Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Yule Mtumwa Mwaminifu’ Apita Mtihani wa Ukaguzi!

‘Yule Mtumwa Mwaminifu’ Apita Mtihani wa Ukaguzi!

‘Yule Mtumwa Mwaminifu’ Apita Mtihani wa Ukaguzi!

“Ni wakati uliowekwa wa hukumu kuanza na nyumba ya Mungu.” —1 Petro 4:17.

1. Yesu alikuta hali gani alipokagua yule “mtumwa”?

SIKU ya Pentekoste 33 W.K., Yesu alimweka rasmi “mtumwa” ili awaandalie chakula “watumishi wake wa nyumbani” wakati unaofaa. Katika mwaka wa 1914, Yesu alitawazwa kuwa Mfalme, na punde wakati ukafika wa kumkagua “mtumwa” huyo. Alikuta kwamba wengi wa jamii hiyo ya “mtumwa” walikuwa ‘waaminifu na wenye busara.’ Hivyo, akaiweka rasmi jamii hiyo “juu ya mali zake zote.” (Mathayo 24:45-47) Hata hivyo, kulikuwa pia na mtumwa mwovu ambaye hakuwa mwaminifu wala mwenye busara.

“Mtumwa Huyo Mwovu”

2, 3. Jamii ya “mtumwa huyo mwovu” ilitoka wapi, nayo ilisitawi jinsi gani?

2 Yesu alimtaja mtumwa mwovu mara tu baada ya kuzungumza kuhusu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Alisema: “Mtumwa huyo mwovu akisema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia,’ naye aanze kuwapiga watumwa wenzake na kula na kunywa pamoja na walevi wa kupindukia, bwana wa mtumwa huyo atakuja katika siku ambayo hatazamii na katika saa ambayo hajui, naye atamwadhibu kwa ukali mkubwa zaidi na kumgawia sehemu yake pamoja na wanafiki. Huko ndiko atalia na kusaga meno.” (Mathayo 24:48-51) Maneno “mtumwa huyo mwovu” yanakazia maneno ya Yesu yaliyotangulia kuhusu mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Naam, wale wanaofanyiza “mtumwa huyo mwovu” walitoka miongoni mwa jamii ya mtumwa mwaminifu. * Jinsi gani?

3 Kabla ya mwaka wa 1914 washiriki wengi wa jamii ya mtumwa mwaminifu walikuwa na matazamio makubwa ya kukutana na Bwana-arusi mbinguni mwaka huo, lakini matazamio yao hayakutimizwa. Kwa sababu hiyo na hali nyingine, wengine walikata tamaa na wachache wakawa wenye uchungu. Baadhi yao walianza ‘kuwapiga’ kwa maneno ndugu zao wa zamani na kushirikiana na “walevi wa kupindukia,” yaani, vikundi vya dini zinazojiita za Kikristo.—Isaya 28:1-3; 32:6.

4. Yesu alishughulikaje na yule ‘mtumwa mwovu’ na wote ambao wameonyesha mtazamo kama wake?

4 Mwishowe, watu hao ambao walikuwa Wakristo walikuja kutambulishwa kuwa ‘mtumwa mwovu,’ naye Yesu akawaadhibu “kwa ukali mkubwa zaidi.” Jinsi gani? Aliwakataa, nao wakapoteza tumaini lao la kwenda mbinguni. Hata hivyo, hawakuharibiwa mara moja. Kwanza, walihitaji kupitia kipindi cha kulia na kusaga meno ‘katika giza lililo nje’ ya kutaniko la Kikristo. (Mathayo 8:12) Tangu siku hizo za mapema watiwa-mafuta wengine wachache wameonyesha mtazamo mbaya kama huo, na kujiunga na yule ‘mtumwa mwovu.’ Baadhi ya “kondoo wengine” wameiga ukosefu wao wa uaminifu. (Yohana 10:16) Adui hao wote wa Kristo wanaishia huko “nje katika giza” hilohilo la kiroho.

