Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni nini kilichotokea wakati wa kisa kinachozungumziwa katika Kutoka 4:24-26, na ni maisha ya nani yaliyokuwa hatarini?

Musa alikuwa safarini akielekea Misri pamoja na mke wake Sipora, na wana wake, Gershomu na Eliezeri, wakati kisa kifuatacho kilipotukia: “Ikawa kwamba walipokuwa barabarani, mahali pa kulala, Yehova akakutana naye, naye akawa akitafuta njia ya kumuua. Mwishowe Sipora akachukua jiwe gumu na kukata govi la mwanawe, akalifanya liguse miguu yake, na kusema: ‘Ni kwa sababu wewe ni bwana-arusi wa damu kwangu.’ Basi akamwachilia. Ndipo akasema: ‘Bwana-arusi wa damu,’ kwa sababu ya tohara.” (Kutoka 4:20, 24-26) Ingawa mistari hii haiko wazi kabisa na hatuwezi kuwa na hakika kuhusu maana yake, Maandiko hutoa ufafanuzi fulani kuhusu mistari hiyo.

Simulizi hilo halitaji waziwazi ni maisha ya nani yaliyokuwa hatarini. Hata hivyo, ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba si maisha ya Musa yaliyokuwa hatarini, kwa kuwa alikuwa tu amepokea mgawo kutoka kwa Mungu wa kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri. (Kutoka 3:10) Haielekei kwamba malaika wa Mungu angehatarisha maisha ya Musa akiwa njiani kwenda kutimiza mgawo huo. Kwa hiyo, ni maisha ya mmoja wa watoto wake yaliyokuwa hatarini. Sheria iliyotolewa mapema kwa Abrahamu kuhusu tohara ilisema: “Mwanamume ambaye hajatahiriwa, ambaye hatatahiri nyama ya govi lake, nafsi hiyo lazima ikatiliwe mbali kutoka kwa watu wake. Yeye amevunja agano langu.” (Mwanzo 17:14) Inaonekana Musa alikuwa amepuuza kumtahiri mwana wake, na hivyo malaika wa Yehova akatisha kumuua mvulana huyo.

Ni miguu ya nani iliyoguswa wakati Sipora alipokata govi la mwana wake ili kurekebisha mambo? Malaika wa Yehova ndiye aliyekuwa na uwezo wa kumuua mwana huyo ambaye hakuwa ametahiriwa. Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kwamba Sipora angegusa miguu ya malaika kwa govi hilo ili kumthibitishia kwamba alikuwa ametii agano hilo.

Maneno haya ya Sipora “wewe ni bwana-arusi wa damu kwangu” si ya kawaida. Yanaonyesha nini kumhusu Sipora? Kwa kukubaliana na matakwa ya agano la tohara, Sipora alikubali kuingia katika uhusiano wa agano pamoja na Yehova. Baadaye, agano la Sheria lililofanywa pamoja na Waisraeli lilionyesha kwamba katika uhusiano wa agano, Yehova anaweza kuonwa kuwa mume huku yule anayefanya agano naye akionwa kuwa mke. (Yeremia 31:32) Kwa hiyo, alipomtaja Yehova (kupitia malaika wake aliyemwakilisha) kuwa “bwana-arusi wa damu,” yaonekana Sipora alikuwa akikubali kutii matakwa ya agano hilo. Ilikuwa kana kwamba alikuwa amekubali kuwa mke katika agano la tohara, huku Yehova Mungu akiwa mume. Vyovyote vile, kwa sababu ya tendo lake muhimu la kutii takwa la Mungu, maisha ya mwana wake hayakuwa hatarini tena.