Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Licha ya Vita Kuna Ongezeko la Ufalme Nchini Liberia

Licha ya Vita Kuna Ongezeko la Ufalme Nchini Liberia

Licha ya Vita Kuna Ongezeko la Ufalme Nchini Liberia

KUMEKUWA na vita vya wenyewe kwa wenyewe huko Liberia kwa zaidi ya miaka kumi. Kufikia katikati ya mwaka wa 2003, waasi walikuwa wamepigana na kuingia mji mkuu, Monrovia. Mashahidi wengi wa Yehova walilazimika kukimbia makao yao, nyakati nyingine mara kadhaa. Mali zao ziliporwa mara nyingi.

Inasikitisha kwamba katika mapigano yaliyotokea katika mji huo, maelfu ya watu waliuawa. Kati yao kulikuwa na Mashahidi wawili, ndugu mmoja na dada mmoja. Ndugu wengine walikabilianaje na hali hiyo ngumu, na ni hatua gani iliyochukuliwa ili kuwasaidia?

Kuwasaidia Wenye Uhitaji

Wakati wote wa mapigano hayo, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Liberia ilipanga kuwapelekea msaada wale wenye uhitaji. Iliwapelekea chakula, vifaa muhimu vya nyumbani, na dawa. Wakati eneo la bandarini lilipokuwa mikononi mwa waasi, ilikuwa vigumu kupata chakula. Ofisi ya tawi ilikuwa imeona kimbele hali hiyo na ilikuwa imeweka vifaa muhimu kwa ajili ya Mashahidi elfu mbili waliokuwa wamekimbilia Majumba ya Ufalme katika sehemu zote za jiji. Akina ndugu waligawa chakula hicho kwa kipimo hivi kwamba kilidumu hadi bandari ilipofunguliwa. Ofisi za tawi za Ubelgiji na Sierra Leone zilituma dawa kwa ndege, nazo ofisi za tawi za Uingereza na Ufaransa zikatuma nguo.

Ingawa hali ilikuwa yenye kukatisha tamaa, ndugu zetu waliendelea kuwa wenye furaha na wenye maoni yanayofaa. Wengi walikuwa na maoni kama ya ndugu mmoja aliyekimbia nyumbani mara tatu. Alisema: “Tunahubiri kuhusu hali hizo; tunaishi katika siku za mwisho.”

Watu Wanaitikia Habari Njema

Kujapokuwa msukosuko nchini mwote, Mashahidi wanaendelea kupata matokeo mazuri katika mahubiri. Kulikuwa na kilele cha juu kabisa cha watangazaji wa Ufalme 3,879 mwezi wa Januari 2003, na waliongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani 15,227 mwezi wa Februari.

Watu wanaitikia upesi habari njema. Kuna mfano mmoja kutoka kijiji fulani huko kusini-mashariki mwa nchi hiyo. Kutaniko moja lilipanga kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo katika kijiji kikubwa cha Bewahn, kilicho mwendo wa miguu wa muda wa saa tano kutoka mahali ambapo wao hukutania kwa ukawaida. Kabla ndugu hawajaenda kijijini kuwaalika watu kwenye Ukumbusho, walimwalika meya wa Bewahn. Alipopokea mwaliko huo, alichukua Biblia yake, akaenda kwa wanakijiji na kuwasomea andiko moja lililoonyeshwa kwenye kikaratasi cha mwaliko, akiwatia moyo wahudhurie Ukumbusho huo. Hivyo, wahubiri walipofika, wakakuta kwamba kazi yao ilikuwa imekwisha fanywa! Meya huyo pamoja na watoto wake na wake zake wawili walihudhuria Ukumbusho. Jumla ya watu 27 walihudhuria. Tangu wakati huo, meya huyo aliacha Kanisa la Methodisti, akaanza kujifunza pamoja na Mashahidi, naye akatoa uwanja wa kujenga Jumba la Ufalme.

Abadili Mtazamo

Pia mwenendo wa ndugu zetu umekuwa na matokeo katika kubadili maoni ya wapinzani fulani wa ile kweli. Fikiria kisa cha mtu aitwaye Opoku. Mhudumu mmoja painia wa pekee alikutana naye alipokuwa akihubiri na kumpa gazeti Mnara wa Mlinzi. Opoku alipendezwa na makala fulani katika gazeti hilo lakini hakuwa na pesa. Baada ya kumweleza kwamba haliuzwi, painia huyo alimwachia gazeti hilo na akapanga kumtembelea tena. Aliporudi, Opoku alimwuliza painia huyo hivi: “Je, unanijua? Washiriki wengi wa dini yenu katika mji wa Harper wananijua. Nilikuwa nikiwafukuza watoto wenu shuleni!” Kisha akaeleza kwamba alikuwa mwalimu mkuu wa shule moja ya sekondari katika mji huo na kwamba alikuwa akiwatesa watoto wa Mashahidi wa Yehova kwa kukataa kusalimu bendera.

Hata hivyo, baada ya Opoku kuona Mashahidi wa Yehova wakionyesha upendo wa Kikristo katika visa vitatu tofauti, alifikiria tena mtazamo wake kuwaelekea. Kwanza, aliwaona Mashahidi wakimtunza ndugu yao wa kiroho ambaye alikuwa mgonjwa sana. Hata walipanga kumpeleka nchi fulani jirani akapate matibabu. Opoku alifikiri kwamba ndugu huyo aliyekuwa mgonjwa alikuwa “mtu mashuhuri” kati ya Mashahidi lakini akapata habari kwamba alikuwa Shahidi wa kawaida tu. Pili, katika miaka ya 1990, Opoku alikuwa mkimbizi huko Côte d’Ivoire. Siku moja alipokuwa na kiu, alienda kununua maji kwa mwanamume fulani kijana. Opoku alikuwa na noti yenye thamani kubwa naye mwanamume huyo hakuwa na chenji, hivyo akampa Opoku maji bila malipo. Alipompa Opoku maji, mwanamume huyo alimwuliza: “Je, unafikiri kuna wakati ambapo watu kama mimi na wewe tutapeana vitu bila malipo?” Opoku alikisia kwamba mwanamume huyo ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, naye mwanamume huyo akamhakikishia kwamba ni Shahidi. Alivutiwa na ukarimu na fadhili za ndugu huyo. Mwishowe, utayari wa yule painia wa pekee wa kumpa gazeti bila malipo ulimsadikishia Opoku kwamba hakuwa na maoni sahihi kuhusu Mashahidi na kwamba alihitaji kuyabadili. Alifanya maendeleo ya kiroho na sasa yeye ni mhubiri asiyebatizwa.

Ingawa ndugu huko Liberia wanaendelea kukabili hali ngumu sana, wanamtumaini Mungu nao wanatangaza kwa uaminifu habari njema kuhusu hali nzuri chini ya utawala wenye uadilifu wa Ufalme wa Mungu. Yehova hatasahau kamwe kazi yao ngumu na upendo wanaoonyesha kwa ajili ya jina lake.—Waebrania 6:10.

[Ramani katika ukurasa wa 30]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

MONROVIA

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wakati wa matatizo, watu wa Yehova hutoa msaada wa kiroho na wa kimwili kwa wale wenye uhitaji