Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtambulisha Mnyama-Mwitu na Alama Yake

Kumtambulisha Mnyama-Mwitu na Alama Yake

Kumtambulisha Mnyama-Mwitu na Alama Yake

JE, WEWE hufurahia kufumbua fumbo? Ili kufanya hivyo, wewe hutafuta vidokezi ambavyo mwishowe vitakusaidia kufumbua fumbo hilo. Katika Neno lake lililoongozwa na roho, Mungu ametoa vidokezi vinavyohitajika ili kujua ile namba 666, jina au alama ya mnyama-mwitu wa Ufunuo sura ya 13.

Katika makala hii, tutachunguza njia nne kuu, au vidokezi muhimu, vitakavyotusaidia kuelewa maana ya alama ya mnyama huyo. Tutachunguza (1) jinsi ambavyo wakati mwingine majina katika Biblia huchaguliwa, (2) utambulisho wa mnyama-mwitu, (3) kinachomaanishwa na namba 666 kuwa “namba ya mwanadamu,” na (4) umuhimu wa namba 6 na kwa nini inaandikwa kwa kurudiwa mara tatu, yaani, 6 kuongeza 60 kuongeza 600, au 666.—Ufunuo 13:18.

Majina ya Biblia Si Vitambulishi Tu

Mara nyingi majina ya Biblia yana maana ya pekee, hasa ikiwa yametolewa na Mungu. Kwa mfano, kwa kuwa Abramu angekuwa baba ya mataifa, Mungu alibadili jina la mzee huyo wa ukoo kuwa Abrahamu, jina linalomaanisha “Baba ya Umati.” (Mwanzo 17:5) Mungu aliwaambia Yosefu na Maria wamwite jina Yesu, mtoto ambaye angezaliwa na Maria, jina linalomaanisha “Yehova Ni Wokovu.” (Mathayo 1:21; Luka 1:31) Kupatana na jina hilo lenye maana ya kipekee, Yehova alifanya iwezekane tupate wokovu kupitia huduma na kifo cha kidhabihu cha Yesu.—Yohana 3:16.

Kwa hiyo, bila shaka jina au namba 666 iliyotolewa na Mungu inamaanisha tabia ambazo Mungu huona kuwa zinamtambulisha mnyama huyo. Bila shaka, ili kuelewa tabia hizo, tunahitaji kumtambulisha mnyama mwenyewe na kujua matendo yake.

Yule Mnyama Afunuliwa

Kitabu cha Biblia cha Danieli kina habari nyingi kuhusu maana ya wanyama wa mfano. Sura ya 7 ina ufafanuzi ulio wazi kuhusu “wanyama wakubwa mno wanne,” simba, dubu, chui, na mnyama mwenye kuogopesha aliye na meno ya chuma, tena makubwa. (Danieli 7:2-7) Danieli anatuambia kwamba wanyama hao wanawakilisha “wafalme,” au falme za kisiasa, zinazotawala milki kubwa kwa kufuatana.—Danieli 7:17, 23.

Kuhusu mnyama wa Ufunuo 13:1, 2, kichapo The Interpreter’s Dictionary of the Bible kinasema kwamba mnyama huyo “ana tabia zote za wale wanyama wanne katika maono ya Danieli . . . Hivyo, mnyama huyo wa kwanza [wa Ufunuo] anawakilisha tawala zote za kisiasa zinazompinga Mungu katika ulimwengu.” Maoni hayo yanaungwa mkono na andiko la Ufunuo 13:7, linalosema hivi kuhusu mnyama huyo: “Akapewa mamlaka juu ya kila kabila na watu na lugha na taifa.” *

Kwa nini Biblia hutumia wanyama kufananisha tawala za kibinadamu? Kuna sababu mbili. Sababu ya kwanza ni kwamba serikali zimemwaga damu kikatili kwa muda wa karne nyingi. Wanahistoria Will na Ariel Durant waliandika: “Vita vimekuwa tukio la kawaida katika historia, na havijapungua kwa sababu ya ustaarabu au demokrasia.” Hapana shaka kwamba “mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza”! (Mhubiri 8:9) Sababu ya pili ni kwamba ‘yule joka mkubwa, Shetani, alimpa huyo mnyama nguvu zake na kile kiti chake cha ufalme na mamlaka kubwa.’ (Ufunuo 12:9; 13:2) Kwa hiyo, utawala wa kibinadamu umetokana na Ibilisi, hivyo unaonyesha mtazamo wa kinyama, kama wa joka huyo.—Yohana 8:44; Waefeso 6:12.

Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba kila utawala wa kibinadamu hutumiwa moja kwa moja na Shetani. Kwa kweli, kwa njia moja, serikali za kibinadamu hutumika zikiwa “mhudumu wa Mungu,” ili kuleta utulivu katika jamii ya kibinadamu, kama sivyo kungekuwa na machafuko. Viongozi fulani wametetea haki za msingi za kibinadamu, kutia ndani haki ya kufurahia ibada ya kweli, jambo ambalo halimpendezi Shetani. (Waroma 13:3, 4; Ezra 7:11-27; Matendo 13:7) Lakini kwa sababu ya uvutano wa Ibilisi, hakuna mwanadamu au shirika la kibinadamu ambalo limewahi kufaulu kuwaletea watu amani na usalama wa kweli. *Yohana 12:31.

“Namba ya Mwanadamu”

Kidokezi cha tatu kinachotusaidia kuelewa maana ya namba 666 ni kwamba namba hiyo inaitwa “namba ya mwanadamu.” Maneno hayo hayawezi kurejelea mwanadamu fulani, kwa kuwa Shetani, wala si mwanadamu, ndiye mwenye mamlaka juu ya mnyama huyo. (Luka 4:5, 6; 1 Yohana 5:19; Ufunuo 13:2, 18) Badala yake, kwa kuwa mnyama huyo ana alama au “namba ya mwanadamu,” hiyo inadokeza kwamba asili yake ni ya kibinadamu, wala si ya roho au roho mwovu, na hivyo hudhihirisha tabia fulani za kibinadamu. Tabia hizo zaweza kuwa nini? Biblia inajibu kwa kusema: “[Wanadamu] wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kwa hiyo, kwa kuwa mnyama huyo ana “namba ya mwanadamu,” hiyo inadokeza kwamba serikali hudhihirisha hali ya mwanadamu ya kutokuwa mkamilifu na yenye dhambi.

Historia inathibitisha kwamba jambo hilo ni kweli. “Kila ustaarabu ambao umewahi kuweko mwishowe umeporomoka,” akasema Henry Kissinger, aliyekuwa Waziri wa Mashauri ya Nchi za Kigeni wa Marekani. “Historia husimulia kuhusu jitihada zilizoshindwa na maazimio yaliyokosa kutimizwa . . . Hivyo, ukiwa mwanahistoria unapaswa kutambua kwamba misiba haiwezi kuepukika.” Maoni ya unyoofu ya Kissinger yanathibitisha ukweli huu wa msingi wa Biblia: “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.

Kwa kuwa tumemtambulisha mnyama na kujua jinsi Mungu anavyomuona, sasa tunaweza kuchunguza sehemu ya mwisho ya fumbo letu, yaani, namba 6 na kwa nini inaandikwa kwa kurudiwa mara tatu, yaani, 666, au 600 kuongeza 60 kuongeza 6.

Kwa Nini Sita Imerudiwa Mara Tatu?

Katika Biblia, namba fulani zina maana ya mfano. Kwa mfano, mara nyingi namba saba hutumiwa kufananisha kitu ambacho ni kamili, au kikamilifu, machoni pa Mungu. Kwa mfano, juma la uumbaji la Mungu lina urefu wa ‘siku’ saba, au vipindi virefu vya wakati, ambapo Mungu anakamilisha kabisa kusudi lake la uumbaji kuelekea dunia. (Mwanzo 1:3–2:3) “Maneno” ya Mungu ni kama fedha “iliyosafishwa mara saba,” hivyo imesafishwa kikamilifu. (Zaburi 12:6; Methali 30:5, 6) Naamani aliyekuwa na ukoma aliambiwa akaoge katika Mto Yordani mara saba na baada ya hapo alipona kabisa.2 Wafalme 5:10, 14.

