Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakazia Fikira ile Thawabu?

Je, Unakazia Fikira ile Thawabu?

Je, Unakazia Fikira ile Thawabu?

KUNA ugonjwa ambao huathiri mtu pole kwa pole. Mwanzoni, ugonjwa huo hufanya mtu asione vizuri kwa upande. Usipotibiwa unaweza kuenea na kuathiri sehemu ya katikati ya jicho. Mwishowe, unaweza kufanya mtu awe kipofu. Huo ni ugonjwa gani? Unaitwa glakoma, nao ndio hufanya watu wengi zaidi wawe vipofu.

Kama vile tuwezavyo kupoteza pole kwa pole uwezo wa kuona, ndivyo tuwezavyo kupoteza uwezo wa kuona ulio muhimu hata zaidi, yaani, uwezo wetu wa kuona wa kiroho. Hivyo, ni muhimu kuendelea kukazia fikira sana mambo ya kiroho.

Kuendelea Kuikazia Fikira ile Thawabu

Kati ya “vitu visivyoonekana” kwa macho yetu halisi ni ile thawabu tukufu ya uzima wa milele ambayo Yehova anawatolea washikamanifu wake. (2 Wakorintho 4:18) Bila shaka, sababu kuu ambayo hufanya Wakristo wamtumikie Mungu ni kwamba wanampenda. (Mathayo 22:37) Hata hivyo, Yehova anataka tuitazamie kwa hamu thawabu yetu. Anataka tumwone kuwa Baba mkarimu ambaye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Hivyo, wale wanaomjua na kumpenda Mungu kikweli huthamini sana baraka alizoahidi na kutamani kuona zikitimizwa.—Waroma 8:19, 24, 25.

Wasomaji wengi wa gazeti hili na lile la Amkeni! ambalo huandamana nalo, hufurahia picha zinazoonyesha dunia itakayokuwa Paradiso. Bila shaka, hatujui kabisa jinsi dunia Paradiso itakavyokuwa, na picha zinazochapishwa ni michoro tu ya wasanii inayotegemea Maandiko ya Biblia kama vile Isaya 11:6-9. Hata hivyo, mwanamke mmoja Mkristo alisema: “Ninapoona picha za Paradiso ya wakati ujao katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, mimi huzitazama kwa makini, kama vile mtu hutazama broshua inayoonyesha sehemu za kutembelea. Mimi hujaribu kuwazia nikiwa katika Paradiso hiyo kwa sababu hapo ndipo ninapotumaini kuwa wakati wa Mungu ufikapo.”

Mtume Paulo alihisi vivyo hivyo kuhusu ‘mwito wake wa kwenda juu.’ Hakuona kuwa amekwisha fikia mwito huo, kwa kuwa alipaswa kuendelea kuwa mwaminifu hadi mwisho. Lakini aliendelea “kujinyoosha kwenda mbele kuelekea mambo yaliyo mbele.” (Wafilipi 3:13, 14) Vivyo hivyo, Yesu alivumilia kifo kwenye mti wa mateso “kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake.”—Waebrania 12:2.

Je, umewahi kutilia shaka kwamba utaingia katika ulimwengu huo mpya? Bila shaka, si vizuri kujitumaini kupita kiasi, kwa kuwa kupata tuzo la uhai hutegemea kuendelea kuwa waaminifu hadi mwisho. (Mathayo 24:13) Hata hivyo, ikiwa tunafanya yote tuwezayo kutimiza matakwa ya Mungu, tuna kila sababu ya kuwa na uhakika wa kupata thawabu hiyo. Kumbuka kwamba Yehova “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Tukimtumaini Yehova atatusaidia kufikia mradi wetu. Kwa kweli, ni jambo lisilopatana na utu wake kutafuta-tafuta sababu ili asiwape thawabu hiyo wale wanaojitahidi kwa unyoofu kumpendeza.—Zaburi 103:8-11; 130:3, 4; Ezekieli 18:32.

