Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dini Ina Uvutano Mzuri au Mbaya?

Je, Dini Ina Uvutano Mzuri au Mbaya?

Je, Dini Ina Uvutano Mzuri au Mbaya?

“NINAUSHUKURU Ukristo kwa yale ambayo umenifanyia, na ninaamini pia kwamba ulimwengu ambao tumeishi kwa miaka 2000 iliyopita unapaswa kushukuru vilevile.”—Dibaji, Two Thousand Years—The First Millennium: The Birth of Christianity to the Crusades.

Maneno hayo ya kuusifu “Ukristo” yalisemwa na Melvyn Bragg, ambaye ni mwandishi na mtangazaji Mwingereza. Maneno yake yanapatana na maoni ya watu wengi duniani wanaohisi kwamba wanapaswa kushukuru sana na kuwa waaminifu kwa dini moja au nyingine. Wanasadiki kwamba dini imekuwa na uvutano mzuri maishani mwao. Kwa mfano, mwandishi mmoja anasema kwamba Uislamu “umechochea ustaarabu mkubwa . . . [ambao] umeunufaisha ulimwengu wote.”

Dini Imetimiza Mema au Mabaya?

Hata hivyo, maneno yanayofuata ya Bragg yanatokeza swali muhimu kuhusu kama kwa kweli dini kwa ujumla imekuwa na uvutano mzuri. Anaongeza kusema: “Ukristo pia unapaswa kunieleza mambo fulani.” Anataka aelezwe nini? Anataka aelezwe, “Kwa nini dini zimekuwa na ‘historia’ ya kutovumilia, uovu, ukatili, na kukataa ujuzi kimakusudi?”

Wengi wangesema kwamba katika historia yote kumekuwa na hali ya kutovumilia, uovu, ukatili, na kukataa ujuzi kimakusudi katika dini nyingi za ulimwengu. Wanaamini kwamba dini hujifanya tu kuwa wafadhili wa wanadamu lakini ukweli ni kwamba zimejaa unafiki, na uwongo japo huonekana isivyo kweli kuwa zenye maadili mema na takatifu. (Mathayo 23:27, 28) Kichapo A Rationalist Encyclopædia kinasema, “Wazo kuu katika vitabu vyetu ni kwamba dini ni ya kipekee kuhusiana na ustaarabu.” Kinaendelea kusema, “Lakini mambo ya hakika katika historia yanapingana kabisa na taarifa hiyo kuhusu dini.”

Ukisoma gazeti lolote leo, utapata mifano mingi sana kuhusu viongozi wa kidini ambao huhubiri upendo, amani, na huruma lakini ambao huchochea chuki na kulitumia jina la Mungu ili kutetea vita vyao vikatili. Haishangazi kwamba watu wengi huhisi kuwa mara nyingi uvutano wa dini huleta madhara katika maisha!

Je, Ni Afadhali Kutokuwa na Dini?

Hata watu fulani wamefikia mkataa kama wa mwanafalsafa Mwingereza Bertrand Russell kwamba ingekuwa afadhali kama mwishowe “dini zote zingetoweka.” Kulingana na maoni yao, suluhisho la matatizo yote ya wanadamu ni kuondolewa kwa dini. Hata hivyo, huenda wakaamua kupuuza ukweli kwamba wale wanaokataa dini wanaweza kusababisha chuki nyingi na ubaguzi kama vile tu wale wanaoiunga mkono. Mwandishi wa masuala ya kidini Karen Armstrong anatukumbusha hivi: “Angalau Maangamizi Makuu yalionyesha kwamba imani zisizo za kidini [zinaweza] kuwa hatari kama tu vita vya dini.”—The Battle for God—Fundamentalism in Judaism, Christianity and Islam.

Kwa hiyo, je, kwa kweli dini ina uvutano mzuri au ndiyo chanzo cha matatizo ya wanadamu? Je, suluhisho la matatizo hayo ni kuondoa dini zote? Chunguza yale ambayo Biblia inasema kuhusu habari hiyo katika makala inayofuata. Huenda ukapata jibu lenye kukushangaza.