5. Mtumwa mwaminifu na mwenye busara alitendaje tofauti na ‘mtumwa mwovu’?

5 Hata hivyo, mtumwa mwaminifu na mwenye busara na ‘mtumwa mwovu’ walipitia ukaguzi uleule. Hata hivyo, badala ya mtumwa mwaminifu kuwa mwenye uchungu, alikubali kurekebishwa upya. (2 Wakorintho 13:11) Upendo wao kwa Yehova na kwa ndugu zao uliimarishwa. Kwa sababu hiyo, wamekuwa “nguzo na tegemezo la ile kweli” katika ‘siku hizi za mwisho’ zenye msukosuko.—1 Timotheo 3:15; 2 Timotheo 3:1.

Mabikira Wenye Busara na Mabikira Wapumbavu

6. (a) Yesu alitoa mfano gani kuonyesha busara ya jamii yake ya mtumwa mwaminifu? (b) Wakristo watiwa-mafuta walitangaza ujumbe gani kabla ya mwaka wa 1914?

6 Baada ya kuzungumza juu ya “mtumwa huyo mwovu,” Yesu alitoa mifano miwili kuonyesha kwa nini Wakristo fulani waliotiwa mafuta wangekuwa waaminifu na wenye busara huku wengine wakikosa sifa hizo. * Yesu alitoa mfano huu ili kuonyesha busara hiyo: “Ufalme wa mbinguni utakuwa kama mabikira kumi waliochukua taa zao na kwenda kumpokea bwana-arusi. Watano kati yao walikuwa wapumbavu, na watano walikuwa wenye busara. Kwa maana wale wapumbavu walichukua taa zao lakini hawakuchukua mafuta pamoja nao, lakini wale wenye busara walichukua mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao.” (Mathayo 25:1-4) Mabikira hao kumi hutukumbusha Wakristo watiwa-mafuta kabla ya mwaka wa 1914. Walikuwa wamepiga hesabu na kujua kwamba bwana-arusi, Yesu Kristo, alikuwa karibu kutokea. Hivyo ‘wakaenda’ kumpokea, huku wakihubiri kwa ujasiri kwamba “nyakati zilizowekwa za mataifa” zingeisha mwaka wa 1914.—Luka 21:24.

7. Wakristo watiwa-mafuta ‘walilala’ kwa njia ya mfano lini na kwa nini?

7 Walipiga hesabu kwa usahihi. Nyakati zilizowekwa za mataifa ziliisha mwaka wa 1914, nao Ufalme wa Mungu chini ya Kristo Yesu ukaanza kufanya kazi. Lakini hilo lilitukia katika mbingu zisizoonekana. Duniani, wanadamu walianza kupatwa na “ole” uliotabiriwa. (Ufunuo 12:10, 12) Kipindi cha ukaguzi kikaanza. Kwa kutoelewa mambo vizuri, Wakristo watiwa-mafuta walifikiri kwamba ‘bwana-arusi alikuwa anakawia.’ Kwa sababu ya kuchanganyikiwa na kuchukiwa na ulimwengu, kwa ujumla watiwa-mafuta walipunguza bidii yao na karibu waache kabisa kazi ya kuhubiri hadharani kwa njia ya mpango. Kama mabikira katika mfano wa Yesu, “walisinzia na kuanza kulala” kiroho, kama vile watu wasio waaminifu waliodai kuwa Wakristo walivyofanya baada ya mitume wa Yesu kufa.—Mathayo 25:5; Ufunuo 11:7, 8; 12:17.

8. Ni nini kilichosababisha mwito: “Huyu hapa bwana-arusi!” na huo ulikuwa wakati wa Wakristo watiwa-mafuta kufanya nini?

8 Kisha mwaka wa 1919 jambo fulani lisilotazamiwa likatukia. Tunasoma: “Katikati ya usiku kukatokea mwito, ‘Huyu hapa bwana-arusi! Nendeni mkampokee.’ Ndipo mabikira wote hao wakasimama na kuzitayarisha taa zao.” (Mathayo 25:6, 7) Wakati ule tu mambo yalionekana kuwa mabaya kabisa, ndipo mwito wa kutenda ulipotokea! Katika mwaka wa 1918, Yesu, “mjumbe wa agano,” alikuja kwenye hekalu la kiroho la Yehova ili kukagua na kulisafisha kutaniko la Mungu. (Malaki 3:1) Sasa, Wakristo watiwa-mafuta walihitaji kwenda nje na kumpokea katika nyua za kidunia za hekalu. Wakati wao wa ‘kutoa nuru’ ulikuwa umefika.—Isaya 60:1; Wafilipi 2:14, 15.

