Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukristo wa Kweli Unasitawi

Ukristo wa Kweli Unasitawi

Ukristo wa Kweli Unasitawi

YESU KRISTO alianza huduma yake iliyokuwa na uvutano mkubwa ulimwenguni katika karne ya kwanza. Ujumbe wake ulikuwa wenye kutia nguvu, kuelimisha, na kuchochea katika njia iliyowashangaza watu. Wengi waliomsikia waliguswa moyo sana na maneno yake.—Mathayo 7:28, 29.

Yesu alikataa kwa ujasiri kujihusisha na mifumo ya kidini na ya kisiasa yenye kukandamiza ya wakati huo lakini alifanya iwe rahisi kwa watu wa kawaida kumfikia. (Mathayo 11:25-30) Alikiri waziwazi kwamba kulikuwa na uvutano wenye kupotosha wa roho waovu duniani na akaonyesha kwamba angeweza kuwashinda kwa nguvu alizopewa na Mungu. (Mathayo 4:2-11, 24; Yohana 14:30) Yesu alifafanua kwa ustadi kwamba kuna uhusiano mkubwa kati ya dhambi na kuteseka, naye akaonyesha kwa upendo kwamba Ufalme wa Mungu utaleta kitulizo cha kudumu. (Marko 2:1-12; Luka 11:2, 17-23) Aliondoa kabisa utaji wa giza ambao kwa muda mrefu ulifunika utu halisi wa Baba yake, na akalijulisha jina la Mungu kwa wote waliotaka kuwa na uhusiano wa karibu pamoja Naye.—Yohana 17:6, 26.

Kwa hiyo, haishangazi kwamba ingawa wanafunzi wa Yesu walipatwa na mateso makali ya kidini na ya kisiasa, walieneza haraka ujumbe wake wenye uvutano mkubwa. Kwa muda wa miaka 30 hivi, makutaniko ya Kikristo yenye bidii yalianzishwa Afrika, Asia, na Ulaya. (Wakolosai 1:23) Kweli rahisi ambazo Yesu alifundisha ziliwaelimisha watu wanyenyekevu na wenye mioyo minyoofu katika Miliki yote ya Roma.—Waefeso 1:17, 18.

Hata hivyo, ingewezekanaje kwa wanafunzi hao wote wapya kutoka hali mbalimbali za kiuchumi, utamaduni, lugha, na dini waungane pamoja katika “imani moja,” kama mtume Paulo alivyoiita? (Waefeso 4:5) Ni nini ambacho kingewafanya waendelee ‘kusema kwa upatano’ ili wasigawanyike? (1 Wakorintho 1:10) Kwa kufikiria mgawanyiko ulioko kati ya wale wanaodai kuwa Wakristo leo, tunapaswa kuchunguza yale ambayo Yesu mwenyewe alifundisha.

Msingi wa Umoja wa Kikristo

Alipokuwa akihukumiwa mbele ya Pontio Pilato, Yesu alitaja msingi wa umoja wa Kikristo. Alisema: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli. Kila mtu aliye upande wa ile kweli huisikiliza sauti yangu.” (Yohana 18:37) Kwa hiyo, kukubali mafundisho ya Yesu pamoja na Maandiko mengine yaliyoongozwa na roho ya Mungu, kunaweza kutokeza umoja wenye nguvu sana kati ya wanafunzi wa kweli wa Kristo.—1 Wakorintho 4:6; 2 Timotheo 3:16, 17.

Bila shaka, wanafunzi wa Yesu wangeuliza maswali ya unyoofu au kutofautiana nyakati nyingine. Ni nini ambacho kingewasaidia? Yesu alieleza: “Huyo atakapofika, roho ya ile kweli, atawaongoza ninyi ndani ya kweli yote, kwa maana hatasema kwa msukumo wake mwenyewe, bali mambo anayoyasikia atasema, naye atawatangazia mambo yanayokuja.” (Yohana 16:12, 13) Hivyo, roho takatifu ya Mungu ingewawezesha wanafunzi wa kweli wa Yesu waelewe ukweli kadiri ulivyofunuliwa na Mungu hatua kwa hatua. Pia, roho hiyo ingewawezesha kutokeza matunda kama vile upendo, shangwe, na amani, ambayo yangewasaidia wawe na umoja.—Matendo 15:28; Wagalatia 5:22, 23.

Yesu hakuruhusu kuwepo na mtengano na migawanyiko kati ya wanafunzi wake; wala hakuwaruhusu wafasiri kweli za Biblia ili zifaane na mapokeo ya kitamaduni na ya kidini ya watu ambao wangekutana nao. Badala yake, usiku wa mwisho aliokuwa pamoja nao, alisali hivi kwa bidii: “Ninawaombea, si hawa tu, bali pia wale wanaoniamini kupitia neno lao; ili wote wapate kuwa kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe, Baba, umo katika muungano pamoja na mimi na mimi nimo katika muungano pamoja na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano pamoja na sisi, ili ulimwengu upate kuamini kwamba ulinituma.” (Yohana 17:20, 21) Hivyo, umoja wa kweli katika roho na kweli ungewatambulisha wanafunzi wa Kristo tangu mwanzo wa Ukristo mpaka leo. (Yohana 4:23, 24) Hata hivyo, makanisa ya leo hayana umoja, yamegawanyika. Kwa nini hali iko hivyo?

