kazi kwa bidii sana ili wapate vitu wanavyoamini vitawaletea furaha na usalama, hasa pesa na vitu vya kimwili. Lakini tetemeko la ardhi, kimbunga, aksidenti, au uhalifu wenye jeuri unaweza kuharibu mali hizo mara moja. Ugonjwa mbaya, talaka, au kukosa kazi kunaweza kubadili maisha ghafula. Ni kweli kwamba huenda usipatwe na mambo hayo. Hata hivyo, mtu anaweza kusumbuka na kuhuzunika kujua tu kwamba jambo baya linaweza kutokea wakati wowote. Na si hayo tu.

Kutokuwa na uhakika ni sawa na kuwa na shaka, na kamusi moja hufafanua neno “shaka” kuwa hali ya kutokuwa na hakika ya jambo ambayo humzuia mtu kufanya maamuzi. Isitoshe, kulingana na kitabu Managing Your Mind, “kutokuwa na hakika ya jambo fulani muhimu husababisha hangaiko na wasiwasi.” Shaka isipoondolewa, inaweza kusababisha hangaiko, kuvunjika moyo, na hasira. Naam, kuwa na wasiwasi kuhusu mambo yanayoweza kutokea au yasiyoweza kutokea kunaweza kudhuru afya yetu ya akili na ya kimwili.

Kwa sababu hiyo, watu wengine hawajali hata kidogo. Wao ni kama kijana mmoja Mbrazili aliyesema: “Kwa nini uwe na wasiwasi kuhusu mambo yatakayotokea? Leo ni leo, na kesho ni kesho.” Maoni kwamba “tule na tunywe” kwa kuwa mambo yote yameshaandikwa na Mungu, yanaweza kusababisha kukata tamaa, huzuni, na mwishowe kifo. (1 Wakorintho 15:32) Ni afadhali zaidi kumgeukia Muumba, Yehova Mungu, ambaye Biblia inasema “habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” (Yakobo 1:17) Tukichunguza Neno la Mungu, Biblia, tutapata shauri na mwongozo mzuri wa kutusaidia kukabiliana na shaka maishani. Pia linaweza kutusaidia kuelewa kwa nini kuna shaka nyingi hivyo.

Kwa Nini Kuna Shaka?

Maandiko yana maoni yanayofaa kuhusu maisha nayo hutusaidia tusitawishe mtazamo unaofaa kuhusu shaka kisha tufanye mabadiliko. Ingawa mambo kama vile uhusiano wa kifamilia, cheo katika jamii, kuwa na akili nyingi, afya nzuri, na kadhalika yanaweza kukupatia usalama wa kadiri fulani, Biblia inaonyesha kwamba hatuwezi kuchukua mambo hayo kivivi hivi au kutarajia maisha yawe shwari tu. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema: “Si wenye mbio wanaoshinda katika mbio, wala wenye nguvu wanaoshinda katika pigano, wala pia wenye hekima wanaopata chakula, wala pia wenye uelewaji wanaokuwa na utajiri, wala wenye ujuzi wanaopata kibali.” Kwa nini? “Kwa sababu wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” Kwa hiyo, Sulemani alionya: “Kama vile samaki wanaonaswa katika wavu mbovu, na kama ndege wanaonaswa katika mtego, ndivyo wana wa binadamu wenyewe wanavyonaswa wakati wenye msiba, unapowaangukia ghafula.”—Mhubiri 9:11, 12.

Yesu Kristo pia alitaja wakati ambapo kizazi kizima kingepatwa na mahangaiko na shaka nyingi sana. Alisema hivi waziwazi: “Kutakuwa na ishara katika jua na mwezi na nyota, na juu ya dunia maumivu makali ya mataifa, bila kujua njia ya kutokea kwa sababu ya kunguruma kwa bahari na msukosuko wake, huku watu wakizimia kwa woga na tarajio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa; kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.” Lakini Yesu alitaja jambo hili lenye kuwatia moyo watu wenye mioyo minyoofu leo: “Wakati mnapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.” (Luka 21:25, 26, 31) Vivyo hivyo, badala ya kuogopa kwa sababu ya kuwa na shaka kuhusu wakati ujao, tuna imani katika Mungu inayotusaidia tupuuze shaka hiyo na badala yake tuzingatie wakati ujao mzuri na wenye usalama.

‘Kuwa na Uhakikisho Kamili wa Tumaini’

Ingawa hatuwezi kuwa na uhakika kuhusu kila jambo tunalosikia, kusoma, au kuona, tuna sababu nzuri ya kumtumaini Muumba. Yeye ndiye Aliye Mkuu Zaidi na pia Baba mwenye upendo anayewajali watoto wake wa kidunia. Mungu alisema hivi kuhusu neno lake mwenyewe: “Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:11.

