Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwahubiria Watu Mahali Pao pa Kazi

Kuwahubiria Watu Mahali Pao pa Kazi

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

Kuwahubiria Watu Mahali Pao pa Kazi

NI JAMBO gani linalofanana kati ya mtume Mathayo, Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana? Wote waliitwa na Yesu walipokuwa mahali pao pa kazi. Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana walikuwa na shughuli nyingi katika kazi yao ya uvuvi Yesu alipowaalika, akisema: “Nifuateni.” Mathayo alikuwa katika ofisi ya kodi alipoalikwa awe mwanafunzi wa Yesu.—Mathayo 4:18-21; 9:9.

Kuhubiria watu mahali pao pa kazi kunaweza kuwa jambo lenye kuthawabisha. Kwa kutambua jambo hilo, hivi karibuni Mashahidi wa Yehova huko Japani walijitahidi sana kuhubiria watu mahali pao pa kazi. Ikawaje? Baada ya muda wa miezi michache, walifanya maelfu ya ziara za kurudia, na wakaanzisha mafunzo 250 hivi ya Biblia. Ona mambo yaliyoonwa yafuatayo.

Mhudumu mmoja wa wakati wote jijini Tokyo alikutana na msimamizi wa mkahawa fulani ambaye alikuwa amezungumza na Shahidi mmoja miaka 30 hivi iliyopita akiwa mvulana shuleni. Ingawa msimamizi huyo hakuelewa mengi kati ya mambo waliyozungumzia wakati huo, alipendezwa na Biblia. Kwa kuwa sasa upendezi wake ulikuwa umeamshwa tena, alikubali mara moja funzo la Biblia lililoongozwa kwa kutumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. * Isitoshe, alipanga ratiba ya kibinafsi ya kusoma Biblia kila jioni kabla ya kulala.

Mhudumu mmoja mwanamke, ambaye ni painia wa pekee alitembelea ofisi fulani. Ingawa msimamizi wa ofisi hiyo hakupatikana, mwanamke mchanga aliyejibu simu ya msimamizi huyo aliuliza, “Je, ungependa kuzungumza nami?” Baada ya mazungumzo mafupi kwenye simu, mwanamke huyo alitoka ofisini na kumwambia painia huyo kwamba alipendezwa kusoma Biblia. Painia huyo wa pekee alipanga kurudi akiwa na Biblia na kuanzisha funzo la Biblia pamoja naye. Painia huyo alikuwa akiongoza funzo hilo asubuhi katika bustani iliyokuwa karibu kabla ya mwanamke huyo kuanza kazi.

Kwenye ofisi nyingine, mtu mmoja alimwona mfanyakazi mwenzake akikubali magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kutoka kwa Shahidi mmoja, lakini akayatupa haraka baada ya Shahidi huyo kuondoka. Mtu huyo aliporudi nyumbani, alimweleza mke wake ambaye ni Shahidi kuhusu tukio hilo na kusema kwamba kama ni yeye ambaye angepewa magazeti hayo angesikiliza kidogo. Binti yake, aliyemsikia akisema hivyo, alimweleza Shahidi anayehubiri eneo hilo la biashara habari hiyo. Shahidi huyo alimtembelea haraka baba ya binti huyo ofisini mwake na kuanzisha funzo la Biblia pamoja naye. Muda si muda, alianza kuhudhuria mikutano ya Jumapili kwa ukawaida.

Kuhubiria watu mahali pao pa kazi kumekuwa na matokeo mengine. Wahubiri wengi nchini Japani wamekuwa stadi katika kufanya ziara za kurudia madukani, viwandani, na maofisini. Isitoshe, kupitia njia hiyo ya kuhubiri, wahubiri wengi wasiotenda wametembelewa na mafunzo yakaanzishwa pamoja nao. Matokeo yamekuwa mazuri sana. Hivi karibuni, kutaniko moja katikati ya jiji la Tokyo liliripoti mafunzo ya Biblia ya nyumbani 108. Idadi hiyo ni mara mbili zaidi ya idadi iliyoripotiwa mwaka mmoja uliopita.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.