Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Usafi wa Kiadili kwa Kuulinda Moyo Wako

Dumisha Usafi wa Kiadili kwa Kuulinda Moyo Wako

Dumisha Usafi wa Kiadili kwa Kuulinda Moyo Wako

“Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.”—METHALI 4:23.

1-3. (a) Mara nyingi watu huonyeshaje kwamba hawathamini usafi wao wa kiadili? Toa mfano. (b) Kwa nini ni muhimu kuchunguza thamani ya usafi wa kiadili?

HUENDA picha hiyo ya kuchorwa ilionekana kuwa ya kizamani. Labda haikufaana na mapambo mengine katika nyumba. Vyovyote vile, yaonekana mwenye picha hiyo hakuihitaji. Hatimaye, picha hiyo iliishia kwa watu wanaonunua bidhaa zilizotumika kisha kuziuza ili wachangishe pesa, nao waliiuza kwa dola 29 za Marekani. Hata hivyo, miaka michache baadaye, mtu aliyeinunua aligundua kwamba ilikuwa na thamani ya dola milioni moja hivi! Naam, picha hiyo ilikuwa mchoro wa kipekee. Ebu wazia jinsi mwenye picha wa kwanza ambaye hakuithamini, alivyohisi!

2 Mara nyingi, jambo kama hilo hutukia kuhusiana na usafi au utakato wa kiadili wa kila mtu. Leo watu wengi sana hawathamini usafi wao wa kiadili. Baadhi yao huuona kuwa jambo la kizamani ambalo halipatani na mtindo wa maisha ya kisasa. Hivyo, wao huupoteza kwa kubadilishana na kitu chenye thamani ndogo. Wengine hubadilishana usafi wao wa kiadili na ngono za muda mfupi za kujifurahisha. Nao wengine huupoteza ili wasionwe kuwa washamba na marika wao au na mtu wa jinsia tofauti.—Methali 13:20.

3 Wengi hutambua wakiwa wamechelewa mno jinsi usafi wao wa kiadili ulivyokuwa wenye thamani. Mara nyingi wao huhuzunika sana kwa kuupoteza. Kama Biblia isemavyo, matokeo ya ukosefu wa adili yanaweza kuwa kama sumu, “machungu kama pakanga.” (Methali 5:3, 4) Kwa kufikiria upotovu wa maadili leo, unawezaje kuthamini na kudumisha usafi wako wa kiadili? Tutazungumzia hatua tatu tunazoweza kuchukua kuhusiana na habari hiyo.

Linda Moyo Wako

4. Moyo wa mfano ni nini, na kwa nini tunapaswa kuulinda?

4 Siri ya kudumisha usafi wa kiadili ni kuulinda moyo. Biblia inasema: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) “Moyo wako” unaotajwa hapa ni nini? Si moyo halisi bali ni moyo wa mfano. Unamaanisha jinsi wewe ulivyo kwa ndani, kutia ndani mawazo, hisia, na makusudio yako. Biblia inasema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5) Yesu aliitaja amri hiyo kuwa kubwa kuliko zote. (Marko 12:29, 30) Ni wazi kwamba moyo huo wetu una thamani kubwa sana. Tunapaswa kuulinda.

5. Moyo unawezaje kuwa wenye thamani na wakati uleule uwe hatari?

5 Hata hivyo, Biblia pia husema kwamba “moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Moyo unawezaje kuwa wenye hila na hatari kwetu? Kwa mfano, gari ni kitu chenye thamani na linaweza kutusaidia kuokoa uhai wa mtu wakati wa dharura. Lakini ikiwa dereva haliendeshi vizuri, gari hilohilo linaweza kuua kwa urahisi. Vivyo hivyo, usipoulinda moyo wako, itakuwa vigumu kudhibiti tamaa zako, na hiyo inaweza kukuletea madhara. Neno la Mungu linasema: “Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mjinga, lakini yeye anayetembea katika hekima ndiye atakayeponyoka.” (Methali 28:26) Naam, unaweza kutembea katika hekima na kuepuka madhara ukitumia mwongozo wa Neno la Mungu kama vile ungetazama ramani kabla ya kuanza safari.—Zaburi 119:105.

