Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tegemea Roho ya Mungu Unaposhughulika na Mabadiliko ya Maisha

Tegemea Roho ya Mungu Unaposhughulika na Mabadiliko ya Maisha

Tegemea Roho ya Mungu Unaposhughulika na Mabadiliko ya Maisha

“Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa.”—2 TIMOTHEO 2:15.

1. Ni mabadiliko gani yanayoweza kutokeza magumu kuhusiana na hali yetu ya kiroho?

ULIMWENGU unaotuzunguka unaendelea kubadilika. Tunaona maendeleo yenye kuvutia ya kisayansi na kiteknolojia na wakati huohuo kuzorota sana kwa maadili. Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, Wakristo wanapaswa kupinga roho ya ulimwengu inayompinga Mungu. Hata hivyo, ulimwengu unapobadilika, nasi pia hubadilika katika njia nyingi. Tunakua na kuwa watu wazima. Tunaweza kupata au kupoteza mali, afya, na wapendwa wetu. Hatuwezi kuzuia mengi ya mabadiliko hayo, nayo yanaweza kutokeza hali mpya na ngumu sana kuhusiana na hali yetu ya kiroho.

2. Maisha ya Daudi yalibadilikaje?

2 Ni watu wachache wanaopatwa na mabadiliko kama yale yaliyompata Daudi, mwana wa Yese. Daudi aliyekuwa kijana mchungaji asiyejulikana, alibadilika upesi sana na kuwa shujaa wa kitaifa. Baadaye, alikuja kuwa mtoro, aliyewindwa kama mnyama na mfalme mwenye wivu. Baada ya hapo, Daudi akawa mfalme na mshindi. Alipatwa na maumivu makali ya dhambi nzito. Alipatwa na msiba na mgawanyiko katika familia yake. Alijipatia mali, akazeeka, na kupatwa na magonjwa yanayotokana na uzee. Hata hivyo, licha ya mabadiliko mengi katika maisha yake, Daudi alimtumaini Yehova na roho Yake katika maisha yake yote. Alifanya yote awezayo ili ‘akubaliwe na Mungu,’ naye Mungu alimbariki. (2 Timotheo 2:15) Ingawa hali zetu zinatofautiana na zile za Daudi, tunaweza kujifunza kutokana na jinsi alivyoshughulikia mambo katika maisha yake. Kielelezo chake kinaweza kutusaidia kuelewa jinsi tunavyoweza kuendelea kupata msaada wa roho ya Mungu tunapokabili mabadiliko maishani mwetu.

Unyenyekevu wa Daudi Ni Kielelezo Kizuri

3, 4. Daudi aliyekuwa kijana mchungaji asiyejulikana, alipataje kuwa mashuhuri katika nchi yake?

3 Akiwa mvulana, Daudi hakuwa mashuhuri hata katika familia yake. Nabii Samweli alipokuja Bethlehemu, baba ya Daudi aliwapitisha wanawe saba kati ya wana wanane mbele ya nabii huyo. Daudi, mwanaye mdogo zaidi, aliachwa akichunga kondoo. Lakini Yehova alikuwa amemchagua Daudi kuwa mfalme wa wakati ujao wa Israeli. Daudi aliitwa kutoka kondeni. Halafu, Biblia inasema: “Samweli akachukua ile pembe ya mafuta, akamtia mafuta katikati ya ndugu zake. Na roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu ya Daudi kuanzia siku hiyo na kuendelea.” (1 Samweli 16:12, 13) Daudi aliitegemea roho hiyo katika maisha yake yote.

4 Muda si muda, mvulana huyo aliyekuwa mchungaji angekuwa mashuhuri katika nchi yake. Alialikwa kumhudumia mfalme na kumchezea muziki. Alimuua shujaa wa vita Goliathi, jitu ambalo hata askari wenye uzoefu wa Israeli waliogopa kulikabili. Baada ya kuwekwa kuwa kiongozi wa wanaume wa vita, Daudi alipigana na Wafilisti na kuwashinda. Watu walimpenda na kutunga nyimbo za kumsifu. Awali, mshauri mmoja wa Mfalme Sauli alisema kwamba Daudi mchanga alikuwa “mwenye ustadi wa kukipiga” kinubi na pia “shujaa, mwanamume mwenye nguvu, na mwanamume wa vita na msemaji mwenye akili na mwanamume mwenye umbo zuri.”—1 Samweli 16:18; 17:23, 24, 45-51; 18:5-7.