Yesu Kristo alifundisha kweli ya Mungu, na wengi waliomsikiliza waliikubali kwa uhakika. Kwa mfano, Wasamaria fulani wanyoofu walimwambia hivi mwanamke aliyemsikiliza Yesu kwanza: “Hatuamini tena kwa sababu ya maneno yako; kwa maana sisi wenyewe tumesikia nasi tunajua kwamba mtu huyu kwa hakika ndiye mwokozi wa ulimwengu.” (Yohana 4:42) Vivyo hivyo leo, ingawa tunaishi nyakati zisizo na usalama, si lazima tutatanike kuhusu mambo tunayopaswa kuamini.

Kuhusu imani ya kidini, wengi wanaonelea kwamba badala ya kujaribu kuelewa mambo, tunapaswa kuyaamini tu. Lakini Luka, mwandishi wa Biblia, alikuwa na maoni tofauti. Alifanya utafiti na kutoa habari sahihi ili wengine wapate “kujua kabisa uhakika wa mambo” aliyoandika. (Luka 1:4) Kwa kuwa huenda watu wa familia na marafiki ambao hawana imani sawa na yetu wakawa na wasiwasi kwamba tutavunjika moyo na kukata tamaa, ni muhimu tuwe tunaweza kutetea imani yetu. (1 Petro 3:15) Tunaweza kuwasaidia wengine wamtumaini Mungu ikiwa tu tunajua kwa usahihi sababu ya kuamini mambo tunayoamini. Biblia humfafanua Yehova kwa maneno haya: “Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; Yeye ni mwadilifu na mnyoofu.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Fikiria maneno hayo ya mwisho: “Yeye ni mwadilifu na mnyoofu.” Tuna uthibitisho gani wa kuwa na uhakika kuhusu maneno hayo? Mtume Petro aliyasadiki kabisa maneno hayo. Alimwambia hivi ofisa mmoja Mroma na jamaa yake: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Petro alisema maneno hayo kwa sababu alikuwa ametoka tu kuona jinsi Mungu mwenyewe alivyoelekeza mambo hivi kwamba familia ya watu wasio Wayahudi, ambao zamani walionwa kuwa wasio safi na wasiokubalika, walikubalika Kwake. Kama Petro, sisi pia tunaweza kusadiki kwamba Mungu ni mwadilifu na hana ubaguzi tunapojionea “umati mkubwa” wa watu ambao sasa ni zaidi ya milioni sita kutoka nchi zaidi ya 230 ulimwenguni ambao wameacha mwenendo wao wa zamani na kutembea katika njia ya uadilifu.—Ufunuo 7:9; Isaya 2:2-4.

Tukiwa Wakristo wa kweli, hatutaki kuwa washupavu au wenye kushikilia maoni bila msingi, bali tunataka kuwa watu wanyenyekevu na wenye kukubali sababu. Hata hivyo, tuna uhakika kuhusu mambo tunayoamini na tunayotarajia wakati ujao. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa karne ya kwanza: “Tunatamani kila mmoja wenu aonyeshe bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho.” (Waebrania 6:11) Vivyo hivyo, habari njema kutoka katika Biblia imetupa “uhakikisho kamili wa tumaini.” Kama Paulo alivyoeleza pia, tumaini hilo linalotegemea kabisa Neno la Mungu “halikatishi tamaa.”—Waroma 5:5.

Isitoshe, tunasadiki kabisa kwamba kuwafundisha wengine habari njema kutoka katika Biblia kunaweza kufanya wawe na uhakika kabisa kuhusu uhusiano wao na Mungu, na hata wahisi wakiwa salama zaidi kihisia-moyo na kimwili. Tunaweza kujiunga na Paulo kusema: “Habari njema tunayohubiri haikutokea katikati yenu kwa maneno peke yake bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu na usadikisho wenye nguvu.”—1 Wathesalonike 1:5.

Baraka Zinazotokana na Usalama wa Kiroho

Ingawa leo hatuwezi kutarajia usalama kamili maishani, kuna mambo tunayoweza kufanya ambayo yatatusaidia kuishi maisha matulivu na salama zaidi. Kwa mfano, kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko la Kikristo kwenye mikutano huleta utulivu kwa kuwa huko tunafunzwa kanuni na maadili yafaayo. Paulo aliandika: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo wa sasa wasitake makuu, na waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie.” (1 Timotheo 6:17) Kwa kujifunza kumtumaini Yehova wala si anasa au vitu vya kimwili vya muda, wengi wameweza kuepuka vivunja moyo na mahangaiko waliyokuwa nayo zamani.—Mathayo 6:19-21.

