Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mlo wa Jioni wa Bwana Huadhimishwaje?

Mlo wa Jioni wa Bwana Huadhimishwaje?

Mlo wa Jioni wa Bwana Huadhimishwaje?

MTUME Mkristo Paulo anaandika hivi anapotoa ufafanuzi kuhusu kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana: “Nilipokea kutoka kwa Bwana kile nilichowapa ninyi pia, kwamba Bwana Yesu katika ule usiku aliokuwa akienda kutolewa alichukua mkate na, baada ya kutoa shukrani, akaumega na kusema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao ni kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’ Akafanya vivyo hivyo kuhusu kile kikombe pia, baada ya yeye kula mlo wa jioni, akisema: ‘Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu. Endeleeni kufanya hivi, kila mara mnapokinywa, kwa kunikumbuka mimi.’ Kwa maana kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki, mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapofika.”—1 Wakorintho 11:23-26.

Kama Paulo anavyosema, Yesu alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana “katika ule usiku [Yesu] aliokuwa akienda kutolewa” na Yuda Iskariote kwa viongozi wa dini ya Kiyahudi waliowalazimisha Waroma wamtundike Kristo. Mlo huo uliadhimishwa Alhamisi jioni, Machi 31, 33 W.K. Yesu alikufa kwenye mti wa mateso Ijumaa alasiri, Aprili 1. Kwa kuwa siku za kalenda ya Wayahudi zilianza jioni hadi jioni ya siku iliyofuata, Mlo wa jioni wa Bwana na kifo cha Yesu Kristo kilitukia siku hiyohiyo, yaani, Nisani 14, 33 W.K.

Wale ambao wangekula mkate na kunywa divai walipaswa ‘kuendelea kufanya hivyo’ kwa kumkumbuka Yesu. Kulingana na tafsiri ya Union Version, Yesu alisema: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” (1 Wakorintho 11:24) Mlo wa Jioni wa Bwana unaitwa pia Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

Kwa Nini Tukumbuke Kifo cha Yesu?

Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza umuhimu wa kifo hicho. Yesu alikufa akiwa mteteaji mkuu wa enzi kuu ya Yehova. Hivyo, aliyathibitisha madai ya Shetani kwamba wanadamu humtumikia Mungu kwa sababu za kibinafsi kuwa ya uwongo. (Ayubu 2:1-5; Methali 27:11) Kupitia kifo chake akiwa mwanadamu mkamilifu, Yesu pia ‘alitoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Adamu alipotenda dhambi dhidi ya Mungu alipoteza uhai mkamilifu wa kibinadamu na tumaini la kuishi milele. Lakini “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Naam, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 6:23.

Kwa hiyo, kifo cha Yesu Kristo kinahusisha maonyesho mawili makuu zaidi ya upendo, yaani, ule upendo mwingi ambao Yehova aliwaonyesha wanadamu kwa kumtoa Mwana wake na ule wa kujidhabihu ambao Yesu aliwaonyesha wanadamu kwa kutoa uhai wake wa kibinadamu kwa hiari. Ukumbusho wa kifo cha Yesu hukazia maonyesho hayo mawili ya upendo. Kwa kuwa sisi ndio tunaonufaika na upendo huo, tunapaswa kushukuru. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuhudhuria mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana.

Maana ya Mkate na Divai

Alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana, Yesu alitumia mkate na kikombe cha divai kuwa mifano. Aliuchukua mkate, na “baada ya kutoa shukrani, akaumega na kusema: ‘Huu [mkate] unamaanisha mwili wangu ambao ni kwa ajili yenu.’” (1 Wakorintho 11:24) Ilibidi mkate huo umegwe ili ugawanywe na kuliwa, nao ulivunjika kwa urahisi kwa kuwa ulitengenezwa kwa unga na maji, bila chachu. Katika Maandiko, chachu hufananisha dhambi. (Mathayo 16:11, 12; 1 Wakorintho 5:6, 7) Yesu hakuwa na dhambi. Kwa hiyo, mwili wake mkamilifu wa kibinadamu ulifaa kuwa dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya wanadamu. (1 Yohana 2:1, 2) Inafaa kama nini kwamba mkate unaotumiwa kuwakilisha mwili wa Kristo usio na dhambi uwe bila chachu!

Pia Yesu alitoa shukrani kwa ajili ya kikombe cha divai nyekundu isiyo na vikolezo na kusema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu.” (1 Wakorintho 11:25) Divai nyekundu katika kikombe huwakilisha damu ya Yesu. Kama vile damu ya ng’ombe-dume na mbuzi waliotolewa dhabihu ilivyohalalisha agano la Sheria kati ya Mungu na taifa la Israeli mwaka wa 1513 K.W.K., ndivyo damu ya Yesu iliyomwagwa alipokufa ilivyohalalisha agano jipya.

