Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kutoka

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kutoka

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kutoka

KITABU cha Kutoka kinasimulia mambo ya hakika kuhusu kukombolewa kwa watu ‘waliotumikishwa chini ya uonevu.’ (Kutoka 1:13) Pia kina masimulizi yenye kusisimua kuhusu kuzaliwa kwa taifa fulani. Kati ya mambo yenye kuvutia zaidi ya kitabu hicho ni miujiza ya ajabu, utungaji wa sheria iliyo bora zaidi, na kujengwa kwa maskani. Kimsingi, hayo ndiyo mambo yanayozungumziwa katika kitabu cha Biblia cha Kutoka.

Kitabu cha Kutoka kilichoandikwa na Musa, nabii Mwebrania, kinasimulia mambo yaliyowapata Waisraeli kwa kipindi cha miaka zaidi ya 145—kuanzia mwaka wa 1657 K.W.K. wakati Yosefu alipokufa hadi kukamilishwa kwa maskani mwaka wa 1512 K.W.K. Hata hivyo, masimulizi hayo si historia tu, bali ni sehemu ya neno la Mungu, au ujumbe wake kwa wanadamu. Kwa hiyo, ‘yako hai nayo yana nguvu.’ (Waebrania 4:12) Hivyo, kitabu cha Kutoka ni muhimu sana kwetu.

‘MUNGU ALISIKIA KUUGUA KWAO’

(Kutoka 1:1–4:31)

Wazao wa Yakobo wanaoishi Misri wanaongezeka haraka sana hivi kwamba kwa amri ya mfalme wanateswa kwa kufanywa kuwa watumwa. Farao hata anatoa amri watoto wote wa kiume wa Israeli wauawe. Musa, mtoto mwenye umri wa miezi mitatu ambaye anachukuliwa na binti ya Farao awe mtoto wake, anaokoka mauaji hayo. Ingawa Musa analelewa katika nyumba ya mfalme, anapokuwa na umri wa miaka 40 anawaunga mkono watu wake na kumuua Mmisri. (Matendo 7:23, 24) Musa analazimika kukimbilia Midiani. Akiwa huko anaoa na kuwa mchungaji. Kwenye mti unaoteketea kimuujiza, Yehova amtuma Musa arudi Misri ili kuwaongoza Waisraeli watoke utumwani. Haruni, ndugu yake, achaguliwa kuwa msemaji wake.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3:1—Yethro alikuwa kuhani wa aina gani? Nyakati za wazee wa ukoo kichwa cha familia alikuwa pia kuhani wa familia yake. Yaonekana Yethro alikuwa kichwa cha kabila fulani la Wamidiani. Kwa kuwa Wamidiani walikuwa wazao wa Abrahamu kupitia Ketura, yaelekea walifahamu ibada ya Yehova.—Mwanzo 25:1, 2.

4:11—Ni katika maana gani Yehova ‘humfanya mtu awe bubu, kiziwi, na kipofu’? Ingawa wakati fulani Yehova amefanya watu fulani wawe vipofu na mabubu, yeye hawezi kulaumiwa kwa kila kisa cha ulemavu. (Mwanzo 19:11; Luka 1:20-22, 62-64) Mambo hayo husababishwa na dhambi tuliyorithi. (Ayubu 14:4; Waroma 5:12) Hata hivyo, kwa kuwa Mungu ameruhusu hali hiyo iendelee anaweza kusema kwamba yeye ndiye ‘huwafanya’ watu wawe mabubu, viziwi, na vipofu.

4:16—Musa ‘angetumikia akiwa Mungu’ kwa Haruni jinsi gani? Musa alikuwa mwakilishi wa Mungu. Hivyo, Musa akawa ‘kama Mungu’ kwa Haruni, aliyesema kwa kumwakilisha Musa.

Mambo Tunayojifunza:

1:7, 14. Yehova aliwategemeza watu wake walipokandamizwa huko Misri. Vivyo hivyo, yeye huwategemeza Mashahidi wake wa siku hizi, hata wanapokabili mateso makali.

