Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Tunavyoonyesha Tunampenda Mungu

Jinsi Tunavyoonyesha Tunampenda Mungu

Jinsi Tunavyoonyesha Tunampenda Mungu

KUSITAWISHA upendo kwa Mungu hakumaanishi kujifunza tu kumhusu. Kama watumishi wa Mungu duniani wanavyoweza kushuhudia, upendo wa kweli kwa Mungu hukua mtu anapojua utu wake, na hata huwa wenye nguvu zaidi anapofahamu matakwa yake na mambo ambayo yeye hupenda na kuchukia.

Kwa upendo, Yehova ametupatia Neno lake, Biblia, naye hujifunua kupitia Neno hilo. Kutokana na Biblia, tunajifunza jinsi Yehova alivyoshughulika na hali mbalimbali. Kama vile tu barua kutoka kwa mpendwa hutufurahisha, vivyo hivyo Biblia hutufurahisha inapotufunulia mambo mapya kuhusu utu wa Yehova.

Hata hivyo, nyakati nyingine tunapokuwa katika huduma ya shambani tunaona kuwa si lazima mtu aanze kumpenda Mungu kwa kuwa tu amejifunza juu yake. Yesu alisema hivi kuhusu Wayahudi fulani wasio na uthamini wa siku zake: “Ninyi mnayachunguza Maandiko, kwa sababu mnafikiri kwamba kwa njia yake mtakuwa na uzima wa milele; . . . lakini ninajua vizuri kwamba ninyi hammpendi Mungu ndani yenu.” (Yohana 5:39, 42) Wengine hutumia miaka mingi wakijifunza matendo yenye upendo ya Yehova na bado hawampendi sana. Kwa nini? Wanashindwa kutafakari maana ya yale wanayojifunza. Kinyume cha hilo, mamilioni ya watu wanyoofu tunaojifunza Biblia pamoja nao huona kwamba upendo wao kwa Mungu huendelea kukua. Kwa nini? Kwa sababu, kama vile sisi wenyewe tulivyofanya, wao hufuata kielelezo cha Asafu. Katika njia gani?

Tafakari kwa Uthamini

Asafu aliazimia kusitawisha upendo kwa Yehova moyoni mwake. Aliandika: “Nitaonyesha hangaiko moyoni . . . Nitavikumbuka vitendo vya Yah; kwa maana nitayakumbuka matendo yako ya ajabu ya zamani za kale. Nami hakika nitautafakari utendaji wako wote, nami nitajishughulisha mwenyewe na matendo yako.” (Zaburi 77:6, 11, 12) Upendo kwa Mungu utakua katika moyo wa mtu anayetafakari njia za Yehova kama mtunga-zaburi alivyofanya.

Isitoshe, uhusiano wetu na Mungu huimarika tunapokumbuka mambo tuliyofurahia katika utumishi wa Yehova. Mtume Paulo alisema kwamba sisi ni “wafanyakazi wenzi” wa Mungu, na urafiki unaoweza kusitawi kati ya wafanyakazi wenzi ni wa pekee sana. (1 Wakorintho 3:9) Tunapomwonyesha Yehova upendo, yeye hufurahi na kuthamini. (Methali 27:11) Hivyo, tunapomwomba Yehova atusaidie kutatua tatizo fulani naye anafanya hivyo, tunajua kwamba yupo pamoja nasi, na upendo wetu kwake huongezeka.

Urafiki kati ya watu wawili husitawi wanapoonyeshana hisia. Vivyo hivyo, tunapomweleza Yehova sababu inayofanya tujitoe kwake, upendo wetu kwake huimarika. Tutajikuta tukitafakari maneno haya ya Yesu: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tutaendelea kumpenda Yehova kwa moyo wetu wote, nafsi yetu yote, akili yetu yote, na kwa nguvu zetu zote?

Kumpenda Yehova kwa Moyo Wetu Wote

Maandiko hurejelea moyo wa mfano, ambao ni yule mtu wa ndani, yaani, tamaa, mtazamo, na hisia zetu. Kwa hiyo, kumpenda Yehova kwa moyo wetu wote humaanisha kwamba tamaa yetu kubwa zaidi ni kumpendeza. (Zaburi 86:11) Tunaonyesha kwamba tuna upendo huo kwa kusitawisha utu ambao anaukubali. Tunajitahidi kumwiga Mungu kwa ‘kuchukia uovu na kushikamana na wema.’—Waroma 12:9.

Upendo wetu kwa Mungu huathiri hisia zetu kuhusu kila jambo. Kwa mfano, huenda kazi tunayofanya ikawa yenye kupendeza au kunasa akili zetu, lakini je, moyo wetu uko katika kazi hiyo? La. Kwanza kabisa sisi ni wahudumu wa Yehova kwa kuwa tunampenda kwa moyo wetu wote. Vivyo hivyo, tungependa kuwapendeza wazazi wetu, mwenzi wetu wa ndoa, na pia mkubwa wetu kazini. Lakini sisi huthibitisha kwamba tunampenda Yehova kwa moyo wetu wote kwa kujitahidi kumpendeza yeye kwanza, kwa kuwa tunastahili kumtanguliza moyoni mwetu.—Mathayo 6:24; 10:37.

