Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jihadhari na Udanganyifu

Jihadhari na Udanganyifu

Jihadhari na Udanganyifu

“Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia . . . udanganyifu mtupu.”—WAKOLOSAI 2:8.

1-3. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba udanganyifu umeenea katika karibu kila sehemu ya maisha ya sasa? (b) Kwa nini tusishangazwe na udanganyifu ulio katika ulimwengu?

“NI WANGAPI kati yenu ambao hawajawahi kudanganywa na mteja?” Miaka kadhaa iliyopita, profesa mmoja wa sheria alifanya uchunguzi kwa kuuliza swali hilo. Itikio likawaje? Anaeleza: “Ni mwanasheria mmoja tu kati ya maelfu ya wanasheria ambaye hakuwa amewahi kudanganywa.” Kwa nini? “Mwanasheria huyo alikuwa ameanza tu kufanya kazi katika shirika fulani kubwa na hakuwa amezungumza na mteja yeyote.” Jambo hilo linaonyesha ukweli wenye kusikitisha kwamba uwongo na udanganyifu ni mambo ya kawaida katika ulimwengu wa leo.

2 Kuna namna mbalimbali za udanganyifu, nao umeenea katika karibu kila sehemu ya maisha ya sasa. Tunapata mifano mingi sana katika vyombo vya habari—wanasiasa wanaodanganya kuhusu matendo yao, wahasibu na wanasheria wanaotia chumvi faida za mashirika, watangazaji wa bidhaa wanaowapotosha wanunuzi, udanganyifu wa watu wanaodai malipo kutoka kwa makampuni ya bima, kutaja tu michache. Kisha kuna udanganyifu wa kidini. Makasisi huwapotosha watu wengi kwa kufundisha mafundisho ya uwongo, kama vile kutokufa kwa nafsi, moto wa mateso, na Utatu.—2 Timotheo 4:3, 4.

3 Je, tunapaswa kushangazwa na udanganyifu huo wote? La, kwa kuwa Biblia ilionya hivi kuhusu “siku za mwisho”: “Watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.” (2 Timotheo 3:1, 13) Tukiwa Wakristo tunahitaji kuwa macho kuhusu maoni yenye kupotosha yanayoweza kutufanya tuache kweli. Kwa kawaida, maswali haya mawili yanazuka: Kwa nini udanganyifu umeenea sana leo, na tunawezaje kujilinda tusidanganywe?

Kwa Nini Kuna Udanganyifu Mwingi Leo?

4. Biblia inaelezaje sababu ya kuenea sana kwa udanganyifu ulimwenguni?

4 Biblia hueleza waziwazi ni kwa nini leo udanganyifu umeenea sana ulimwenguni. Mtume Yohana aliandika kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) ‘Mwovu huyo’ ni Shetani Ibilisi. Yesu alisema hivi kumhusu: “Hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haimo ndani yake. Anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.” Basi, si jambo la kushangaza kwamba ulimwengu huu unaonyesha roho, maadili, na udanganyifu wa huyo mtawala wake.—Yohana 8:44; 14:30; Waefeso 2:1-3.

5. Shetani amezidishaje jitihada zake za udanganyifu wakati huu wa mwisho, naye ameazimia hasa kuwapotosha nani?

5 Wakati huu wa mwisho, Shetani amezidisha jitihada zake. Ametupwa duniani. Anajua kwamba wakati wake ni mfupi naye ana “hasira kali.” Kwa kuwa ameazimia kuangamiza wanadamu wengi iwezekanavyo, yeye ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9, 12) Shetani hadanganyi mara moja moja tu, bali yeye hujitahidi daima kuwapotosha wanadamu. * Anatumia njia yoyote ile ya udanganyifu anayoweza kupata, kutia ndani ujanja na hila, ili kupofusha akili za wasioamini na kuwazuia wasimkaribie Mungu. (2 Wakorintho 4:4) Stadi huyo wa udanganyifu ameazimia hasa kuwameza wale wanaomwabudu Mungu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24; 1 Petro 5:8) Usisahau kamwe kwamba Shetani amedai hivi: ‘Ninaweza kumgeuza mtu yeyote asimtumikie Mungu.’ (Ayubu 1:9-12) Na tuchunguze baadhi ya “mbinu za udanganyifu” za Shetani na jinsi ya kujilinda nazo.—Waefeso 6:11, Jewish New Testament.