Kwa kujua jinsi Yehova anavyohisi kuhusu watu wake tunapata tumaini ambalo ni sifa muhimu sawa na imani yetu. (1 Wakorintho 13:13) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tumaini” katika Biblia lina wazo la “kutazamia mema” kwa hamu. Akiwa na tumaini hilo akilini, mtume Paulo aliandika: “Tunatamani kila mmoja wenu aonyeshe bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho, ili msiwe goigoi, bali muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” (Waebrania 6:11, 12) Ona kwamba tukiendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu, tunaweza kuwa na hakika kwamba tumaini letu litatimizwa. Tofauti na matumaini mengi ya ulimwengu, ‘tumaini hili halikatishi tamaa.’ (Waroma 5:5) Basi tunawezaje kudumisha tumaini letu likiwa hai na kulikazia fikira sana?

Jinsi ya Kuboresha Uwezo Wetu wa Kuona wa Kiroho

Macho yetu hayawezi kuona vizuri vitu viwili kwa wakati mmoja. Ndivyo ilivyo na uwezo wetu wa kuona wa kiroho. Bila shaka, kukazia fikira mambo ya mfumo huu kutafanya tusiweze kukazia fikira vizuri ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu. Baada ya muda, huenda tukaacha kuvutiwa na ulimwengu huo mpya na kuusahau kabisa kwa sababu ya kutoukazia fikira vizuri. Huo ungekuwa msiba ulioje! (Luka 21:34) Hivyo, ni muhimu kama nini kudumisha ‘jicho rahisi,’ linalokazia Ufalme wa Mungu na thawabu ya uzima wa milele!—Mathayo 6:22.

Si rahisi kudumisha jicho rahisi sikuzote. Tunalazimika kushughulika na matatizo ya kila siku, na huenda tukakabili vikengeusha-fikira na hata vishawishi maishani. Chini ya hali hizo, tunawezaje kuendelea kukazia fikira Ufalme na ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu bila kupuuza shughuli nyingine muhimu? Na tuchunguze njia tatu.

Jifunze Neno la Mungu kila siku. Kusoma Biblia na kujifunza kwa ukawaida vichapo vinavyozungumzia Biblia hutusaidia kukazia fikira mambo ya kiroho. Ni kweli kwamba huenda ikawa tumejifunza Neno la Mungu kwa miaka mingi, lakini lazima tuendelee kujifunza kama vile tu tunavyohitaji kuendelea kula chakula ili kuendeleza uhai wetu. Hatuachi kula eti kwa sababu tu tumekula mara nyingi sana wakati uliopita. Kwa hiyo, hata kama tunaijua Biblia kadiri gani tunahitaji kuendelea kula chakula cha kiroho kinachotokana nayo ili tumaini letu liendelee kuwa hai na kuimarisha imani na upendo wetu.—Zaburi 1:1-3.

Tafakari Neno la Mungu kwa uthamini. Kwa nini ni muhimu kutafakari? Kuna sababu mbili. Kwanza, kutafakari hutuwezesha kushika na kuthamini kutoka moyoni mambo tunayosoma. Pili, kutafakari hutusaidia tusimsahau Yehova, kazi zake za ajabu, na tumaini ambalo ametuahidi. Kwa mfano: Waisraeli waliotoka Misri pamoja na Musa walijionea matendo yaliyodhihirisha nguvu za Yehova. Pia waliona jinsi alivyowalinda kwa upendo alipowaongoza kuelekea nchi ambayo wangerithi. Hata hivyo, mara tu Waisraeli walipofika nyikani wakiwa njiani kwenda katika Nchi ya Ahadi, walianza kulalamika, jambo linaloonyesha kwamba walikuwa wamepungukiwa sana na imani. (Zaburi 78:11-17) Walikuwa na tatizo gani?

Watu waliacha kumkazia fikira Yehova na tumaini zuri alilowaahidi, na badala yake wakakazia fikira starehe na mambo ya kimwili. Ingawa walishuhudia miujiza mingi, Waisraeli wengi wakawa walalamikaji wasio na imani. Andiko la Zaburi 106:13 linasema: “Upesi wakasahau kazi [za Yehova].” Kwa sababu ya kupuuza mambo kwa njia hiyo isiyoweza kusameheka, kizazi hicho hakikuingia katika Nchi ya Ahadi.