1:17-21. Yehova hutukumbuka “kwa ajili ya wema.”—Nehemia 13:31.

3:7-10. Yehova husikiliza kilio cha watu wake.

3:14. Sikuzote Yehova hutimiza makusudi yake. Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatimiza matumaini yetu yanayotegemea Biblia.

4:10, 13. Musa alikosa uhakika sana katika uwezo wake wa kusema hivi kwamba hata baada ya Mungu kumhakikishia kwamba atamsaidia, Musa alimwomba amtume mtu mwingine akazungumze na Farao. Hata hivyo, Yehova alimtumia Musa naye akampa hekima na nguvu alizohitaji ili kutimiza mgawo wake. Badala ya kukazia fikira kupungukiwa kwetu, tunaweza kumtegemea Yehova na hivyo kutimiza kwa uaminifu kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

MIUJIZA YA AJABU YALETA UKOMBOZI

(Kutoka 5:1–15:21)

Musa na Haruni wanasimama mbele ya Farao, wakimwomba awaruhusu Waisraeli waende kumfanyia Yehova sherehe nyikani. Mtawala huyo wa Misri anakataa katakata. Yehova anamtumia Musa kuleta mapigo makali moja baada ya lingine. Ni baada tu ya pigo la kumi kwamba Farao anawaruhusu Waisraeli waondoke. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, Farao na jeshi lake wanawafuata mbio-mbio. Lakini Yehova anawafungulia watu wake njia katikati ya Bahari Nyekundu na kuwakomboa. Wamisri wanaowafuata wanakufa wakati maji ya bahari yanapowafunika.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

6:3—Ni katika njia gani Abrahamu, Isaka, na Yakobo hawakulijua jina la Mungu? Wazee hao wa ukoo walilitumia jina la Mungu na kupokea ahadi zake. Hata hivyo, hawakujua wala kujionea Yehova akitimiza ahadi hizo.—Mwanzo 12:1, 2; 15:7, 13-16; 26:24; 28:10-15.

7:1—Musa alifanywaje kuwa “Mungu kwa Farao”? Musa alipewa uwezo na mamlaka ya kimungu juu ya Farao. Hivyo, hakupaswa kumwogopa mfalme huyo.

7:22—Makuhani wa Misri walipata wapi maji ambayo hayakuwa yamegeuzwa kuwa damu? Huenda walitumia maji yaliyokuwa yamechotwa kwenye Mto Nile kabla ya pigo hilo. Pia yaonekana kwamba maji safi yangeweza kupatikana kwa kuchimba visima kwenye udongo wenye unyevunyevu kandokando ya Mto Nile.—Kutoka 7:24.

8:26, 27—Kwa nini Musa alisema kwamba dhabihu za Waisraeli zingekuwa “chukizo kwa Wamisri”? Wamisri waliabudu wanyama mbalimbali. Hivyo, kutajwa kwa dhabihu kulifanya ombi la Musa kwamba Waisraeli waruhusiwe kwenda kumtolea Yehova dhabihu, liwe halali na lenye kusadikisha zaidi.

12:29—Ni nani waliohesabiwa kuwa wazaliwa wa kwanza? Watoto wa kiume tu ndio waliohesabiwa kuwa wazaliwa wa kwanza. (Hesabu 3:40-51) Farao mwenyewe alikuwa mzaliwa wa kwanza lakini hakuuawa. Alikuwa na familia yake mwenyewe. Pigo la kumi liliua mzaliwa wa kwanza wa kiume bali si kichwa cha familia.

12:40—Waisraeli walikaa Misri kwa muda gani? Ile miaka 430 inayotajwa hapa inatia ndani wakati ambapo wana wa Israeli walikaa katika nchi ya Misri na katika nchi ya Kanaani. Abrahamu mwenye umri wa miaka 75 alivuka Mto Frati mwaka wa 1943 K.W.K. akielekea Kanaani. (Mwanzo 12:4) Kuanzia wakati huo hadi Yakobo mwenye umri wa miaka 130 alipoingia Misri, miaka 215 ilikuwa imepita. (Mwanzo 21:5; 25:26; 47:9) Hiyo inamaanisha kwamba baada ya hapo Waisraeli walikaa Misri kwa miaka mingine 215.