Jilinde Dhidi ya Udanganyifu wa Waasi-Imani

6, 7. (a) Huenda waasi-imani wakatoa dai gani? (b) Maandiko huonyeshaje waziwazi kile ambacho waasi-imani wanataka?

6 Shetani ametumia waasi-imani kwa muda mrefu ili kuwashawishi watumishi wa Mungu. (Mathayo 13:36-39) Huenda waasi-imani wakadai kwamba wanamwabudu Yehova na kuiamini Biblia, lakini wao hukataa sehemu yenye kuonekana ya tengenezo lake. Wengine hata hurudia mafundisho yenye kumvunjia Mungu heshima ya “Babiloni Mkubwa,” ile miliki ya ulimwengu ya dini za uwongo. (Ufunuo 17:5; 2 Petro 2:19-22) Chini ya mwongozo wa roho ya Mungu, waandikaji wa Biblia walitumia maneno yenye nguvu kufunua malengo na mbinu za waasi-imani.

7 Waasi-imani wana malengo gani? Wengi wao hawatosheki tu kuacha dini ambayo wakati mmoja waliiona kuwa ya kweli. Mara nyingi wanataka kuondoka na wengine. Badala ya kuondoka na kufanya wanafunzi wao wenyewe, waasi-imani wengi hujaribu “kuwavuta wanafunzi [yaani, wanafunzi wa Kristo] wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:29, 30) Mtume Paulo alitoa onyo hili muhimu kuhusu walimu wa uwongo: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake.” (Wakolosai 2:8) Hivyo ndivyo hasa waasi-imani wengi hujaribu kufanya. Kama vile mteka-nyara humteka mtu asiye na habari kutoka kwa familia yake, waasi-imani huwafanya washiriki wa kutaniko ambao huwatumaini kuwa windo lao, wakitafuta kuwaondoa katika kundi.

8. Waasi-imani hutumia njia zipi ili kutimiza malengo yao?

8 Waasi-imani hutumia njia zipi kutimiza malengo yao? Mara nyingi wao hutumia udanganyifu, kweli nusu-nusu, na uwongo mtupu. Yesu alijua kwamba wafuasi wake wangenyanyaswa na wale ambao ‘wangewanenea kila neno baya kwa uwongo.’ (Mathayo 5:11, Union Version) Wapinzani hao wenye chuki wangesema uwongo kwa lengo la kuwadanganya wengine. Mtume Petro alionya kuhusu waasi-imani ambao wangetumia “maneno yasiyo ya kweli,” waeneze ‘mafundisho ya udanganyifu,’ na ‘kupotosha Maandiko’ ili kutimiza malengo yao. (2 Petro 2:3, 13; 3:16) Inasikitisha kwamba waasi-imani hufaulu ‘kuipindua imani ya wengine.’—2 Timotheo 2:18.

9, 10. (a) Tunawezaje kujilinda tusidanganywe na waasi-imani? (b) Kwa nini hatuhangaiki ikiwa ufahamu wetu kuhusu kusudi la Mungu unahitaji kurekebishwa?

9 Tunawezaje kujilinda tusidanganywe na waasi-imani? Kwa kutii shauri la Neno la Mungu linalosema: “Waangalieni wale wanaosababisha migawanyiko na kusababisha kukwazika kinyume cha fundisho ambalo mmejifunza, nanyi mjiepushe nao.” (Waroma 16:17) Sisi ‘hujiepusha nao’ kwa kukataa katakata hoja zao, iwe ni kupitia mazungumzo ya moja kwa moja, vichapo, au Internet. Kwa nini sisi huchukua msimamo huo? Kwanza, ni kwa sababu Neno la Mungu hutuagiza tufanye hivyo, na tunaamini kwamba Yehova hututakia mema sikuzote.—Isaya 48:17, 18.

