Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pingeni Roho ya Ulimwengu Unaobadilika

Pingeni Roho ya Ulimwengu Unaobadilika

Pingeni Roho ya Ulimwengu Unaobadilika

“Sisi tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu.”—1 WAKORINTHO 2:12.

1. Hawa alidanganywa katika njia zipi?

“YULE nyoka—alinidanganya.” (Mwanzo 3:13) Kwa maneno hayo machache, yule mwanamke wa kwanza, Hawa, alijaribu kueleza sababu iliyofanya amwasi Yehova Mungu. Alisema kweli, lakini hiyo haikufanya asiwe na hatia ya kosa lake. Baadaye, mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “[Hawa] alidanganywa kabisa.” (1 Timotheo 2:14) Alidanganywa aamini kwamba tendo lake la kutotii, yaani, kula tunda lililokatazwa, lingemnufaisha na kumfanya awe kama Mungu. Pia alidanganywa asiweze kumtambua yule aliyempotosha. Hakujua kwamba nyoka alikuwa akitumiwa tu na Shetani Ibilisi.—Mwanzo 3:1-6.

2. (a) Shetani huwapotoshaje watu leo? (b) “Roho ya ulimwengu” ni nini, na tutachunguza maswali gani sasa?

2 Tangu wakati wa Adamu na Hawa, Shetani ameendelea kudanganya watu. Kwa kweli, yeye ndiye “anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Bado anatumia mbinu zilezile. Ingawa hatumii tena nyoka halisi, yeye anaendelea kujificha ili asitambuliwe. Kwa kutumia vitumbuizo, vyombo vya habari, na njia nyingine, Shetani huwapotosha watu waamini kwamba hawahitaji wala hawanufaiki na mwongozo wenye upendo wa Mungu. Kampeni ya Ibilisi ya kudanganya imefanya watu kila mahali wawe na roho ya kuasi sheria na kanuni za Biblia. Katika Biblia hiyo inaitwa “roho ya ulimwengu.” (1 Wakorintho 2:12) Roho hiyo ina uvutano mkubwa juu ya imani, mitazamo, na mienendo ya wale wasiomjua Mungu. Roho hiyo hudhihirishwaje, na tunawezaje kuepuka uvutano wake wenye kupotosha? Na tuone.

Maadili Yanazorota

3. Kwa nini “roho ya ulimwengu” inazidi kudhihirika leo?

3 Leo, “roho ya ulimwengu” inazidi kudhihirika. (2 Timotheo 3:1-5) Yaelekea umeona kwamba maadili yanazidi kuzorota. Biblia inaeleza sababu. Baada ya kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu mwaka wa 1914, vita vilitokea mbinguni. Shetani na malaika zake waovu walishindwa nao wakatupwa kwenye ujirani wa dunia. Akiwa mwenye ghadhabu, Shetani amezidisha kampeni yake ya kudanganya dunia yote. (Ufunuo 12:1-9, 12, 17) Anajitahidi kutumia kila njia awezayo “ili kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa.” (Mathayo 24:24) Tukiwa watu wa Mungu, sisi ndio hushambuliwa zaidi na Shetani. Yeye hujitahidi kuharibu hali yetu ya kiroho ili tupoteze kibali cha Yehova na tazamio la kuishi milele.

4. Watumishi wa Yehova huionaje Biblia, nao ulimwengu huionaje?

4 Shetani hujaribu kuidharau Biblia, kitabu chenye thamani ambacho hutufundisha kumhusu Muumba wetu mwenye upendo. Watumishi wa Yehova wanaipenda na kuithamini Biblia. Tunajua kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho, bali si neno la mwanadamu. (1 Wathesalonike 2:13; 2 Timotheo 3:16) Hata hivyo, ulimwengu wa Shetani ungependa tuwe na maoni tofauti. Kwa mfano, utangulizi wa kitabu kimoja kinachoishambulia Biblia unasema: “Biblia si ‘takatifu’ wala si ‘neno la Mungu.’ Haikuandikwa na watakatifu walioongozwa na roho ya Mungu, bali iliandikwa na makasisi wenye kujitakia makuu.” Wale wanaoshawishiwa kuamini madai hayo huenda wakasadiki kwa urahisi maoni yaliyopotoka kwamba wako huru kumwabudu Mungu wapendavyo, au kutomwabudu hata kidogo.—Methali 14:12.

