Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Hutuandalia Mahitaji Yetu ya Kila Siku

Yehova Hutuandalia Mahitaji Yetu ya Kila Siku

Yehova Hutuandalia Mahitaji Yetu ya Kila Siku

“Acheni kuhangaika kwa wasiwasi; kwa maana . . . Baba yenu anajua mnahitaji mambo hayo.”—LUKA 12:29, 30.

1. Yehova huwaandaliaje wanyama?

JE, UMEWAHI kumtazama shomoro au ndege mwingine akidonoa-donoa udongo? Labda ulijiuliza kama ndege huyo angepata chakula chochote kwa kufanya hivyo. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alionyesha tunaweza kujifunza jambo fulani kutokana na jinsi Yehova anavyowaandalia ndege. Alisema: “Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu au kuvuna au kukusanya ghalani; na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha wao. Je, ninyi si bora kuliko wao?” (Mathayo 6:26) Yehova huwaandalia viumbe wake chakula kwa njia za ajabu.—Zaburi 104:14, 21; 147:9.

2, 3. Ni mambo gani ya kiroho tunayoweza kujifunza kutokana na uhakika wa kwamba Yesu alitufunza tuombe mkate wetu wa kila siku?

2 Kwa nini basi Yesu alitaja ombi hili katika sala yake ya kielelezo: “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii”? (Mathayo 6:11) Tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na ombi hilo. Kwanza, linatukumbusha kwamba Yehova ndiye Mwandalizi Mkuu. (Zaburi 145:15, 16) Wanadamu wanaweza kupanda na kulima, lakini Mungu tu ndiye anayeweza kufanya vitu vikue kiroho na kimwili. (1 Wakorintho 3:7) Vitu tunavyokula na kunywa ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Matendo 14:17) Tunapomwomba atutimizie mahitaji yetu ya kila siku, tunamwonyesha kwamba tunathamini maandalizi hayo. Bila shaka, ombi hilo halituondolei daraka la kufanya kazi ikiwa tunaweza kufanya hivyo.—Waefeso 4:28; 2 Wathesalonike 3:10.

3 Pili, kumwomba “mkate kwa ajili ya siku hii” huonyesha kwamba hatupaswi kuhangaika kupita kiasi kuhusu wakati ujao. Yesu pia alisema: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote. Kwa hiyo, msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.” (Mathayo 6:31-34) Sala ya kuomba “mkate kwa ajili ya siku hii” inatuwekea kielelezo cha kuishi maisha rahisi ya “ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu.”—1 Timotheo 6:6-8.

Chakula cha Kiroho Siku kwa Siku

4. Ni matukio gani katika maisha ya Yesu na ya Waisraeli yanayokazia umuhimu wa kula chakula cha kiroho?

4 Sala yetu ya kuomba mkate wa kila siku inapaswa pia kutukumbusha kwamba tunahitaji chakula cha kiroho kila siku. Ingawa Yesu alikuwa na njaa kali baada ya kufunga kwa muda mrefu, alikataa kishawishi cha Shetani cha kugeuza mawe yawe mkate, aliposema: “Imeandikwa, ‘Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’” (Mathayo 4:4) Hapa Yesu alimnukuu nabii Musa aliyewaambia Waisraeli hivi: “[Yehova] alikunyenyekeza, akakuacha ukae na njaa, akakulisha mana, ambayo hukuwa umeijua wala baba zako hawakuwa wameijua; ili kukufanya ujue kwamba mwanadamu haishi kwa mkate tu bali mwanadamu huishi kwa kila neno la kinywa cha Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 8:3) Njia ambayo Yehova alitumia kutoa mana iliwaandalia Waisraeli chakula cha kimwili na pia kuwafunza mambo fulani ya kiroho. Mojawapo ya mambo hayo ni kwamba walipaswa “kuokota kila mtu kiasi chake siku baada ya siku.” Iwapo wangekusanya mana nyingi kuliko mahitaji yao ya siku, mabaki yangeanza kunuka na kutokeza wadudu. (Kutoka 16:4, 20) Hata hivyo, haikuwa hivyo siku ya sita ambayo walipaswa kukusanya mana kiasi cha siku mbili kwa ajili ya siku ya Sabato. (Kutoka 16:5, 23, 24) Kwa hiyo, mana hiyo iliwakumbusha kwamba walipaswa kutii na kwamba maisha yao hayakutegemea mkate tu bali “kila neno la kinywa cha Yehova.”