15:8—Je, maji ‘yaliyogandamana’ ya Bahari Nyekundu yalikuwa yameshikamana? Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa ‘gandamana’ humaanisha kunywea au kushikamana. Katika Ayubu 10:10 neno hilo linatumiwa kuhusiana na kuganda kwa maziwa. Hivyo, hiyo haimaanishi kwamba maji yaliyogandamana yalishikamana kama barafu. Kama “upepo wenye nguvu wa mashariki” unaotajwa katika Kutoka 14:21 ulikuwa baridi vya kutosha kugandisha maji, ni wazi kwamba baridi hiyo kali ingalitajwa. Kwa kuwa maji hayo hayakuwa yameshikiliwa na chochote, yalionekana kana kwamba yamegandamana au yameshikamana.

Mambo Tunayojifunza:

7:14–12:30. Yale Mapigo Kumi hayakutokea vivi hivi tu. Yalitabiriwa nayo yakatukia wakati barabara. Mapigo hayo kumi huonyesha wazi kwamba Muumba anaweza kudhibiti maji, nuru ya jua, wadudu, wanyama, na wanadamu! Mapigo hayo pia huonyesha kwamba Mungu anaweza kuwaangamiza maadui wake na wakati huohuo kuwalinda waabudu wake.

11:2; 12:36. Yehova huwabariki watu wake. Yaonekana alihakikisha kwamba Waisraeli sasa walipewa malipo kwa ajili ya kazi waliyofanya Misri. Waliingia Misri wakiwa watu huru, si kama mateka wa vita ambao walipaswa kutumikishwa.

14:30. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawakomboa waabudu wake kwenye “dhiki kuu” inayokuja.—Mathayo 24:20-22; Ufunuo 7:9, 14.

YEHOVA APANGA TAIFA LA KITHEOKRASI

(Kutoka 15:22–40:38)

Miezi mitatu baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri, wanapiga kambi chini ya Mlima Sinai. Wakiwa huko wanapokea Amri Kumi na sheria nyingine, wanafanya agano pamoja na Yehova, na wanakuwa taifa la kitheokrasi. Musa anakaa siku 40 mlimani na kupokea maagizo kuhusu ibada ya kweli na ujenzi wa maskani ya Yehova, yaani, hekalu lenye kubebeka. Wakati huohuo, Waisraeli wanatengeneza na kuabudu ndama ya dhahabu. Anaposhuka kutoka mlimani, Musa anaona hayo na kukasirika sana hivi kwamba anavunja yale mabamba mawili ya mawe aliyopewa na Mungu. Baada ya wakosaji kuadhibiwa ifaavyo, Musa anapanda tena mlimani na kupewa mabamba mengine mawili. Anaporudi, ujenzi wa maskani unaanza. Mwishoni mwa mwaka wa kwanza wa Waisraeli wakiwa huru, hema hilo zuri na vitu vyote vilivyomo ndani vinakamilishwa na kupangwa. Kisha Yehova analijaza utukufu wake.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

20:5—Yehova huletaje ‘adhabu kwa sababu ya kosa la akina baba’ juu ya vizazi vijavyo? Mtu anapofikia utu uzima, yeye huhukumiwa kulingana na mwenendo na mtazamo wake. Lakini taifa la Israeli na hata vizazi vya baadaye vilipatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya kuabudu sanamu. Hata Waisraeli waliokuwa waaminifu waliathiriwa katika maana ya kwamba haikuwa rahisi kwao kudumisha utimilifu katika taifa lililoasi imani.