5. (a) Mwandishi mmoja alidai nini kuhusu dini zinazoikubali Biblia? (b) Maoni fulani ya kawaida katika ulimwengu hutofautianaje na vile Biblia husema? (Tia ndani sanduku kwenye ukurasa unaofuata.)

5 Mashambulizi ya moja kwa moja au yasiyo ya moja kwa moja dhidi ya Biblia, pamoja na unafiki wa kidini wa wale wanaodai kuiunga mkono, yamefanya wengi wachukizwe na dini, kutia ndani dini zinazoikubali Biblia. Dini zinashambuliwa na vyombo vya habari na wasomi. Mwandishi mmoja anasema: “Watu wengi wana maoni yasiyofaa kuhusu Dini ya Kiyahudi na ya Ukristo. Wale walio na maoni yanayofaa huziona kuwa zenye kuvutia kwa kuwa ni za kizamani; nao wale wasio na maoni yanayofaa huziona kuwa zimepitwa na wakati, nazo huzuia ukuzi wa akili na maendeleo ya kisayansi. Katika miaka ya hivi karibuni dharau imegeuka kuwa dhihaka na uhasama ulio wazi.” Mara nyingi uhasama huo hutokana na wale ambao hukana kwamba kuna Mungu na ambao wamekuwa “wajinga katika kufikiri kwao.”—Waroma 1:20-22.

6. Ulimwengu una maoni gani kuhusu mazoea ya kingono yanayoshutumiwa na Mungu?

6 Kwa hiyo, haishangazi kwamba watu wanazidi kuacha viwango vya Mungu kuhusu mwenendo. Kwa mfano, Biblia husema kwamba uhusiano wa kingono kati ya watu wa jinsi moja ni ‘jambo chafu.’ (Waroma 1:26, 27) Pia inasema kwamba wale wanaozoea kufanya uasherati na uzinzi hawataurithi Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 6:9) Hata hivyo, mazoea hayo ya kingono yanakubaliwa katika nchi nyingi na pia huonyeshwa kuwa yenye kuvutia katika vitabu, magazeti, nyimbo, sinema, na vipindi vya televisheni. Wale ambao hupinga mazoea hayo huonwa kuwa na akili finyu, wenye uchambuzi, na washamba. Badala ya kuona viwango vya Mungu kuwa wonyesho kwamba anatujali na kutupenda, ulimwengu huviona viwango hivyo kuwa vinawazuia wasipate uhuru na uradhi.—Methali 17:15; Yuda 4.

7. Tunapaswa kujiuliza maswali gani?

7 Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu unaozidi kumpinga Mungu, lingekuwa jambo la hekima kwetu kuchunguza mtazamo na maadili yetu. Pindi kwa pindi, tunapaswa kujichunguza kwa sala na kwa unyoofu ili kuhakikisha kwamba hatupeperuki pole kwa pole na kuacha kufuata maoni na viwango vya Yehova. Kwa mfano, huenda tukajiuliza: ‘Je, mimi hufurahia habari fulani ambazo ningeepuka miaka kadhaa iliyopita? Je, nimeanza kukubali mazoea yanayoshutumiwa na Mungu? Je, ninachukua mambo ya kiroho kwa uzito kama zamani au nimeanza kuyapuuza? Je, maisha yangu yanaonyesha kwamba ninatanguliza mambo ya Ufalme?’ (Mathayo 6:33) Kutafakari mambo hayo kutatusaidia kupinga roho ya ulimwengu.

