Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ehudi Avunja Nira ya Mkandamizaji

Ehudi Avunja Nira ya Mkandamizaji

Ehudi Avunja Nira ya Mkandamizaji

HILI ni simulizi la kweli kuhusu ujasiri na kutumia mbinu. Lilitukia miaka 3,000 hivi iliyopita. Simulizi hili la Biblia linaanza kwa maneno haya: “Wana wa Israeli wakaanza tena kufanya yaliyo mabaya machoni pa Yehova. Ndipo Yehova akaacha Egloni mfalme wa Moabu apate nguvu juu ya Israeli, kwa sababu walifanya yaliyo mabaya machoni pa Yehova. Zaidi ya hayo, akakusanya wana wa Amoni na Amaleki juu yao. Ndipo wakaenda, wakapiga Israeli na kulichukua jiji la mitende. Na wana wa Israeli wakaendelea kumtumikia Egloni mfalme wa Moabu kwa miaka kumi na minane.”—Waamuzi 3:12-14.

Eneo la Wamoabu lilikuwa mashariki ya Mto Yordani na Bahari ya Chumvi. Lakini walikuwa wamevuka mto huo na kuchukua eneo lililo karibu na Yeriko, yaani, “jiji la mitende,” na hivyo kuwatumikisha Waisraeli. (Kumbukumbu la Torati 34:3) Egloni, mfalme wa Moabu alikuwa “mtu mnene sana,” naye aliwatoza Waisraeli ushuru wenye kulemea na wenye kufedhehesha kwa miaka 20 hivi. (Waamuzi 3:17) Hata hivyo, kudai kwake ushuru kuliwapa Waisraeli nafasi ya kumwondoa mkandamizaji huyo.

Simulizi hilo linasema: “Wana wa Israeli wakaanza kumwita Yehova awape msaada. Basi Yehova akawasimamishia mwokozi, Ehudi mwana wa Gera, Mbenyamini, mwanamume mwenye kutumia mkono wa kushoto. Baada ya muda wana wa Israeli wakapeleka ushuru kupitia mkono wake kwa Egloni mfalme wa Moabu.” (Waamuzi 3:15) Bila shaka, Yehova alihakikisha kwamba Ehudi amechaguliwa kupeleka ushuru huo. Haijulikani kama alikuwa amewahi kufanya kazi hiyo kabla ya hapo. Hata hivyo, jinsi ambavyo Ehudi alijitayarisha kwa makini kwa ajili ya mkutano huo na mbinu alizotumia zinadokeza kwamba huenda kwa kiasi fulani alifahamu jumba la Egloni na mambo ambayo angetarajia huko. Katika hayo yote, jambo lililo muhimu ni kwamba Ehudi alitumia mkono wa kushoto.

Je, Alikuwa Mlemavu au Shujaa wa Vita?

Katika Kiebrania, maneno “mwenye kutumia mkono wa kushoto” yanamaanisha ‘aliyefungwa, kilema, au aliyezuiwa asitumie mkono wa kuume.’ Je, hilo linamaanisha kwamba Ehudi alikuwa mlemavu, na labda mkono wake wa kuume ulikuwa umelemaa? Ona yale Biblia inayosema kuhusu “watu 700 waliochaguliwa” katika kabila la Benyamini ambao walitumia mkono wa kushoto. Andiko la Waamuzi 20:16 linasema: “Kila mmoja wa hao alikuwa mtupa-mawe kwa kombeo na angeweza kupiga shabaha unywele, bila kukosea.” Yaelekea walichaguliwa kwa sababu ya uhodari wao katika vita. Wasomi fulani wa Biblia husema kwamba mtu “mwenye kutumia mkono wa kushoto” ni yule aliyetumia mikono yote miwili.—Waamuzi 3:15.

