Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Baada ya Gharika, Noa alimtuma njiwa nje ya safina ambaye alirudi na “jani bichi la mzeituni.” Njiwa huyo alipata wapi jani hilo?

Biblia hutuambia kwamba ‘maji yalizidi mno duniani hivi kwamba milima yote mirefu ambayo ilikuwa chini ya mbingu zote ilifunikwa.’ (Mwanzo 7:19) Maji ya Gharika yalipopungua, Noa alimtuma njiwa mara moja kila juma, kwa muda wa majuma matatu. Mara ya pili, njiwa huyo alirudi akiwa na ‘jani bichi la mzeituni lililokuwa katika mdomo wake. Hivyo, Noa akajua kwamba maji yalikuwa yamepungua kutoka juu ya dunia.’—Mwanzo 8:8-11.

Bila shaka, sasa hatuna namna ya kujua muda ambao maji yalifunika sehemu fulani za dunia, kwa kuwa ni wazi kwamba Gharika ilibadilisha sura ya dunia. Hata hivyo, inaonekana kwamba maji yalifunika sehemu nyingi kwa muda mrefu hivi kwamba miti mingi ilikufa. Lakini yaonekana miti fulani haikufa, na hivyo ikatokeza miche tena maji yalipopungua.

Kichapo, The New Bible Dictionary, kinasema hivi kuhusu mzeituni: “Unapokatwa, miche mipya huchipuka kutoka kwenye shina, hivi kwamba visiki vitano vipya hivi vinaweza kumea. Kwa kawaida, mizeituni [iliyo karibu kufa] hutokeza miche kwa njia hiyo.” Ni “kana kwamba miti hiyo haiwezi kufa,” chasema kichapo The New Schaff-Herzog Encyclopedia of Religious Knowledge. Leo hakuna binadamu anayejua kikamili kuhusu kiasi cha chumvi na joto la maji ya gharika. Hivyo, hatuwezi kuwa na hakika kuhusu jinsi maji hayo yangeweza kuathiri mizeituni na mimea mingine.

Hata hivyo, mzeituni-mwitu hauwezi kustahimili hali ya baridi, kama ile inayopatikana milimani. Kwa kawaida, miti hiyo humea katika maeneo yaliyo chini ya meta 1,000, ambako wastani wa joto ni zaidi ya nyuzi 10 Selsiasi. Kitabu The Flood Reconsidered kinasema, “Hivyo Noa angeweza kujua kutokana na jani lililokuwa limetoka tu kuchumwa kwamba mabonde ya chini yalikuwa yamekauka.” Noa alipomwachilia njiwa juma moja baadaye, njiwa huyo hakurudi, ikionyesha kwamba kulikuwa na mimea mingi zaidi na angeweza kupata mahali pa kutulia.—Mwanzo 8:12.