6, 7. (a) Utakatifu ni nini, na kwa nini sifa hiyo ni muhimu kwa watumishi wa Yehova? (b) Tunajuaje kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kudhihirisha utakatifu wa Yehova?

6 Kwa kawaida moyo wetu hautuelekezi kwenye usafi wa kiadili. Lazima tuuelekeze. Njia moja ya kufanya hivyo ni kutafakari thamani ya kweli ya kuwa safi kiadili. Sifa hiyo inahusiana sana na utakatifu, yaani, usafi, utakato, na kujitenga na dhambi. Utakatifu ni sifa yenye thamani ambayo ni sehemu muhimu ya utu wa Yehova Mungu. Kuna mistari mingi ya Biblia inayohusianisha sifa hiyo na Yehova. Hata Biblia inasema kwamba “Utakatifu ni wa Yehova.” (Kutoka 28:36) Hata hivyo, sifa hiyo ya hali ya juu inatuhusuje sisi wanadamu wasio wakamilifu?

7 Yehova anatuambia hivi katika Neno lake: “Muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.” (1 Petro 1:16) Naam, tunaweza kuuiga utakatifu wa Yehova; tunaweza kuwa safi mbele zake, na kudumisha usafi wetu wa kiadili. Kwa hiyo, tunapojiepusha na matendo yasiyo safi na yenye kutia unajisi, tunakuwa na tumaini la kupata pendeleo kuu na zuri, yaani, kudhihirisha sifa ya Mungu Aliye Juu Zaidi! (Waefeso 5:1) Hatupaswi kufikiri kwamba hatuwezi kufanya hivyo, kwa kuwa Yehova ni Bwana mwenye hekima na usawaziko, asiyedai tufanye mambo yanayozidi uwezo wetu. (Zaburi 103:13, 14; Yakobo 3:17) Ni kweli kwamba jitihada inatakiwa ili kudumisha usafi wa kiroho na wa kiadili. Hata hivyo, mtume Paulo alisema kwamba “unyoofu wa moyo na usafi wa kiadili . . . unamfaa Kristo.” (2 Wakorintho 11:3) Tunapaswa kujitahidi kudumisha usafi wa kiadili ili tumpendeze Kristo na Baba yake. Hiyo ni kwa sababu wametuonyesha upendo mwingi sana hivi kwamba hatuwezi kuwalipa. (Yohana 3:16; 15:13) Inafaa tuonyeshe shukrani kwa kuishi maisha safi kiadili. Kwa kuona kwamba usafi wetu wa kiadili ni njia ya kuonyesha shukrani kwa Yehova, tutauthamini na kuulinda moyo wetu.

8. (a) Tunawezaje kuulisha moyo wa mfano? (b) Mazungumzo yetu yanaweza kufunua nini kutuhusu?

8 Tunaulinda moyo wetu pia kwa jinsi tunavyojilisha. Tunahitaji kulisha akili na moyo wetu chakula kizuri cha kiroho kwa ukawaida, na kukazia fikira habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Wakolosai 3:2) Hata mazungumzo yetu yanapaswa kuonyesha kwamba tunakazia fikira mambo hayo. Ikiwa tuna zoea la kuzungumza mambo ya kimwili na yasiyo ya adili, tunafunua jambo fulani kuhusu jinsi moyo wetu ulivyo. (Luka 6:45) Badala ya kufanya hivyo, na tuwe na zoea la kuzungumza mambo ya kiroho na yenye kujenga. (Waefeso 5:3) Ili kuulinda moyo wetu, kuna mambo mengine hatari sana tunayopaswa kuepuka. Acheni, tuzungumzie mawili kati ya hayo.

Ukimbieni Uasherati

9-11. (a) Kwa nini wale wanaopuuza shauri la 1 Wakorintho 6:18 wanaelekea sana kujihusisha na dhambi nzito ya uasherati? Toa mfano. (b) Ikiwa tunaukimbia uasherati, tunaepuka nini? (c) Ayubu mwaminifu alituwekea kielelezo gani cha pekee?

