Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini andiko la 1 Wakorintho 10:8 linasema kwamba Waisraeli 23,000 ndio waliuawa katika siku moja kwa kufanya uasherati, huku Hesabu 25:9 likisema ni Waisraeli 24,000?

Kuna sababu kadhaa zinazoweza kutusaidia kuelewa tofauti kati ya idadi ya Waisraeli wanaotajwa katika mistari hiyo miwili. Mojawapo ya sababu za msingi zaidi ni kwamba idadi kamili inaweza kuwa kati ya 23,000 na 24,000, na hivyo tunaweza kutumia mojawapo ya idadi hizo kama idadi kamili.

Fikiria uwezekano mwingine. Mtume Paulo alitaja masimulizi hayo kuhusu Waisraeli huko Shitimu kuwa kielelezo cha kuwaonya Wakristo katika Korintho la kale, jiji ambalo lilijulikana sana kwa maisha yaliyopotoka kiadili. Aliandika: “Wala tusifanye uasherati, kama baadhi yao walivyofanya uasherati, na kuanguka, 23,000 kati yao katika siku moja.” Akitaja wale waliouawa na Yehova kwa sababu ya kufanya uasherati, Paulo alisema kwamba idadi yao ilikuwa 23,000.—1 Wakorintho 10:8.

Hata hivyo, kitabu cha Hesabu sura ya 25 kinatuambia kwamba ‘Israeli alijishikamanisha na Baali wa Peori; nayo hasira ya Yehova ikaanza kuwaka juu ya Israeli.’ Ndipo, akamwamuru Musa awaue “wote walio vichwa vya watu.” Musa naye akawaamuru waamuzi watekeleze amri hiyo. Mwishowe, Finehasi alipotenda kwa haraka na kumuua Mwisraeli aliyemwingiza mwanamke Mmidiani katika kambi, “tauni ikakomeshwa.” Masimulizi hayo yanamalizika kwa maneno haya: “Waliokufa kutokana na tauni hiyo walijumlika kuwa 24,000.”—Hesabu 25:1-9.

Yaonekana idadi inayotolewa katika kitabu cha Hesabu inatia ndani wale “walio vichwa vya watu” ambao waliuawa na waamuzi, na wale waliouawa moja kwa moja na Yehova. Huenda ikawa kwamba waamuzi waliwaua vichwa vya watu elfu moja, hivyo kufanya jumla ya wote waliouawa kuwa 24,000. Hata kama wale waliokuwa vichwa vya watu au viongozi wa maasi walifanya uasherati, wakashiriki katika sherehe, au wakakubaliana na wale waliofanya mambo hayo, walikuwa na hatia ya ‘kujishikamanisha na Baali wa Peori.’

Kuhusu neno ‘kujishikamanisha,’ kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema kwamba neno hilo linaweza kumaanisha “kuungana na mtu mwingine.” Waisraeli walikuwa watu waliojiweka wakfu kwa Yehova, lakini ‘walipojishikamanisha na Baali wa Peori,’ walivunja uhusiano huo pamoja na Mungu. Miaka 700 hivi baadaye, Yehova alisema hivi kuwahusu Waisraeli kupitia nabii Hosea: “Wao wenyewe waliingia kwa Baali wa Peori, nao wakajiweka wakfu kwa kitu kile cha aibu, wakawa wenye kuchukiza kama kile kitu walichokipenda.” (Hosea 9:10) Wote waliofanya hivyo walistahili hukumu kali ya Mungu. Hivyo, Musa akawakumbusha hivi wana wa Israeli: “Macho yenu wenyewe ndiyo yaliyoona mambo ambayo Yehova alifanya katika kile kisa cha Baali wa Peori, kwamba kila mtu aliyemfuata Baali wa Peori ndiye ambaye Yehova Mungu wako aliangamiza kutoka katikati yako.”—Kumbukumbu la Torati 4:3.