5. Yehova hutuandaliaje chakula cha kiroho kila siku?

5 Vivyo hivyo, tunahitaji kula chakula cha kiroho kila siku ambacho Yehova huandaa kupitia Mwana wake. Ili kutimiza kusudi hilo,Yesu amemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili aandae ‘chakula kwa wakati unaofaa’ kwa ajili ya watu wa nyumba ya imani. (Mathayo 24:45) Jamii hiyo ya mtumwa mwaminifu huandaa chakula kingi cha kiroho kupitia vifaa vya kujifunzia Biblia na pia hututia moyo tusome Biblia kila siku. (Yoshua 1:8; Zaburi 1:1-3) Kama Yesu, sisi pia tunaweza kupata chakula cha kiroho kwa kujitahidi kila siku kujifunza na kufanya mapenzi ya Yehova.—Yohana 4:34.

Msamaha wa Dhambi

6. Tunapaswa kuomba msamaha kwa madeni gani, naye Yehova yuko tayari kuyafutilia mbali kwa masharti gani?

6 Ombi linalofuata katika sala ya kielelezo ni: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” (Mathayo 6:12) Hapa Yesu hakuwa akizungumzia madeni ya pesa bali kusamehewa dhambi zetu. Katika maandishi ya Luka kuhusu sala ya kielelezo, ombi hilo linasema: “Utusamehe dhambi zetu, kwa maana sisi wenyewe pia humsamehe kila mtu aliye na deni letu.” (Luka 11:4) Hivyo, tunapofanya dhambi, ni kana kwamba tunakuwa na deni kwa Yehova. Lakini Mungu wetu mwenye upendo yuko tayari ‘kufuta,’ au kufutilia mbali deni hilo tukitubu kikweli, ‘tukigeuka,’ na kumwomba msamaha kwa msingi wa imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo.—Matendo 3:19; 10:43; 1 Timotheo 2:5, 6.

7. Kwa nini tunapaswa kuomba msamaha kila siku?

7 Kwa upande mwingine, tunafanya dhambi tunapokosa kufikia viwango vya Yehova vya uadilifu. Kwa sababu ya dhambi tuliyorithi, sote hukosea katika kusema, kutenda, na kuwaza au kwa kukosa kufanya mambo tunayopaswa kufanya. (Mhubiri 7:20; Waroma 3:23; Yakobo 3:2; 4:17) Kwa hiyo, iwe tunajua au hatujui kama tulifanya dhambi, tunapaswa kuomba msamaha wa dhambi zetu tunaposali kila siku.—Zaburi 19:12; 40:12.

8. Sala ya kuomba msamaha inapaswa kutochochea kufanya nini, nasi tutanufaikaje?

8 Kabla ya kuomba msamaha tunapaswa kujichunguza kwa unyoofu, tutubu, na kuungama, tukiwa na imani katika uwezo wa kukomboa wa damu ya Kristo iliyomwagwa. (1 Yohana 1:7-9) Ili kuonyesha kwamba sala yetu ni ya unyoofu, tunapaswa kuunga mkono ombi letu la msamaha kwa “matendo yanayostahili toba.” (Matendo 26:20) Hivyo, tunaweza kuwa na imani kwamba Yehova yuko tayari kutusamehe dhambi. (Zaburi 86:5; 103:8-14) Tukisamehewa dhambi tutakuwa na amani ya akili isiyo na kifani, yaani, “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira” ambayo ‘itailinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.’ (Wafilipi 4:7) Lakini sala ya kielelezo ya Yesu hutufunza mengi zaidi kuhusu yale tunayopaswa kufanya ili kusamehewa dhambi zetu.

Ili Tusamehewe Ni Lazima Tusamehe

9, 10. (a) Yesu aliongeza ufafanuzi gani katika sala ya kielelezo, nao ulikazia jambo gani? (b) Yesu alitoa mfano gani mwingine kuonyesha kwamba tunahitaji kuwa wenye kusamehe?

9 Inapendeza kuona kwamba ombi la ‘kusamehewa madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu,’ ndiyo tu sehemu ya sala ya kielelezo ambayo Yesu alifafanua. Baada ya kumaliza sala hiyo, aliongeza: “Kwa maana ikiwa mnawasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia; lakini ikiwa hamtawasamehe watu makosa yao, Baba yenu naye hatawasamehe makosa yenu.” (Mathayo 6:14, 15) Hivyo, Yesu alionyesha wazi kwamba ili Yehova atusamehe ni lazima tuwe tayari kuwasamehe wengine.—Marko 11:25.