Katika kutaniko, tunafurahia pia ushirika mchangamfu wa kidugu ambao hutusaidia katika njia nyingi. Wakati mmoja katika huduma yake, mtume Paulo na wale aliosafiri nao walihisi “mkazo mkubwa mno” na hawakuwa na “uhakika kabisa hata juu ya uhai [wao].” Paulo alipata wapi msaada na kitulizo? Bila shaka, tumaini lake katika Mungu halikufifia. Hata hivyo, alitiwa moyo na kufarijiwa na Wakristo wenzake waliomsaidia. (2 Wakorintho 1:8, 9; 7:5-7) Leo, wakati misiba ya asili au maafa mengine yanapotokea, mara nyingi ndugu zetu Wakristo huwa wa kwanza kufika ili kuwasaidia kimwili na kiroho Wakristo wenzao na pia wengine wenye uhitaji.

Sala ni njia nyingine ya kutusaidia kukabiliana na hali zenye shaka maishani. Sikuzote tunaweza kumwendea Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo tunapopatwa na mahangaiko yasiyotazamiwa. “Yehova atakuwa kilele salama kwa ajili ya mtu yeyote aliyekandamizwa, kilele salama wakati wa taabu.” (Zaburi 9:9) Wazazi wa kibinadamu wanaweza kushindwa kuwalinda watoto wao. Hata hivyo, Mungu yuko tayari kutusaidia kukabiliana na hofu na shaka. Kwa kumtwika Yehova mahangaiko yetu katika sala, tunaweza kuwa na uhakika kwamba anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.”—Waefeso 3:20.

Je, wewe husali kwa Mungu kwa ukawaida? Je, unasadiki kwamba Mungu husikiliza sala zako? “Mama yangu aliniambia kwamba ninapaswa kusali kwa Mungu,” akasema msichana mmoja huko São Paulo. “Lakini nikajiuliza: ‘Kwa nini nizungumze na mtu ambaye hata simjui?’ Hata hivyo, andiko la Mithali 18:10 lilinisaidia kuelewa kwamba tunahitaji msaada wa Mungu na tunapaswa kuzungumza naye katika sala.” Andiko hilo linasema: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.” Tunawezaje kweli kusitawisha tumaini na uhakika katika Yehova tusipozungumza naye kwa ukawaida? Ili tupate baraka zinazotokana na usalama wa kiroho, tunahitaji kuwa na zoea la kusali kutoka moyoni kila siku. Yesu alisema: “Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.”—Luka 21:36.

Jambo jingine tunaloweza kuwa na uhakika nalo ni tumaini letu katika Ufalme wa Mungu. Ona maneno ya andiko la Danieli 2:44: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” Tumaini hilo ni thabiti na tunaweza kuwa na uhakika nalo. Mara nyingi ahadi za wanadamu hukosa kutimia, lakini sikuzote tunaweza kutumaini ahadi ya Yehova. Mungu anategemeka naye ni kama mwamba tunaoweza kuutegemea. Tunaweza kuhisi kama Daudi aliyesema: “Mungu wangu ni mwamba wangu. Nitamkimbilia, ngao yangu na pembe yangu ya wokovu, kilele changu salama, na mahali pangu pa kukimbilia, Mwokozi wangu; unaniokoa kutoka katika jeuri.”—2 Samweli 22:3.

Kitabu kilichotajwa juu, Managing Your Mind, kinaongeza kusema: “Kadiri mtu anavyofikiri kuhusu mambo mabaya yanayoweza kutokea, ndivyo mambo hayo huzidi kuonekana kama yatatukia, na ndivyo inavyokuwa vigumu zaidi kukabiliana nayo.” Hivyo basi, kwa nini tujiruhusu kulemewa na mahangaiko na shaka za ulimwengu? Badala yake, tutumaini ahadi hakika za Mungu wala si mambo yenye shaka ya ulimwengu. Kwa kuwa na imani thabiti katika ahadi zenye kutegemeka za Yehova, tuna uhakika huu: “Yeyote anayemwamini hatakata tamaa.”—Waroma 10:11.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba wanadamu watabarikiwa wakati ujao

[Blabu katika ukurasa wa 30]

“Yeyote anayemwamini hatakata tamaa”

[Picha katika ukurasa wa 31]

Habari njema ya Ufalme huwaletea watu usalama