Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Fanya Kazi ya Mweneza-injili”

“Fanya Kazi ya Mweneza-injili”

“Fanya Kazi ya Mweneza-injili”

“Tunza akili zako katika mambo yote, . . . fanya kazi ya mweneza-injili.” —2 Timotheo 4:5.

1. Yesu aliwapa wafuasi wake kazi gani?

JINA la Yehova na makusudi yake yanatangazwa duniani kote. Hiyo ni kwa sababu watu wa Mungu waliojiweka wakfu wamechukua kwa uzito kazi ambayo Yesu Kristo aliwapa wafuasi wake aliposema hivi: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mathayo 28:19, 20.

2. Mwangalizi Timotheo alipokea maagizo gani, na ni katika njia gani moja waangalizi Wakristo wanaweza kutimiza huduma yao?

2 Wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walichukua kazi hiyo kwa uzito. Kwa mfano, mtume Paulo alimhimiza hivi Timotheo, mwangalizi mwenzake Mkristo: “Fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.” (2 Timotheo 4:5) Leo, njia moja ambayo mwangalizi hutimiza huduma yake ni kwa kuwa mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii, ambaye hushiriki katika huduma ya shambani kwa ukawaida. Kwa mfano, mwangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko ana pendeleo lenye kuthawabisha la kuwa mstari wa mbele katika kazi ya kuhubiri na kuwazoeza wengine. Paulo alitimiza daraka lake la kutangaza habari njema, naye alisaidia kuwazoeza wengine kwa ajili ya huduma.—Matendo 20:20; 1 Wakorintho 9:16, 17.

Waeneza-Injili wa Zamani Wenye Bidii

3, 4. Ni mambo gani ambayo Filipo alifanya akiwa mweneza-injili?

3 Wakristo wa mapema walijulikana kuwa waeneza-injili wenye bidii. Fikiria Filipo, aliyekuwa mweneza-injili. Alikuwa mmoja kati ya “wanaume saba waliothibitishwa . . . wenye kujaa roho na hekima” ambao walichaguliwa kugawanya chakula kila siku bila upendeleo kati ya wajane Wakristo waliozungumza Kigiriki na wale waliozungumza Kiebrania huko Yerusalemu. (Matendo 6:1-6) Baada ya utumishi huo wa pekee kwisha nao Wakristo wote isipokuwa mitume wakatawanyika kwa sababu ya mateso, Filipo alienda Samaria. Akiwa huko, alitangaza habari njema na kutiwa nguvu kupitia roho takatifu ili kufukuza roho waovu, kuponya vilema, na watu waliopooza. Wasamaria wengi walikubali ujumbe wa Ufalme na kubatizwa. Waliposikia habari hizo, mitume waliokuwa Yerusalemu waliwatuma mitume Petro na Yohana kwenda Samaria ili waamini hao wapya waliobatizwa waweze kupokea roho takatifu.—Matendo 8:4-17.

4 Kisha, roho ya Mungu ikamwongoza Filipo akutane na towashi Mwethiopia aliyekuwa barabarani kwenda Gaza. Baada ya Filipo kumfafanulia vizuri unabii wa Isaya, ‘mwanamume huyo ambaye alikuwa na mamlaka chini ya Kandake malkia wa Waethiopia,’ alimwamini Yesu Kristo na kubatizwa. (Matendo 8:26-38) Baada ya hapo, Filipo alienda Ashdodi kisha Kaisaria, ‘huku akitangaza habari njema kwa majiji yote yaliyokuwa kwenye njia hiyo.’ (Matendo 8:39, 40) Bila shaka, aliweka kielelezo kizuri katika kufanya kazi ya mweneza-injili!

5. Binti wanne wa Filipo walijulikana hasa kwa jambo gani?

5 Bado Filipo alikuwa mwenye bidii katika huduma huko Kaisaria miaka 20 hivi baadaye. Paulo na Luka walipokaa nyumbani kwake, “alikuwa na binti wanne, mabikira, waliotoa unabii.” (Matendo 21:8-10) Bila shaka, binti hao walikuwa wamezoezwa vizuri kiroho, wenye bidii katika huduma, na hata walikuwa na pendeleo la kutoa unabii. Leo, wazazi wanapokuwa na bidii katika huduma, wana na binti zao watawaiga nao watachochewa kufanya kazi ya kueneza injili katika maisha yao yote.