10 Pili, tunapenda tengenezo ambalo limetufunza kweli zenye thamani ambazo huonyesha waziwazi kwamba tumejitenga na Babiloni Mkubwa. Wakati huohuo tunatambua kwamba hatuna ujuzi kamili kuhusu kusudi la Mungu; ufahamu wetu umeendelea kurekebishwa katika miaka ambayo imepita. Wakristo washikamanifu wanaridhika kumngojea Yehova kuhusiana na marekebisho hayo yote. (Methali 4:18) Wakati huohuo, hatutaliacha tengenezo ambalo Mungu anafurahia kulitumia, kwa kuwa tunaona waziwazi kwamba analibariki.—Matendo 6:7; 1 Wakorintho 3:6.

Jilinde Dhidi ya Kujidanganya

11. Kwa nini wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kujidanganya?

11 Wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo ambao Shetani hatasita kuutumia, yaani, kujidanganya. Andiko la Yeremia 17:9 linasema, “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” Naye Yakobo aliandika hivi: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe.” (Yakobo 1:14) Moyo wetu unaposhawishiwa, huenda ukafanya dhambi ionekane kuwa yenye kuvutia na isiyo na madhara. Maoni kama hayo ni ya udanganyifu, kwa kuwa mtu anapotenda dhambi mwishowe atapatwa na uharibifu.—Waroma 8:6.

12. Tunaweza kuangukia mtego wa kujidanganya katika njia gani?

12 Ni rahisi kuangukia mtego wa kujidanganya. Huenda moyo wenye hila ukatufanya tusione uzito wa kasoro fulani tuliyo nayo au tujitetee kuhusiana na dhambi nzito. (1 Samweli 15:13-15, 20, 21) Moyo wetu ambao ni hatari unaweza pia kutafuta njia za kujitetea kuhusiana na mwenendo wenye kutilika shaka. Kwa mfano, fikiria vitumbuizo. Vitumbuizo fulani vinafaa na vinafurahisha. Hata hivyo, vitumbuizo vingi vya ulimwengu huu vinavyopatikana kupitia sinema, vipindi vya televisheni, na Internet, ni vichafu na visivyo vya adili. Ni rahisi kujisadikisha kwamba tunaweza kutazama vitumbuizo vichafu bila madhara yoyote. Wengine hata husema, “Kuna ubaya gani kuvitazama na havinisumbui dhamiri?” Lakini watu hao ‘wanajidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli.’—Yakobo 1:22.

13, 14. (a) Ni mfano gani wa Kimaandiko unaoonyesha kwamba dhamiri yetu haitoi mwongozo salama sikuzote? (b) Tunawezaje kujilinda dhidi ya kujidanganya?

13 Tunawezaje kujilinda dhidi ya kujidanganya? Kwanza, tunahitaji kukumbuka kwamba dhamiri ya mwanadamu haitegemeki sikuzote. Fikiria mfano wa mtume Paulo. Kabla hajawa Mkristo, aliwatesa wafuasi wa Kristo. (Matendo 9:1, 2) Huenda dhamiri yake haikumsumbua wakati huo. Lakini ni wazi kwamba ilikuwa imepotoshwa. Paulo alisema, “Nilikosa ujuzi nami nilitenda kwa ukosefu wa imani.” (1 Timotheo 1:13) Kwa hiyo, hata kama vitumbuizo fulani havisumbui dhamiri yetu, hiyo haimaanishi hata kidogo kwamba mwenendo wetu unafaa. Dhamiri nzuri ambayo imezoezwa ifaavyo na Neno la Mungu ndiyo tu inayoweza kutoa mwongozo salama.

14 Kuna madokezo fulani yafaayo tunayohitaji kukumbuka ili kuepuka kujidanganya. Jichunguze kupitia sala. (Zaburi 26:2; 2 Wakorintho 13:5) Kujichunguza kwa unyoofu kunaweza kukusaidia utambue kwamba unahitaji kufanya mabadiliko fulani kuhusu maoni na mwenendo wako. Wasikilize wengine. (Yakobo 1:19) Kwa kuwa tuna mwelekeo wa kutoona makosa yetu tunapojichunguza, ni jambo la hekima kuwasikiliza Wakristo wenzetu wakomavu ambao watatueleza waziwazi jinsi tulivyo. Ikiwa unafanya maamuzi au unajiendesha katika njia zinazotilika shaka machoni pa waabudu wenzako wenye uzoefu na wenye usawaziko, unaweza kujiuliza, ‘Je, huenda ikawa dhamiri yangu haijazoezwa vizuri au moyo wangu unanidanganya?’ Jifunze kwa ukawaida Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia. (Zaburi 1:2) Kufanya hivyo kutakusaidia upatanishe mawazo, mitazamo, na hisia zako na kanuni za Mungu.

