Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dini Ndiyo Chanzo cha Matatizo ya Wanadamu?

Je, Dini Ndiyo Chanzo cha Matatizo ya Wanadamu?

Je, Dini Ndiyo Chanzo cha Matatizo ya Wanadamu?

“DINI huchochea mizozo au inakuwa kama dawa ya kulevya inayotia ganzi dhamiri ya mwanadamu na kumpumbaza akili ili apuuze mambo halisi yasiyompendeza. . . . Hufanya wanadamu wawe na akili finyu, ushirikina, wajawe na chuki na woga.” Mtu huyo aliyekuwa mishonari wa Methodisti ambaye aliandika maneno hayo aliongeza kusema: “Shutuma hizo ni za kweli. Kuna dini mbaya na nzuri.”—Start Your Own Religion.

Huenda wengine wakasema, ‘Huo ni uchambuzi usiofaa.’ Hata hivyo, ni nani anayeweza kukana mambo halisi ya historia? Kwa ujumla, dini, ambayo imefafanuliwa kuwa “utumishi na ibada kwa Mungu au kiumbe mwenye nguvu zinazozidi za wanadamu”—imekuwa na sifa mbaya sana. Dini inapaswa kutuelimisha na kutuchochea. Lakini mara nyingi huchochea mizozo, ubaguzi, na chuki. Kwa nini dini hufanya hivyo?

“Malaika wa Nuru” Mwenye Kupotosha

Biblia inatoa jibu rahisi sana. Kwa kujifanya kuwa “malaika wa nuru,” Shetani Ibilisi amepotosha mamilioni ya watu wafuate mafundisho yake badala ya yale ya Mungu. (2 Wakorintho 11:14) Mtume Yohana alionyesha kwamba uvutano wa Shetani ni mwingi sana hivi kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Yohana alijua kwamba Shetani alikuwa ‘akiipotosha dunia nzima inayokaliwa.’—Ufunuo 12:9.

Matokeo yamekuwaje? Shetani ameanzisha dini ambazo huonekana kuwa takatifu. Dini hizo ‘hujifanya tu kwa nje kwamba zinamcha Mungu’ lakini matunda yake maovu hufunua kabisa jinsi zilivyo. (2 Timotheo 3:5, Biblia Habari Njema; Mathayo 7:15-20) Badala ya kusaidia kutatua matatizo ya wanadamu, kwa kweli, dini huchangia matatizo hayo.

Usitupilie mbali wazo hilo kuwa lisiloaminika au lisilopatana na akili. Kumbuka kwamba ili mtu adanganywe, ni lazima awe hajui ukweli wa mambo. Mtume Paulo alitoa mfano kuhusu jambo hilo alipoandika: “Vitu ambavyo mataifa huvitoa dhabihu wao huvitoa dhabihu kwa roho waovu, na si kwa Mungu.” (1 Wakorintho 10:20) Yaelekea watu hao wangeshtuka kufahamu kwamba walikuwa wakiabudu roho waovu. Walifikiri kwamba walikuwa wakiabudu mungu mzuri au miungu ya aina fulani. Hata hivyo, ukweli ni kwamba walikuwa wamedanganywa na “majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu,” ambao hushirikiana na Shetani katika jitihada zake za kupotosha wanadamu.—Waefeso 6:12.

Kwa mfano, na tuchunguze jinsi Shetani alivyoweza kuwadanganya na kuwapotosha wengi wanaoitwa Wakristo ambao waliamua kupuuza onyo la mtume Yohana kuhusu uvutano huo mwovu.—1 Wakorintho 10:12.

Mafundisho ya Yesu Yalitoka kwa Mungu

Yesu Kristo alisema, “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Naam, yale aliyofundisha yalitoka kwa Mungu Mweza Yote. Kwa hiyo, mafundisho ya Yesu yalikuwa yenye nguvu na yaliwaelimisha sana wale waliomsikiliza. ‘Hayakutia ganzi dhamiri ya mwanadamu au kupumbaza akili yake apuuze mambo halisi yasiyompendeza.’ Badala yake, mafundisho ya Yesu yaliwaweka watu huru na mafundisho ya kidini yenye makosa na falsafa za wanadamu zilizotokana na ulimwengu uliokuwa “katika giza kiakili” kwa sababu ya udanganyifu wa Ibilisi.—Waefeso 4:18; Mathayo 15:14; Yohana 8:31, 32.

Wakristo wa kweli walitambuliwa kwa imani iliyodhihirishwa na sifa nzuri zilizotokezwa na roho takatifu ya Mungu, bali si kujidai tu wanamcha Mungu. (Wagalatia 5:22, 23; Yakobo 1:22; 2:26) Upendo ndiyo sifa kuu kati ya sifa hizo, nayo ndiyo huwatambulisha Wakristo wa kweli.—Yohana 13:34, 35.

Hata hivyo, ona hoja hii muhimu: Wala Yesu wala mitume wake hawakutazamia kutaniko la Kikristo libaki vile lilivyokuwa mwanzoni. Walijua kwamba uasi-imani ungetokea na kwamba dini ya kweli ingefunikwa kwa muda fulani.

Dini ya Kweli Yafunikwa kwa Muda Fulani

Katika mfano kuhusu ngano na magugu, Yesu alitabiri kwamba dini ya kweli ingekuwa karibu kufunikwa kabisa kwa muda fulani. Soma habari hiyo katika Mathayo 13:24-30, 36-43. Yesu alipanda ngano shambani, yaani, “mbegu nzuri,” iliyofananisha wanafunzi wake waaminifu ambao wangefanyiza kutaniko la kwanza la Kikristo. Alionya kwamba baada ya muda fulani “adui,” Shetani Ibilisi, angepanda “magugu” katika shamba hilohilo la ngano. Magugu hayo ni watu waliodai kumfuata Yesu Kristo lakini wakayakataa mafundisho yake.

Muda mfupi tu baada ya kifo cha mitume wa Yesu, kulitokea watu fulani waliokuwa “magugu,” ambao walipendelea mafundisho yaliyopotoka ya wanadamu badala ya “neno la Yehova.” (Yeremia 8:8, 9; Matendo 20:29, 30) Hivyo, Ukristo bandia uliopotoka ukatokea ulimwenguni. Ukristo huo uliongozwa na yule ambaye Biblia humwita “mwasi-sheria,” yaani, jamii ya makasisi iliyopotoka ambayo ilijaa “kila udanganyifu usio wa uadilifu.” (2 Wathesalonike 2:6-10) Yesu alitabiri kwamba hali hiyo ingebadilika “katika umalizio wa mfumo wa mambo.” Wakristo walio mfano wa ngano wangekusanywa pamoja, na mwishowe “magugu” yangeharibiwa.

Ukristo huo bandia ndio unaopaswa kulaumiwa kwa “karne nyingi za ukatili mkubwa” na giza la kiroho lililofunika dini zinazojiita za Kikristo katika karne zilizofuata. Mtume Petro aliona kimbele mambo hayo na vitendo vingine vyote vya upotovu na jeuri ambavyo dini hizo zimefanya tangu wakati huo, naye kwa kufaa akatabiri kwamba “kwa sababu ya hao [wanaodai kuwa Wakristo] ile njia ya kweli i[nge]tukanwa.”—2 Petro 2:1, 2.

“Huchochea Hasira na Chuki”

Bila shaka, si Jumuiya ya Wakristo tu ambayo imefanya dini ziwe na sifa mbaya. Kwa mfano, fikiria dini ambazo ‘wafuasi wake wana imani kali,’ ambazo Karen Armstrong, aliyekuwa mtawa, anasema zimetokana na ‘dini kubwa-kubwa.’ Armstrong anasema kuwa njia moja tunayoweza kutumia kuamua kama dini ni nzuri ni kwa kuchunguza kama dini hiyo “huonyesha huruma kwa matendo.” Dini zenye wafuasi wenye imani kali zimekuwa na sifa gani? Armstrong anaandika, “Dini zenye imani kali ziwe za Kiyahudi, Kikristo, au Kiislamu, haziwezi kuthibitisha ni za kweli ikiwa zinachochea hasira na chuki.” (The Battle for God—Fundamentalism in Judaism, Christianity and Islam) Lakini je, ni “dini zenye imani kali” tu ambazo zimeshindwa kuthibitisha ni za kweli na hivyo “kuchochea hasira na chuki”? Historia inaonyesha kwamba kuna dini nyingine pia.