Ni lazima uongeze nambari moja kwa sita ili kupata saba. Kwa kweli, huo ni mfano unaofaa wa kitu kisicho kikamilifu, au chenye kasoro machoni pa Mungu. (1 Mambo ya Nyakati 20:6, 7) Isitoshe, kuandika sita kwa kuirudia mara tatu, kuwa 666, hukazia sana hali hiyo ya kutokamilika. Ili kuthibitisha kwamba maoni hayo ni sahihi, namba 666 inatajwa kuwa “namba ya mwanadamu,” kama tulivyoona. Hivyo, historia ya mnyama huyo, ‘namba yake ya mwanadamu,’ na namba 666 yenyewe, yote yanaonyesha waziwazi hali ya kupungukiwa kabisa au kushindwa kabisa machoni pa Yehova.

Kupungukiwa kwa mnyama huyo hutukumbusha yale yaliyosemwa kuhusu Mfalme Belshaza wa Babiloni la kale. Kupitia Danieli, Yehova alimwambia mtawala huyo hivi: “Wewe umepimwa katika mizani, ukaonekana kuwa umepungukiwa.” Usiku huohuo Belshaza aliuawa nayo Milki ya Babilonia yenye nguvu ikaanguka. (Danieli 5:27, 30) Vivyo hivyo, hukumu ya Mungu juu ya mnyama huyo wa kisiasa na wote walio na alama yake, humaanisha mwisho wake na wale wanaomuunga mkono. Hata hivyo, katika hukumu hii, Mungu hatakomesha tu mfumo mmoja wa kisiasa, bali kila salio la utawala wa kibinadamu. (Danieli 2:44; Ufunuo 19:19, 20) Hivyo, ni muhimu tuepuke kupata alama yenye kuleta kifo ya mnyama huyo!

Ile Alama Yatambulishwa

Mara tu baada ya kufunua maana ya ile namba 666, kitabu cha Ufunuo kinataja wafuasi 144,000 wa Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, ambao jina lake na jina la Baba yake, Yehova, limeandikwa juu ya mapaji ya nyuso zao. Majina hayo huwatambulisha kuwa mali ya Yehova na Mwana wake, nao hujivunia kutoa ushahidi juu yao. Vivyo hivyo, wale walio na alama ya mnyama hutangaza kwamba wanamtumikia mnyama huyo. Hivyo, ile alama, iwe kwenye mkono wa kulia au kwenye paji la uso, ni ishara inayomtambulisha mwenye alama hiyo kuwa anaitukuza na kuiunga mkono mifumo ya kisiasa ya ulimwengu iliyo kama mnyama. Wale walio na alama hiyo humpa “Kaisari” vitu ambavyo vinastahili kupewa Mungu. (Luka 20:25; Ufunuo 13:4, 8; 14:1) Jinsi gani? Kwa kutukuza taifa, nembo zake, na uwezo wake wa kijeshi, ambao wao huutegemea ili kupata tumaini na wokovu. Ibada yoyote wanayomtolea Mungu wa kweli ni kazi bure.

Tofauti na hilo, Biblia hutuhimiza: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote. Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” (Zaburi 146:3, 4) Wale wanaotii shauri hilo la hekima hawakati tamaa serikali zinapokosa kutimiza ahadi zao, au viongozi wenye ushawishi mkubwa wa kisiasa wanapopoteza umashuhuri.—Methali 1:33.

Hiyo haimaanishi kwamba Wakristo wa kweli hukaa kitako bila kufanya lolote kuhusu matatizo ya mwanadamu. Kinyume cha hilo, wanatangaza kwa bidii ile serikali moja ambayo itatatua matatizo ya wanadamu. Serikali hiyo ni Ufalme wa Mungu ambao wao huuwakilisha.—Mathayo 24:14.