‘Usipeperushwe Kamwe’

8. Mtu anawezaje kukengeuka na kumwacha Yehova?

8 Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Ni lazima kwetu kuyakazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo tuliyosikia, ili tusipeperushwe kamwe.” (Waebrania 2:1) Meli inapoanza kupeperuka na kuacha njia haiwezi kufika mahali inapoenda. Nahodha asipofikiria mwelekeo wa upepo na mkondo wa bahari, ni rahisi meli yake ipeperuke na kuacha bandari yenye usalama na kukwama kwenye ufuo wenye miamba. Vivyo hivyo, tusipofikiria kweli zenye thamani za Neno la Mungu, huenda ikawa rahisi kupeperuka na kumwacha Yehova, na kuharibikiwa na hali ya kiroho. Si lazima uache ukweli kabisa ndipo upate hasara hiyo. Kwa kweli, wengi hawamkatai Yehova ghafula na kimakusudi. Mara nyingi, pole kwa pole watu hao hujihusisha na jambo fulani ambalo huwakengeusha fikira wasitii Neno la Mungu. Bila kujua, wao hukengeuka na kuingia katika dhambi. Kama nahodha aliyelala, watu hao hawaamki hadi inapokuwa kuchelewa mno.

9. Yehova alimbariki Sulemani katika njia zipi?

9 Fikiria maisha ya Sulemani. Yehova alimfanya kuwa mfalme wa Israeli. Mungu alimruhusu Sulemani ajenge hekalu na akamwagiza aandike sehemu fulani za Biblia. Yehova alizungumza naye mara mbili na kumpa utajiri, umashuhuri, na utawala wenye amani. Isitoshe, Yehova alimbariki Sulemani kwa kumpa hekima nyingi. Biblia inasema: “Mungu akaendelea kumpa Sulemani hekima na uelewaji kwa wingi sana na ukunjufu wa moyo, kama mchanga ulio kando ya bahari. Na hekima ya Sulemani ilikuwa pana zaidi kuliko hekima ya watu wengine wote wa Mashariki na kuliko hekima yote ya Misri.” (1 Wafalme 4:21, 29, 30; 11:9) Bila shaka, huenda mtu akafikiri kwamba Sulemani alipaswa kuwa mwaminifu zaidi kwa Mungu. Lakini, Sulemani alipeperuka na kuwa mwasi-imani. Ilitukiaje?

10. Sulemani alishindwa kutii mwongozo gani, na matokeo yakawaje?

10 Sulemani alijua na kuielewa vizuri sana Sheria ya Mungu. Yaelekea angependezwa na maagizo yaliyowekwa kwa ajili ya wale waliokuwa wafalme wa Israeli. Kati ya maagizo hayo, moja lilisema: “[Mfalme] asizidishe wake kwa ajili yake, ili moyo wake usigeuke kando.” (Kumbukumbu la Torati 17:14, 17) Licha ya mwongozo huo ulio wazi, Sulemani alijipatia wanawake mia saba, na masuria mia tatu. Wengi wa wanawake hao waliabudu miungu ya kigeni. Hatujui kwa nini Sulemani alijipatia wake wengi hivyo, wala hatujui jinsi alivyojitetea kwa kufanya hivyo. Tunachojua ni kwamba hakutii mwongozo wa Mungu uliokuwa wazi. Matokeo yalikuwa sawa kabisa na jinsi Yehova alivyoonya. Tunasoma hivi: ‘Mwishowe wake za Sulemani waliugeuza moyo wake kufuata miungu mingine.’ (1 Wafalme 11:3, 4) Hatua kwa hatua, alipoteza hekima yake ya kimungu. Alipeperuka. Baada ya muda, tamaa ya Sulemani ya kuwapendeza wake zake wapagani ilifanya asiwe na tamaa ya kumtii na kumpendeza Mungu. Inasikitisha kama nini kwa kuwa Sulemani ndiye aliyeandika maneno haya hapo awali: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki”!—Methali 27:11.

Roho ya Ulimwengu Ina Nguvu

11. Mambo tunayolisha akili huathirije kufikiri kwetu?

11 Kielelezo cha Sulemani kinatufundisha kwamba ni hatari kufikiri kwamba kwa sababu tunajua ukweli, uvutano wa kilimwengu hautaathiri kufikiri kwetu. Kama vile chakula halisi huathiri mwili wetu, ndivyo yale tunayolisha akili zetu yanavyoweza kuathiri kufikiri kwetu na mtazamo wetu. Kwa kutambua jambo hilo, mashirika mbalimbali hutumia mabilioni ya dola kila mwaka kutangaza bidhaa zao. Ili matangazo yawe yenye matokeo, watangazaji hutumia maneno na picha zenye kuvutia ili kuamsha tamaa ya mnunuzi. Pia watangazaji wanajua kwamba kwa kawaida watu hawatashawishiwa kwenda mara moja kununua bidhaa wanapoona tangazo mara moja au mara mbili tu. Lakini, mwishowe wanunuzi wataanza kuvutiwa na bidhaa baada ya kuona tangazo tena na tena. Kutangaza bidhaa kuna matokeo, la sivyo, hakuna yeyote ambaye angetumia pesa kufanya matangazo hayo. Matangazo yana uvutano mkubwa juu ya kufikiri na mitazamo ya watu.

