Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Faraja kwa Wanaoteseka

Faraja kwa Wanaoteseka

Faraja kwa Wanaoteseka

WAKATI wanaume na wanawake waaminifu wa zamani walipopatwa na mateso, walimwomba Mungu kwa bidii awape mwongozo. Hata hivyo, walichukua pia hatua za kupunguza mateso hayo, kama vile kutumia akili ili kuwaepa wakandamizaji. Kwa mfano, kumtegemea Yehova pamoja na jitihada za kibinafsi zilimwezesha Daudi kuvumilia magumu yaliyompata. Namna gani sisi leo?

Unapopatwa na mateso, yaelekea unachukua hatua ya kutatua tatizo lako. Kwa mfano, ikiwa huna kazi utajitahidi kupata kazi inayofaa ambayo itakutegemeza wewe pamoja na familia yako. (1 Timotheo 5:8) Au ikiwa una ugonjwa fulani, utatafuta matibabu yanayofaa. Inapendeza kwamba Yesu, ambaye alikuwa na nguvu kutoka kwa Mungu za kuponya aina zote za magonjwa, alikiri kwamba ‘wenye kuugua ndio wanaohitaji tabibu.’ (Mathayo 9:12) Hata hivyo, huenda magumu yako yasiondolewe sikuzote; huenda ukalazimika kuendelea kuyavumilia kwa muda fulani.

Kwa nini usisali kwa Yehova Mungu kuhusu jambo hilo? Kwa mfano, tunapotafuta kazi, kumtegemea Mungu katika sala kutatusaidia kushinda kishawishi chochote cha kukubali kazi inayopingana na kanuni za Biblia. Pia hatutaruhusu pupa au upendo wa pesa ‘utupotoshe kutoka kwenye imani.’ (1 Timotheo 6:10) Naam, tunapofanya maamuzi muhimu kuhusu kazi, familia, au afya tunaweza kufuata himizo hili la Daudi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”—Zaburi 55:22.

Sala ya kutoka moyoni itatusaidia pia kudumisha akili timamu ili tusilemewe na mateso. Mtume Paulo, aliyekuwa Mkristo wa kweli aliandika hivi: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” Sala ya unyoofu inaweza kutufariji jinsi gani? “Amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Amani ya Mungu ni “yenye ubora unaozidi fikira zote.” Kwa hiyo, inaweza kututuliza tunapolemewa na hisia zenye kusumbua. Amani hiyo ‘italinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili,’ na hivyo kutusaidia kuepuka kutenda haraka-haraka bila hekima, jambo linaloweza kuzidisha mateso yetu.

Sala inaweza hata kutokeza mabadiliko makubwa kuhusiana na hali fulani. Mtume Paulo alipofungwa huko Roma, aliwaomba Wakristo wenzake kwa unyenyekevu wasali kwa ajili yake. Kwa nini Paulo aliwaomba wafanye hivyo? Aliwaandikia, “Lakini ninawahimiza ninyi zaidi hasa mfanye hivyo, ili nirudishwe kwenu upesi inavyowezekana.” (Waebrania 13:19) Yaani, Paulo alijua kwamba kama Yehova angesikiliza sala zilizotolewa bila kukoma na waamini wenzake, hali zingeweza kubadilika kuhusiana na wakati ambapo angeachiliwa.—Filemoni 22.

Je, sala itabadili matokeo ya mateso yetu? Inawezekana. Lakini tunapaswa kutambua kwamba huenda Yehova Mungu asijibu sala zetu kwa njia ambayo tungetaka. Paulo alisali mara kadhaa kuhusu ‘mwiba wake katika mwili,’ ambao labda ulikuwa tatizo fulani la kimwili. Lakini badala ya kuondoa tatizo hilo, Mungu alimwambia Paulo hivi: “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha wewe; kwa maana nguvu zangu zinakamilishwa katika udhaifu.”—2 Wakorintho 12:7-9.

Kwa hiyo, huenda tatizo letu lisitoweke mara moja. Hata hivyo, tutakuwa na nafasi ya kuthibitisha kwamba tunamtegemea Baba yetu wa kimbingu. (Yakobo 1:2-4) Uwe na hakika kwamba hata kama Yehova Mungu hataliondoa tatizo hilo, anaweza ‘kuifanya pia njia ya kutokea kusudi tuweze kulivumilia.’ (1 Wakorintho 10:13) Ni muhimu kutambua kwamba Yehova anaitwa “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Mungu anaweza kutuandalia kile tunachohitaji ili kuvumilia, nasi tuna tumaini la kuishi milele.

Neno la Mungu, Biblia, linaahidi kwamba Yehova “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:3, 4) Je, ni vigumu sana kuamini kwamba kutakuwa na ulimwengu usio na mateso? Huenda ikawa vigumu kuamini iwapo umezoea hali ngumu. Hata hivyo, Mungu anaahidi kwamba atatuweka huru kutokana na woga na maafa, na bila shaka kusudi lake litafanikiwa.—Isaya 55:10, 11.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kutoka hali ya kukata tamaa hadi kupata kitulizo