Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahubiri Yasiyo Rasmi Katika Eneo Wanakozungumza Kiingereza Huko Mexico

Mahubiri Yasiyo Rasmi Katika Eneo Wanakozungumza Kiingereza Huko Mexico

Mahubiri Yasiyo Rasmi Katika Eneo Wanakozungumza Kiingereza Huko Mexico

ALIPOKUWA akiwangojea wasafiri wenzake huko Athene, mtume Paulo alitumia wakati huo kuhubiri isivyo rasmi. Biblia inasema: “Alianza kujadiliana . . . kila siku sokoni pamoja na wale waliokuwapo.” (Matendo 17:17) Akiwa safarini kutoka Yudea kwenda Galilaya, Yesu alimhubiria isivyo rasmi mwanamke Msamaria kando ya kisima. (Yohana 4:3-26) Je, wewe hutumia kila nafasi kuzungumza kuhusu habari njema ya Ufalme wa Mungu?

Mahubiri yasiyo rasmi yanafaa sana katika eneo wanakozungumza Kiingereza huko Mexico. Watalii hutembelea hoteli za kitalii, wanafunzi wa chuo kikuu huja na kwenda, nao wageni ambao wamestaafu nchini Mexico hutembelea bustani na mikahawa. Wengi wa Mashahidi wa Yehova wanaojua Kiingereza wamekuwa stadi katika kuanzisha mazungumzo na watu hao. Hata wanakuwa macho sana kuzungumza na yeyote anayeonekana kuwa mgeni au anayezungumza Kiingereza. Na tuone jinsi wanavyofanya hivyo.

Mara nyingi, Mashahidi wanaotoka nchi za kigeni ambao wanatumikia katika eneo ambako Kiingereza kinazungumzwa, hujitambulisha kwa watu wanaoonekana waziwazi kuwa wageni na kuwauliza nchi wanazotoka. Kwa kawaida mgeni humuuliza Shahidi huyo kile anachofanya nchini Mexico na hiyo humpatia nafasi ya kumweleza imani ya Kikristo. Kwa mfano, Gloria ambaye anatumikia katika eneo la Kiingereza la Oaxaca, ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi, huona kwamba ni rahisi zaidi kuanzisha mazungumzo kwa njia hiyo. Alipokuwa akirudi nyumbani kutoka mahubiri yasiyo rasmi katikati mwa mji, Gloria alisimamishwa na mume na mke kutoka Uingereza. Mwanamke huyo alisema: “Siamini kwamba ninaona mwanamke mweusi akitembea kwenye barabara za Oaxaca!” Badala ya kukasirika, Gloria alicheka, nao wakaanza kuzungumza kuhusu sababu iliyomfanya aje Mexico. Mwanamke huyo alimwalika Gloria aje nyumbani kwake kunywa kahawa. Baada ya kupanga siku ambayo wangekutana tena, Gloria alimpa mwanamke huyo magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, lakini mwanamke huyo akakataa, akisema kwamba yeye haamini kuna Mungu. Gloria alimjibu kwamba alifurahia kuzungumza na watu wasioamini kuna Mungu na angependa kusikia maoni yake kuhusu makala “Je, Tunahitaji Majengo ya Ibada?” Mwanamke huyo alikubali na kusema: “Kama unaweza kunisadikisha kwamba kuna Mungu, basi utakuwa umetimiza jambo muhimu.” Walizungumzia mambo kadhaa yenye kuvutia huku wakifurahia kahawa. Baadaye, mume na mke huyo walirudi Uingereza, lakini mazungumzo yakaendelea kupitia barua pepe.

Gloria pia alianza kuzungumza na mwanafunzi mmoja kutoka Washington D.C., ambaye alikuja Oaxaca kufanya kazi ya kujitolea pamoja na wanawake wenyeji ili aweze kukamilisha digrii yake ya pili. Baada ya kumpongeza Saron kwa jitihada zake, Gloria alimweleza kwa nini alikuwa Mexico. Hiyo ilifanya wawe na mazungumzo mazuri kuhusu Biblia, na mambo ambayo Mungu atawafanyia maskini na pia watu wote. Saron alisema kwamba ni jambo linaloshangaza kwamba ingawa hakuwa amewahi kamwe kuzungumza na Mashahidi huko Marekani, mmoja kati ya watu aliokutana nao mara ya kwanza nchini Mexico, alikuwa Shahidi wa Yehova! Saron alikubali kujifunza Biblia na akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo mara moja.