12. (a) Shetani huathirije kufikiri kwa watu? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Wakristo wanaweza kuathiriwa?

12 Kama mtangazaji bidhaa, Shetani hueneza mawazo yake kwa kuyafanya yaonekane kuwa yenye kuvutia, akijua kwamba baada ya muda anaweza kuwashawishi watu wakubali maoni yake. Kupitia vitumbuizo na njia nyingine, Shetani huwadanganya watu waamini kwamba wema ni ubaya na ubaya ni wema. (Isaya 5:20) Hata Wakristo wa kweli wamenaswa na kampeni ya Shetani ya kueneza habari za uwongo. Biblia huonya: “Neno lililoongozwa na roho linasema kwa hakika kwamba katika vipindi vya nyakati za mwisho wengine wataanguka kutoka kwenye imani, wakisikiliza maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha na mafundisho ya roho waovu, kwa unafiki wa watu wanaosema uwongo, waliotiwa alama katika dhamiri zao kama kwa chuma cha kutilia alama.”—1 Timotheo 4:1, 2; Yeremia 6:15.

13. Mashirika mabaya ni nini, nayo mashirika yetu hutuathirije?

13 Hakuna asiyeweza kuathiriwa na roho ya ulimwengu. Uvutano wa mfumo wa Shetani una nguvu. Kwa hekima, Biblia hutuhimiza hivi: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Mashirika mabaya yanaweza kuhusisha chochote au yeyote—hata kutanikoni—ambaye anadhihirisha roho ya ulimwengu. Tukisema kwamba mashirika mabaya hayawezi kutudhuru, basi tunaweza pia kusema kwamba mashirika mazuri hayawezi kutusaidia. Tungekuwa tumekosea kama nini! Biblia inaeleza jambo hilo waziwazi inaposema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.

14. Tunaweza kuipinga roho ya ulimwengu katika njia zipi?

14 Ili kupinga roho ya ulimwengu, lazima tushirikiane na watu wenye hekima, yaani, wale wanaomtumikia Yehova. Tunapaswa kulisha akili zetu mambo yanayojenga imani yetu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.” (Wafilipi 4:8) Kwa kuwa tuliumbwa tukiwa na uwezo wa kuchagua kati ya lililo zuri na lililo baya, tunaweza kuchagua mambo tunayoweza kufikiria. Sikuzote na tuchague kufikiria mambo yatakayotusaidia kumkaribia Yehova zaidi.

Roho ya Mungu Ina Nguvu Zaidi

15. Wakristo katika jiji la kale la Korintho walikuwaje tofauti na wakaaji wengine wa jiji hilo?

15 Tofauti na wale wanaopotoshwa na roho ya ulimwengu, Wakristo wa kweli wanaongozwa na roho takatifu ya Mungu. Paulo aliliandikia kutaniko la Korintho hivi: “Sisi tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu, ili tuyajue mambo ambayo Mungu ametupa sisi kwa fadhili.” (1 Wakorintho 2:12) Jiji la kale la Korintho lilikuwa limemezwa kabisa na roho ya ulimwengu. Wakaaji wake walikuwa wamepotoka sana kiadili hivi kwamba baadaye maneno “kuwa kama Wakorintho” yalimaanisha “kufanya uasherati.” Shetani alikuwa amepofusha akili za watu hao. Hivyo, hawakumwelewa Mungu wa kweli. (2 Wakorintho 4:4) Lakini kupitia roho yake takatifu, Yehova alifungua macho ya Wakorintho fulani, na kuwawezesha kuijua kweli. Roho yake iliwachochea na kuwaongoza kufanya mabadiliko makubwa maishani mwao ili wapate kibali na baraka zake. (1 Wakorintho 6:9-11) Ingawa roho ya ulimwengu ilikuwa yenye nguvu, roho ya Yehova ilikuwa yenye nguvu zaidi.