5. Ni nini ambacho kingemfanya Daudi awe na kiburi, na tunajuaje kwamba hakuwa mwenye kiburi?

5 Yaonekana Daudi alikuwa na sifa zote nzuri ambazo mtu angetamani kuwa nazo, ambazo ni umashuhuri, sura nzuri, ujana, ufasaha, ustadi wa kupiga muziki, ustadi wa vita, na kibali cha Mungu. Yoyote kati ya sifa hizo ingemfanya awe na kiburi, lakini haikuwa hivyo. Ona jinsi Daudi alivyomjibu Mfalme Sauli, ambaye alimpa binti yake awe mke wake. Daudi alisema hivi kwa unyenyekevu wa kweli: “Mimi ni nani na watu wa ukoo wangu ni nani, familia ya baba yangu, katika Israeli, hata niwe mwana-mkwe wa mfalme?” (1 Samweli 18:18) Msomi mmoja aliandika hivi kwa kufafanua mstari huo: “Daudi alimaanisha kwamba, wala sifa zake, wala cheo chake, wala ukoo wake, haungemfanya adai kwamba alistahili heshima ya kuwa mwana-mkwe wa mfalme.”

6. Kwa nini tusitawishe unyenyekevu?

6 Daudi alikuwa mnyenyekevu kwa sababu alitambua kwamba Yehova ni mkuu sana na hawezi kulinganishwa kwa njia yoyote na wanadamu wasio wakamilifu. Daudi alistaajabu kwamba Mungu hata humtambua mwanadamu. (Zaburi 144:3) Pia Daudi alijua kwamba umashuhuri wowote ambao huenda alikuwa nao ulitokana na uhakika wa kwamba Yehova alionyesha unyenyekevu, akijishusha kumtegemeza, kumlinda, na kumtunza. (Zaburi 18:35) Tunajifunza jambo zuri kama nini! Vipawa vyetu, mafanikio yetu, na mapendeleo yetu hayapaswi kamwe kufanya tuwe wenye kiburi. Mtume Paulo aliandika: “Kwa kweli, una nini ambacho hukupokea? Basi, ikiwa kwa kweli ulikipokea, kwa nini unajisifu kana kwamba hukukipokea?” (1 Wakorintho 4:7) Tunapaswa kusitawisha na kudumisha unyenyekevu ili kupata roho takatifu ya Mungu na kibali chake.—Yakobo 4:6.

“Msijilipize Kisasi”

7. Daudi alipata nafasi gani ya kumuua Mfalme Sauli?

7 Ingawa umashuhuri wa Daudi haukumfanya awe mwenye kiburi, ulifanya Mfalme Sauli, ambaye roho ya Mungu ilikuwa imemwacha, awe na wivu mkatili. Ingawa Daudi hakuwa amefanya kosa lolote, alikimbia ili kuokoa maisha yake na kwenda kuishi nyikani. Pindi moja, alipokuwa anaendelea kumfuata Daudi, Mfalme Sauli aliingia pangoni, bila kujua kwamba Daudi na watu wake walikuwa wamejificha ndani. Wanaume wa Daudi walimhimiza atumie nafasi ambayo ilionekana kuwa imeandaliwa na Mungu ili amuue Sauli. Tunaweza kuwazia wakimnong’onezea Daudi hivi gizani: “Hii ndiyo siku ambayo Yehova anakuambia, ‘Tazama! Ninamtia adui yako mkononi mwako, nawe umtendee kama inavyoonekana vema machoni pako.’”—1 Samweli 24:2-6.