9 Yehova alimwongoza mtume Paulo kwa roho aandike shauri ambalo limewasaidia wengi kuilinda mioyo yao na kudumisha usafi wa kiadili. Paulo alisema: “Ukimbieni uasherati.” (1 Wakorintho 6:18) Ona kwamba hakusema tu, “Jiepusheni na uasherati.” Wakristo wanapaswa kufanya mengi zaidi. Wanapaswa kukimbia mambo hayo yasiyo ya adili kama vile wangekimbia jambo linalohatarisha maisha yao. Tukipuuza shauri hilo, huenda ikawa rahisi sana kujihusisha na dhambi nzito ya uasherati na kupoteza kibali cha Mungu.

10 Tuseme mama amemwosha na kumvalisha mvulana wake mdogo ili kumtayarisha kwa ajili ya tukio fulani muhimu. Mvulana huyo anaomba ruhusa akacheze nje kabla ya familia kuondoka, naye mama yake anakubali kwa sharti moja. Anamwambia: “Usiende karibu na kidimbwi hicho cha maji machafu. Ukijichafua, utaadhibiwa.” Baada ya dakika chache, anamwona mvulana huyo akiyumba-yumba karibu sana na kidimbwi hicho. Hajajichafua bado, lakini anapuuza onyo la mama yake kwamba asikaribie kidimbwi hicho, na yaelekea sana kwamba mvulana huyo atakuwa taabani. (Methali 22:15) Vijana wengi na watu wazima wanaopaswa kuwa waangalifu zaidi hufanya kosa kama hilo. Jinsi gani?

11 Wakati huu ambapo watu wengi sana wameshindwa na “hamu za ngono yenye kufedhehesha,” aina mpya ya biashara imetokea ambayo inasambaza habari kuhusu ngono haramu. (Waroma 1:26, 27) Ponografia imeenea sana katika magazeti, vitabu, video, na Internet. Bila shaka, wale wanaoamua kutazama picha hizo hawaukimbii uasherati. Wanauchezea-chezea na kujihatarisha, huku wakipuuza onyo la Biblia. Badala ya kuulinda moyo, wanautia sumu kwa kutazama picha zinazoonyesha mambo waziwazi ambazo huenda zikachukua muda mrefu kufutika akilini. (Methali 6:27) Na tujifunze kutokana na Ayubu mwaminifu, aliyefanya agano na macho yake ili asitazame mambo ambayo yangemshawishi kufanya mabaya. (Ayubu 31:1) Bila shaka, tunahitaji kuiga kielelezo chake.

12. Wenzi Wakristo wanawezaje ‘kuukimbia uasherati’ wakati wa uchumba?

12 Ni muhimu hasa ‘kuukimbia uasherati’ wakati wa uchumba. Pindi hiyo inapaswa kuwa wakati wa furaha, wenye matumaini na matazamio mengi, lakini vijana fulani wanaochumbiana huuharibu kwa kucheza-cheza na uasherati. Kwa kufanya hivyo, kila mmoja anaharibia mwenzake msingi bora wa kuwa na ndoa nzuri, yaani, uhusiano unaotegemea upendo usio na ubinafsi, kujizuia, na kumtii Yehova Mungu. Wenzi fulani Wakristo walijihusisha na ukosefu wa adili wakati wa uchumba wao. Baada ya kuoana, mke alikiri kwamba dhamiri yake ilimsumbua, hata ikamharibia furaha wakati wa arusi yake. Alikiri hivi: “Nimeomba msamaha kwa Yehova mara nyingi, lakini ingawa miaka saba imepita tangu wakati huo, bado dhamiri yangu hunisumbua.” Ni muhimu kwamba wale wanaofanya dhambi hizo watafute msaada wa wazee Wakristo. (Yakobo 5:14, 15) Hata hivyo, wenzi wengi Wakristo hutenda kwa hekima na kuepuka hatari hizo wakati wa uchumba. (Methali 22:3) Wanaweka mipaka kuhusu kuonyeshana upendo. Wao huandamana na mtu wa tatu na huepuka kuwa peke yao mahali pasipo na watu.

13. Kwa nini Wakristo hawapaswi kuchumbia mtu asiyemtumikia Yehova?

13 Yaelekea Wakristo wanaoanzisha uchumba na watu wasiomtumikia Yehova watakabili matatizo makubwa. Kwa mfano, unawezaje kuanzisha uhusiano na mtu asiyempenda Yehova Mungu? Ni muhimu kwamba Wakristo wajifunge nira tu na wale wanaompenda Yehova na kuheshimu viwango vyake vya usafi wa kiadili. Neno la Mungu hutuambia hivi: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. Kwa maana kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria? Au nuru ina ushirika gani na giza?”—2 Wakorintho 6:14.