23:19; 34:26—Amri ya kutotokosa mwana-mbuzi katika maziwa ya mama yake ilikuwa na maana gani? Ilisemekana kwamba wapagani walikuwa na desturi ya kumtokosa mwana-mbuzi (au mnyama mwingine mchanga) katika maziwa ya mama yake ili kupata mvua. Isitoshe, kwa kuwa maziwa ya mama ni ya kumlisha mtoto wake, kumtokosa kungekuwa tendo la ukatili. Sheria hiyo iliwasaidia watu wa Mungu wajue kwamba wanapaswa kuwa na huruma.

23:20-23—Ni malaika gani anayetajwa katika andiko hili, na ilikuwaje kwamba jina la Yehova lilikuwa “ndani yake”? Yaelekea, malaika huyo alikuwa Yesu kabla hajawa mwanadamu. Alitumiwa kuwaongoza Waisraeli wakiwa njiani kuelekea Nchi ya Ahadi. (1 Wakorintho 10:1-4) Jina la Yehova liko “ndani yake” katika maana ya kwamba Yesu ndiye mteteaji na mtakasaji mkuu zaidi wa jina la Baba yake.

32:1-8, 25-35—Kwa nini Haruni hakuadhibiwa kwa kutengeneza ndama ya dhahabu? Haruni hakukubaliana kabisa na ibada ya sanamu. Baadaye, yaonekana alijiunga na Walawi wenzake waliosimama upande wa Mungu dhidi ya wale waliompinga Musa. Baada ya wale waliokuwa na hatia kuuawa, Musa aliwakumbusha watu kwamba walikuwa wamefanya dhambi kubwa, akionyesha kwamba si Haruni peke yake aliyehurumiwa na Yehova.

33:11, 20—Mungu alizungumzaje na Musa “uso kwa uso?” Maneno hayo huonyesha mazungumzo ya kirafiki kati ya watu wawili. Musa alizungumza na mwakilishi wa Mungu na kupokea maagizo ya Yehova kupitia kwake. Lakini Musa hakumwona Yehova, kwa kuwa ‘hakuna mtu anayeweza kumwona Mungu na bado aishi.’ Kwa kweli, Yehova hakuzungumza na Musa kibinafsi. Sheria “ilipitishwa kupitia malaika kwa mkono wa mpatanishi,” lasema andiko la Wagalatia 3:19.

Mambo Tunayojifunza:

15:25; 16:12. Yehova huwatunza vizuri watu wake.

18:21. Wanaume wanaopewa madaraka katika kutaniko la Kikristo wanapaswa kuwa wenye uwezo, wenye kumwogopa Mungu, wenye kutegemeka, na wasio na ubinafsi.

20:1–23:33. Yehova ndiye Mpaji-Sheria mkuu zaidi. Waisraeli walipotii sheria zake, waliweza kumwabudu kwa utaratibu na kwa furaha. Yehova ana tengenezo la kitheokrasi leo. Tunaposhirikiana nalo tunapata furaha na usalama.

Kina Maana Sana Kwetu

Kitabu cha Kutoka hufunua nini kumhusu Yehova? Kinaonyesha kwamba yeye ni Mwandalizi mwenye upendo, Mkombozi asiye na kifani, na Mtimizaji wa ahadi zake. Yeye ni Mungu anayewapanga watu wake kitengenezo chini ya utawala wake.

Unapofanya usomaji wa Biblia wa kila juma ili kujitayarisha kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, bila shaka utachochewa sana na mambo unayojifunza katika kitabu cha Kutoka. Unapochunguza habari inayotajwa katika sehemu, “Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa,” utapata ufahamu zaidi kuhusu mistari fulani ya Biblia. Habari iliyo chini ya kichwa, “Mambo Tunayojifunza” itakuonyesha jinsi unavyoweza kunufaika na usomaji wa Biblia wa kila juma.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Yehova alimtuma Musa, aliyekuwa mtu mpole kuwaongoza Waisraeli kutoka utumwani

[Picha katika ukurasa wa 25]

Yale Mapigo Kumi yalionyesha kwamba Muumba anaweza kudhibiti maji, nuru ya jua, wadudu, wanyama, na wanadamu

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Kupitia Musa, Yehova aliwapanga Waisraeli kuwa taifa la kitheokrasi