Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Timiza kwa Ukamili Huduma Yako”

“Timiza kwa Ukamili Huduma Yako”

“Timiza kwa Ukamili Huduma Yako”

“Timiza kwa ukamili huduma yako.”—2 TIMOTHEO 4:5.

1, 2. Ingawa Wakristo wote ni waeneza-injili, wazee wanapaswa kutimiza matakwa gani kulingana na Biblia?

JE, WEWE ni mtangazaji wa Ufalme? Ikiwa ndivyo, mshukuru Yehova Mungu kwa pendeleo hilo zuri. Je, wewe ni mzee katika kutaniko? Hilo ni pendeleo lingine kutoka kwa Yehova. Lakini hatupaswi kusahau kamwe kwamba elimu au uwezo wa kusema kwa ufasaha hautustahilishi kuwa wahudumu au waangalizi kutanikoni. Yehova hutustahilisha vya kutosha kwa ajili ya huduma, na wanaume fulani kati yetu wana pendeleo la kutumika wakiwa waangalizi kwa sababu wametimiza viwango hususa vya Biblia.—2 Wakorintho 3:5, 6; 1 Timotheo 3:1-7.

2 Wakristo wote waliojiweka wakfu hufanya kazi ya kueneza injili, lakini waangalizi, au wazee hasa, wanahitaji kuweka kielelezo kizuri katika huduma. Wazee “wanaofanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha” wanatambuliwa na Mungu na Kristo, na pia Mashahidi wenzao. (1 Timotheo 5:17; Waefeso 5:23; Waebrania 6:10-12) Vyovyote vile, mafundisho ya mzee yanapaswa kuwa yenye kujenga kiroho, kwa kuwa mtume Paulo alimwambia hivi mwangalizi Timotheo: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe; nao watageuza masikio yao kutoka kwenye kweli, nao watageuzwa kando kufuata hadithi za uwongo. Ingawa hivyo, wewe tunza akili zako katika mambo yote, vumilia uovu, fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.”—2 Timotheo 4:3-5.

3. Ni nini kinachohitaji kufanywa ili mafundisho ya uwongo yasihatarishe hali ya kiroho ya kutaniko?

3 Ili kuhakikisha kwamba mafundisho ya uwongo hayahatarishi hali ya kiroho ya kutaniko, mwangalizi anapaswa kutii shauri hili la Paulo: “Tunza akili zako katika mambo yote, . . . timiza kwa ukamili huduma yako.” (2 Timotheo 4:5) Naam, mzee anastahili ‘kutimiza kwa ukamili huduma yake.’ Anapaswa kuitimiza kikamili kabisa. Mzee anayetimiza huduma yake kikamili hushughulikia ifaavyo madaraka yake yote, bila kupuuza daraka lolote au kutolishughulikia kikamili. Mtu kama huyo ni mwaminifu hata katika mambo madogo.—Luka 12:48; 16:10.

4. Ni nini kinachoweza kutusaidia kutimiza huduma yetu kwa ukamili?

4 Ili kutimiza huduma yetu kikamili sikuzote haimaanishi kwamba utumie wakati zaidi, bali uutumie vizuri. Wakristo wote wanaweza kutimiza mengi katika huduma wakifanya mambo kwa usawaziko na kwa ukawaida. Ili mzee atumie wakati mwingi zaidi kwa ajili ya utumishi wa shambani, anahitaji kupanga mambo yake vizuri ili ratiba yake iwe na usawaziko na ajue mambo atakayowapa wengine wafanye na kuwaonyesha jinsi ya kuyafanya. (Waebrania 13:17) Kwa kawaida, mzee anayeheshimiwa pia hutimiza daraka lake, kama Nehemia, ambaye alishiriki kibinafsi katika ujenzi wa kuta za Yerusalemu. (Nehemia 5:16) Nao watumishi wote wa Yehova wanapaswa kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri Ufalme.—1 Wakorintho 9:16-18.