Ni Nani Wanaopaswa Kula na Kunywa?

Ili kuwatambua wale wanaostahili kula na kunywa mifano ya Ukumbusho, tunahitaji kuelewa agano jipya ni nini na ni nani walio katika agano hilo. Biblia inasema: “‘Tazama! Siku zinakuja,’ asema Yehova, ‘nami nitafanya agano jipya pamoja na nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda . . . Nitaitia sheria yangu ndani yao, nami nitaiandika katika moyo wao. Nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. . . . Nitalisamehe kosa lao, na dhambi yao sitaikumbuka tena.’”—Yeremia 31:31-34.

Agano jipya huwawezesha wanadamu fulani wawe na uhusiano wa pekee pamoja na Yehova Mungu. Kupitia agano hilo, kikundi fulani cha watu huwa watu wake naye Yehova huwa Mungu wao. Sheria ya Yehova huandikwa ndani yao, katika mioyo yao, na hata wale ambao si Wayahudi waliotahiriwa wanaweza kuwa na uhusiano huo pamoja na Mungu kupitia agano jipya. (Waroma 2:29) Luka, mwandikaji wa Biblia, anaandika kuhusu kusudi la Mungu la ‘kuelekeza uangalifu Wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 15:14) Kulingana na 1 Petro 2:10, ‘wakati mmoja wao walikuwa si watu, lakini sasa wao ni watu wa Mungu.’ Biblia huwaita “Israeli wa Mungu,” yaani, Israeli wa kiroho. (Wagalatia 6:16; 2 Wakorintho 1:21) Kwa hiyo, agano jipya ni agano kati ya Yehova Mungu na Israeli wa kiroho.

Jioni ya mwisho akiwa pamoja na wanafunzi wake, Yesu mwenyewe pia alifanya agano lingine pamoja nao. Aliwaambia, “Nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:29) Hilo ni agano la Ufalme. Hesabu ya wanadamu wasio wakamilifu ambao wako katika agano la Ufalme ni 144,000. Baada ya kufufuliwa na kwenda mbinguni, watatawala pamoja na Kristo wakiwa wafalme na makuhani. (Ufunuo 5:9, 10; 14:1-4) Kwa hiyo, wale walio katika agano jipya pamoja na Yehova Mungu wako pia katika agano la Ufalme pamoja na Yesu Kristo. Wao tu ndio wanaostahili kula na kunywa mifano ya Mlo wa Jioni wa Bwana.

Wale wanaostahili kula na kunywa mifano ya Ukumbusho wanajuaje kwamba wana uhusiano wa pekee pamoja na Mungu na kwamba ni warithi pamoja na Kristo? Paulo anaeleza: “Roho [takatifu] yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu [mtazamo wetu wa akili] kwamba sisi ni watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi ni watoto, sisi pia ni warithi: warithi wa Mungu kwelikweli, lakini warithi pamoja na Kristo, mradi tu tunateseka pamoja ili pia tutukuzwe pamoja.”—Waroma 8:16, 17.

Kupitia roho yake takatifu, au nguvu ya utendaji, Mungu huwatia mafuta wale watakaokuwa warithi pamoja na Kristo. Hilo huwahakikishia kwamba wao ni warithi wa Ufalme. Roho takatifu huwapa Wakristo waliotiwa mafuta tumaini la kuishi mbinguni. Wao huona mambo yote ambayo Biblia husema kuhusu maisha ya kimbingu kuwa yanawahusu. Isitoshe, wako tayari kudhabihu chochote kinachohusiana na maisha ya kidunia, kutia ndani uhai duniani, na pia uhusiano wote wa kibinadamu. Ingawa Wakristo watiwa-mafuta wanatambua kwamba maisha katika Paradiso ya kidunia yatakuwa mazuri, hilo si tumaini lao. (Luka 23:43) Kwa kuwa tumaini lao thabiti la kwenda mbinguni linategemea utendaji wa roho ya Mungu wala si maoni ya uwongo ya kidini, kwa kufaa Wakristo hao hula na kunywa mifano ya Ukumbusho.

Namna gani ikiwa mtu hana uhakika kabisa kwamba yuko katika agano jipya na pia agano la Ufalme? Namna gani ikiwa roho ya Mungu haitoi ushahidi kwamba yeye ni mrithi pamoja na Kristo? Basi atakuwa amekosea kula na kunywa mifano ya Ukumbusho. Kwa kweli, Mungu hatafurahi ikiwa mtu atajifanya kimakusudi kuwa ana mwito wa kwenda mbinguni akawe mfalme na kuhani, huku akijua kabisa kwamba hakupokea mwito huo.—Waroma 9:16; Ufunuo 22:5.

Tunapaswa Kuuadhimisha Mara Ngapi?