Kwa kweli kabila la Benyamini lilikuwa mashuhuri kwa kuwa na wanaume waliotumia mkono wa kushoto. Andiko la 1 Mambo ya Nyakati 12:1, 2 linataja Wabenyamini kuwa “wanaume wenye nguvu, wasaidizi katika vita, wenye upinde, wanaotumia mkono wa kuume na kutumia mkono wa kushoto wakiwa na mawe au wakiwa na mishale katika upinde.” Kichapo kimoja cha kitaalamu kinasema kwamba huenda walipata uwezo huo “kupitia kufunga mkono wa kuume wa mtoto mchanga, na hivyo ‘kumzuia asitumie mkono huo,’ huku wakimzoeza kutumia mkono wa kushoto kwa ustadi.” Kwa kawaida, maadui wa Waisraeli walizoezwa kukabiliana na mashujaa wa vita waliotumia mkono wa kuume. Hivyo, mazoezi ambayo adui alipata yangekuwa bure iwapo angekutana kwa ghafula na askari anayetumia mkono wa kushoto.

“Neno la Siri” kwa Mfalme

Hatua ya kwanza ambayo Ehudi alichukua ni ‘kujifanyia upanga’ wenye makali kuwili ambao ulikuwa mfupi kuweza kufichwa chini ya mavazi yake. Huenda alitarajia kupekuliwa. Kwa kawaida panga ziliwekwa upande wa kushoto wa mwili, ambapo watu waliotumia mkono wa kuume wangeweza kuzichomoa upesi. Kwa kuwa alitumia mkono wa kushoto, Ehudi alificha silaha yake “chini ya vazi lake kwenye paja lake la kuume,” upande ambao yaelekea walinzi wa mfalme hawangepekua. Kwa hiyo, Ehudi ‘akampa Egloni mfalme wa Moabu ushuru huo’ bila kuzuiwa.—Waamuzi 3:16, 17.

Habari kuhusu matukio ya mwanzo-mwanzo katika ua wa Egloni hazijatajwa. Biblia inasema tu hivi: “Ikawa kwamba [Ehudi] alipokuwa amemaliza kutoa ule ushuru, mara moja akawaambia watu waende zao, wale waliobeba ule ushuru.” (Waamuzi 3:18) Baada ya kupeleka ushuru huo, Ehudi aliwasindikiza wale walioubeba hadi mahali salama mbali na makao ya Egloni, kisha akawaaga na kurudi. Kwa nini? Je, alikuwa ameingia kwa mfalme pamoja na wanaume hao kwa sababu ya ulinzi, kufuata utaratibu, au labda walikuwa tu wabebaji wa ushuru? Na je, alitaka waondoke kwa sababu ya usalama wake kabla ya kutekeleza mbinu yake? Hata sababu iwe nini, Ehudi alirudi kwa ujasiri katika jumba la mfalme akiwa peke yake.

“[Ehudi] akageuka na kurudi alipofika mahali penye machimbo yaliyokuwa katika Gilgali, akasema: ‘Nina neno la siri kwako, Ee mfalme.’” Biblia haielezi jinsi alivyofaulu kuingia tena mbele za Egloni. Je, walinzi hawakushuku chochote? Je, walifikiri kwamba Mwisraeli mmoja hangeweza kuhatarisha uhai wa bwana wao? Kwa kurudi peke yake, je, Ehudi alionyesha kwamba alikuwa akiwasaliti Waisraeli wenzake? Vyovyote vile, Ehudi alitafuta nafasi ya kuzungumza faraghani pamoja na mfalme, naye akaipata.—Waamuzi 3:19.

