Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Una Utukufu Kuliko Milima”

“Una Utukufu Kuliko Milima”

Fahari ya Uumbaji wa Yehova

“Una Utukufu Kuliko Milima”

INAVUTIA sana kutazama machweo kutoka kilele cha Mlima Fuji. Jua jekundu huangaza theluji nyeupe na mawe ya lava ya rangi ya kijivujivu. Siku mpya inapoanza, kivuli cha mlima huo hufunika eneo kubwa lenye vilima na mabonde.

Milima yenye fahari kama vile Mlima Fuji, jina lililoandikwa kwa herufi zinazomaanisha “-sio na kifani,” hutustaajabisha daima. Huenda ukubwa wake ukatunyenyekeza! Milima ina fahari sana hivi kwamba watu wengi wanaamini kuwa miungu walikaa kwenye vile vilele virefu zaidi, ambavyo mara nyingi hufunikwa na ukungu na mawingu.

Yehova, Muumba stadi wa milima hiyo, ndiye Mungu pekee anayesifiwa na vilele vyake. Yeye pekee ndiye “Mfanyizaji wa milima.” (Amosi 4:13) Karibu robo ya dunia ni milima, na Mungu alipoumba sayari yetu alitokeza nguvu fulani ambazo mwishowe zilifanyiza vilele na safu za milima zenye kuvutia sana. (Zaburi 95:4) Kwa mfano, inaaminika kwamba safu za milima ya Himalaya na Andes zilifanyizwa na minyanyuko mikubwa iliyotokea ndani kabisa kwenye uso wa dunia, na kusonga kwa miamba mikubwa katika sehemu fulani za uso wa dunia.

Sisi wanadamu hatuelewi kabisa milima ilitokeaje na kwa sababu gani. Hata hatuwezi kujibu maswali haya ambayo Ayubu mwadilifu aliulizwa: “Ulikuwa wapi mimi, [Yehova] nilipoweka msingi wa dunia? . . . Vikalio vyake vimeingizwa ndani ya nini?”—Ayubu 38:4-6.

Hata hivyo, tunajua kwamba uhai wetu unategemea milima. Milima ndiyo vyanzo vya asili vya maji, kwa kuwa mito yote mikubwa hupata maji yake kutoka milimani na nusu ya wakaaji wa dunia hutegemea milima ili kupata maji. (Zaburi 104:13) Gazeti New Scientist linasema: “Sita kati ya mimea mikuu 20 inayotoa chakula duniani hupatikana milimani.” Chini ya hali nzuri za kimazingira katika ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu, “kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”—Zaburi 72:16; 2 Petro 3:13.

Milima inapotajwa, wengi hukumbuka milima ya Ulaya ya Alps. Vilele vya milima hiyo, kutia ndani vya Mlima Civetta unaoonyeshwa hapa, vinathibitisha kwa njia nzuri kwamba kuna Muumba. (Zaburi 98:8) Vinamsifu Yehova, ambaye “anaifanya imara milima kwa nguvu zake.”—Zaburi 65:6. *

Fahari ya milima ya Alps yenye vilele na sehemu zenye kuinuka zenye barafu, pande zilizofunikwa kwa theluji, mabonde na maziwa, na makonde inavutia sana. Mfalme Daudi alimtaja Yehova kuwa ‘ndiye hufanya milima ichipushe majani mabichi.’—Zaburi 147:8.

Huenda safu za milima kama hizi za Guilin, China, zisionekane zenye kuvutia sana zinapolinganishwa na Milima ya Alps, lakini zinavutia kwa njia ya pekee. Milima hii iliyo kandokando ya Mto Li, ambayo ina safu za vilele vya mawe ya chokaa, huwavutia wageni kwa umaridadi wake. Unapotazama maji safi yakitiririka kwenye milima hiyo yenye ukungu, huenda ukakumbuka maneno haya ya mtunga-zaburi: “[Yehova] anatuma mabubujiko ndani ya mabonde yenye vijito; yanaendelea kusonga mbele katikati ya milima.”—Zaburi 104:10.

Kwa kufaa, tunavutiwa na milima kwa sababu tunaiona kuwa sehemu yenye fahari ya uandalizi wenye upendo wa Muumba kwa ajili ya hali njema na furaha ya wanadamu. Hata hivyo, ingawa huenda milima ikavutia sana, fahari yake haiwezi kulinganishwa na utukufu wa Yehova. Kwa kweli, yeye ‘ana utukufu kuliko milima.’—Zaburi 76:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona Kalenda ya 2004 ya Mashahidi wa Yehova, Machi/Aprili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Asilimia kumi ya wakaaji wa dunia huishi katika maeneo yenye milima. Lakini hali hiyo haiwazuii hata kidogo watangazaji wa habari njema ya Ufalme wa Mungu. Wahudumu hao Wakristo wanafanya kazi hiyo kwa bidii katika maeneo mengi yenye milima. Na “jinsi inavyopendeza juu ya milima miguu ya yeye anayeleta habari njema, yeye anayetangaza amani, yeye anayeleta habari njema za jambo bora, yeye anayetangaza wokovu!”—Isaya 52:7.

Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Milima mirefu ni ya mbuzi wa milimani.” (Zaburi 104:18) Mbuzi wa milimani, kama mbuzi-mwitu wa Nubia mwenye pembe zenye kuvutia, ni kati ya wanyama wa milimani ambao ni vigumu sana kuteleza. Wao hutembea kwenye miamba iliyochongoka ambayo ni myembamba sana hivi kwamba huonekana kana kwamba haiwezi kupitika. Mbuzi hao wana uwezo wa kuishi katika maeneo ambayo ni vigumu kufikika. Hiyo inachangiwa kwa kadiri fulani na jinsi kwato zao zilivyo. Mpasuko wa kwato hizo unaweza kupanuka kutokana na uzito wa mbuzi huyo, na hivyo kumwezesha asiteleze anaposimama au kutembea juu ya miamba myembamba iliyochongoka. Mbuzi hao wameumbwa kwa ustadi kwelikweli!

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mlima Fuji, Honshu, Japani