10 Katika pindi nyingine, Yesu alitoa mfano kuonyesha uhitaji wa kusamehe ikiwa tunatarajia Yehova atusamehe. Alitaja mfalme mmoja ambaye kwa fadhili alifutilia mbali deni kubwa sana alilomdai mtumwa fulani. Baadaye, mfalme huyo alimwadhibu vikali mtumwa huyo alipokataa kufutilia mbali deni ndogo zaidi alilomdai mtumwa mwenzake. Yesu alimaliza mfano wake kwa kusema: “Vivyo hivyo Baba yangu wa mbinguni atashughulika nanyi pia ikiwa kila mmoja wenu hatamsamehe ndugu yake kutoka moyoni mwake.” (Mathayo 18:23-35) Jambo ambalo Yesu alifunza ni wazi: Deni la dhambi ambalo Yehova amemsamehe kila mmoja wetu ni kubwa sana likilinganishwa na kosa lolote ambalo huenda tumetendewa na mtu mwingine. Isitoshe, Yehova hutusamehe kila siku. Hakika basi, tunaweza kuwasamehe wengine makosa ambayo wao hututendea mara kwa mara.

11. Tunapaswa kufuata shauri gani lililotolewa na mtume Paulo ikiwa tunatarajia Yehova atusamehe, na kutakuwa na matokeo gani mazuri?

11 Mtume Paulo aliandika: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Waefeso 4:32) Kusameheana huchangia amani kati ya Wakristo. Paulo aliendelea kuhimiza hivi: “Kama waliochaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:12-14) Mambo hayo yote yamo katika sala ambayo Yesu alitufunza: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.”

Ulinzi Tunapopatwa na Jaribu

12, 13. (a) Ombi la pili kutoka mwisho katika sala ya kielelezo linamaanisha nini? (b) Ni nani aliye Mjaribu mkuu, na inamaanisha nini kusali tusiingizwe katika jaribu?

12 Ombi la pili kutoka mwisho katika sala ya Yesu ya kielelezo ni: “Usituingize katika jaribu.” (Mathayo 6:13) Je, Yesu alimaanisha kwamba tunapaswa kumwomba Yehova asituingize katika jaribu? La, kwa sababu mwanafunzi Yakobo aliongozwa na roho ya Mungu aandike: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Isitoshe, mtunga-zaburi aliandika: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Yehova hangojei kwa hamu tufanye makosa, naye hakika hajaribu kufanya tujikwae. Hivyo, sehemu hii ya sala ya kielelezo inamaanisha nini?

13 Shetani Ibilisi ndiye anayejaribu kufanya tujikwae, kutuangusha kwa matendo ya hila, na hata kutumeza. (Waefeso 6:11) Yeye ndiye Mjaribu mkuu. (1 Wathesalonike 3:5) Kwa kusali ili tusiingizwe katika jaribu, tunamwomba Yehova asiruhusu tuanguke tunapopatwa na jaribu. Tunamwomba atusaidie ili “Shetani asitushinde akili,” na tusishindwe na majaribu. (2 Wakorintho 2:11) Tunasali ili tudumu “mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi” na kupata ulinzi wa kiroho ambao hupewa wale wanaotambua enzi kuu ya Yehova katika yote wanayofanya.—Zaburi 91:1-3.

14. Mtume Paulo anatuhakikishiaje kwamba Yehova hatatuacha tukimtegemea tunapopatwa na jaribu?

14 Tunaweza kuwa na hakika kwamba ikiwa hiyo ndiyo tamaa yetu ya unyoofu, ambayo tunaonyesha kupitia sala na matendo yetu, Yehova hatatuacha kamwe. Mtume Paulo anatuhakikishia hivi: “Hakuna jaribu ambalo limewapata ninyi ila lile lililo kawaida kwa watu. Lakini Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.

“Utukomboe Kutokana na Yule Mwovu”

15. Kwa nini ni muhimu zaidi sasa kusali tukombolewe kutokana na yule mwovu?

15 Kulingana na hati zenye kutegemeka zaidi za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, sala ya Yesu ya kielelezo inamalizika kwa maneno haya: “Utukomboe kutokana na yule mwovu.” * (Mathayo 6:13) Tunahitaji sana kulindwa dhidi ya Ibilisi wakati huu wa mwisho. Hiyo ni kwa sababu Shetani na roho wake waovu wanapigana na mabaki ya watiwa-mafuta “wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu,” wakiwa pamoja na waandamani wao wa “umati mkubwa.” (Ufunuo 7:9; 12:9, 17) Mtume Petro aliwaonya Wakristo hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu. Lakini chukueni msimamo mkampinge yeye, mkiwa imara katika imani.” (1 Petro 5:8, 9) Shetani angependa kukomesha kazi yetu ya kuhubiri, naye hujaribu kutuogopesha kupitia wawakilishi wake duniani—wawe viongozi wa kidini, wafanyabiashara, au wanasiasa. Lakini Yehova atatukomboa tukisimama imara. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Basi, jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—Yakobo 4:7.

