Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa kuwa Walawi hawakuwa na urithi katika Israeli la kale, Mlawi Hanameli angewezaje kumuuzia shamba binamu yake Yeremia aliyekuwa Mlawi, kama inavyoonyeshwa katika Yeremia 32:7?

Yehova alimwambia Haruni hivi kuhusu Walawi: ‘Hamtakuwa na urithi, wala hakuna fungu lolote litakalokuwa lenu katikati ya Israeli.’ (Hesabu 18:20) Hata hivyo, Walawi walipewa majiji 48 pamoja na viwanja vyao vya malisho. Majiji hayo yalikuwa yametawanyika sehemu mbalimbali katika Nchi ya Ahadi. Mji wa nyumbani wa Yeremia ulikuwa Anathothi, mojawapo ya majiji yaliyopewa “wana wa Haruni, makuhani.”—Yoshua 21:13-19; Hesabu 35:1-8; 1 Mambo ya Nyakati 6:54, 60.

Katika Mambo ya Walawi 25:32-34, tunaona kwamba Yehova aliwapa maagizo hususa kuhusu “haki ya kukomboa” shamba lililomilikiwa na Walawi. Yaonekana, familia fulani za Walawi zingekuwa na haki za urithi kuhusiana na umilikaji, matumizi, na uuzaji wa viwanja fulani hususa. Kwa kawaida, haki hizo zingetia ndani kuuza na kukomboa shamba. * Katika njia nyingi, Walawi walimiliki na kutumia mali sawa na makabila mengine ya Israeli.

Yaelekea, mashamba hayo ya Walawi yalirithiwa kutoka familia moja hadi nyingine. Hata hivyo, kuhusu “haki ya kukomboa” Walawi waliruhusiwa kuuza na kununua kwa Walawi wenzao tu. Pia, inaonekana kwamba mashamba yaliyoruhusiwa kuuzwa na kununuliwa ni yale yaliyokuwa kwenye majiji, kwa kuwa “kiwanja cha malisho cha majiji yao” hakikupaswa kuuzwa kwa sababu kilikuwa “miliki mpaka wakati usio na kipimo kwa ajili yao.”—Mambo ya Walawi 25:32, 34.

Kwa hiyo, yaonekana shamba ambalo Yeremia alikomboa kutoka kwa Hanameli ni lile ambalo lingeweza kumilikiwa na wengine kupitia ukombozi. Huenda lilikuwa karibu na jiji. Yehova mwenyewe alithibitisha kwamba “shamba” lililohusika lilikuwa la Hanameli na kwamba Yeremia alikuwa na ‘haki ya kulikomboa.’ (Yeremia 32:6, 7) Yehova alitumia ununuzi huo kwa njia ya mfano ili kukazia ahadi yake kwamba baada ya kukaa uhamishoni Babiloni, Waisraeli wangerudi kudai nchi iliyokuwa urithi wao.—Yeremia 32:13-15.

Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Hanameli alikuwa amemiliki shamba kwa njia isiyofaa huko Anathothi. Hakuna kitu kinachoonyesha kwamba alivunja sheria ya Yehova kwa kumwomba Yeremia anunue shamba hilo lililokuwa Anathothi au kwamba Yeremia alitumia vibaya haki yake ya kukomboa kwa kununua shamba hilo.—Yeremia 32:8-15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika karne ya kwanza W.K., Mlawi Barnaba aliuza shamba alilomiliki, naye akatoa pesa alizopata ili kuwasaidia wafuasi wa Kristo wenye uhitaji huko Yerusalemu. Huenda shamba hilo lilikuwa ama Palestina ama Kipro. Au inawezekana kwamba hicho kilikuwa tu kiwanja cha kuzikia ambacho Barnaba alikuwa amenunua katika eneo la Yerusalemu.—Matendo 4:34-37.