5. Tunapaswa kuionaje huduma yetu?

5 Tuna kazi yenye shangwe kama nini ya kutangaza Ufalme wa kimbingu uliosimamishwa! Bila shaka, tunathamini pendeleo la kushiriki katika kuhubiri habari njema katika dunia yote inayokaliwa kabla ya mwisho kuja. (Mathayo 24:14) Ingawa sisi si wakamilifu, tunaweza kutiwa moyo na maneno haya ya Paulo: “Sisi tuna hazina hii [ya huduma] katika vyombo vya udongo, ili nguvu zinazopita zile za kawaida ziwe za Mungu na si zile za kutoka ndani yetu wenyewe.” (2 Wakorintho 4:7) Naam, tunaweza kutumikia kwa njia inayokubalika, lakini kwa nguvu na hekima kutoka kwa Mungu tu.—1 Wakorintho 1:26-31.

Kutoa Mrudisho wa Utukufu wa Mungu

6. Kulikuwa na tofauti gani kati ya Israeli wa asili na wa kiroho?

6 Akirejelea Wakristo watiwa-mafuta, Paulo anasema kwamba Mungu “ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu wa agano jipya.” Mtume huyo anatofautisha agano jipya lililofanywa pamoja na Israeli wa kiroho kupitia Yesu Kristo na agano la Sheria la kale lililofanywa pamoja na Waisraeli wa asili kupitia Musa. Paulo anaongeza kusema kwamba Musa aliposhuka kutoka Mlima Sinai akiwa na mabamba ya mawe yaliyokuwa na zile Amri Kumi, uso wake uling’aa sana hivi kwamba Waisraeli hawangeweza kumkazia macho. Lakini baada ya muda, jambo fulani zito zaidi lilitokea kwa sababu “nguvu zao za akili zilitiwa uzito” na mioyo yao ikafunikwa na utaji. Hata hivyo, mtu anapojitoa kwa Yehova kwa moyo wote, utaji huo huondolewa. Akirejelea tena huduma ambayo wale walio katika agano jipya walipewa, Paulo anasema: ‘Sisi sote, tunatoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova tukiwa na nyuso zisizo na utaji.’ (2 Wakorintho 3:6-8, 14-18; Kutoka 34:29-35) Leo “kondoo wengine” wa Yesu pia wana pendeleo la kutoa kama kioo mrudisho wa utukufu wa Yehova.—Yohana 10:16.

7. Wanadamu wanawezaje kurudisha kama kioo utukufu wa Mungu?

7 Wanadamu wenye dhambi wanawezaje kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, ingawa hakuna mtu anayeweza kuona uso wake na kuishi? (Kutoka 33:20) Tunapaswa kutambua kwamba Yehova mwenyewe ana utukufu na pia ana kusudi tukufu la kutetea enzi yake kupitia Ufalme wake. Kweli zinazohusu Ufalme huo ni sehemu ya “mambo makuu ya Mungu” yaliyoanza kutangazwa na wale waliomwagiwa roho takatifu siku ya Pentekoste 33 W.K. (Matendo 2:11) Kwa mwongozo wa roho hiyo, wangeweza kutimiza kwa ukamili huduma waliyopewa.—Matendo 1:8.

8. Paulo aliazimia kufanya nini kuhusiana na huduma?

8 Paulo aliazimia kutozuiwa na chochote kutimiza huduma yake kwa ukamili. Aliandika hivi: “Kwa kuwa sisi tuna huduma hii kulingana na rehema tuliyoonyeshwa, hatufi moyo; bali tumeyakataa mambo ya kichinichini ambayo ni ya kuonea aibu, si kutembea kwa ujanja, wala kulichanganya na kitu neno la Mungu, bali kwa kufanya kweli iwe wazi tukijipendekeza kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu.” (2 Wakorintho 4:1, 2) Kupitia ile ambayo Paulo anaita “huduma hii,” ukweli hudhihirika nayo nuru ya kiroho huenezwa.

9, 10. Inawezekanaje kurudisha kama kioo utukufu wa Yehova?

9 Paulo anaandika hivi kuhusu Chanzo cha nuru halisi na ya kiroho: “Mungu ndiye aliyesema: ‘Nuru na iangaze kutoka katika giza,’ naye ameangaza juu ya mioyo yetu ili kuimulika kwa ujuzi wenye utukufu juu ya Mungu kwa uso wa Kristo.” (2 Wakorintho 4:6; Mwanzo 1:2-5) Kwa kuwa tumepewa pendeleo lisilo na kifani la kuwa wahudumu wa Mungu, na tudumishe usafi ili tukiwa kama vioo turudishe utukufu wa Yehova.