Waeneza-Injili Wenye Bidii Leo

6. Waeneza-injili wa karne ya kwanza walipata mafanikio gani?

6 Yesu Kristo alisema hivi katika unabii wake muhimu unaohusu siku zetu na wakati wa mwisho: “Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:10) Mwisho ungekuja baada ya habari njema kuhubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Paulo na waeneza-injili wengine wa karne ya kwanza walipotangaza habari njema, wengi waliamini, makutaniko yakaanzishwa sehemu nyingi katika Milki yote ya Roma. Wazee waliowekwa rasmi kutumika katika makutaniko hayo, walishirikiana na ndugu na dada zao katika kueneza injili kila mahali. Neno la Yehova liliendelea kukua na kusitawi siku hizo kama linavyofanya leo, kwa sababu mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi hiyo ya kueneza injili. (Matendo 19:20) Je, wewe ni mmoja wa wasifaji hao wenye furaha wa Yehova?

7. Watangazaji wa Ufalme wanafanya nini leo?

7 Leo watangazaji wengi wa Ufalme wanatumia nafasi zinazojitokeza za kupanua zaidi kazi yao ya kueneza injili. Maelfu wamekuwa mishonari, nao mamia ya maelfu wanaeneza injili kwa wakati wote wakiwa mapainia wa kawaida na wasaidizi. Pia wanaume, wanawake, na watoto wanafanya kazi nzuri sana ya kutangaza Ufalme kwa bidii. Naam, Yehova anawabariki sana watu wake wote wanapomtumikia bega kwa bega wakiwa waeneza-injili Wakristo.—Sefania 3:9.

8. Ni kazi gani ya kutia alama inayofanywa sasa, nayo inafanywa na nani?

8 Mungu amewapa wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta daraka la kutangaza habari njema duniani kote. “Kondoo wengine” wa Kristo wanaozidi kuongezeka wanawaunga mkono katika kazi hiyo ya kueneza injili. (Yohana 10:16) Kinabii, kazi hii inayookoa uhai inafananishwa na kuweka alama kwenye mapaji ya uso ya wale wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yanayofanyika sasa. Hivi karibuni, waovu wataharibiwa. Ni pendeleo lililoje sasa kuwapelekea wakaaji wa dunia kweli zenye kuokoa uhai!—Ezekieli 9:4-6, 11.

9. Wapya wanaweza kusaidiwaje katika huduma?

9 Ikiwa tumekuwa tukishiriki katika kazi ya kueneza injili kwa muda fulani, yaelekea tunaweza kufanya jambo fulani ili kuwasaidia wapya kutanikoni. Huenda pindi kwa pindi tukawaomba waandamane nasi katika huduma. Wale wanaotumikia wakiwa wazee wanatiwa moyo wafanye yote wawezayo kuwajenga waamini wenzao kiroho. Jitihada nzuri za waangalizi wanyenyekevu zinaweza kuwasaidia sana wengine wawe waeneza-injili wenye bidii na wenye matokeo.—2 Petro 1:5-8.

Kutoa Ushahidi Nyumba kwa Nyumba

10. Kristo na wafuasi wake wa mapema waliweka kielelezo gani katika huduma?

10 Yesu Kristo aliwawekea wafuasi wake kielelezo kizuri cha kueneza injili. Neno la Mungu linasema hivi kuhusu huduma ya Kristo na mitume wake: ‘Alisafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu. Na wale kumi na wawili walikuwa pamoja naye.’ (Luka 8:1) Namna gani mitume wenyewe? Baada ya roho takatifu kumwagwa siku ya Pentekoste 33 W.K., “kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.”—Matendo 5:42.

11. Kulingana na Matendo 20:20, 21, mtume Paulo alifanya nini katika huduma yake?

11 Kwa kuwa mtume Paulo alieneza injili kwa bidii, angeweza kuwaambia hivi wazee Wakristo wa Efeso: “Sikuepuka kuwaambia ninyi lolote kati ya mambo yenye faida wala kuwafundisha ninyi hadharani na nyumba kwa nyumba.” Paulo alipokuwa ‘akifundisha nyumba kwa nyumba,’ je, alikuwa akitembelea nyumba za waabudu wenzake, akifanya ziara za uchungaji kwa walioamini? La, kwa kuwa anaendelea kueleza: “Nilitoa ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki pia juu ya toba kwa Mungu na imani katika Bwana wetu Yesu.” (Matendo 20:20, 21) Kwa ujumla wale ambao tayari wamejiweka wakfu kwa Yehova hawahitaji mafundisho juu ya “toba kwa Mungu na imani katika Bwana wetu Yesu.” Paulo aliwazoeza wazee Wakristo wa Efeso kufanya huduma ya nyumba kwa nyumba huku akiwafundisha wasioamini juu ya toba na imani. Kwa kufanya hivyo, Paulo aliiga njia ya kuhubiri iliyoanzishwa na Yesu.

12, 13. Kupatana na Wafilipi 1:7, watu wa Yehova wamefanya nini kuhusu haki yao ya kuhubiri?