16. Yehova hutumia nini kuwasaidia watumishi wake wanapopatwa na majaribu?

16 Yehova aliruhusu Mwana wake ajaribiwe. Lakini Yesu alipompinga Ibilisi akitumia Neno la Mungu kuwa ulinzi, Yehova alituma malaika kumwimarisha. (Mathayo 4:1-11) Vivyo hivyo, Yehova hutumia malaika zake kutusaidia tukisali kwa imani na kumfanya kuwa kimbilio letu. (Zaburi 34:7; 91:9-11) Mtume Petro aliandika: “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, lakini kuwaweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya ile siku ya hukumu ili wakatiliwe mbali.”—2 Petro 2:9.

Ukombozi Kamili Unakaribia

17. Kwa kutupatia sala ya kielelezo Yesu alionyeshaje mambo ya kutangulizwa?

17 Katika sala ya kielelezo, Yesu anaonyesha mambo ya kutangulizwa. Hangaiko letu kuu linapaswa kuwa kutakaswa kwa jina kuu na takatifu la Yehova. Kwa kuwa Yehova atatumia Ufalme wake wa Kimasihi kutekeleza jambo hilo, tunasali Ufalme huo uje ili uharibu falme au serikali zote za wanadamu ambazo si kamilifu, na kuhakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yatatendeka kikamili mbinguni na pia duniani. Tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso linategemea kutakaswa kwa jina la Yehova na kutambuliwa ulimwenguni pote kwa enzi yake kuu ya uadilifu. Baada ya kusali kuhusu mambo hayo muhimu sana, tunaweza kusali kuhusu mahitaji yetu ya kila siku, msamaha wa dhambi zetu, na kukombolewa kutoka katika majaribu, na mbinu za ujanja za yule mwovu, Shetani Ibilisi.

18, 19. Sala ya Yesu ya kielelezo inatusaidiaje kuendelea kukesha na kufanya tumaini letu liwe “imara mpaka mwisho”?

18 Kukombolewa kabisa kutoka kwa yule mwovu na mfumo wake uliopotoka kunakaribia. Shetani anajua vizuri sana kwamba ana ‘kipindi kifupi tu cha wakati’ cha kudhihirisha ‘hasira yake kali’ duniani, hasa juu ya watumishi waaminifu wa Yehova. (Ufunuo 12:12, 17) Katika ishara yenye mambo mengi ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alitabiri matukio yenye kusisimua, ambayo baadhi yake yatatukia wakati ujao. (Mathayo 24:3, 29-31) Tutakapoona mambo hayo yakitukia, tumaini letu la kukombolewa litakuwa jangavu zaidi. Yesu alisema: “Mambo haya yanapoanza kutukia, simameni wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”—Luka 21:25-28.

19 Sala fupi ya kielelezo ambayo Yesu aliwafunza wanafunzi wake inatutolea mwongozo mzuri kuhusu mambo tunayopaswa kutaja katika sala zetu mwisho unapokaribia. Na tuwe na hakika kwamba Yehova ataendelea kutuandalia mahitaji yetu ya kiroho na ya kimwili hadi mwisho kabisa. Tukiendelea kukesha katika sala tutaweza ‘kushikilia sana uhakika tuliokuwa nao mwanzoni imara mpaka mwisho.’—Waebrania 3:14; 1 Petro 4:7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Baadhi ya Biblia za zamani kama vile Union Version, humalizia Sala ya Bwana kwa maneno haya ya kumsifu Mungu: “Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.” Kichapo The Jerome Biblical Commentary kinasema: “Maneno hayo ya kumsifu Mungu . . . hayapatikani katika [hati] zenye kutegemeka zaidi.”

Kwa Kupitia

• Ni mambo gani yanayotiwa ndani katika ombi letu la kupata “mkate kwa ajili ya siku hii”?

• Eleza ombi “utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.”

• Inamaanisha nini tunapomwomba Yehova asituingize katika jaribu?

• Kwa nini tunahitaji kumwomba Yehova ‘atukomboe kutokana na yule mwovu’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ili tusamehewe, ni lazima tuwasamehe wengine

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]

Lydekker