16. Tunawezaje kupokea na kudumisha roho ya Mungu?

16 Hali iko hivyo leo. Roho takatifu ya Yehova ndiyo nguvu kuu zaidi katika ulimwengu wote, naye huitoa kwa wingi kwa wote wanaoomba kwa imani ili waipate. (Luka 11:13) Hata hivyo, ili kupata roho ya Mungu, tunahitaji kufanya mengi zaidi kuliko tu kuipinga roho ya ulimwengu. Tunapaswa kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kulitumia maishani mwetu ili roho yetu, yaani, mwelekeo wetu wa akili, upatanishwe na kufikiri kwa Mungu. Tukifanya hivyo, Yehova atatuimarisha kupinga mbinu yoyote ambayo huenda Shetani akatumia ili kuharibu hali yetu ya kiroho.

17. Mambo yaliyompata Loti yanaweza kutufariji katika njia zipi?

17 Ingawa Wakristo si sehemu ya ulimwengu, wao wako katika ulimwengu. (Yohana 17:11, 16) Hakuna yeyote kati yetu anayeweza kuepuka kabisa roho ya ulimwengu, kwa kuwa huenda tukafanya kazi au kuishi na wale ambao hawampendi Mungu wala njia zake. Je, sisi tunahisi kama Loti “aliyetaabishwa sana,” hata kuteseka, kwa sababu ya vitendo vya kuasi sheria vilivyofanywa na watu wa Sodoma ambao aliishi kati yao? (2 Petro 2:7, 8) Ikiwa ndivyo, tunaweza kupata kitia-moyo. Yehova alimlinda na kumwokoa Loti, naye anaweza kutulinda na kutuokoa pia. Baba yetu mwenye upendo anaona na anajua hali zetu, naye anaweza kutusaidia na kutupatia nguvu tunazohitaji ili tudumishe hali nzuri ya kiroho. (Zaburi 33:18, 19) Tukimtegemea, kumtumaini, na kumuomba, atatusaidia kuipinga roho ya ulimwengu, hata hali yetu iwe ngumu kadiri gani.—Isaya 41:10.

18. Kwa nini tunapaswa kuthamini uhusiano wetu pamoja na Yehova?

18 Katika ulimwengu uliotengwa na Mungu na kudanganywa na Shetani, sisi watu wa Yehova tumebarikiwa kuijua ile kweli. Hivyo, tuna furaha na amani ambayo ulimwengu hauna. (Isaya 57:20, 21; Wagalatia 5:22) Tunafurahia tumaini zuri la kuishi milele katika Paradiso, ambako roho ya ulimwengu huu unaoangamia haitakuwapo tena. Kwa hiyo, na tuthamini uhusiano wetu mzuri pamoja na Mungu na kuwa macho kurekebisha mwelekeo wowote wa kupeperuka kiroho. Na tuzidi kumkaribia Yehova, naye atatusaidia kuipinga roho ya ulimwengu.—Yakobo 4:7, 8.

Je, Unaweza Kueleza?

• Shetani amewadanganya na kuwapotosha watu katika njia zipi?

• Tunawezaje kuepuka kupeperuka na kumwacha Yehova?

• Ni nini huonyesha kwamba roho ya ulimwengu ni yenye nguvu?

• Tunawezaje kupokea na kudumisha roho inayotoka kwa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Chati katika ukurasa wa 11]

TOFAUTI KATI YA HEKIMA YA ULIMWENGU NA HEKIMA YA MUNGU

Hakuna kweli kamili—watu hubuni kweli yao.

‘Neno la Mungu ni kweli.’—Yohana 17:17.

Tegemea hisia zako ili kuamua kati ya lililo zuri na lililo baya.

“Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.”—Yeremia 17:9.

Fanya utakalo.

“Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.

Mali ni ufunguo wa kupata furaha.

“Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.”—1 Timotheo 6:10.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Sulemani alipeperuka akaacha ibada ya kweli na kuanza kuabudu miungu ya uwongo

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kama mtangazaji bidhaa, Shetani hueneza roho ya ulimwengu. Je, wewe huipinga?