10 Watu walio katika giza la kiroho hawawezi kuona utukufu wa Yehova au mrudisho wa utukufu huo kupitia Yesu Kristo, yule Musa Mkuu. Lakini tukiwa watumishi wa Yehova, tunapokea nuru tukufu kutoka katika Maandiko na kuiangazia wengine. Ili wale walio katika giza la kiroho sasa wasiharibiwe, wanahitaji nuru kutoka kwa Mungu. Kwa hiyo, tukiwa na shangwe na bidii, tunatii amri ya Yehova ya kuangaza nuru gizani kwa utukufu wake.

Nuru Yenu na Iangaze Kwenye Mafunzo ya Biblia ya Nyumbani

11. Yesu alisema nini kuhusu kuangaza nuru yetu, na ni ipi njia moja ya kufanya hivyo katika huduma yetu?

11 Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu. Jiji haliwezi kufichwa likiwa limesimama juu ya mlima. Watu huwasha taa na kuiweka, si chini ya kikapu cha kupimia, bali juu ya kinara cha taa, nayo huangazia watu wote waliomo ndani ya nyumba. Vivyo hivyo acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:14-16) Mwenendo wetu mzuri unaweza kufanya wengine wamtukuze Mungu. (1 Petro 2:12) Njia mbalimbali tunazotumia kueneza Injili hutupa nafasi nyingi za kuangaza nuru yetu. Mojawapo ya makusudi yetu mkuu ni kuangaza nuru ya kiroho kutoka katika Neno la Mungu kwa kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye matokeo. Hii ni njia muhimu sana ya kutimiza huduma yetu kwa ukamili. Ni madokezo gani yanayoweza kutusaidia kuongoza mafunzo ya Biblia yanayogusa mioyo ya watu wanaotafuta kweli?

12. Sala inahusianaje na kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani?

12 Kusali kwa Yehova kuhusu jambo hilo huonyesha tamaa yetu kubwa ya kuongoza mafunzo ya Biblia. Pia sala huonyesha tunaona umuhimu wa kuwasaidia wengine wamjue Mungu. (Ezekieli 33:7-9) Bila shaka, Yehova atajibu sala zetu naye atabariki jitihada zetu nyingi katika huduma. (1 Yohana 5:14, 15) Lakini hatusali ili kupata tu mtu wa kujifunza naye Biblia nyumbani. Baada ya kuanzisha funzo, kusali na kutafakari kuhusu mahitaji hususa ya mwanafunzi huyo kutatusaidia kuongoza funzo kwa njia yenye matokeo kila pindi.—Waroma 12:12.

13. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye matokeo?

13 Ili kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye matokeo, ni lazima tujitayarishe vizuri kwa ajili ya kila kipindi cha kujifunza. Tukihisi kana kwamba hatustahili, huenda ikafaa kutazama jinsi mwangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko anavyoongoza funzo la kila juma. Pindi kwa pindi, tunaweza kuandamana na wahubiri wa Ufalme ambao wamepata matokeo mazuri katika kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani. Bila shaka, tunapaswa kufikiria hasa mtazamo na njia za kufundisha za Yesu Kristo.

14. Tunawezaje kuufikia moyo wa mwanafunzi wa Biblia?

14 Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya Baba yake wa mbinguni na kuzungumza na wengine kumhusu Mungu. (Zaburi 40:8) Alikuwa mwenye tabia-pole naye alifanikiwa kuifikia mioyo ya wale waliomsikiliza. (Mathayo 11:28-30) Kwa hiyo, na tujitahidi kufikia mioyo ya wanafunzi wetu wa Biblia. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kujitayarisha kwa ajili ya kila funzo tukifikiria hali hususa za mwanafunzi. Kwa mfano, ikiwa anatoka katika jamii isiyoamini Biblia, huenda ikatubidi kumsadikisha kwamba Biblia ni ya kweli. Basi ni wazi kwamba tutalazimika kusoma maandiko mengi na kuyaeleza.

Wasaidie Wanafunzi Waelewe Mifano

15, 16. (a) Tunawezaje kumsaidia mwanafunzi ambaye haelewi mfano fulani unaotumiwa katika Biblia? (b) Tunaweza kufanya nini ikiwa mojawapo ya vichapo vyetu vinatumia mfano ambao ni mgumu kwa mwanafunzi fulani wa Biblia kuuelewa?