14, 15. (a) Watu fulani wana maoni gani yasiyo sahihi kuhusu maana ya neno “uasherati”? (b) “Uasherati” unahusisha matendo gani, na Wakristo wanawezaje ‘kuukimbia uasherati’?

14 Ujuzi ni muhimu pia. Hatuwezi kuukimbia uasherati ifaavyo iwapo hatuujui vizuri. Leo, watu fulani duniani wana maoni yasiyo sahihi kuhusu maana ya “uasherati.” Wanafikiri kwamba wanaweza kutosheleza tamaa zao za ngono bila kufunga ndoa, maadamu tu wataepuka tendo la ngono. Hata taasisi fulani mashuhuri za afya zinazojitahidi kupunguza idadi ya mimba za matineja zisizotakiwa, zimewatia moyo vijana wafanye ngono zilizopotoka ambazo hazitokezi mimba. Kwa kusikitisha, shauri hilo linapotosha. Kuepuka kupata mimba nje ya ndoa si sawa na kudumisha usafi wa kiadili, nayo maana halisi ya neno “uasherati” ni pana sana.

15 Neno la Kigiriki por·neiʹa, linalotafsiriwa kuwa “uasherati,” lina maana pana sana. Linahusu uhusiano wa kingono kati ya watu wasiofunga ndoa na hukazia kutumia vibaya viungo vya uzazi. Por·neiʹa inatia ndani vitendo kama vile ngono za kinywa, ngono za mkundu, na kumpiga mtu mwingine punyeto, vitendo ambavyo kwa kawaida huhusianishwa na nyumba za makahaba. Watu wanaofikiri kwamba matendo hayo si “uasherati” wanajidanganya wenyewe nao wamenaswa na mojawapo ya mitego ya Shetani. (2 Timotheo 2:26) Isitoshe, kudumisha usafi wa kiadili humaanisha mengi zaidi kuliko kujiepusha tu na tendo lolote lile la uasherati. Ili ‘kuukimbia uasherati,’ tunapaswa kuepuka kila namna ya uchafu wa kingono na mwenendo mpotovu unaoweza kuongoza kwenye dhambi nzito ya por·neiʹa. (Waefeso 4:19) Kwa kufanya hivyo tunadumisha usafi wa kiadili.

Epuka Hatari ya Kuwachezea Wengine Kimapenzi

16. Kulingana na mfano mmoja wa Biblia, kuonyeshana mapenzi kunafaa katika hali gani?

16 Hatari nyingine tunayohitaji kujihadhari nayo ili kudumisha usafi wetu wa kiadili ni kuchezea wengine kimapenzi. Huenda watu fulani wakadai kwamba kuchezea wengine kimapenzi ni jambo la kujifurahisha tu kati ya watu wa jinsia tofauti ambalo haliwezi kuleta madhara. Ni kweli kwamba kuna wakati na mahali pa kuonyeshana mapenzi. Isaka na Rebeka walionekana ‘wakichezacheza’ pamoja na ilikuwa wazi kwa watazamaji kwamba hawakuwa ndugu na dada. (Mwanzo 26:7-9) Hata hivyo, walikuwa mume na mke na hakukuwa na ubaya wowote wa kuonyeshana upendo. Lakini kuchezea wengine kimapenzi ni jambo tofauti kabisa.

17. Kuchezea wengine kimapenzi ni nini, na tatizo hilo linaweza kudhibitiwaje?

17 Kuchezea wengine kimapenzi kunaweza kufafanuliwa hivi: kuonyesha unapendezwa na mtu kimapenzi bila kuwa na kusudi la kufunga ndoa naye. Si rahisi kumwelewa mwanadamu, kwa hiyo kuna njia nyingi za kuchezea wengine kimapenzi na baadhi ya njia hizo hazitambuliki kwa urahisi. (Methali 30:18, 19) Kwa hiyo, jambo hilo haliwezi kushughulikiwa kwa kuweka sheria madhubuti. Badala yake, jambo fulani bora kuliko sheria linahitajiwa, yaani, kujichunguza kwa unyoofu na kutumia kanuni za Biblia kwa kuongozwa na dhamiri.

