Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kweli Itawaweka Ninyi Huru”

“Kweli Itawaweka Ninyi Huru”

“Kweli Itawaweka Ninyi Huru”

KWA kuwa Yehova Mungu ndiye Mweza Yote, Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, na Muumba wa vitu vyote, yeye peke yake ndiye mwenye uhuru kamili, usio na mipaka. (Mwanzo 17:1; Yeremia 10:7, 10; Danieli 4:34, 35; Ufunuo 4:11) Viumbe wengine wote wanapaswa kujiendesha kulingana na uwezo waliopewa bila kuvuka mipaka, na kujitiisha chini ya sheria zake zinazoongoza ulimwengu wote. (Isaya 45:9; Waroma 9:20, 21) Kwa mfano, fikiria nguvu za uvutano, na sheria za utendanaji wa kemikali, matokeo ya nguvu za jua, na ukuzi; sheria za adili; haki na matendo ya wengine ambayo huathiri uhuru wa mtu. Kwa hiyo, uhuru wa viumbe wote wa Mungu una mipaka.

Uhuru Unaotokana na Kristo. Mtume Paulo alizungumza kuhusu uhitaji wa wanadamu wa kuwekwa huru kutokana na “utumwa wa uharibifu.” (Waroma 8:21) Yesu Kristo aliwaambia hivi Wayahudi waliomwamini: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” Yesu alionyesha kwamba wale waliofikiri kuwa wana uhuru kwa sababu tu walikuwa wazao halisi wa Abrahamu, walikuwa watumwa wa dhambi, kisha akasema: “Kwa hiyo Mwana akiwaweka ninyi huru, mtakuwa huru kwelikweli.”—Yohana 8:31-36; linganisha Waroma 6:18, 22.

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanasema kwamba wafuasi wa Kristo wako huru. Paulo alionyesha kwamba walikuwa “watoto, si wa kijakazi, bali wa yule mwanamke huru” ambaye anamwita “Yerusalemu la juu.” (Wagalatia 4:26, 31) Kisha anahimiza hivi: “Kristo alituweka huru tuwe na uhuru wa namna hiyo. Kwa hiyo simameni imara, na msijiache wenyewe kufungwa tena katika nira ya utumwa.” (Wagalatia 5:1) Wakati huo, watu fulani waliodai kwa uwongo kuwa Wakristo walikuwa wakishirikiana na makutaniko ya Galatia. Walikuwa wakijaribu kuwashawishi Wakristo wa Galatia wapuuze uhuru wao katika Kristo kwa kujaribu kupata uadilifu kupitia kazi za Sheria, badala ya imani katika Kristo. Kwa hiyo, Paulo alionya kwamba wangekosa fadhili zisizostahiliwa za Kristo.—Wagalatia 5:2-6; 6:12, 13.

Kutokana na jinsi mitume walivyozungumza waziwazi na kutangaza habari njema kwa uhuru wa kusema tunaona kwamba, Wakristo wa mapema hawakuwa chini ya utumwa wa dhambi na kifo, wala hawakuogopa. (2 Timotheo 1:7; Matendo 4:13; Wafilipi 1:18-20) Waliuona uhuru huo wa kusema kumhusu Kristo kuwa kitu chenye thamani, kinachopaswa kusitawishwa, kulindwa, na kudumishwa ili wakubaliwe na Mungu. Pia ilifaa wasali ili kupata uhuru huo.—1 Timotheo 3:13; Waebrania 3:6; Waefeso 6:18-20.

Kutumia Uhuru wa Kikristo Ifaavyo. Waandikaji Wakristo walioongozwa na roho ya Mungu na ambao walitambua kusudi la Mungu la kutuonyesha fadhili zisizostahiliwa kupitia Kristo, waliwashauri Wakristo mara nyingi walinde uhuru wao na wasiutumie kama udhuru wa kujihusisha na kazi za mwili au kama kifuniko cha ubaya. (Wagalatia 5:13; 1 Petro 2:16) Yakobo alizungumza kuhusu ‘kuchunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru’ na kusema kwamba mtu ambaye si msikiaji msahaulifu, bali ni mtendaji, atakuwa mwenye furaha.—Yakobo 1:25.

Mtume Paulo alifurahia uhuru aliopata kupitia Kristo lakini hakutumia uhuru wake kujipendeza au kuwaumiza wengine. Katika barua yake kwa kutaniko la Korintho, alionyesha kwamba hangeumiza dhamiri ya mtu mwingine kwa kufanya jambo ambalo alikuwa na uhuru wa Kimaandiko kulifanya lakini ambalo lingemsumbua mtu asiye na ujuzi wa kutosha, ambaye labda dhamiri yake ingeumizwa na tendo la Paulo. Anataja mfano wa kula nyama iliyotolewa kwa sanamu kabla haijapelekwa sokoni kuuzwa. Kula nyama hiyo kungemfanya mtu aliye na dhamiri dhaifu achambue uhuru wa Paulo wa kuila na hivyo mtu huyo angekuwa kama hakimu wa Paulo, jambo ambalo halingefaa. Kwa hiyo, Paulo alisema: “Kwa nini iwe kwamba uhuru wangu unahukumiwa na dhamiri ya mtu mwingine? Ikiwa nakula nikiwa na shukrani, kwa nini nitukanwe juu ya kile ninachotolea shukrani?” Hata hivyo, mtume huyo aliazimia kutumia uhuru wake kwa njia inayojenga na isiyodhuru.—1 Wakorintho 10:23-33.

Vivyo hivyo, watumishi wote wa kweli wa Yehova wanaweza kunufaika na uhuru wa Kikristo. Tunapofanya hivyo kwa njia ya kimungu, basi bila shaka kweli imetuweka huru.