9, 10. Kwa nini Wakristo fulani walikuwa “wenye busara” na wengine “wapumbavu” mwaka wa 1919?

9 Lakini ona kwamba baadhi ya wanawake hao wachanga katika mfano huo walikuwa na tatizo. Yesu aliendelea kusema: “Wale wapumbavu wakawaambia wale wenye busara, ‘Tupeni sisi kiasi fulani cha mafuta yenu, kwa sababu taa zetu zinakaribia kuzimika.’” (Mathayo 25:8) Bila mafuta, taa hizo hazingeweza kutoa nuru. Hivyo, mafuta ya taa hutukumbusha Neno la Mungu la kweli na roho yake takatifu, ambayo huwatia nguvu waabudu wa kweli wawe wachukuaji nuru. (Zaburi 119:130; Danieli 5:14) Kabla ya mwaka wa 1919, Wakristo watiwa-mafuta wenye busara walikuwa wamejitahidi kutambua mapenzi ya Mungu japo udhaifu wao wa muda. Hivyo, mwito wa kutoa nuru ulipotolewa, walikuwa tayari.—2 Timotheo 4:2; Waebrania 10:24, 25.

10 Hata hivyo, watiwa-mafuta fulani hawakuwa tayari kujidhabihu au kujikakamua, ingawa walitamani sana kuwa pamoja na Bwana-arusi. Kwa hiyo, wakati ulipofika wa kuhubiri habari njema kwa bidii, wao hawakuwa tayari. (Mathayo 24:14) Hata walijaribu kupunguza bidii ya wenzao, kwa kuwaomba wawagawie mafuta yao. Katika mfano wa Yesu, mabikira wenye busara walijibuje? Walisema: “Labda huenda tusiwe na ya kutosha kwa ajili yetu na kwa ajili yenu. Badala yake, shikeni njia mwende kwa wale wanaoyauza mkajinunulie.” (Mathayo 25:9) Vivyo hivyo, mwaka wa 1919 Wakristo watiwa-mafuta waliokuwa waaminifu walikataa kufanya lolote ambalo lingepunguza uwezo wao wa kutoa nuru. Hivyo, walipita mtihani huo wa ukaguzi.

11. Mabikira wapumbavu walipatwa na nini?

11 Yesu anamalizia kwa kusema: “[Mabikira wapumbavu] walipokuwa wakienda zao kununua, bwana-arusi akafika, na wale mabikira waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye kwenye karamu ya arusi; nao mlango ukafungwa. Baadaye wale mabikira wengine pia wakaja, wakisema, ‘Bwana, bwana, tufungulie!’ Akajibu, akasema, ‘Ninawaambia ninyi kweli, Siwajui ninyi.’” (Mathayo 25:10-12) Naam, baadhi yao hawakuwa tayari kumpokea Bwana-arusi alipowasili. Hivyo, wakaanguka mtihani wa ukaguzi na kupoteza nafasi ya kuhudhuria karamu ya arusi mbinguni. Ilihuzunisha kama nini!

Mfano wa Talanta

12. (a) Yesu alitumia mfano gani kuhusu sifa ya uaminifu? (b) Mtu ‘aliyeenda ng’ambo’ ni nani?

12 Baada ya kutoa mfano kuhusu busara, Yesu alitoa mfano mwingine kuhusu sifa ya uaminifu. Alisema: “Ni kama wakati ambapo mtu, akiwa karibu kusafiri ng’ambo, aliwaita watumwa wake na kuwapa mali zake. Akampa mmoja talanta tano, mwingine mbili, na mwingine moja, kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe, naye akaenda ng’ambo.” (Mathayo 25:14, 15) Mtu anayetajwa katika mfano huo ni Yesu mwenyewe, ambaye ‘alienda ng’ambo’ alipopanda mbinguni mwaka wa 33 W.K. Lakini kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwapa wanafunzi wake waaminifu “mali zake.” Jinsi gani?

13. Yesu alitayarishaje shamba kubwa la utendaji na kuwapa ‘watumwa’ wake ruhusa ya kufanya biashara?

13 Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alianza kutayarisha shamba kubwa la utendaji kwa kuhubiri habari njema za Ufalme katika nchi yote ya Israeli. (Mathayo 9:35-38) Kabla ya ‘kwenda ng’ambo,’ aliwapa wanafunzi waaminifu shamba hilo akisema: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:18-20) Kwa maneno hayo Yesu aliwapa “watumwa” wake ruhusa ya kufanya biashara hadi atakaporudi, “kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe.”