Hivyo, unaposoma Biblia au vichapo vya kujifunzia Biblia, chukua wakati utafakari yale unayosoma. Kutafakari huko ni muhimu ili uendelee kukua kiroho. Kwa mfano, unaposoma Zaburi 106, ambayo imetajwa kwa sehemu hapo juu, tafakari sifa za Yehova. Ona jinsi alivyowaonyesha Waisraeli subira na rehema na jinsi alivyotenda yote aliyoweza ili kuwasaidia kufika kwenye Nchi ya Ahadi. Ona pia jinsi walivyoendelea kumwasi. Wazia jinsi Yehova alivyoumia wakati rehema na subira yake ilipojaribiwa na watu wasiojali na wasiothamini lolote. Isitoshe, tunapotafakari mistari ya 30 na 31, inayoeleza jinsi Finehasi alivyosimama imara na kwa ujasiri kwa ajili ya uadilifu, tunahakikishiwa kwamba Yehova hawasahau washikamanifu wake na kwamba yeye huwathawabisha sana.

Tumia kanuni za Biblia katika maisha yako. Tunapofuata kanuni za Biblia, tunajionea jinsi shauri la Yehova linavyofanya kazi. Andiko la Methali 3:5, 6 linasema: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” Fikiria jinsi ambavyo mienendo isiyo ya adili ya watu wengi imewaletea madhara ya kiakili, kihisia-moyo, na matatizo ya kimwili. Kwa kujihusisha na raha za muda, watu hao wanapata ole kwa miaka mingi au hata katika maisha yao yote. Kinyume kabisa na watu hao, wale wanaotembea katika ‘njia yenye nafasi ndogo’ huonja kimbele jinsi maisha yatakavyokuwa katika mfumo mpya, na hilo huwatia moyo waendelee kutembea katika njia inayoongoza kwenye uhai.—Mathayo 7:13, 14; Zaburi 34:8.

Inaweza kuwa vigumu kufuata kanuni za Biblia. Mara kwa mara, tunapokuwa katika hali ngumu, huenda tukaona kwamba suluhisho lisilotegemea Biblia linaweza kuleta kitulizo mara moja. Kwa mfano, hali zinapokuwa ngumu kifedha, huenda tukashawishika kutotanguliza mambo ya Ufalme. Hata hivyo, wale wanaotenda kwa imani na kudumisha uwezo wao wa kuona wa kiroho, wanahakikishiwa kwamba mwishowe “mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli.” (Mhubiri 8:12) Huenda Mkristo akalazimika kufanya kazi ya ziada pindi kwa pindi, lakini hapaswi kamwe kuwa kama Esau aliyepuuza mambo ya kiroho, na kuyaona kuwa si muhimu.—Mwanzo 25:34; Waebrania 12:16.

Yesu alieleza waziwazi wajibu wetu tukiwa Wakristo. Tunapaswa ‘kuendelea kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wa Mungu.’ (Mathayo 6:33) Tukifanya hivyo, Yehova atatuonyesha upendo wake kama baba kwa kuhakikisha kwamba mahitaji yetu ya kimwili yatatimizwa. Bila shaka, hataki tulemewe na mahangaiko kuhusu mambo anayosema atayashughulikia. Mahangaiko hayo ya kupita kiasi ni kama ugonjwa wa glakoma wa kiroho. Ukipuuzwa utafanya tuone tu mambo ya kimwili na mwishowe utatufanya vipofu kiroho. Tukibaki katika hali hiyo, siku ya Yehova itakuja “kama mtego.” Huo ungekuwa msiba ulioje!—Luka 21:34-36.

Endelea Kukaza Fikira Kama Yoshua

Na tuendelee kukazia fikira sana tumaini letu tukufu la Ufalme, na kutotanguliza mambo mengine. Kwa kuendelea kujifunza, kutafakari, na kutumia kanuni za Biblia kwa ukawaida, tunaweza kuendelea kuwa na hakika kuhusu tumaini letu kama vile Yoshua. Baada ya kuwaongoza Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, alisema: “Mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.”—Yoshua 23:14.

Tumaini la Ufalme na likuimarishe, na likufurahishe linapodhihirika katika mawazo, hisia, maamuzi, na utendaji wako.—Methali 15:15; Waroma 12:12.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je, umewahi kutilia shaka kwamba utaingia katika ulimwengu mpya?

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kutafakari ni sehemu muhimu ya funzo la Biblia

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kazia fikira mambo yanayohusu Ufalme