Kwa Nini Makanisa Yamegawanyika?

Sababu moja iliyo wazi ambayo imefanya kuwe na imani na mapokeo tofauti-tofauti kati ya wale wanaodai kuwa Wakristo leo ni kwamba hawafuati mafundisho ya Yesu. Mwandishi mmoja alisema hivi: “Kama ilivyokuwa wakati uliopita, siku hizi Wakristo wana mwelekeo wa kukubali tu Maandiko ya Biblia yanayopatana na mahitaji yao na kupuuza yale yasiyopatana na mapokeo ya dini zao za kienyeji.” Yesu na mitume wake walitabiri kwamba hali ingekuwa hivyo.

Kwa mfano, mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kumwandikia hivi Timotheo mwangalizi mwenzake: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe; nao watageuza masikio yao kutoka kwenye kweli, nao watageuzwa kando kufuata hadithi za uwongo.” Je, Wakristo wote wangepotoshwa? La. Paulo anaendelea kusema: “Wewe tunza akili zako katika mambo yote, vumilia uovu, fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.” (2 Timotheo 4:3-5; Luka 21:8; Matendo 20:29, 30; 2 Petro 2:1-3) Timotheo pamoja na Wakristo wengine waaminifu waliishi kupatana na shauri hilo lililoongozwa na roho ya Mungu.

Wakristo wa Kweli Bado Wana Umoja

Kama Timotheo, leo Wakristo wa kweli wanatunza akili zao kwa kukataa hoja za kibinadamu na kukubali Maandiko tu kuwa msingi wa imani yao ya kidini. (Wakolosai 2:8; 1 Yohana 4:1) Kwa kuwaiga Wakristo wa karne ya kwanza, Mashahidi wa Yehova wanatimiza huduma yao katika nchi zaidi ya 230, wakiwapelekea watu kila mahali ujumbe wa awali wa Yesu, yaani, habari njema ya Ufalme. Fikiria njia nne muhimu ambazo kwa umoja wanamwiga Yesu na kufuata Ukristo wa kweli hata wawe wanaishi wapi.

Imani yao inategemea Neno la Mungu. (Yohana 17:17) Kasisi mmoja wa parokia fulani huko Ubelgiji aliandika hivi kuwahusu: “Jambo moja tunaloweza kujifunza kutoka kwao [Mashahidi wa Yehova] ni nia yao ya kusikiliza Neno la Mungu na ujasiri wao wa kulihubiri.”

Wanategemea Ufalme wa Mungu ulete kitulizo kutokana na matatizo ya ulimwengu. (Luka 8:1) Huko Barranquilla, Kolombia, Shahidi mmoja alizungumza na Antonio, aliyekuwa mfuasi shupavu wa kikundi fulani cha kisiasa. Shahidi huyo hakumuunga mkono, wala kutetea imani yoyote ya kisiasa. Badala yake, alijitolea kujifunza Biblia pamoja na Antonio na dada zake bila malipo. Muda si muda, Antonio akatambua kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la maskini nchini Kolombia na duniani pote.

Wanaliheshimu jina la Mungu. (Mathayo 6:9) Mashahidi wa Yehova walipokutana kwa mara ya kwanza na Maria, aliyekuwa Mkatoliki mnyoofu ambaye anaishi Australia, aliwaruhusu Mashahidi hao wamwonyeshe jina la Mungu katika Biblia. Aliitikiaje? “Nilipoona jina la Mungu kwa mara ya kwanza katika Biblia, nililia. Niliguswa moyo sana kutambua kwamba ningeweza kujua na kulitumia jina la Mungu.” Maria aliendelea kujifunza Biblia, na kwa mara ya kwanza maishani mwake, akapata kujua utu wa Yehova na kusitawisha uhusiano wenye kudumu pamoja naye.

Wameunganishwa na upendo. (Yohana 13:34, 35) Tahariri moja katika gazeti la The Ladysmith-Chemainus Chronicle, nchini Kanada, ilisema: “Hata uwe unafuata dini au hufuati dini yoyote, unapaswa kuwapongeza Mashahidi wa Yehova 4,500 waliofanya kazi mchana na usiku kujenga Jumba la Kusanyiko lenye ukubwa wa meta 2,300 za mraba huko Cassidy, katika juma moja na nusu lililopita . . . Kufanya kazi hiyo bila mabishano, mgawanyiko, au kujitakia makuu ni jambo linalotambulisha Ukristo wa kweli.”

Kwa hiyo, fikiria uthibitisho uliopo. Ukristo wa kweli unaendelea kusitawi duniani pote, huku wanatheolojia, mishonari, na waenda-kanisani wa dini zinazojiita za Kikristo wakiendelea kutazamia mapambano katika makanisa yao. Kwa kweli, Wakristo wa kweli wanaendelea na huduma waliyopewa ya kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Ikiwa wewe ni mmoja kati ya wale “wanaougua na kulia” kwa sababu ya machukizo yanayofanywa na unasumbuliwa na migawanyiko iliyo katika dini zinazojiita za Kikristo, tunakualika ujiunge na Mashahidi wa Yehova kumwabudu Yehova, Mungu wa pekee wa kweli, katika ibada ya Kikristo yenye umoja.—Ezekieli 9:4; Isaya 2:2-4.