15 Huenda mwanafunzi wa Biblia asielewe mfano fulani uliotumiwa katika Maandiko. Kwa mfano, huenda asielewe Yesu alimaanisha nini aliposema kuhusu kuweka taa kwenye kinara cha taa. (Marko 4:21, 22) Yesu alikuwa akirejelea taa ya mafuta ya zamani yenye utambi. Taa hiyo iliwekwa kwenye kinara cha pekee na hivyo nuru yake ingeweza kuangaza sehemu fulani ya nyumba. Ili kufafanua mfano huo wa Yesu, huenda ikakubidi kufanya utafiti kuhusu habari iliyo chini ya kichwa “Lamp” (Taa) na “Lampstand” (Kinara cha Taa) katika kitabu kama vile Insight on the Scriptures. * Lakini inathawabisha kama nini unapoenda kwenye funzo la Biblia ukiwa na ufafanuzi ambao mwanafunzi wa Biblia atauelewa na kuufurahia!

16 Huenda kitabu cha kujifunzia Biblia kikatumia mfano mgumu kwa mwanafunzi fulani kuuelewa. Tumia wakati kufafanua mfano huo, au tumia mfano mwingine unaokazia jambo hilohilo. Labda kichapo fulani kinakazia kwamba ni muhimu kuwa na mwenzi mzuri na ushirikiano katika ndoa. Kwa mfano, huenda kitabu kikataja mtu anayebembea kwenye bembea, kisha anajiachilia, huku akitarajia mwenzake amshike. Badala ya kutumia mfano huo, uhitaji wa kuwa na ushirikiano na mwenzi mzuri unaweza kulinganishwa na watu wanaoshirikiana kwa kupokezana makatoni wanapopakua mashua.

17. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Yesu kuhusu mifano?

17 Ili kutumia mfano tofauti, huenda tukahitaji kujitayarisha kimbele. Hata hivyo, hiyo ni njia ya kuonyesha kwamba tunapendezwa kibinafsi na mwanafunzi wa Biblia. Yesu alitumia mifano rahisi ili kuelewesha habari ngumu. Tunapata mifano hiyo katika Mahubiri yake ya Mlimani, nayo Biblia inaonyesha kwamba mafundisho yake yalikuwa na matokeo mazuri kwa wasikilizaji wake. (Mathayo 5:1–7:29) Yesu alieleza mambo kwa subira kwa sababu alipendezwa sana na wengine.—Mathayo 16:5-12.

18. Ni nini linalopendekezwa kuhusu maandiko yaliyoonyeshwa katika vichapo vyetu?

18 Kupendezwa na wengine kutatuchochea ‘kujadiliana nao kwa kutumia Maandiko.’ (Matendo 17:2, 3) Ili kufanya hivyo tunahitaji kujifunza kwa unyoofu na kwa sala huku tukitumia kwa hekima vichapo vinavyoandaliwa na “msimamizi-nyumba mwaminifu.” (Luka 12:42-44) Kwa mfano, kitabu kama Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele kinanukuu maandiko mengi. * Kwa sababu hakuna nafasi ya kutosha, baadhi ya maandiko hayo yameonyeshwa tu. Wakati wa funzo la Biblia, ni muhimu kusoma na kueleza angalau baadhi ya maandiko hayo yaliyoonyeshwa. Kwani, mafundisho yetu yanategemea Neno la Mungu, nalo lina nguvu nyingi. (Waebrania 4:12) Itumie Biblia sana kila mnapojifunza, mkisoma mengi ya maandiko yaliyoonyeshwa katika mafungu. Msaidie mwanafunzi aone yale ambayo Biblia husema kuhusu habari au mwenendo fulani. Jitahidi kumwonyesha jinsi atakavyonufaika kwa kumtii Mungu.—Isaya 48:17, 18.

Uliza Maswali Yanayochochea Fikira

19, 20. (a) Kwa nini tutumie maswali ya maoni tunapoongoza funzo la Biblia la nyumbani? (b) Tunaweza kufanya nini ikiwa tunahitaji kuchunguza zaidi habari fulani?