Jilinde Dhidi ya Uwongo wa Shetani

15, 16. (a) Shetani hutumia uwongo gani ili kutudanganya? (b) Tunawezaje kuepuka tusipotoshwe na uwongo huo?

15 Shetani hutumia aina mbalimbali za uwongo ili kutudanganya. Yeye hujaribu kutusadikisha kwamba mali huleta furaha na uradhi, lakini mara nyingi inakuwa kinyume. (Mhubiri 5:10-12) Angependa tuamini kwamba ulimwengu huu mwovu utadumu milele, ingawa kuna uthibitisho ulio wazi kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Shetani huendeleza wazo la kwamba hakuna madhara ya kuishi maisha yasiyo ya adili hata ingawa mara nyingi matokeo huwa mabaya kwa watu wanaofuatia anasa. (Wagalatia 6:7) Tunawezaje kuepuka tusipotoshwe na uwongo huo?

16 Nufaika na mifano ya Biblia. Biblia ina mifano yenye kuonya kuhusu watu waliopotoshwa na uwongo wa Shetani. Walipenda vitu vya kimwili, wakasahau uharaka wa nyakati walimoishi, au wakafanya uasherati na matokeo yakawa mabaya. (Mathayo 19:16-22; 24:36-42; Luka 16:14; 1 Wakorintho 10:8-11) Jifunze kutokana na vielelezo vya wakati huu. Inasikitisha kwamba mara kwa mara Wakristo fulani husahau uharaka wa nyakati tunamoishi nao huanza kuamini kwamba wanakosa jambo fulani zuri kwa kumtumikia Mungu. Huenda wakaacha kweli ili kufuatia zile zinazoitwa eti anasa. Hata hivyo, watu hao wanakanyaga “udongo unaoteleza,” kwa kuwa hivi karibuni watapatwa na madhara ya mwenendo wao wa kutomwogopa Mungu. (Zaburi 73:18, 19) Ni jambo la hekima kujifunza kutokana na makosa ya wengine.—Methali 22:3.

17. Kwa nini Shetani anaendeleza uwongo kwamba Yehova hatupendi wala hatuthamini?

17 Kuna uwongo mwingine ambao Shetani ametumia kwa matokeo sana, yaani, uwongo kwamba Yehova hatupendi wala hatuthamini. Shetani amewachunguza wanadamu wasio wakamilifu kwa miaka mingi sana. Anajua vizuri kwamba hali yetu ya kiroho inaweza kudhoofika tukivunjika moyo. (Methali 24:10) Hivyo, yeye huendeleza uwongo kwamba hatuna thamani yoyote machoni pa Mungu. ‘Tukiangushwa chini” na kusadikishwa kwamba Yehova hatujali, huenda tukashawishiwa kuacha kumtumikia. (2 Wakorintho 4:9) Hivyo ndivyo yule Mdanganyifu mkuu anavyotaka! Hivyo basi, tunawezaje kujilinda tusipotoshwe na uwongo huo wa Shetani?

18. Biblia hutuhakikishiaje kwamba Yehova anatupenda?

18 Tafakari yale ambayo Biblia husema kuhusu upendo wa Mungu kwetu. Neno la Mungu linatumia mifano iliyo wazi ili kutuhakikishia kwamba Yehova anatuona na kutupenda tukiwa mtu mmoja-mmoja. Yeye huweka machozi yako katika “kiriba” chake, jambo linalomaanisha kwamba anaona na kukumbuka machozi unayotoa unapojitahidi kubaki mwaminifu. (Zaburi 56:8) Anajua wakati ‘unapovunjika moyo’ naye huwa karibu nawe nyakati hizo. (Zaburi 34:18) Anajua kila jambo kukuhusu, kutia ndani hesabu ya ‘nywele zenyewe za kichwa chako.’ (Mathayo 10:29-31) Zaidi ya yote, Mungu ‘alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee’ kwa ajili yako. (Yohana 3:16; Wagalatia 2:20) Huenda nyakati nyingine ukaona ni vigumu kuamini kwamba maandiko hayo yanakuhusu wewe binafsi. Hata hivyo, tunapaswa kuliamini neno la Yehova. Anataka tuamini kwamba anatupenda tukiwa mtu mmoja-mmoja wala si tukiwa kikundi tu.