12 Huduma ya nyumba kwa nyumba inaweza kuwa ngumu. Kwa mfano, watu wengine huudhika tunapowatembelea nyumbani kwao tukiwa na ujumbe wa Biblia. Nia yetu si kuwaudhi. Hata hivyo, huduma ya nyumba kwa nyumba inaungwa mkono na Maandiko, nasi huchochewa na upendo wetu kwa Mungu na kwa jirani kutoa ushahidi kwa njia hiyo. (Marko 12:28-31) Ili “kutetea na kuthibitisha kisheria” haki yetu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, tumepeleka kesi mahakamani, kutia ndani Mahakama Kuu ya Marekani. (Wafilipi 1:7) Katika maamuzi yake karibu yote, mahakama hiyo imetuunga mkono. Ufuatao ni mojawapo ya maamuzi hayo:

13 “Kugawanya trakti za kidini kwa mkono ni njia ya zamani sana iliyotumiwa na mishonari kueneza injili, nayo ilianza kutumiwa tangu mashini za kupiga chapa zibuniwe. Hiyo imekuwa njia yenye matokeo sana ambayo imetumiwa na dini mbalimbali kwa miaka mingi. Leo, njia hiyo ya kueneza injili inatumiwa kwa kiwango kikubwa na madhehebu mbalimbali ambayo wahudumu wake hutangaza Injili kwa kutembelea maelfu ya watu nyumbani kwao wakitafuta wafuasi. . . . Kulingana na Marekebisho ya Kwanza [ya Katiba ya Marekani], kazi hiyo ya kidini ina umuhimu sawa na ibada inayofanywa makanisani au mahubiri ya jukwaani.”—Murdock dhidi ya Pennsylvania, 1943.

Kwa Nini Tuendelee Kuhubiri?

14. Huduma yetu inaweza kuwavutiaje watu hatua kwa hatua?

14 Kuna sababu nyingi za kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kila mara tunapomtembelea mwenye nyumba sisi hujaribu kupanda mbegu ya ukweli wa Biblia. Tunapofanya ziara za kurudia, tunajaribu kuitia maji. Na mwenye nyumba anaweza kuvutiwa na ukweli huo hatua kwa hatua kwa kuwa Paulo aliandika: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji, lakini Mungu akaendelea kuikuza.” (1 Wakorintho 3:6) Kwa hiyo, na tuendelee ‘kupanda na kutia maji,’ tukiwa na hakika kwamba Yehova ‘ataikuza.’

15, 16. Kwa nini sisi huwatembelea watu nyumbani kwao tena na tena?

15 Tunafanya kazi ya kueneza injili kwa sababu maisha ya watu yamo hatarini. Kwa kuhubiri tunaweza kujiokoa wenyewe na wale wanaotusikiliza. (1 Timotheo 4:16) Kama tungejua kwamba maisha ya mtu fulani yamo hatarini, je, tungechukua hatua moja tu ya kizembe kumsaidia? Sivyo! Kwa kuwa wokovu unahusika, tunawatembelea watu nyumbani kwao tena na tena. Hali huendelea kubadilika. Huenda mtu ambaye pindi fulani alikuwa na shughuli nyingi sana asiweze kutusikiliza, akawa tayari kusikiliza ujumbe wa Biblia pindi nyingine. Mtu mwingine katika familia hiyo anaweza kutukaribisha, na hivyo tunaweza kuanzisha mazungumzo ya Biblia naye.

16 Hali na mtazamo wa wenye nyumba unaweza kubadilika. Kwa mfano, huenda maumivu yanayotokana na kufiwa na mpendwa yakamfanya mtu asikilize ujumbe wa Ufalme. Tunatumaini kumfariji mtu huyo, kumsaidia atambue uhitaji wake wa kiroho, na kumwonyesha jinsi uhitaji huo unavyoweza kutoshelezwa.—Mathayo 5:3, 4.

17. Ni ipi iliyo sababu kuu zaidi inayofanya tuhubiri?

17 Sababu kuu zaidi inayofanya tuhubiri nyumba kwa nyumba au tushiriki katika aina nyingine za huduma ya Kikristo ni ile tamaa ya kuwajulisha wengine jina la Yehova. (Kutoka 9:16; Zaburi 83:18) Inathawabisha kama nini wakati kazi yetu ya kueneza injili inapowasaidia wapendao kweli na uadilifu wawe wasifaji wa Yehova! Mtunga-zaburi aliimba: “Enyi vijana, nanyi mabikira pia, enyi wazee pamoja na wavulana. Na walisifu jina la Yehova, kwa maana jina lake peke yake liko juu sana lisiweze kufikiwa. Utukufu wake uko juu ya dunia na mbingu.”—Zaburi 148:12, 13.