Wageni wengi wamehamia hoteli za kitalii kwenye fuo za Mexico, wakitamani hali za kiparadiso. Laurel hutumia tamaa hiyo kuanzisha mazungumzo huko Acapulco, huku akiwauliza watu kama hali za kiparadiso za Acapulco ni bora kuliko za mahali walipotoka na ni nini kinachowapendeza kuhusu jiji hilo. Kisha yeye huwaeleza kwamba hivi karibuni dunia yote itakuwa paradiso halisi. Alitumia njia hiyo kuanzisha funzo la Biblia na mwanamke Mkanada aliyekutana naye katika ofisi ya tiba ya mifugo. Je, njia hiyo inaweza kuwa na matokeo mahali unapoishi?

‘Barabarani na Katika Viwanja vya Watu Wote’

Mara nyingi mazungumzo huanzishwa barabarani na katika viwanja vya watu wote kwa kuuliza: “Je, unazungumza Kiingereza?” Wamexico wengi huzungumza Kiingereza kwa sababu ya kazi yao au kwa sababu waliishi Marekani.

Shahidi mmoja na mke wake walizungumza na mwanamke mmoja mzee aliyekuwa katika kiti cha magurudumu kilichokuwa kikisukumwa na muuguzi fulani. Walimuuliza mwanamke huyo kama anazungumza Kiingereza. Naye akajibu kwamba anakizungumza kwa kuwa aliishi Marekani kwa miaka mingi. Alikubali magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, ambayo hakuwa amewahi kuyasoma, naye akawaambia anaitwa Consuelo na kuwapa anwani yake. Walipomtembelea siku nne baadaye, walikuta kwamba anaishi katika hospitali inayosimamiwa na watawa wa kike Wakatoliki. Mwanzoni, ilikuwa vigumu kuzungumza na Consuelo kwa kuwa watawa hao walikuwa na shaka, nao wakasema kwamba Consuelo hangeweza kuwapokea. Mashahidi hao waliwasihi watawa hao wamjulishe Consuelo kwamba wamefika na wangependa kumsalimu. Consuelo aliwakaribisha Mashahidi hao. Tangu wakati huo, mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 86 amefurahia kujifunza Biblia kwa ukawaida, ingawa watawa hao wanamsema vibaya. Pia amehudhuria mikutano kadhaa ya Kikristo.

Andiko la Methali 1:20 linasema: “Hekima ya kweli huendelea kulia kwa sauti kubwa barabarani. Hutoa sauti yake katika viwanja vya watu wote.” Ona jinsi ilivyokuwa katika kiwanja cha watu wote cha San Miguel de Allende. Siku moja asubuhi na mapema, Ralph alimfikia mwanamume mmoja mwenye umri wa makamo aliyekuwa amekalia benchi. Mwanamume huyo alishangaa sana kupewa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kisha akamweleza Ralph kuhusu maisha yake.

Alikuwa mkongwe wa vita vya Vietnam na hisia zake ziliathiriwa sana kwa kuona wafu wengi hivi kwamba alipatwa na matatizo ya akili akiwa jeshini. Alikuwa amerudishwa kambini kutoka mstari wa mbele wa mapigano. Akiwa kambini, alipewa kazi ya kuosha maiti za askari na kuzitayarisha ili zisafirishwe Marekani. Sasa, miaka 30 baadaye, bado alikuwa akiota ndoto mbaya na kuogopa. Asubuhi hiyo alipokuwa ameketi kwenye kiwanja hicho, alikuwa akisali kimyakimya ili apate msaada.

Mkongwe huyo wa vita alikubali vitabu na pia mwaliko wa kwenda kwenye Jumba la Ufalme. Baada ya kuhudhuria mkutano, alisema kwamba kwa muda wa saa mbili alizokuwa katika Jumba la Ufalme, alihisi amani kwa mara ya kwanza katika miaka 30. Mwanamume huyo alikaa San Miguel de Allende kwa muda mfupi, lakini alifurahia kujifunza Biblia mara kadhaa na kuhudhuria mikutano yote hadi aliporudi nyumbani. Mipango ilifanywa ili aendelee kujifunza.