Kwa kweli, Shetani ametokeza miliki ya ulimwengu ya dini za uwongo, zinazotambulishwa na hasira, chuki, na umwagikaji mwingi wa damu. Biblia inaiita miliki hiyo “Babiloni Mkubwa, mama . . . wa machukizo ya dunia,” nayo inafananishwa na kahaba aliyepanda juu ya mfumo wa kisiasa ulio kama mnyama. Ni muhimu kutambua kwamba kahaba huyo ndiye anayelaumika kwa “damu . . . ya wale wote ambao wameuawa juu ya dunia.”—Ufunuo 17:4-6; 18:24.

Si Kila Mtu Ambaye Amedanganywa

Hata hivyo, historia inaonyesha kwamba si kila mtu ambaye amedanganywa. Hata wakati ambapo hali zilikuwa mbaya zaidi, Melvyn Bragg anasema kwamba “watu wengi wenye sifa nzuri walitenda mema ingawa walizungukwa na watu wengi waovu.” Wakristo wa kweli waliendelea ‘kumwabudu Mungu kwa roho na kweli.’ (Yohana 4:21-24) Walikuwa tofauti na dini za ulimwengu zilizokuwa zimejifanya kuwa kahaba kwa “kuunga mkono mamlaka za kijeshi.” Walikataa kushirikiana na Kanisa na Serikali ambazo historia inazionyesha kuwa “mkataba uliofanyizwa na Shetani wala si Yesu wa Nazareti.”—Two Thousand Years—The Second Millennium: From Medieval Christendom to Global Christianity.

Hivi karibuni, Mashahidi wa Yehova wamejulikana kwa sababu ya uvutano wao mzuri. Ili wajiepushe kabisa na dini za uwongo, wametegemeza imani na matendo yao katika Biblia tu, ambayo ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (2 Timotheo 3:16, 17) Na kama Wakristo wa karne ya kwanza, wamefuata amri ya Yesu ya kutokuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:17-19; 17:14-16) Kwa mfano, katika Ujerumani ya Nazi, walikataa kuvunja kanuni za Kikristo na hivyo hawakufaa kulingana na nadharia ya Nazi. Hitler aliwachukia kwa msimamo wao. Kitabu kimoja cha shule kinasema: “Mashahidi wa Yehova . . . walifuata fundisho la Biblia kwamba wasitumie silaha kwa sababu yoyote ile. Kwa hiyo, walikataa kutumika jeshini au kushirikiana kwa vyovyote na Nazi. Kwa kulipiza kisasi, kikosi maalumu cha walinzi wa Hitler kilifunga gerezani familia nzima-nzima za Mashahidi wa Yehova. Karibu sehemu moja ya tatu ya Mashahidi wa Yehova [nchini Ujerumani] waliuawa katika kambi za mateso.”—Germany—1918-45.

Bila shaka, watu mmoja-mmoja wajasiri katika dini mbalimbali waliteseka kwa ajili ya imani yao. Lakini Mashahidi wa Yehova waliteswa wakiwa kikundi cha kidini kilichoungana. Bila shaka, wengi wao walishikilia kwa uthabiti kanuni hii ya msingi ya Kimaandiko: ‘Mtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:29; Marko 12:17.

Chanzo cha Matatizo

Kwa hiyo, si kweli kabisa kwamba dini ndiyo chanzo cha matatizo yote ya mwanadamu. Dini za uwongo ndizo chanzo cha matatizo hayo. Hata hivyo, Mungu anakusudia kuondoa dini zote za uwongo hivi karibuni. (Ufunuo 17:16, 17; 18:21) Anatoa amri hii kwa yeyote anayependa haki na uadilifu: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimekusanyika pamoja mpaka mbinguni, naye Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki.” (Ufunuo 18:4, 5) Naam, Mungu mwenyewe anachukizwa sana na dini ‘zinazochochea mizozo, zinazotia ganzi dhamiri ya wanadamu na kupumbaza akili yao wasione mambo halisi yasiyowapendeza, wawe na akili finyu, ushirikina, wajawe na chuki na woga’!

Wakati huu Mungu anawakusanya wale wanaopenda kweli katika dini safi. Hiyo ni dini ambayo hufuata kanuni na mafundisho ya Muumba mwenye upendo, haki, na huruma. (Mika 4:1, 2; Sefania 3:8, 9; Mathayo 13:30) Unaweza kuwa mshiriki wa dini hiyo. Ikiwa ungependa kupata habari zaidi kuhusu jinsi ya kutambua dini safi, jihisi huru kuwaandikia wachapishaji wa gazeti hili, au utafute msaada kutoka kwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Watu wa malezi yote wamepata shangwe katika dini safi