8. Kwa nini Daudi alijizuia asilipize kisasi?

8 Daudi alikataa kumdhuru Sauli. Kwa kuwa alikuwa na imani na subira, aliridhika kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Baada ya mfalme huyo kuondoka pangoni, Daudi alimwita kwa sauti na kumwambia: “Yehova na ahukumu kati yangu na wewe; na Yehova anilipizie kisasi kutoka kwako, lakini mkono wangu mwenyewe hautakuja juu yako.” (1 Samweli 24:12) Ingawa alijua kwamba Sauli alikuwa amefanya kosa, Daudi hakulipiza kisasi, wala hakumtukana Sauli. Katika pindi nyingine kadhaa, Daudi alijizuia asilipize kisasi. Badala yake, alimtegemea Yehova arekebishe mambo.—1 Samweli 25:32-34; 26:10, 11.

9. Kwa nini hatupaswi kulipiza kisasi tukipingwa au kunyanyaswa?

9 Kama Daudi, unaweza kujikuta katika hali ngumu. Labda unapingwa au unanyanyaswa na wanashule wenzako, wafanyakazi wenzako, watu wa familia, au watu wengine ambao hawakubali imani yako. Usilipize kisasi. Mngojee Yehova na kumwomba roho yake takatifu ikusaidie. Yaelekea watu hao wasioamini watavutiwa na mwenendo wako mzuri na kuwa waamini. (1 Petro 3:1) Hata iweje, uwe na hakika kwamba Yehova anaona hali yako naye atachukua hatua fulani kuihusu katika wakati wake unaofaa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’”—Waroma 12:19.

“Sikiliza Nidhamu”

10. Daudi alianguka katika dhambi jinsi gani, naye alijaribuje kuificha?

10 Baada ya miaka kadhaa kupita, Daudi akawa mfalme mpendwa na mashuhuri sana. Daudi alionyesha uaminifu wa pekee maishani mwake, na pia akaandika zaburi za kumsifu Yehova, mambo ambayo kwa urahisi yanaweza kufanya ufikiri kwamba hangeanguka katika dhambi nzito kamwe. Hata hivyo, alianguka. Siku moja, mfalme alipokuwa juu ya dari alimwona mwanamke mrembo akioga na kuulizia habari zake. Alipojua kwamba mwanamke huyo aliitwa Bath-Sheba na kwamba mume wake, Uria, alikuwa vitani, Daudi alituma watu wamlete naye akafanya ngono naye. Baadaye, aligundua kwamba mwanamke huyo alishika mimba. Jambo hilo lingemletea aibu iliyoje kama lingejulikana! Chini ya Sheria ya Musa, uzinzi ni tendo lililostahili adhabu ya kifo. Yaonekana mfalme alifikiri kwamba dhambi hiyo ingeweza kufichwa. Hivyo, akalitumia jeshi ujumbe na kuagiza kwamba Uria arudi Yerusalemu. Daudi alitumaini kwamba Uria angelala na Bath-Sheba usiku huo, lakini hakufanya hivyo. Akiwa amefadhaika, Daudi alimwambia Uria arudi vitani na kumpa barua ampelekee Yoabu, kamanda wa jeshi. Barua hiyo iliagiza kwamba Uria awekwe mahali ambapo angeweza kushambuliwa na kuuawa. Yoabu alitii, naye Uria akauawa. Baada ya Bath-Sheba kumaliza kipindi cha kuomboleza kama ilivyokuwa desturi, Daudi alimchukua awe mke wake.—2 Samweli 11:1-27.

11. Nathani alimsimulia Daudi kisa gani, naye Daudi alitendaje?

11 Njama yake ilionekana kufanikiwa, ingawa Daudi alipaswa kujua kwamba Yehova aliona kila kitu. (Waebrania 4:13) Baada ya miezi kadhaa kupita, mtoto alizaliwa. Ndipo, Mungu akamtuma nabii Nathani kwa Daudi. Nabii huyo alimsimulia mfalme kisa ambacho tajiri fulani aliyekuwa na kondoo wengi alimchinja kondoo mmoja tu aliyependwa wa mtu maskini. Kisa hicho kilimfanya Daudi atake sana kuona haki ikitekelezwa lakini hakujua kwamba kisa hicho kilikuwa na maana iliyofichwa. Daudi alimhukumu mara moja tajiri huyo. Akiwaka hasira, Daudi alimwambia Nathani hivi: “Mtu huyo aliyefanya hivyo anastahili kufa!”—2 Samweli 12:1-6.