Ufalme wa Mungu Ndio Tumaini Pekee la Wanadamu

Ufalme wa Mungu ndio uliokuwa kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu alipokuwa duniani. (Luka 4:43) Katika sala yake ya kielelezo, ambayo wakati mwingine inaitwa Sala ya Bwana, Yesu aliwafundisha wafuasi wake waombe Ufalme huo uje na mapenzi ya Mungu yafanywe duniani. (Mathayo 6:9, 10) Ufalme ni serikali ambayo itatawala dunia nzima kutoka mbinguni, wala si kutoka katika mji mkuu fulani duniani. Hivyo, Yesu aliuita “ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 11:12.

Yesu Kristo ndiye anayefaa kuwa Mfalme wa Ufalme huo kwa kuwa alikufa kwa ajili ya wale ambao watakuwa raia zake. (Isaya 9:6, 7; Yohana 3:16) Hivi karibuni, Mtawala huyo mkamilifu, ambaye sasa ni mtu wa roho mwenye uwezo atamtupa mnyama-mwitu, wafalme wake, na majeshi yake katika “ziwa la moto linalowaka kwa kiberiti,” ambalo linafananisha uharibifu kamili. Na mambo bado. Yesu pia atamwondoa Shetani, jambo ambalo hakuna mwanadamu anaweza kulifanya.—Ufunuo 11:15; 19:16, 19-21; 20:2, 10.

Ufalme wa Mungu utawaletea amani raia zake wote watiifu. (Zaburi 37:11, 29; 46:8, 9) Hata huzuni, maumivu, na kifo havitakuwapo tena. Hilo ni tazamio tukufu kama nini kwa wale wasiokubali kutiwa alama ya yule mnyama!—Ufunuo 21:3, 4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ili kupata habari zaidi kuhusu mistari hiyo, ona sura ya 28 ya kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 11 Ingawa Wakristo wa kweli wanatambua kwamba mara nyingi tawala za kibinadamu zinatenda kama wanyama, wao hujitiisha kwa “mamlaka zilizo kubwa” za kiserikali kama wanavyoagizwa na Biblia. (Waroma 13:1) Hata hivyo, mamlaka hizo zinapowaamuru watende kinyume cha sheria za Mungu, wao ‘humtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:29.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

Vidokezi Vinavyotusaidia Kuelewa Maana ya Namba 666

1. Mara nyingi majina ya Biblia hufunua jambo fulani kuhusu tabia au maisha ya mwenye jina hilo, kama vile Abrahamu, Yesu, na wengine wengi. Vivyo hivyo, jina la mnyama huyo huonyesha tabia zake.

2. Katika kitabu cha Biblia cha Danieli, wanyama mbalimbali wanawakilisha falme au miliki za wanadamu zenye kufuatana. Mnyama huyo wa Ufunuo 13:1, 2 anayewakilisha mfumo wa kisiasa wa ulimwenguni pote, anapewa nguvu na kuongozwa na Shetani.

3. Kwa kuwa mnyama huyo ana alama au “namba ya mwanadamu,” hiyo inaonyesha kwamba asili yake ni ya kibinadamu, wala si ya roho mwovu. Hivyo, hudhihirisha hali ya mwanadamu ya kutokuwa mkamilifu na yenye dhambi.

4. Machoni pa Mungu, namba sita kuonyesha hali ya kutokamilika kwa kuwa imepungua kwa nambari moja ili iwe saba, namba ambayo kulingana na Biblia ni kamilifu. Ile alama ya 666 hukazia hali ya kupungukiwa kwa kurudia namba hiyo mara tatu.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Utawala wa kibinadamu umeshindwa, nao unafananishwa vizuri na ile namba 666

[Hisani]

Starving child: UNITED NATIONS/Photo by F. GRIFFING

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu Kristo ataleta utawala mkamilifu duniani