Kuhubiri Isivyo Rasmi Kazini na Shuleni

Je, wewe hujitambulisha kuwa Shahidi wa Yehova kazini? Adrián, ambaye hukodisha nyumba za kukaa wakati wa likizo huko Cape San Lucas, hufanya hivyo. Kwa sababu hiyo, mfanyakazi mwenzake Judy, anasema hivi: “Kama ungeniambia kwamba ningekuwa Shahidi wa Yehova miaka mitatu tu iliyopita, ningesema ‘Haiwezekani kabisa!’ Lakini niliamua kuisoma Biblia. Niliwaza, ‘Haiwezi kuwa vigumu, kwa kuwa ninapenda kusoma.’ Hata hivyo, baada ya kusoma kurasa sita nilitambua kwamba nilihitaji msaada. Niliona kwamba Adrián, mfanyakazi mwenzangu, ndiye tu ambaye angeweza kunisaidia. Nilipenda kuzungumza naye kwa sababu yeye tu ndiye aliyekuwa mtu mwadilifu kazini.” Adrián alijitolea mara moja kuja pamoja na mchumba wake, Katie, na kumjibu Judy maswali yake yote. Katie alianza kujifunza Biblia pamoja naye, na baada ya muda mfupi, Judy akabatizwa na kuwa Shahidi.

Namna gani kuhubiri isivyo rasmi shuleni? Wanafunzi wawili Mashahidi waliokuwa wakijifunza Kihispania katika chuo kikuu walikosa kwenda chuoni siku moja ili wahudhurie kusanyiko la Kikristo. Waliporudi, waliombwa waeleze kwa Kihispania walichoenda kufanya siku hiyo. Walitumia nafasi hiyo kutoa ushahidi kadiri walivyoweza katika Kihispania. Silvia, mwalimu wao, alipendezwa sana na unabii wa Biblia. Alikubali kujifunza Biblia katika Kiingereza na sasa yeye ni mhubiri wa habari njema. Washiriki kadhaa wa familia yake wanajifunza pia. Silvia anasema: “Nilipata kile ambacho nimekuwa nikitafuta maishani.” Naam, kuhubiri isivyo rasmi kunaweza kuwa na matokeo mazuri.

Kutumia Nafasi Nyingine

Ukiwa na sifa ya ukaribishaji-wageni unaweza kupata nafasi ya kutoa ushahidi. Jim na Gail, ambao wanatumikia huko San Carlos, Sonora, waliona kwamba jambo hilo ni la kweli. Mwanamke mmoja aliyekuwa anatembeza mbwa zake saa 12 asubuhi alisimama kwa kuvutiwa na ua wao. Jim na Gail walimkaribisha kunywa kahawa. Ilikuwa ni mara yake ya kwanza akiwa na umri wa miaka 60 kusikia kuhusu Mashahidi na tazamio la kuishi milele. Funzo la Biblia lilianzishwa.

Adrienne pia huwatendea wageni kwa fadhili. Alipokuwa akila katika mkahawa mmoja huko Cancún mvulana mmoja alimfikia na kumwuliza kama anatoka Kanada. Alipojibu kwamba anatoka Kanada, mvulana huyo alimweleza kwamba yeye na mama yake walikuwa wakimsaidia dada yao kuandika ripoti moja ya shule kuhusu Wakanada. Mama yake ambaye huzungumza Kiingereza alisongea karibu. Baada ya kumjibu mama huyo kwa subira maswali aliyouliza kuhusu Wakanada, Adrienne alisema: “Lakini kuna sababu muhimu sana iliyofanya nitoke Kanada na kuja hapa—kusaidia watu wajifunze Biblia. Je, ungependa kujifunza Biblia?” Mwanamke huyo alijibu kwamba angependa kufanya hivyo. Alikuwa ameacha kanisa lake miaka kumi iliyopita, naye alikuwa anajaribu kujifunza Biblia peke yake. Alimpa Adrienne anwani na namba yake ya simu, kisha akaanzisha funzo nzuri la Biblia.