Kumpenda Yehova kwa Nafsi Yetu Yote

Katika Maandiko neno “nafsi” kimsingi hurejelea mtu mwenyewe na vilevile uhai wetu. Kwa hiyo, kumpenda Yehova kwa nafsi yetu yote humaanisha kutumia maisha yetu kumsifu na kuthibitisha kwamba tunampenda.

Bila shaka, huenda tukapendezwa na mambo mengine maishani, kama vile kujifunza kazi fulani, kufanya biashara, au kulea watoto. Lakini wakati huohuo, tunathibitisha kwamba tunampenda Yehova kwa nafsi yote kwa kufanya mambo kwa njia yake na “kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake” huku tukiacha mambo mengine maishani yachukue nafasi ya pili. (Mathayo 6:33) Pia, ibada ya moyo wote inamaanisha kuwa wenye bidii. Sisi humwonyesha Yehova kwamba tunampenda kwa kuhubiri kwa bidii ujumbe wa Ufalme, kwa kutoa maelezo yenye kujenga kwenye mikutano, au kwa kuwasaidia ndugu na dada zetu Wakristo. Katika kila jambo, tunaendelea ‘kufanya mapenzi ya Mungu kwa nafsi yote.’—Waefeso 6:6.

Yesu alionyesha anampenda Mungu kwa moyo wote kwa kujikana mwenyewe. Alitanguliza mapenzi ya Mungu nayo mahitaji yake yakachukua nafasi ya pili. Yesu alitualika tufuate kielelezo chake. Alisema: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.” (Mathayo 16:24, 25) Kujikana wenyewe humaanisha kujiweka wakfu. Kunamaanisha kwamba tunampenda Mungu sana hivi kwamba tunajitoa kuwa mali yake, kama vile Mwisraeli aliyempenda sana bwana wake katika nyakati za Biblia alivyojitoa awe mtumwa wake milele. (Kumbukumbu la Torati 15:16, 17) Kujiweka wakfu kwa Yehova huthibitisha kwamba tunampenda.

Kumpenda Yehova kwa Akili Yetu Yote

Kumpenda Yehova kwa akili yetu yote humaanisha kufanya kila tuwezalo ili kuelewa utu, makusudi, na matakwa ya Yehova. (Yohana 17:3; Matendo 17:11) Tunaonyesha upendo wetu kwa Yehova kwa kutumia uwezo wetu wote wa akili kusaidia wengine wampende pia na kwa kuboresha ustadi wetu wa kufundisha. Mtume Petro alitusihi, “Kazeni akili zenu kwa ajili ya utendaji.” (1 Petro 1:13) Pia tunajitahidi kupendezwa na wengine, hasa watumishi wenzetu wa Mungu. Tunajua hali zao na kutambua wakati inapofaa kuwapongeza au wanapohitaji kufarijiwa.

Tunamwonyesha Yehova kwamba tunampenda kwa akili yetu yote kwa kujitiisha kwake kiakili. Tunajitahidi kuona mambo kama anavyoyaona, kumtambua tunapofanya maamuzi, na kuwa na hakika kwamba njia yake ndiyo bora zaidi. (Methali 3:5, 6; Isaya 55:9; Wafilipi 2:3-7) Lakini tunaweza kutumia nguvu zetu jinsi gani tunapoendelea kuonyesha upendo wetu kwa Mungu?

Kumpenda Yehova kwa Nguvu Zetu Zote

Vijana wengi katika kutaniko la Kikristo hutumia nguvu zao kumsifu Yehova. (Methali 20:29; Mhubiri 12:1) Njia moja ambayo vijana wengi Wakristo huonyesha kwamba wanampenda Yehova kwa nguvu zao zote ni kwa kufanya upainia, yaani, huduma ya wakati wote. Mama wengi hushiriki huduma hiyo watoto wao wanapokuwa shuleni. Wazee waaminifu ambao hufanya ziara za uchungaji na pia kutunza familia zao huonyesha kwamba wanampenda Yehova kwa nguvu zao zote. (2 Wakorintho 12:15) Yehova huwapa nguvu wale wanaomtumaini, ili waweze kuonyesha upendo wao kwake kwa kumsifu, huku wakitumia nguvu zao.—Isaya 40:29; Waebrania 6:11, 12.

Upendo utakua ukisitawishwa kwa njia inayofaa. Kwa hiyo, tunaendelea kutumia wakati ili kutafakari. Tunakumbuka mambo ambayo Yehova ametufanyia na kwa nini anastahili ujitoaji wetu. Tukiwa wazao wa Adamu wasio wakamilifu, hatuwezi kamwe kustahili kupokea “mambo ambayo Mungu amewatayarishia wale wanaompenda,” lakini tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa nafsi yetu yote. Na tuendelee kufanya hivyo!—1 Wakorintho 2:9.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu kupitia matendo