18. Ni nini huwachochea watu fulani wawachezee wengine kimapenzi, na kwa nini jambo hilo ni hatari?

18 Tukichunguza hisia zetu kwa unyoofu, yaelekea wengi wetu tutakubali kwamba tunafurahi wakati tunapotambua kwamba mtu fulani wa jinsia tofauti anapendezwa nasi kimapenzi. Hilo ni jambo la kawaida. Lakini je, sisi huchezea wengine kimapenzi ili tuonyeshwe upendezi huo, tujihisi tu kuwa bora, au kufanya wengine wahisi hivyo? Ikiwa ndivyo, je, tumefikiria maumivu ambayo huenda tukawa tunawasababishia wengine? Kwa mfano, andiko la Methali 13:12 linasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” Tukimchezea mtu kimapenzi kwa makusudi, huenda tusijue jinsi mtu huyo anavyoathirika. Huenda akawa na matazamio ya uchumba na hata kufunga ndoa baadaye. Mtu anaweza kukata tamaa kabisa kutokana na jambo hilo. (Methali 18:14) Ni jambo la kikatili kuchezea hisia za wengine kimakusudi.

19. Kuwachezea wengine kimapenzi kunaweza kuhatarishaje ndoa za Kikristo?

19 Ni muhimu sana kwa watu waliofunga ndoa kuepuka kuchezea wengine kimapenzi. Kuonyesha unapendezwa kimapenzi na mtu aliyefunga ndoa, au mtu aliyefunga ndoa kuonyesha upendezi huo kwa mtu asiye mwenzi wake ni kosa. Kwa kusikitisha, baadhi ya Wakristo wana maoni yenye makosa kwamba ni sawa kusitawisha hisia za kimapenzi kuelekea mtu wa jinsia tofauti ambaye si mwenzi wao. Wengine humweleza “rafiki” huyo mahangaiko yao ya moyoni hata kumfunulia mambo ya kibinafsi ambayo hawamwelezi mwenzi wao. Kwa sababu hiyo, hisia za kimapenzi huongezeka na hivyo kuanza kumtegemea kihisia “rafiki” huyo, jambo ambalo linaweza kudhoofisha na hata kuiharibu ndoa. Wakristo waliofunga ndoa wanapaswa kukumbuka shauri la hekima la Yesu kuhusu uzinzi, kwamba huanza katika moyo. (Mathayo 5:28) Kwa hiyo, na tuulinde moyo wetu na kuepuka hali zinazoweza kusababisha madhara kama hayo.

20. Tunapaswa kuazimia kuuonaje usafi wetu wa kiadili?

20 Kwa kweli, si rahisi kudumisha usafi wa kiadili katika ulimwengu wa sasa uliopotoka kiadili. Hata hivyo, kumbuka kwamba ni rahisi zaidi kudumisha usafi wako wa kiadili kuliko kuupata tena baada ya kuupoteza. Bila shaka, Yehova anaweza “kusamehe kwa njia kubwa” na anaweza kuwatakasa wale wanaotubu dhambi zao kikweli. (Isaya 55:7) Lakini Yehova hawakingi wale wanaofanya uasherati wasipatwe na matokeo ya matendo yao. Matokeo hayo yanaweza kudumu kwa miaka mingi, hata katika maisha yao yote. (2 Samweli 12:9-12) Unapaswa kudumisha usafi wako wa kiadili kwa kuulinda moyo wako. Uone msimamo wako safi na wa kiadili mbele za Yehova Mungu kuwa kitu chenye thamani sana na usikipoteze kamwe!

Ungejibuje?

• Usafi wa kiadili ni nini, na kwa nini ni muhimu sana?

• Tunaweza kuulinda moyo wetu jinsi gani?

• Ni nini kinachohusika katika kuukimbia uasherati?

• Kwa nini tunapaswa kuepuka kuchezea wengine kimapenzi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 11]

Gari linaweza kuwa hatari lisipoendeshwa vizuri

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ni nini kinachoweza kutokea tukipuuza maonyo?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Usafi wa kiadili wakati wa uchumba huleta furaha na pia humletea Mungu heshima