12. Yehova alitoa hukumu gani dhidi ya Daudi?

12 “Wewe mwenyewe ndiye yule mwanamume!” nabii huyo akasema. Daudi alikuwa amejihukumu mwenyewe. Bila shaka, hasira ya Daudi ilibadilika mara moja na kuwa aibu na huzuni kuu. Kwa kushtuka sana, Daudi alimsikiliza Nathani alipotoa hukumu ya Yehova isiyoweza kuepukika. Hakumwambia neno lolote la kumfariji. Daudi alikuwa amelidharau neno la Yehova kwa kufanya lililo baya. Alimuua Uria kwa upanga wa adui. Hivyo, upanga haungeondoka nyumbani mwa Daudi. Alikuwa amemchukua mke wa Uria kisiri. Hivyo, uovu kama huo ungempata hadharani, bali si katika siri.—2 Samweli 12:7-12.

13. Daudi aliitikiaje nidhamu ya Yehova?

13 Daudi anaweza kupongezwa kwamba hakukataa kosa lake, wala hakumgombeza nabii Nathani. Hakuwalaumu wengine wala kujitetea kuhusiana na kosa lake. Alipoelezwa kuhusu dhambi yake, Daudi alikubali kosa lake na kusema: “Nimemtendea Yehova dhambi.” (2 Samweli 12:13) Zaburi ya 51 inaonyesha maumivu makali yaliyotokana na kosa lake na uzito wa toba yake. Alimsihi Yehova hivi: “Usinitupilie mbali na uso wako; wala usiniondolee roho yako takatifu.” Aliamini kwamba Yehova, katika rehema zake, hangeudharau “moyo uliovunjika na kupondwa” kwa sababu ya dhambi. (Zaburi 51:11, 17) Daudi aliendelea kutegemea roho ya Mungu. Ingawa Yehova alimsamehe Daudi yeye hakumlinda asipatwe na matokeo mabaya ya dhambi yake.

14. Tunapaswa kuitikiaje nidhamu ya Yehova?

14 Sote si wakamilifu na hufanya dhambi. (Waroma 3:23) Wakati mwingine tunaweza kuanguka katika dhambi nzito kama vile Daudi. Kama vile baba mwenye upendo huwatia nidhamu watoto wake, Yehova huwarekebisha wale wanaojitahidi kumtumikia. Hata hivyo, ingawa nidhamu ina manufaa, si rahisi kuikubali. Hata wakati mwingine ni “yenye kuhuzunisha.” (Waebrania 12:6, 11) Lakini ‘tukisikiliza nidhamu,’ tunaweza kupatanishwa na Yehova. (Methali 8:33) Ili tuendelee kupata baraka za roho ya Yehova, ni lazima tukubali kurekebishwa na kujitahidi kupata kibali chake.

Usiutumaini Utajiri Usio Hakika

15. (a) Watu fulani hutumiaje utajiri wao? (b) Daudi alitamani kutumia mali yake jinsi gani?

15 Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Daudi alitoka katika jamii ya tabaka la juu au familia yenye mali. Hata hivyo, wakati wa utawala wake, Daudi alipata mali nyingi. Kama unavyojua, watu wengi hujirundikia mali, hujaribu kuiongeza kwa pupa, au kuitumia kwa ubinafsi. Wengine hutumia pesa zao kujitukuza. (Mathayo 6:2) Daudi alitumia mali yake kwa njia tofauti. Alitamani kumtukuza Yehova. Daudi alimweleza Nathani tamaa yake ya kumjengea Yehova hekalu ili kuliweka ndani sanduku la agano, ambalo wakati huo lilikuwa Yerusalemu ‘likikaa katikati ya vitambaa vya mahema.’ Yehova alipendezwa na yale ambayo Daudi alikusudia kufanya, lakini kupitia Nathani akamwambia Daudi kwamba Sulemani mwanaye ndiye angejenga hekalu hilo.—2 Samweli 7:1, 2, 12, 13.

