Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mapenzi ya Mungu Yanafanywa?

Je, Mapenzi ya Mungu Yanafanywa?

Je, Mapenzi ya Mungu Yanafanywa?

“Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:10.

JULIO na Christina walitazama kwa hofu huku watoto wao wanne wakiteketea kwa moto hadi kifo. Gari lao lililokuwa limeegeshwa liligongwa na dereva aliyekuwa mlevi, kisha likashika moto. Marcos, mtoto wao wa tano, aliokolewa katika moto huo, lakini alikuwa amechomeka na sura yake kuharibika kabisa. Alikuwa na umri wa miaka tisa. Baba yake alihuzunika sana. Alijifariji na pia kuifariji familia yake kwa maneno haya: “Hata hali ziweje, nzuri au mbaya, tunapaswa kuelewa kwamba haya ni mapenzi ya Mungu.”

Tukio lenye kuhuzunisha kama hilo linapotokea, watu wengi wanakuwa na maoni hayohayo. Wao husema, ‘Ikiwa Mungu ana nguvu zote na anatujali, lazima yale ambayo yametukia yawe yanatunufaisha kwa njia fulani, ingawa huenda ikawa vigumu kuelewa jambo hilo.’ Je, unakubaliana na maoni hayo?

Mara nyingi maneno ya Yesu katika ile iitwayo Sala ya Bwana ambayo imenukuliwa juu, hufanya watu wafikiri kwamba lolote linalotukia, liwe zuri au baya, ni udhihirisho wa mapenzi ya Mungu. Mapenzi ya Mungu yanafanywa mbinguni, sivyo? Tunaposali ‘Mapenzi yako yatendeke duniani,’ je, hatumaanishi kwamba yale yanayotukia duniani ni mapenzi ya Mungu?

Watu wengi wana shaka kuhusiana na maoni hayo. Kulingana nao, yanaonyesha kwamba Mungu hajali hisia za viumbe wake wa kibinadamu. Wanauliza, ‘Ingewezaje kuwa mapenzi ya Mungu mwenye upendo kwamba watu wasio na hatia wapatwe na mambo yenye kutisha?’ ‘Ikiwa Mungu anataka tujifunze jambo fulani kutokana na mambo mabaya yanayotokea, hilo linaweza kuwa jambo gani?’ Labda hivyo ndivyo unavyohisi.

Kuhusiana na jambo hilo, mwanafunzi Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, aliandika: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Mungu hasababishi maovu. Kwa hiyo, ni wazi kwamba si mambo yote yanayotukia duniani leo ambayo ni mapenzi ya Mungu. Biblia pia inataja mapenzi ya mwanadamu, mapenzi ya mataifa, na hata mapenzi ya Ibilisi. (Yohana 1:13; 2 Timotheo 2:26; 1 Petro 4:3) Je, unakubali kwamba yale yaliyoipata familia ya Julio na Christina hayakuwa mapenzi ya Baba wa mbinguni mwenye upendo?

Hivyo, Yesu alimaanisha nini alipowafundisha wanafunzi wake wasali: ‘Mapenzi yako na yatendeke’? Je, Yesu alikuwa tu anamwomba Mungu aingilie kati hali fulani hususa, au alikuwa akitufundisha tuombe kitu fulani muhimu na chema zaidi, yaani, badiliko ambalo sote tunaweza kutumainia? Na tuchunguze zaidi yale ambayo Biblia inasema.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

Car: Dominique Faget-STF/AFP/Getty Images; child: FAO photo/B. Imevbore