14. Kwa nini wanafunzi wote hawakutazamiwa wafanye biashara kwa kiwango kilekile?

14 Maneno hayo yanaonyesha kwamba hali za Wakristo wote wa karne ya kwanza hazikufanana. Hali za wengine, kama vile Paulo na Timotheo, ziliwawezesha kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. Huenda hali za wengine zilifanya iwe vigumu sana kushiriki katika kazi hiyo. Kwa mfano, Wakristo fulani walikuwa watumwa, wengine walikuwa wagonjwa, wazee, au wenye madaraka ya familia. Bila shaka, kulikuwa na mapendeleo fulani kutanikoni ambayo baadhi ya wanafunzi hawakuyapata. Baadhi ya wanawake na wanaume watiwa-mafuta hawakufundisha kutanikoni. (1 Wakorintho 14:34; 1 Timotheo 3:1; Yakobo 3:1) Hata hivyo, bila kujali hali zao, wanafunzi wote wa Kristo waliotiwa mafuta, wanaume kwa wanawake, walipewa mgawo wa kufanya biashara, nao walitumia vizuri nafasi na hali zao katika huduma ya Kikristo. Leo wanafunzi wa Kristo hufanya vivyo hivyo.

Wakati wa Ukaguzi Waanza!

15, 16. (a) Wakati wa kufanya hesabu ulifika lini? (b) Ni nafasi gani mpya za “kufanya biashara” ambazo wale walio waaminifu walipewa?

15 Katika mfano huo Yesu anaendelea kusema: “Baada ya muda mrefu bwana wa watumwa hao alikuja na kufanya hesabu pamoja nao.” (Mathayo 25:19) Katika mwaka wa 1914—bila shaka muda mrefu baada ya 33 W.K.—kuwapo kwa Kristo Yesu akiwa mfalme kulianza. Mnamo mwaka wa 1918, miaka mitatu na nusu baadaye, alikuja kwenye hekalu la Mungu la kiroho na kutimiza maneno haya ya Petro: “Ni wakati uliowekwa wa hukumu kuanza na nyumba ya Mungu.” (1 Petro 4:17; Malaki 3:1) Ulikuwa wakati wa kufanya hesabu.

16 Watumwa, yaani, ndugu za Yesu watiwa-mafuta, wamefanyaje na “talanta” za Mfalme? Kuanzia mwaka wa 33 W.K. na kuendelea, kutia ndani miaka iliyotangulia mwaka wa 1914, wengi walikuwa wakifanya “biashara” ya Yesu kwa bidii. (Mathayo 25:16) Hata wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu, walionyesha tamaa kubwa ya kumtumikia Bwana. Wakati huo ilifaa wale walio waaminifu wapewe nafasi mpya za “kufanya biashara.” Mwisho wa mfumo huu wa mambo ulikuwa umefika. Habari njema ilipaswa kuhubiriwa duniani kote. “Mavuno ya dunia” yalipaswa kuvunwa. (Ufunuo 14:6, 7, 14-16) Washiriki wa mwisho wa jamii ya ngano walipaswa kutafutwa na “umati mkubwa” kukusanywa.—Ufunuo 7:9; Mathayo 13:24-30.

17. Wakristo waaminifu waliotiwa mafuta ‘waliingiaje katika shangwe ya bwana wao’?

17 Wakati wa mavuno ni wakati wa furaha. (Zaburi 126:6) Hivyo, inafaa kwamba Yesu alipowapa madaraka zaidi ndugu zake watiwa-mafuta mwaka wa 1919, alisema: ‘Mlikuwa waaminifu juu ya mambo machache. Nitawaweka juu ya mambo mengi. Ingieni katika shangwe ya bwana wenu.’ (Mathayo 25:21, 23) Isitoshe, hatuwezi kuwazia furaha ambayo Bwana alipata alipotawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. (Zaburi 45:1, 2, 6, 7) Jamii ya mtumwa mwaminifu inapata furaha hiyo pia kwa kumwakilisha Mfalme na kuzidisha mambo yanayohusu ufalme wake. (2 Wakorintho 5:20) Furaha yao inaonyeshwa katika maneno haya ya kinabii ya Isaya 61:10: “Hakika nitafurahi katika Yehova. Nafsi yangu itakuwa na shangwe katika Mungu wangu. Kwa maana amenivika mavazi ya wokovu.”