Kueneza Injili Hutunufaisha Kibinafsi

18. Tunanufaikaje kwa kufanya kazi ya kueneza injili?

18 Kufanya kazi ya kueneza injili hutunufaisha kibinafsi katika njia mbalimbali. Kwenda nyumba kwa nyumba tukiwa na habari njema hutusaidia kusitawisha unyenyekevu, hasa tusipokaribishwa vizuri. Ili tuwe waeneza-injili wenye matokeo, tunahitaji kuwa kama Paulo, ambaye ‘alikuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote awaokoe wengine.’ (1 Wakorintho 9:19-23) Uzoefu katika huduma hutusaidia tuwe wenye busara. Kwa kumtegemea Yehova na kuchagua maneno yanayofaa, tunaweza kutumia shauri hili la Paulo: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.”—Wakolosai 4:6.

19. Roho takatifu huwasaidiaje waeneza-injili?

19 Kazi ya kueneza injili hutuchochea pia tutegemee roho takatifu ya Mungu. (Zekaria 4:6) Nayo matunda ya roho hiyo ambayo ni “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia” hudhihirika katika huduma yetu. (Wagalatia 5:22, 23) Kazi hiyo huathiri jinsi tunavyoshughulika na watu, kwa kuwa kutii mwongozo wa roho hiyo hutusaidia tuonyeshe upendo, tuwe wenye furaha na amani, wastahimilivu na wenye fadhili, tuonyeshe wema na imani, na kudhihirisha upole na kujizuia tunapotangaza habari njema.

20, 21. Ni zipi baadhi ya manufaa na baraka za kuendelea kueneza injili kwa bidii?

20 Baraka nyingine tunayopata tukiwa waeneza-injili ni kwamba tunakuwa wenye huruma zaidi. Watu wanapotutajia matatizo yao kama vile magonjwa, ukosefu wa kazi, matatizo ya nyumbani, hatutendi kama washauri, bali tunawatia moyo na kuwafariji kwa maandiko. Tunawajali watu waliopofushwa kiroho lakini ambao wanaonekana kuwa wanapenda uadilifu. (2 Wakorintho 4:4) Na ni baraka iliyoje kuwasaidia kiroho wale ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima’!—Matendo 13:48.

21 Kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kueneza injili hutusaidia kukazia fikira mambo ya kiroho. (Luka 11:34) Bila shaka, jambo hilo linanufaisha kwa kuwa tusipofanya hivyo, tunaweza kushindwa na majaribu ya kufuatia vitu vya kimwili ambayo ni mengi sana katika ulimwengu huu. Mtume Yohana aliwahimiza Wakristo hivi: “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu. Zaidi ya hayo, ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:15-17) Tukiendelea kuwa wenye bidii katika kueneza injili, huku tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, hatutaupenda ulimwengu.—1 Wakorintho 15:58.

Jiwekee Hazina Mbinguni

22, 23. (a) Ni hazina gani ambazo Wakristo waeneza-injili huweka? (b) Makala inayofuata itatusaidiaje?

22 Kuhubiri Ufalme kwa bidii huleta manufaa yenye kudumu. Yesu alionyesha hilo aliposema: “Acheni kujiwekea hazina duniani, ambako nondo na kutu hula, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni, ambako nondo na kutu havili, na ambako wezi hawavunji na kuiba. Kwa maana mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.”—Mathayo 6:19-21.

23 Na tuendelee kuweka hazina mbinguni, huku tukitambua kwamba pendeleo kuu zaidi ya yote ni kumwakilisha Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova, tukiwa Mashahidi wake. (Isaya 43:10-12) Tunapofanya kazi yetu tukiwa wahudumu wa Mungu, yaelekea tutahisi kama mwanamke mmoja Mkristo mwenye umri wa miaka 90 na kitu aliyesema hivi kuhusu utumishi wake wa muda mrefu kwa Mungu: “Ninamshukuru Yehova kwa kunivumilia kwa miaka hiyo yote, nami husali kwa bidii ili aendelee kuwa Baba yangu mwenye upendo milele.” Ikiwa sisi pia tunathamini uhusiano wetu pamoja na Mungu, bila shaka tutataka kufanya kazi ya kueneza injili kwa ukamili. Makala inayofuata itatusaidia kuona jinsi tunavyoweza kutimiza huduma yetu kwa ukamili.

Ungejibuje?

• Kwa nini tufanye kazi ya mweneza-injili?

• Unaweza kusema nini kuhusu kazi ya waeneza-injili wa zamani na wa sasa?

• Kwa nini tunatoa ushahidi nyumba kwa nyumba?

• Unanufaikaje kibinafsi kwa kufanya kazi ya mweneza-injili?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Leo kuna waeneza-injili wenye furaha kama Filipo na binti zake

[Picha katika ukurasa wa 14]

Unanufaikaje kibinafsi unapowaeleza wengine habari njema?