Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watumishi wa Mungu Wanafanana na Miti Katika Maana Gani?

Watumishi wa Mungu Wanafanana na Miti Katika Maana Gani?

Watumishi wa Mungu Wanafanana na Miti Katika Maana Gani?

AKIZUNGUMZA kuhusu mtu anayependezwa na kanuni za Biblia na kuzitumia maishani mwake, mtunga-zaburi anasema: “Hakika atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.” (Zaburi 1:1-3) Kwa nini ulinganisho huo unafaa?

Miti inaweza kuishi kwa muda mrefu sana. Kwa mfano, inasemekana kwamba mizeituni fulani katika eneo la Mediterania imeishi kwa miaka elfu moja hadi elfu mbili. Vivyo hivyo, mibuyu ya Afrika ya kati huishi kwa miaka mingi sana, na inaaminika kwamba msindano fulani wa California umeishi kwa miaka 4,600. Mara nyingi, miti ya msituni iliyokomaa huwa na manufaa kwa mazingira. Kwa mfano, miti mirefu hukinga miti michanga kwa kivuli chake, nayo majani yanayoanguka kutoka katika miti hiyo hurutubisha udongo.

Kwa kawaida, miti mirefu zaidi ulimwenguni hukua pamoja misituni, nayo hutegemezana. Kwa kuwa huenda mizizi yake ikawa imesokotana, miti kadhaa inaweza kuhimili dhoruba vizuri zaidi kuliko mti mmoja kondeni. Pia mizizi mingi iliyosokotana huuwezesha mti kupata maji na lishe ya kutosha kutoka katika udongo. Katika hali fulani, mizizi inaweza kupenya ndani ya udongo na kuwa mirefu kuliko mti wenyewe, au inaweza kusambaa katika eneo kubwa zaidi kuliko matawi yake.

Huenda mtume Paulo alikuwa akigusia mti fulani alipoeleza kwamba Wakristo wanapaswa ‘kuendelea kutembea katika muungano na Kristo, wakiwa wametia mizizi na kujengwa katika yeye na kuimarishwa katika imani.’ (Wakolosai 2:6, 7) Naam, Wakristo wanaweza kubaki imara katika imani ikiwa tu wametia mizizi kabisa katika Kristo.—1 Petro 2:21.

Watumishi wa Mungu wanaweza kufananishwa na miti katika njia gani nyingine? Kama vile miti iliyomea pamoja hutegemezana, ndivyo wale wote wanaoshirikiana kwa ukaribu na kutaniko la Kikristo hupata utegemezo kutoka kwa waamini wenzao. (Wagalatia 6:2) Wakristo waaminifu waliokomaa, ambao wametia mizizi kiroho huwasaidia waamini wapya waendelee kuwa imara katika imani, hata wanapokabili upinzani ulio kama dhoruba. (Waroma 1:11, 12) Wakristo wapya wanaweza kufanya maendeleo kiroho chini ya “kivuli” chenye ulinzi cha watumishi wa Mungu wenye ujuzi zaidi. (Waroma 15:1) Washiriki wote wa kutaniko la Kikristo ulimwenguni hunufaika na chakula cha kiroho kinachoandaliwa na “miti mikubwa ya uadilifu,” yaani, mabaki ya watiwa-mafuta.—Isaya 61:3.

Inafurahisha kama nini kwamba watumishi wote wa Mungu wana tazamio la kuona utimizo wa ahadi inayopatikana kwenye Isaya 65:22, ambayo inasema: “Siku za watu wangu zitakuwa kama siku za mti.”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 28]

Godo-Foto