18. Kwa nini wengine hawakupita mtihani wa ukaguzi, na ilikuwaje?

18 Inasikitisha kwamba wengine hawakupita mtihani wa ukaguzi. Tunasoma: “Yule aliyekuwa amepokea talanta moja akaja na kusema, ‘Bwana nilijua wewe ni mtu mwenye kudai, ambaye huvuna mahali ambapo hukupanda na kukusanya mahali ambapo hukupepeta. Kwa hiyo nikaogopa na kwenda zangu na kuficha talanta yako katika udongo. Tazama, hiki hapa kilicho chako.’” (Mathayo 25:24, 25) Vivyo hivyo, Wakristo fulani watiwa-mafuta hawakufanya “biashara.” Kabla ya mwaka wa 1914 hawakuwa na bidii ya kuwaeleza wengine tumaini lao, nao hawakutaka kuanza kufanya hivyo mwaka wa 1919. Yesu alitendaje kuhusiana na dharau yao? Aliwanyang’anya mapendeleo yao yote. ‘Walitupwa nje katika giza ambako walilia na kusaga meno yao.’—Mathayo 25:28, 30.

Ukaguzi Unaendelea

19. Ukaguzi unaendelea katika njia gani, nao Wakristo wote watiwa-mafuta wameazimia kufanya nini?

19 Bila shaka, wengi wa wale ambao wangekuwa watumwa watiwa-mafuta wa Kristo wakati wa mwisho hawakuwa wakimtumikia Yehova wakati Yesu alipoanza ukaguzi mwaka wa 1918. Je, walikaguliwa? Ndiyo. Ukaguzi ulianza tu mwaka wa 1918/1919, wakati mtumwa mwaminifu na mwenye busara akiwa jamii alipopita mtihani wa ukaguzi. Wakristo mmoja-mmoja waliotiwa mafuta wanaendelea kukaguliwa hadi watiwe muhuri wa kudumu. (Ufunuo 7:1-3) Kwa kutambua jambo hilo, ndugu za Kristo watiwa-mafuta wameazimia kuendelea “kufanya biashara” kwa uaminifu. Wameazimia pia kuwa wenye busara na kuweka mafuta mengi vya kutosha ili nuru iendelee kung’aa zaidi. Wanajua kwamba kila mmoja wao anapokufa akiwa mwaminifu, Yesu atampokea na kukaa naye mbinguni.—Mathayo 24:13; Yohana 14:2-4; 1 Wakorintho 15:50, 51.

20. (a) Leo kondoo wengine wameazimia kufanya nini? (b) Wakristo watiwa-mafuta wanajua nini?

20 Umati mkubwa wa kondoo wengine wamewaiga ndugu zao watiwa-mafuta. Wanajua kwamba ujuzi wao wa makusudi ya Mungu huwafanya wawe na daraka kubwa. (Ezekieli 3:17-21) Hivyo, kwa msaada wa Neno la Yehova na roho yake takatifu, wao pia huweka mafuta mengi vya kutosha kupitia funzo na mikutano ya Kikristo. Nao huangaza nuru yao kwa kuhubiri na kufundisha na hivyo “kufanya biashara” pamoja na ndugu zao watiwa-mafuta. Hata hivyo, Wakristo watiwa-mafuta wanafahamu vizuri kwamba wao ndio waliopewa talanta. Lazima watoe hesabu kuhusu jinsi mali za Bwana zinavyosimamiwa duniani. Ingawa wao ni wachache, hawawezi kuwatwika umati mkubwa daraka lao. Kwa kuzingatia hilo, mtumwa mwaminifu na mwenye busara anaendelea kuongoza katika kutunza biashara ya Mfalme na kushukuru kwa msaada wa washiriki wenye bidii wa umati mkubwa. Washiriki wa umati mkubwa wanatambua daraka la ndugu zao watiwa-mafuta nao huona ni pendeleo kufanya kazi chini ya usimamizi wao.