16. Daudi alifanya matayarisho gani kwa ajili ya ujenzi wa hekalu?

16 Daudi alikusanya vifaa ambavyo vingetumiwa katika ujenzi huo mkubwa naye akamwambia Sulemani hivi: “Nimetayarisha kwa ajili ya nyumba ya Yehova talanta mia moja elfu za dhahabu na talanta milioni moja za fedha, na hakuna namna ya kupima uzito wa shaba na chuma kwa sababu zimekuwa nyingi sana; nami nimetayarisha mbao na mawe, lakini utaviongeza vitu hivyo.” Alichanga talanta 3,000 za dhahabu na 7,000 za fedha kutoka katika hazina yake mwenyewe. * (1 Mambo ya Nyakati 22:14; 29:3, 4) Daudi alitoa kwa ukarimu ili kuonyesha imani na ujitoaji wake kwa Yehova Mungu, wala si kujionyesha. Kwa kutambua Chanzo cha utajiri wake, alimwambia Yehova hivi: “Maana kila kitu hutoka kwako, nasi tumekupa kutoka katika mkono wako mwenyewe.” (1 Mambo ya Nyakati 29:14) Moyo mkarimu wa Daudi ulimchochea afanye yote awezayo ili kuendeleza ibada safi.

17. Shauri katika 1 Timotheo 6:17-19 linawahusuje matajiri na maskini?

17 Vivyo hivyo, na tutumie mali zetu kufanya mema. Badala ya kuishi maisha ya kufuatia vitu vya kimwili, ni afadhali kutafuta kibali cha Mungu, kwa kuwa hiyo ndiyo njia ya kupata hekima na furaha ya kweli. Paulo aliandika hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo wa sasa wasitake makuu, na waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie; wafanye mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki, wakijiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.” (1 Timotheo 6:17-19) Hata hali yetu ya kiuchumi iweje, na tutegemee roho ya Mungu na kuishi maisha yatakayotufanya tuwe “tajiri kwa Mungu.” (Luka 12:21) Hakuna kitu chenye thamani zaidi kuliko kuwa na msimamo unaokubalika na Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo.

Jitoe kwa Mungu Ukiwa Mtu Aliyekubaliwa

18. Daudi aliweka kielelezo kizuri kwa Wakristo katika njia gani?

18 Katika maisha yake yote, Daudi alitafuta kibali cha Yehova. Aliimba hivi: “Unionyeshe kibali, Ee Mungu, unionyeshe kibali, kwa maana nafsi yangu imekukimbilia wewe.” (Zaburi 57:1) Hakumtumaini Yehova bure. Daudi alizeeka akiwa mwenye ‘kushiba siku.’ (1 Mambo ya Nyakati 23:1) Ingawa Daudi alifanya makosa mazito, anakumbukwa kuwa mmoja wa mashahidi wengi wa Mungu walioonyesha imani ya kipekee.—Waebrania 11:32.

19. Tunawezaje kujitoa kwa Mungu tukiwa watu wanaokubalika?

19 Unapokabili hali zinazobadilika maishani, kumbuka kwamba Yehova anaweza kukutegemeza, kukuimarisha, na kukurekebisha kama alivyomfanyia Daudi. Kama Daudi, mtume Paulo alikabili mabadiliko mengi maishani mwake. Lakini yeye pia aliendelea kuwa mwaminifu kwa kutegemea roho ya Mungu. Aliandika: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:12, 13) Tukimtegemea Yehova, atatusaidia kufanikiwa maishani, kwa kuwa anataka tufanikiwe. Tukimsikiliza na kumkaribia, atatuimarisha kufanya mapenzi yake. Na tukiendelea kutegemea roho ya Mungu, tutaweza ‘kujitoa kwa Mungu tukiwa watu waliokubaliwa’ sasa na milele.—2 Timotheo 2:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Kulingana na viwango vya leo, mchango ambao Daudi alitoa, una thamani ya zaidi ya dola 1,200,000,000 za Marekani.

Ungejibuje?

• Tunawezaje kujilinda dhidi ya kiburi?

• Kwa nini hatupaswi kulipiza kisasi?

• Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu nidhamu?

• Kwa nini tunapaswa kumtumaini Mungu wala si utajiri?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Daudi alitegemea roho ya Mungu na kujitahidi kupata kibali chake. Je, unafanya vivyo hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 18]

“Kila kitu hutoka kwako, nasi tumekupa kutoka katika mkono wako mwenyewe”