19 Yesu alitumia maswali kwa ustadi ili kuwasaidia watu wafikiri. (Mathayo 17:24-27) Tukiuliza maswali ya maoni yasiyomwaibisha mwanafunzi wa Biblia, huenda majibu yake yakafunua jinsi anavyofikiri kuhusu habari fulani. Huenda tukaona kwamba bado anaamini mambo fulani yasiyopatana na maandiko. Kwa mfano, labda anaamini Utatu. Sura ya tatu ya kitabu Ujuzi inasema kwamba neno “Utatu” halipatikani katika Biblia. Kitabu hicho hunukuu na kutaja maandiko yanayoonyesha kwamba Yehova ni tofauti na Yesu na kwamba roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu, wala si mtu. Huenda ikatosha tu kusoma na kuzungumzia maandiko hayo ya Biblia. Lakini namna gani ikiwa maelezo zaidi yanahitajiwa? Labda baada ya funzo litakalofuata, tunaweza kutumia wakati kuzungumzia habari hiyo kama inavyofafanuliwa na kichapo kingine cha Mashahidi wa Yehova kama vile broshua Je! Uamini Utatu? Baada ya hapo, tunaweza kuendelea na funzo tukitumia kitabu Ujuzi.

20 Namna gani mwanafunzi akijibu swali la maoni kwa njia inayoshangaza au hata inayokatisha tamaa? Iwapo kuvuta sigara au habari nyingine yenye kugusa hisia inahusika, huenda tukapendekeza tuendelee na funzo kisha tuzungumzie jambo hilo baadaye. Tunapojua kwamba mwanafunzi huyo bado anavuta sigara tunaweza kutafuta habari katika vichapo vyetu inayoweza kumsaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Tunapojitahidi kufikia moyo wa mwanafunzi, tunaweza kusali kwa Yehova amsaidie kukua kiroho.

21. Ni nini kinachoweza kutokea tukibadili njia zetu za kufundisha ili zifaane na mahitaji hususa ya mwanafunzi wa Biblia?

21 Kwa kujitayarisha vizuri na kwa msaada wa Yehova, bila shaka tutaweza kubadili njia zetu za kufundisha ili zifaane na mahitaji hususa ya mwanafunzi wa Biblia. Kadiri muda unavyosonga, tunaweza kumsaidia asitawishe upendo kwa Mungu. Huenda pia tukafaulu kumsaidia aliheshimu na kulithamini tengenezo la Yehova. Inaridhisha kama nini mwanafunzi wa Biblia atakapokiri kwamba ‘Kwa kweli Mungu yupo katikati yetu’! (1 Wakorintho 14:24, 25) Kwa hiyo, na tuongoze mafunzo ya Biblia yenye matokeo na kufanya yote tuwezayo kuwasaidia wengine wawe wanafunzi wa Yesu.

Hazina Inayopaswa Kuthaminiwa

22, 23. Ni nini kinachohitajiwa ili tutimize huduma yetu kwa ukamili?

22 Ili kutimiza huduma yetu kwa ukamili, ni lazima tutegemee nguvu kutoka kwa Mungu. Akirejelea huduma, Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake waliotiwa mafuta: “Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu zinazopita zile za kawaida ziwe za Mungu na si zile za kutoka ndani yetu wenyewe.”—2 Wakorintho 4:7.

23 Tuwe watiwa-mafuta au “kondoo wengine,” sisi ni kama vyombo vya udongo vilivyo dhaifu. (Yohana 10:16) Hata hivyo, Yehova anaweza kutupatia nguvu tunazohitaji ili kutimiza migawo yetu hata iwe tunakabili mikazo ya aina gani. (Yohana 16:13; Wafilipi 4:13) Kwa hiyo, na tumtumaini Yehova kabisa, tuthamini sana utumishi wetu, na kutimiza huduma yetu kwa ukamili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 18 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungejibuje?

• Wazee wanaweza kufanya nini ili watimize huduma yao kwa ukamili?

• Tunawezaje kuboresha ustadi wetu wa kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani?

• Unaweza kufanya nini mwanafunzi wa Biblia asipoelewa mfano fulani au akihitaji habari zaidi kuhusu jambo fulani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Wazee wa Kikristo hufundisha kutanikoni na husaidia kuwazoeza waamini wenzao katika huduma

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye matokeo ni njia moja ya kuangaza nuru yetu