19, 20. (a) Kwa nini ni muhimu kutambua na kukataa uwongo wa Shetani kwamba Yehova hakupendi? (b) Mwangalizi mmoja asafiriye amewasaidiaje watu waliovunjika moyo?

19 Tambua na ukatae uwongo. Ukijua kwamba mtu fulani anasema uwongo, unaweza kujilinda usidanganywe naye. Hivyo pia, kule kujua kuwa Shetani anataka uamini uwongo kwamba Yehova hakupendi kunaweza kukusaidia sana. Mkristo mmoja alisema hivi kuhusu makala fulani ya Mnara wa Mlinzi iliyoonya juu ya mbinu za Shetani: “Sikutambua kamwe kwamba Shetani hujaribu kutumia hisia zangu ili kunivunja moyo. Kujua jambo hilo hunichochea kushinda hisia hizo.”

20 Fikiria kisa cha mwangalizi fulani asafiriye katika nchi moja ya Amerika Kusini. Anapofanya ziara za uchungaji kwa waamini wenzake waliovunjika moyo, mara nyingi yeye huwauliza, ‘Je, unaamini Utatu?’ Kwa kawaida mwamini huyo aliyevunjika moyo hujibu, ‘La,’ kwa kuwa anatambua kwamba huo ni mojawapo wa uwongo wa Shetani. Kisha mzee huyo asafiriye huuliza, ‘Je, unaamini kuna moto wa mateso?’ Naye hupata jibu lilelile.’ Halafu yeye humwambia mwamini huyo kwamba kuna uwongo mwingine wa Shetani ambao kwa kawaida hautambuliki kuwa uwongo. Yeye humwonyesha kitabuMkaribie Yehova, * ukurasa wa 249, fungu la 21, linalofunua uwongo kwamba Yehova hatupendi tukiwa mtu mmoja-mmoja. Mwangalizi huyo asafiriye anasema kwamba yeye hupata matokeo mazuri kwa kuwasaidia waliovunjika moyo watambue na kuukataa uwongo huo wa Shetani.

Jilinde Dhidi ya Udanganyifu

21, 22. Kwa nini hatumo gizani kuhusu mbinu za udanganyifu za Shetani, nasi tunapaswa kuazimia kufanya nini?

21 Wakati huu wa umalizio wa siku za mwisho, haishangazi kwamba Shetani ataendelea kusambaza uwongo na udanganyifu mwingi sana. Tunashukuru kwamba Yehova ametufunulia mbinu za udanganyifu za Shetani. Biblia pamoja na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambavyo vinazungumzia Biblia, hufunua waziwazi mbinu mbovu za Ibilisi. (Mathayo 24:45) Kujua hali mapema hutusaidia kujitayarisha ili kuikabili.—2 Wakorintho 2:11.

22 Kwa hiyo, na tujilinde dhidi ya hoja za waasi-imani. Na tuazimie kuepuka mtego wenye hila wa kujidanganya. Na tutambue na kukataa uwongo wote wa Shetani. Kwa kufanya hivyo, tutalinda uhusiano wetu pamoja na “Mungu wa ukweli,” anayechukia udanganyifu.—Zaburi 31:5; Methali 3:32.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema kwamba aina ya kitenzi ambacho kimetafsiriwa ‘anaipotosha’ katika Ufunuo 12:9, “kinaonyesha kitendo cha kuendelea ambacho kimekuwa zoea.”

^ fu. 20 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini kuna udanganyifu mwingi sana ulimwenguni leo?

• Tunawezaje kujilinda tusidanganywe na waasi-imani?

• Tunawezaje kujilinda dhidi ya mwelekeo wowote wa kujidanganya?

• Tunawezaje kuepuka kupotoshwa na uwongo wa Shetani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katikia ukurasa wa 17]

Usijidanganye kuhusu vitumbuizo

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ili kujilinda dhidi ya kujidanganya, jichunguze kupitia sala, wasikilize wengine, na kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu