Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Lazima Watu wa Mungu Wapende Fadhili

Lazima Watu wa Mungu Wapende Fadhili

Lazima Watu wa Mungu Wapende Fadhili

“Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?”—MIKA 6:8.

1, 2. (a) Kwa nini hatupaswi kushangaa kwamba Yehova anatazamia watu wake waonyeshe fadhili? (b) Tunapaswa kuchunguza maswali gani kuhusu fadhili?

YEHOVA ni Mungu wa fadhili. (Waroma 2:4; 11:22) Bila shaka, wenzi wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, walithamini sana fadhili za Mungu. Katika bustani ya Edeni, walizungukwa na uumbaji wenye kuonekana, jambo lililothibitisha kwamba Mungu ana fadhili kuelekea wanadamu, ambao wangeweza kuufurahia uumbaji huo. Naye Mungu anaendelea kuwa mwenye fadhili kwa wote, hata kwa watu waovu na wasio na shukrani.

2 Kwa kuwa wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu, wana uwezo wa kudhihirisha sifa za kimungu. (Mwanzo 1:26) Hivyo, haishangazi kwamba Yehova anatarajia tuonyeshe fadhili. Kama vile andiko la Mika 6:8 lisemavyo, ni lazima watu wa Mungu ‘wapende fadhili.’ Lakini fadhili ni nini? Nayo inahusianaje na sifa nyingine za kimungu? Kwa kuwa wanadamu wanaweza kuonyesha fadhili, kwa nini ulimwengu ni mahali penye ukatili hivyo? Kwa nini sisi tukiwa Wakristo tunapaswa kujitahidi kuonyesha fadhili tunaposhughulika na wengine?

Fadhili Ni Nini?

3. Ungefafanuaje fadhili?

3 Fadhili huonyeshwa kwa kuhangaikia hali njema ya wengine. Inaonyeshwa kwa kuwasaidia wengine na kuzungumza nao kwa ufikirio. Kuwa mwenye fadhili humaanisha kutenda mema badala ya kutenda mambo yenye kudhuru. Mtu mwenye fadhili ni mpole, mwenye urafiki, huruma, na neema. Yeye ni mkarimu na huwaonyesha wengine ufikirio. Mtume Paulo aliwashauri Wakristo hivi: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Hivyo basi, fadhili ni sehemu ya vazi la mfano la kila Mkristo wa kweli.

4. Yehova amechukuaje hatua ya kwanza katika kuonyesha wanadamu fadhili?

4 Yehova Mungu amechukua hatua ya kwanza katika kuonyesha fadhili. Kama Paulo alivyosema, wakati “Mwokozi wetu, Mungu, alipoonyesha fadhili na upendo kwa mwanadamu” ndipo ‘alipotuokoa kupitia kuoshwa kulikotuleta kwenye uzima na kupitia kutufanya sisi kuwa wapya kwa roho takatifu.’ (Tito 3:4, 5) Mungu ‘huwaosha,’ au huwasafisha, Wakristo watiwa-mafuta katika damu ya Yesu, akitumia manufaa ya dhabihu ya fidia ya Kristo kwa ajili yao. Wao pia hufanywa wapya kupitia roho takatifu na kuwa ‘viumbe wapya,’ wakiwa wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho. (2 Wakorintho 5:17) Isitoshe, Mungu huonyesha upendo na fadhili kwa “umati mkubwa,” ambao ‘umefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.’—Ufunuo 7:9, 14; 1 Yohana 2:1, 2.

5. Kwa nini wale wanaoongozwa na roho ya Mungu wanapaswa kuwaonyesha wengine fadhili?

5 Pia, fadhili ni sehemu ya matunda ya roho takatifu au nguvu za utendaji za Mungu. Paulo alisema: “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia. Hakuna sheria juu ya mambo hayo.” (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo basi, wale wanaoongozwa na roho ya Mungu wanapaswa kuwaonyesha wengine fadhili.

Fadhili ya Kweli Si Udhaifu

6. Ni wakati gani fadhili zinaweza kuwa udhaifu, na kwa nini?

6 Watu fulani huona fadhili kuwa udhaifu. Wanaona kwamba lazima nyakati nyingine mtu awe mgumu, na hata mjeuri ili wengine wamtambue. Hata hivyo, ukweli ni kwamba mtu anahitaji nguvu kwelikweli ili kuonyesha fadhili za kweli na kuepuka kuonyesha fadhili zisizofaa. Kwa kuwa fadhili za kweli ni sehemu ya matunda ya roho ya Mungu, fadhili hizo haziwezi kuwa mtazamo dhaifu wa kupuuza mwenendo mbaya. Kwa upande mwingine, fadhili zisizofaa ni udhaifu ambao humfanya mtu afumbie macho mwenendo mbaya.

7. (a) Eli alionyeshaje kwamba alikuwa mlegevu? (b) Kwa nini wazee wanapaswa kuwa waangalifu wasionyeshe fadhili zisizofaa?

7 Kwa mfano, fikiria Eli, kuhani mkuu wa Israeli. Alilegea katika kuwaadhibu wana wake, Hofni na Finehasi, waliokuwa wakitumikia wakiwa makuhani kwenye maskani. Kwa kuwa hawakuridhika na fungu la dhabihu ambalo Sheria ya Mungu iliagiza wapewe, walimwambia mtumishi adai kwa nguvu nyama mbichi kutoka kwa mwenye kutoa dhabihu kabla ya kufukiza moshi wa mafuta kwenye madhabahu. Pia wana wa Eli walifanya uasherati na wanawake waliotumikia kwenye mwingilio wa maskani. Hata hivyo, badala ya kuwaachisha Hofni na Finehasi kazi ya ukuhani, Eli aliwakemea tu kwa upole. (1 Samweli 2:12-29) Haishangazi kwamba “neno kutoka kwa Yehova lilikuwa limekuwa haba siku hizo”! (1 Samweli 3:1) Lazima wazee Wakristo wawe waangalifu ili wasionyeshe fadhili zisizofaa kwa wakosaji ambao wanaweza kuhatarisha hali ya kiroho ya kutaniko. Ukiwa na fadhili za kweli hutapuuza maneno na matendo maovu ambayo huvunja kanuni za Mungu.

8. Yesu alionyeshaje fadhili za kweli?

8 Yesu Kristo, ambaye ni Kielelezo chetu, hakuonyesha kamwe fadhili zisizofaa. Aliweka kielelezo bora sana katika kuonyesha fadhili za kweli. Kwa mfano, ‘aliwaonyesha watu upendo mwororo kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ Watu wanyoofu hawakuogopa kumfikia Yesu, hata walimletea watoto wao wadogo. Wazia fadhili na huruma alizoonyesha ‘alipowachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki.’ (Mathayo 9:36; Marko 10:13-16) Ingawa Yesu alikuwa mwenye fadhili, alikuwa pia imara alipotetea yaliyo sawa machoni pa Baba yake wa mbinguni. Yesu hakuvumilia uovu kamwe; alikuwa na nguvu kutoka kwa Mungu za kuwashutumu viongozi wa kidini wanafiki. Kama inavyoonyeshwa katika Mathayo 23:13-26, alirudia mara kadhaa maneno haya: “Ole wenu ninyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki!”

Fadhili na Sifa Nyingine za Kimungu

9. Sifa ya fadhili inahusianaje na ustahimilivu na wema?

9 Sifa ya fadhili inahusiana na sifa nyingine zinazotokezwa na roho ya Mungu. Sifa hiyo imeorodheshwa katikati ya “ustahimilivu” na “wema.” Kwa kweli, mtu anayesitawisha sifa ya fadhili, huionyesha kwa kuwa mstahimilivu. Anakuwa mwenye subira hata kwa watu wasio na fadhili. Sifa ya fadhili inahusiana na wema katika maana ya kwamba, mara nyingi sifa hiyo huonyeshwa kwa kufanya mambo yanayowanufaisha wengine. Nyakati nyingine, neno la Kigiriki linalotumiwa katika Biblia kumaanisha “fadhili” linaweza kutafsiriwa kuwa “wema.” Wapagani walishangazwa sana na jinsi Wakristo wa mapema walivyoonyesha sifa hiyo hivi kwamba kulingana na Tertullian, waliwaita wafuasi hao wa Yesu ‘watu ambao wanaonyesha fadhili kwa kiwango cha juu zaidi.’

10. Fadhili na upendo zinahusianaje?

10 Kuna uhusiano kati ya fadhili na upendo. Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Na kuhusu upendo huo Paulo alisema: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili.” (1 Wakorintho 13:4) Sifa ya fadhili pia imehusianishwa na upendo katika maneno “fadhili zenye upendo,” ambayo yametumiwa mara nyingi katika Biblia. Hizi ni fadhili zinazotokana na upendo mshikamanifu. Nomino ya Kiebrania inayotafsiriwa “fadhili zenye upendo” inahusisha mengi zaidi ya upendo mwororo. Ni fadhili ambazo hushikamana kwa upendo na kitu fulani hadi kusudi la kitu hicho litimie. Fadhili zenye upendo za Yehova, au upendo mshikamanifu, huonyeshwa katika njia mbalimbali. Kwa mfano, sifa hiyo huonekana katika matendo yake ya kuokoa na kulinda.—Zaburi 6:4; 40:11; 143:12.

11. Fadhili zenye upendo za Mungu hutupa uhakikisho gani?

11 Fadhili zenye upendo za Yehova huwavuta watu kwake. (Yeremia 31:3) Watumishi waaminifu wa Mungu wanapohitaji kukombolewa au kusaidiwa, wanajua kwamba hakika atawaonyesha fadhili zenye upendo. Hatakosa kufanya hivyo. Hivyo, wanaweza kusali kwa imani kama mtunga-zaburi aliyesema: “Nami nimezitegemea fadhili zako zenye upendo; moyo wangu na ushangilie katika wokovu wako.” (Zaburi 13:5) Kwa kuwa upendo wa Mungu ni mshikamanifu, watumishi wake wanaweza kumtegemea kabisa. Wamehakikishiwa hivi: “Yehova hatawaacha watu wake, wala hatauacha urithi wake mwenyewe.”—Zaburi 94:14.

Kwa Nini Ulimwengu Una Ukatili Mwingi?

12. Utawala wenye kukandamiza ulianza lini na jinsi gani?

12 Jibu la swali hilo linahusiana na yale yaliyotukia katika bustani ya Edeni. Mapema katika historia ya wanadamu, kiumbe mmoja wa roho ambaye aligeuka kuwa mwenye ubinafsi na kiburi, alipanga njama ya kuwa mtawala wa ulimwengu. Kwa sababu hiyo, yeye akawa “mtawala wa ulimwengu huu,” mwenye kukandamiza kwelikweli. (Yohana 12:31) Mtawala huyo akaitwa Shetani Ibilisi, mpinzani mkuu wa Mungu na mwanadamu. (Yohana 8:44; Ufunuo 12:9) Njama yake yenye ubinafsi ya kuanzisha utawala wenye kupinga utawala wenye fadhili wa Yehova ilifichuliwa punde baada ya Hawa kuumbwa. Kwa hiyo, utawala mbaya ulianza wakati Adamu alipokataa utawala wa Mungu, na hivyo kukataa kabisa fadhili Zake. (Mwanzo 3:1-6) Badala ya kupata uhuru wa kweli, Adamu na Hawa walijikuta chini ya uvutano wa Ibilisi wenye ubinafsi na wenye kiburi, hivyo wakawa raia za utawala wake.

13-15. (a) Ni nini baadhi ya matokeo ya kukataa utawala mwadilifu wa Yehova? (b) Kwa nini ulimwengu huu ni mahali penye ukatili?

13 Na tufikirie baadhi ya matokeo ya utawala huo. Adamu na Hawa walifukuzwa kutoka eneo la dunia lililokuwa paradiso. Waliondoka katika bustani nzuri ambapo wangeweza kupata kwa urahisi mimea na matunda yenye kujenga afya, nao wakaenda kuishi maisha magumu nje ya bustani ya Edeni. Mungu alimwambia Adamu: “Kwa sababu uliisikiliza sauti ya mke wako ukala matunda ya mti ambao nilikupa amri hii kuuhusu, ‘Usile matunda yake,’ udongo umelaaniwa kwa sababu yako. Kwa maumivu utakula mazao yake siku zote za maisha yako. Nao utakuzalia miiba na mibaruti.” Laana iliyotolewa juu ya udongo ilimaanisha kwamba sasa ingekuwa vigumu sana kuulima. Wazao wa Adamu waliathiriwa sana na matokeo ya kulaaniwa kwa udongo, uliotokeza miiba na mibaruti, hivi kwamba Lameki, baba ya Noa, alitaja kuhusu ‘maumivu ya mikono yao yaliyoletwa na udongo ambao Yehova aliulaani.’—Mwanzo 3:17-19; 5:29.

14 Adamu na Hawa pia walipoteza utulivu na kuingia katika taabu. Mungu alimwambia Hawa hivi: “Nitazidisha sana maumivu ya mimba yako; kwa uchungu utazaa watoto, na tamaa yako itakuwa kwa mume wako, naye atakutawala.” Baadaye, Kaini, mzaliwa wa kwanza wa Adamu na Hawa, alitenda kitendo kikatili cha kumuua ndugu yake Abeli.—Mwanzo 3:16; 4:8.

15 “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” akasema mtume Yohana. (1 Yohana 5:19) Leo, ulimwengu unadhihirisha sifa mbovu kama za mtawala wake ambazo zinatia ndani ubinafsi na kiburi. Haishangazi kwamba umejaa ukatili! Lakini hali hazitakuwa hivyo milele. Yehova atahakikisha kwamba chini ya Ufalme wake watu wataonyesha fadhili na huruma nyingi badala ya ukatili.

Kutakuwa na Fadhili Nyingi Chini ya Ufalme wa Mungu

16. Kwa nini utawala wa Mungu kupitia Kristo Yesu ni wenye fadhili, na hilo hufanya tuwe na wajibu gani?

16 Yehova pamoja na Kristo Yesu, Mfalme wa Ufalme Wake aliyewekwa, wanataka raia zao wawe na sifa ya fadhili. (Mika 6:8) Yesu Kristo alituonyesha kimbele kwamba serikali aliyopewa na Baba yake ingekuwa yenye fadhili. (Waebrania 1:3) Tunaweza kuona hilo kutokana na maneno ya Yesu yaliyowafunua viongozi wa uwongo wa kidini, ambao waliwakandamiza watu kwa mizigo mizito. Alisema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:28-30) Watawala wengi wa kidunia, wawe wa kidini au wengineo, huwachosha watu kwa sheria nyingi sana na kwa kuwafanyiza kazi bila shukrani. Hata hivyo, Yesu anawataka wafuasi wake wafanye mambo kulingana na mahitaji na uwezo wao. Nira ya Yesu ni yenye fadhili na yenye kuburudisha kwelikweli! Je, hatuchochewi kumwiga katika kuwaonyesha wengine fadhili?—Yohana 13:15.

17, 18. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba wale watakaotawala pamoja na Kristo mbinguni na wawakilishi wake duniani wataonyesha fadhili?

17 Maneno ya Yesu yenye kuvutia kwa mitume wake hukazia jinsi Ufalme wa Mungu ulivyo tofauti kabisa na utawala wa wanadamu. Biblia inasema: “Kukatokea pia bishano kali kati yao [wanafunzi] juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote. Lakini akawaambia: ‘Wafalme wa mataifa hupiga ubwana juu yao, na wale walio na mamlaka juu yao huitwa Wafadhili. Ingawa hivyo, ninyi hampaswi kuwa hivyo. Lakini acheni yule aliye mkuu zaidi ya wote kati yenu awe kama aliye mdogo zaidi ya wote, na yule anayetenda kama mkuu kama yule anayehudumu. Kwa maana ni nani aliye mkuu zaidi, yule anayeketi mezani au yule anayehudumu? Je, si yule anayeketi mezani? Lakini mimi nimo katikati yenu kama yule anayehudumu.’”—Luka 22:24-27.

18 Watawala wa kibinadamu hujaribu kuimarisha ukuu wao kwa ‘kupiga ubwana’ juu ya watu na kwa kutafuta majina makubwa ya vyeo kana kwamba majina hayo huwafanya wawe bora kuliko raia zao. Lakini Yesu alisema kwamba ukuu wa kweli hutokana na kuwahudumia wengine, ukifanya hivyo kwa bidii bila kuacha. Wote watakaotawala pamoja na Kristo mbinguni au watakaotumikia duniani wakiwa wawakilishi wake, lazima wajitahidi kufuata kielelezo chake cha unyenyekevu na fadhili.

19, 20. (a) Yesu alionyeshaje namna Yehova alivyo mwenye fadhili nyingi? (b) Tunawezaje kumwiga Yehova katika kuonyesha fadhili?

19 Na tuchunguze shauri lingine la upendo ambalo Yesu alitoa. Akionyesha namna Yehova alivyo mwenye fadhili nyingi, Yesu alisema: “Mkiwapenda wale wanaowapenda ninyi, hilo linawapa sifa gani? Kwa maana hata watenda-dhambi huwapenda wale wanaowapenda wao. Na mkiwatendea mema wale wanaowatendea ninyi mema, kwa kweli hilo linawapa sifa gani? Hata watenda-dhambi hufanya vivyo hivyo. Pia, mkikopesha bila faida wale ambao mnatumaini kupokea kutoka kwao, hilo linawapa sifa gani? Hata watenda-dhambi huwakopesha watenda-dhambi bila faida ili wapate kurudishiwa kwa kadiri ileile. Badala yake, endeleeni kuwapenda adui zenu na kutenda mema na kukopesha bila faida, bila kutumainia kurudishiwa chochote; na thawabu yenu itakuwa kubwa, nanyi mtakuwa wana wa Aliye Juu Zaidi, kwa sababu yeye ni mwenye fadhili kuwaelekea wasio na shukrani na waovu. Endeleeni kuwa wenye rehema, kama vile Baba yenu alivyo mwenye rehema.”—Luka 6:32-36.

20 Fadhili za kimungu hazina ubinafsi. Mungu hatarajii watu wamlipe au wampe kitu fulani ili awaonyeshe fadhili hizo. Kwa fadhili Yehova “hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:43-45; Matendo 14:16, 17) Kwa kumwiga Baba yetu wa mbinguni, sisi hatuepuki tu kuwadhuru watu wasio na shukrani bali huwatendea mema, hata wale ambao wametutendea kama maadui. Kwa kuonyesha fadhili, tunawadhihirishia Yehova na Yesu kwamba tunatamani kuishi chini ya Ufalme wa Mungu, wakati ambapo watu wataonyesha fadhili na sifa nyingine za kimungu katika mahusiano yao yote.

Kwa Nini Tuonyeshe Fadhili?

21, 22. Kwa nini tunapaswa kuonyesha fadhili?

21 Ni muhimu sana kwa Mkristo wa kweli kuonyesha fadhili. Hiyo huthibitisha kwamba tuna roho ya Mungu. Isitoshe, tunapoonyesha fadhili za kweli, tunamwiga Yehova Mungu na Kristo Yesu. Pia fadhili ni takwa kwa wale watakaokuwa raia za Ufalme wa Mungu. Basi, ni lazima tupende fadhili na kujizoeza kuionyesha.

22 Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha fadhili katika maisha yetu? Makala inayofuata itazungumzia habari hiyo.

Unajibuje

• Fadhili ni nini?

• Kwa nini ulimwengu ni mahali penye ukatili?

• Tunajuaje kwamba kutakuwa na fadhili nyingi chini ya utawala wa Mungu?

• Kwa nini ni muhimu kwa wale wanaotamani kuishi chini ya Ufalme wa Mungu kuonyesha fadhili?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wazee Wakristo hujitahidi kuonyesha fadhili wanaposhughulika na kundi

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yehova atawaonyesha watumishi wake fadhili zenye upendo wakati wa magumu

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kwa fadhili Yehova huruhusu jua liangaze na mvua inyeshe juu ya wanadamu wote