Je, kifo cha Yesu kinapaswa kukumbukwa kila juma au labda kila siku? Kristo alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana na kuuawa isivyo haki siku ya Pasaka. Pasaka hiyo iliadhimishwa mara moja tu kila mwaka, mnamo Nisani 14, nayo iliwakumbusha Waisraeli kukombolewa kwao kutoka utumwani Misri. (Kutoka 12:6, 14; Mambo ya Walawi 23:5) Kwa hiyo, kifo cha “Kristo pasaka yetu” kinapaswa kukumbukwa mara moja tu kila mwaka, si kila juma au kila siku. (1 Wakorintho 5:7) Wakristo wanapoadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana, wao hufuata utaratibu uleule ambao Yesu alifuata alipoanzisha mlo huo.

Hivyo basi, maneno haya ya Paulo yanamaanisha nini: “Kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki, mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapofika”? (1 Wakorintho 11:26) Katika andiko hilo Paulo alitumia neno linalomaanisha “kila wakati ambapo,” au “wakati wowote ambapo.” Hivyo, alikuwa akisema kwamba wakati wowote ambapo Wakristo watiwa-mafuta wangekula na kunywa mifano, wangekuwa wakitangaza imani yao katika dhabihu ya fidia ya Yesu.

Wakristo watiwa-mafuta wangeendelea kukumbuka kifo cha Kristo “mpaka atakapofika.” Mwadhimisho huo ungeendelea hadi wakati ambapo Yesu angekuja kuwapokea wafuasi wake watiwa-mafuta waingie mbinguni kwa kuwafufua wawe viumbe wa roho wakati wa “kuwapo” kwake. (1 Wathesalonike 4:14-17) Hilo lapatana na maneno haya ya Kristo kwa mitume wake waaminifu 11: “Nikienda na kuwatayarishia ninyi mahali, nitakuja tena nami nitawapokea ninyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo.”—Yohana 14:3.

Mlo Huo Una Maana Gani Kwako?

Je, ni lazima kula na kunywa mifano ya Ukumbusho ili kunufaika na dhabihu ya Yesu na kupokea uzima wa milele duniani? La. Biblia haidokezi popote kwamba baada ya kufufuliwa duniani, watu wenye kumwogopa Mungu kama vile Noa, Abrahamu, Sara, Isaka, Rebeka, Yosefu, Musa, na Daudi watakula na kunywa mifano hiyo. Hata hivyo, itawabidi wao pamoja na wote wanaotamani kuishi milele duniani waonyeshe imani katika Mungu na Kristo na katika uandalizi wa Yehova wa dhabihu ya fidia ya Yesu. (Yohana 3:36; 14:1) Ili kupata uzima wa milele, lazima wewe pia uonyeshe imani kama hiyo. Kuhudhuria mwadhimisho wa kifo cha Kristo kutakukumbusha dhabihu hiyo kubwa na kunapaswa kufanya uwe mwenye shukrani zaidi kwa dhabihu hiyo.

Mtume Yohana alikazia umuhimu wa dhabihu ya Yesu aliposema: “Ninawaandikia ninyi [watiwa-mafuta wenzangu] mambo haya ili msitende dhambi. Na bado, yeyote akitenda dhambi, tuna msaidizi kwa Baba, Yesu Kristo, mtu mwadilifu. Na yeye ni dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:1, 2) Watiwa-mafuta wanaweza kusema kwamba dhabihu ya Yesu ni upatanisho kwa ajili ya dhambi zao. Lakini dhabihu hiyo pia ni kwa ajili ya dhambi za ulimwengu wote, nayo huwawezesha wanadamu watiifu wapate uzima wa milele!

Je, utahudhuria ukumbusho wa kifo cha Yesu, Aprili 4, 2004? Ukumbusho huo utaadhimishwa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova katika mahali pao pa kukutania. Ukihudhuria, utanufaika kwa kusikiliza hotuba muhimu sana ya Biblia. Utakumbushwa mambo mengi sana ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wametufanyia. Pia utanufaika kiroho kukutanika pamoja na wale ambao wana heshima kubwa kwa Mungu na Kristo na kwa dhabihu ya fidia ya Yesu. Huenda tukio hilo likaimarisha tamaa yako ya kupokea fadhili zisizostahiliwa za Mungu, ambazo huongoza kwenye uzima wa milele. Usiruhusu chochote kikuzuie. Hudhuria mwadhimisho huo wenye kuchangamsha moyo, ambao humletea heshima na kumfurahisha Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kifo cha Yesu kinahusisha maonyesho mawili makuu zaidi ya upendo

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mkate usiotiwa chachu na divai ni mifano inayofaa ya mwili wa Yesu usio na dhambi, na damu yake iliyomwagwa