21. Ni himizo gani linalowahusu Wakristo wote kabla ya mwaka wa 1919 hadi siku zetu?

21 Hivyo, ingawa mifano hiyo miwili inafafanua matukio ya mwaka wa 1919 au karibu na wakati huo, kanuni za mifano hiyo zinahusu Wakristo wote wa kweli katika siku zote za mwisho. Kwa njia hiyo, ingawa himizo ambalo Yesu alitoa mwishoni mwa mfano wa mabikira kumi kwanza linahusu Wakristo watiwa-mafuta kabla ya mwaka wa 1919, bado kanuni zake zinahusu kila Mkristo. Sote na tutii maneno haya ya Yesu: “Endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”—Mathayo 25:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kwa njia inayofanana na hiyo, baada ya mitume kufa, “mbwa-mwitu wenye kukandamiza” walitoka miongoni mwa wazee Wakristo waliotiwa mafuta.—Matendo 20:29, 30.

^ fu. 6 Kwa mazungumzo zaidi kuhusu mfano wa Yesu, ona sura ya 5 na ya 6 ya kitabu Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani,” kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Yesu aliwakagua lini wafuasi wake, naye alikuta hali gani?

• Kwa nini Wakristo fulani watiwa- mafuta walisitawisha mtazamo wa ‘mtumwa mwovu’?

• Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna busara kiroho?

• Ni katika njia gani tunaweza kuendelea “kufanya biashara” kwa kuwaiga ndugu za Yesu watiwa-mafuta walio waaminifu?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 16]

YESU ANAKUJA LINI?

Mathayo sura ya 24 na ya 25, husema kwamba Yesu ‘angekuja’ katika maana mbalimbali. Ili “kuja,” Yesu hahitaji kuondoka mahali fulani na kwenda mahali pengine. Badala yake ‘anakuja’ katika maana ya kuelekeza fikira zake kwa wanadamu au kwa wafuasi wake, mara nyingi ili kuwahukumu. Hivyo, mnamo mwaka wa 1914 ‘alikuja’ ili kuwapo kwake kuanze akiwa Mfalme aliyetawazwa. (Mathayo 16:28; 17:1; Matendo 1:11) Katika mwaka wa 1918 ‘alikuja’ akiwa mjumbe wa agano na kuanza kuwahukumu wale waliodai kumtumikia Yehova. (Malaki 3:1-3; 1 Petro 4:17) Kwenye Har-magedoni, ‘atakuja’ ili kuwahukumu maadui wa Yehova.—Ufunuo 19:11-16.

Kuja (au, kuwasili) kunakotajwa mara kadhaa katika Mathayo 24:29-44 na 25:31-46 kutatukia wakati wa “dhiki kuu.” (Ufunuo 7:14) Kwa upande mwingine, kuja kunakotajwa mara kadhaa katika Mathayo 24:45 hadi 25:30 kunahusu hukumu yake dhidi ya wale wanaodai kuwa wanafunzi wake kuanzia 1918 na kuendelea. Kwa mfano, si jambo la akili kusema kwamba kuthawabishwa kwa mtumwa mwaminifu, kuhukumiwa kwa wale mabikira wapumbavu, na kuhukumiwa kwa yule mtumwa goigoi, aliyeficha talanta ya Bwana wake, kutatukia Yesu ‘atakapokuja’ wakati wa dhiki kuu. Hiyo ingemaanisha kwamba wakati huo wengi wa watiwa-mafuta watapatikana kuwa wasio waaminifu na hivyo mahali pao kuchukuliwa na wengine. Hata hivyo, andiko la Ufunuo 7:3 linaonyesha kwamba watumwa wote wa Kristo waliotiwa mafuta watakuwa ‘wametiwa muhuri’ wa kudumu kufikia wakati huo.

[Picha katika ukurasa wa 14]

‘Mtumwa mwovu’ hakubarikiwa mwaka wa 1919

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mabikira wenye busara walikuwa tayari bwana-arusi alipofika

[Picha katika ukurasa wa 17]

Watumwa waaminifu walikuwa wamefanya “biashara”

Mtumwa goigoi hakuwa amefanya hivyo

[Picha katika ukurasa wa 18]

Watiwa-mafuta na “umati mkubwa” wanaendelea kuangaza nuru yao