Simulizi hilo lililoongozwa na roho linaendelea: “Ehudi akamjia [Egloni] alipokuwa ameketi katika chumba chake cha darini chenye baridi ambacho kilikuwa chake binafsi. Naye Ehudi akaendelea kusema: ‘Nina neno linalotoka kwa Mungu kwa ajili yako.’” Ehudi hakuwa akirejelea ujumbe wa mdomo kutoka kwa Mungu. Alikuwa akifikiria tu kutumia upanga wake. Labda kwa kutarajia kusikia ujumbe fulani kutoka kwa mungu wake Kemoshi, mfalme huyo “akasimama kutoka katika kiti chake cha ufalme.” Kufumba na kufumbua, Ehudi alichomoa silaha yake naye akaichomeka katika tumbo la Egloni. Yaelekea mpini wa upanga huo haukuwa na kipande kilichokingamana. Hivyo, “mpini pia ukazidi kuingia ndani ukiufuata upanga huo na mafuta yakaufunika upanga huo, . . . na mavi yakaanza kutoka nje,” kupitia jeraha hilo au yakatoka yenyewe kwa njia ya kawaida.—Waamuzi 3:20-22.

Atoroka Bila Magumu Yoyote

Bila kupoteza wakati akijaribu kuuchomoa upanga wake, “Ehudi akatoka nje kupitia tundu la hewa, lakini akaifunga kwa ufunguo milango ya chumba cha dari. Naye akatoka nje. Na watumishi wa [Egloni] wakaja na kuanza kuangalia, na tazama, milango ya chumba cha dari ilikuwa imefungwa kwa ufunguo. Kwa hiyo wakasema: ‘Ameenda haja katika chumba chake cha ndani chenye baridi.’”—Waamuzi 3:23, 24.

“Tundu la hewa” ambalo Ehudi alipitia lilikuwa nini? Kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema, “Maana kamili ya neno la Kiebrania haijulikani,” lakini “inadokezwa kwamba neno hilo linamaanisha ‘ukumbi wa kuingilia.’” Je, Ehudi aliifunga milango kwa ufunguo akiwa ndani kisha akatoka kupitia njia nyingine? Au je, aliifunga akiwa nje kwa kutumia ufunguo wa mfalme aliyekuwa mfu? Je, baada ya kufunga alitembea polepole na kupita mbele ya walinzi kana kwamba hakuna jambo lolote lililokuwa limetukia? Biblia haielezi. Lakini, hata Ehudi awe alitumia njia gani, watumishi wa Egloni hawakushuku chochote mara moja walipopata milango ikiwa imefungwa. Walifikiri tu kwamba mfalme “ameenda haja.”

Watumishi wa mfalme walipokuwa wakisitasita, Ehudi alitoroka. Kisha akawaita Waisraeli wenzake na kuwaambia: “Nifuateni, kwa maana Yehova amewatia adui zenu, Wamoabu, mkononi mwenu.” Kwa kuteka vivuko muhimu kijeshi vya Yordani, wanaume wa Ehudi waliwazuia Wamoabu wasiokuwa na kiongozi kurudi nchini mwao. Hivyo, “wakati huo [Waisraeli] wakapiga Moabu, karibu wanaume elfu kumi, kila mmoja akiwa ni mwenye nguvu na kila mmoja akiwa ni mwanamume shujaa; wala hakuna hata mtu mmoja aliyepona. Na Moabu wakatiishwa siku hiyo chini ya mkono wa Israeli; na nchi haikuwa na usumbufu wowote tena kwa miaka 80.”—Waamuzi 3:25-30.

Mambo Tunayoweza Kujifunza

Mambo yaliyotukia siku za Ehudi yanatufunza kwamba tukifanya mabaya machoni pa Yehova tutapatwa na madhara. Kwa upande mwingine, Yehova huwasaidia wale wanaotubu na kumgeukia.

Mbinu za Ehudi hazikufaulu kwa sababu ya werevu wake au kwa sababu maadui hawakuwa na uwezo. Kutimizwa kwa makusudi ya Mungu hakutegemei uwezo wa kibinadamu. Ehudi alifaulu hasa kwa sababu Mungu alimuunga mkono kwa kuwa alitenda kulingana na mapenzi Yake yasiyoshindwa ili kuwaokoa watu Wake. Mungu alimsimamisha Ehudi, ‘na wakati Yehova alipowasimamishia watu wake waamuzi, Yehova alikuwa pamoja na mwamuzi huyo.’—Waamuzi 2:18; 3:15.