“Tupa Mkate Wako Juu ya Uso wa Maji”

Mara nyingi, kuzungumzia kweli ya Biblia kila wakati hutuwezesha kuwahubiria watu ambao hawakupata nafasi ya kutosha au nafasi yoyote ya kusikia ujumbe wa Ufalme. Kwenye mkahawa mmoja wenye shughuli nyingi katika mji wa bandarini wa Zihuatanejo, Shahidi mmoja aliwakaribisha mume na mke ambao walikuwa wageni waketi kwenye meza yake kwa sababu mkahawa huo ulikuwa umejaa. Wageni hao walikuwa wakisafiri kwa meli sehemu mbalimbali kwa miaka saba. Walisema kwamba hawakupendezwa na Mashahidi wa Yehova. Baada ya kukutana nao kwenye mkahawa huo, Shahidi huyo aliwatembelea kwenye mashua yao na kuwaalika nyumbani kwake. Walikubali magazeti zaidi ya 20, vitabu 5, nao wakaahidi kwamba wangewatafuta Mashahidi kwenye bandari ambayo wangetembelea baada ya hapo.

Kwenye mkahawa mmoja ulio katika eneo la maduka huko Cancún, Jeff na Deb waliona familia moja iliyokuwa na mtoto mrembo wa kike. Waliposema kuhusu mtoto huyo, wazazi wake waliwakaribisha kula piza. Familia hiyo ilikuwa inatoka India. Hawakuwa wamewahi kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova, wala kuona vichapo vyetu. Waliondoka eneo hilo la maduka wakiwa na vichapo kadhaa vya Mashahidi.

Jambo kama hilo lilitukia kwenye kisiwa kilicho karibu na pwani ya Yucatán. Mume na mke Mchina waliokuwa wameoana hivi karibuni walimwomba Jeff awapige picha, naye akakubali kwa furaha. Alipozungumza nao alitambua kwamba ingawa walikuwa wameishi Marekani kwa miaka 12 iliyopita, hawakuwa wamewahi kuwaona au kuwasikia Mashahidi wa Yehova! Kisha wakawa na mazungumzo yenye kupendeza. Jeff aliwatia moyo wawatafute Mashahidi watakaporudi nyumbani.

Huenda kukawa na tukio la pekee katika eneo unaloishi na ukapata nafasi ya kuhubiri isivyo rasmi. Wakati rais wa Marekani alipokuja kumtembelea rais wa Mexico kwenye shamba lake kubwa la mifugo karibu na Guanajuato, waandishi wa habari kutoka sehemu zote za ulimwengu waliripoti tukio hilo. Familia moja ya Mashahidi iliamua kutumia nafasi hiyo kuhubiri katika Kiingereza. Ilipata matokeo mazuri. Kwa mfano, mwandishi mmoja wa habari alikuwa ameripoti vita mbalimbali, kama vile vya Kosovo na Kuwait. Mwandishi mwenzake alikufa mikononi mwake baada ya kupigwa risasi na askari wa kushika doria. Aliposikia juu ya ufufuo, mwandishi huyo alimshukuru Mungu—huku akitokwa na machozi—kwa kumwezesha kujua kwamba maisha yana kusudi. Alisema kwamba ingawa hangewaona Mashahidi hao tena, hangesahau kamwe habari hizo njema kuhusu ufufuo.

Kama vile ambavyo tumeona, mara nyingi hatuwezi kujua matokeo yatakuwaje baada ya kuhubiri. Hata hivyo, Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema: “Tupa mkate wako juu ya uso wa maji, kwa maana baada ya siku nyingi utaupata tena.” Pia alisema: “Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike; kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa, hapa au pale, au ikiwa zote mbili zitakuwa njema.” (Mhubiri 11:1, 6) Naam, “tupa mkate wako” juu ya maji mengi kwa bidii na “panda mbegu zako” kwa ukarimu, kama Paulo na Yesu walivyofanya na kama wanavyofanya Mashahidi hao wa siku hizi nchini Mexico, katika eneo ambako Kiingereza kinazungumzwa.