Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mapenzi ya Mungu Yatakapofanywa Duniani

Mapenzi ya Mungu Yatakapofanywa Duniani

Mapenzi ya Mungu Yatakapofanywa Duniani

YESU alipowafundisha wanafunzi wake wasali, “Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni,” alikuwa akizungumzia jambo analojua kwa kuwa alikuwa ameishi mbinguni na Baba yake. (Mathayo 6:10; Yohana 1:18; 3:13; 8:42) Kabla ya kuja duniani, Yesu alikuwa ameishi wakati ambapo kila jambo lililotukia mbinguni na duniani lilipatana na mapenzi ya Mungu. Huo ulikuwa wakati wa furaha na wa kuridhika na mambo yaliyotimizwa.—Methali 8:27-31.

Kwanza Mungu aliumba viumbe wa roho ambao ni ‘malaika zake, walio na uwezo katika nguvu, na wanaolitenda neno lake.’ Walikuwa na bado wao ni ‘wahudumu wake, wanaofanya mapenzi yake.’ (Zaburi 103:20, 21) Je, kila malaika alikuwa na uhuru wa kusema na wa kuchagua? Ndiyo, na wakati dunia ilipoumbwa, ‘wana hao wa Mungu walianza kupaaza sauti kwa kushangilia.’ (Ayubu 38:7) Kushangilia kwao kulionyesha kwamba walipendezwa kibinafsi na kusudi hilo la Mungu, nao walikubaliana nalo.

Baada ya kuumba dunia, Mungu aliitayarisha ili ikaliwe na wanadamu na mwishowe akaumba mwanamume na mwanamke wa kwanza. (Mwanzo, sura ya 1) Je, malaika walistahili pia kushangilia? Masimulizi yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanasema: “Kisha Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana,” naam, kilikuwa kikamilifu, bila kasoro.—Mwanzo 1:31.

Kusudi la Mungu lilikuwa nini kwa wazazi wetu wa kwanza na wazao wao? Kulingana na Mwanzo 1:28, kusudi hilo pia lilikuwa zuri sana: “Mungu akawabariki na Mungu akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.’” Ili kutimiza kazi hiyo bora, wazazi wetu wa kwanza na pia wazao wao walihitaji kuendelea kuishi milele. Hakuna jambo linaloonyesha kwamba kungekuwa na msiba, ukosefu wa haki, huzuni, au kifo.

Wakati huo mapenzi ya Mungu yalikuwa yakifanywa mbinguni na duniani. Wale waliofanya mapenzi yake wangefurahia sana kufanya hivyo. Shida ilitokea wapi?

Tatizo fulani lisilotazamiwa lilitukia kuhusiana na mapenzi ya Mungu. Hilo halikuwa tatizo lisiloweza kutatuliwa. Lakini lingesababisha huzuni ya muda mrefu, ambayo ingefanya mapenzi ya Mungu kwa wanadamu yasieleweke vizuri. Sote tumeathiriwa na huzuni inayosababishwa na tatizo hilo. Hilo lilikuwa tatizo gani?

Mapenzi ya Mungu Wakati wa Uasi

Mmoja wa ‘wana wa roho wa Mungu’ aliona inawezekana kuvuruga mapenzi ya Mungu kwa mwanadamu. Kusudi la mwana huyo lilikuwa kujinufaisha mwenyewe. Kadiri kiumbe huyo wa roho alivyozidi kufikiria jambo hilo, ndivyo lilivyozidi kuvutia na kuonekana kuwa linawezekana. (Yakobo 1:14, 15) Huenda alifikiri kwamba kama angewashawishi wenzi wawili wa kwanza wamsikilize badala ya kumsikiliza Mungu, basi Mungu angelazimika kuvumilia utawala mwingine wa upinzani. Labda alifikiri kwamba Mungu hangewaua, kwa kuwa jambo hilo lingemaanisha kushindwa kwa kusudi lake. Badala yake, Yehova Mungu angebadili kusudi lake na kukubali mamlaka ya kadiri ya Shetani ambaye sasa wanadamu wangemtii. Kwa kufaa, baadaye mwasi huyo aliitwa Shetani, yaani, “Mpinzani.”—Ayubu 1:6.

Kwa kuchochewa na tamaa yake, Shetani alizungumza na mwanamke huyo. Alimhimiza apuuze mapenzi ya Mungu na kuwa na uhuru wa kujiamulia mema na mabaya, akisema: “Hakika hamtakufa. . . . mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:1-5) Mwanamke huyo alifikiri kwamba jambo hilo lingeweza kumletea uhuru, naye aliona kwamba maisha yake yangekuwa bora kama angemsikiliza Shetani. Baadaye, alimshawishi mume wake ajiunge naye.—Mwanzo 3:6.

Hayo hayakuwa mapenzi ya Mungu kwa Adamu na Hawa. Yalikuwa mapenzi yao wenyewe, nayo yangeleta msiba mkubwa. Tayari Mungu alikuwa amewaambia kwamba kutotii kungetokeza kifo. (Mwanzo 3:3) Hawakuumbwa wafanikiwe bila kuongozwa na Mungu. (Yeremia 10:23) Isitoshe, wangekuwa wasio wakamilifu, na sasa wangepitisha hali hiyo ya kutokuwa wakamilifu na kifo kwa wazao wao. (Waroma 5:12) Shetani hangeweza kubatilisha matokeo hayo.

Je, mambo hayo yalibadili milele kusudi, au mapenzi ya Mungu kwa wanadamu na dunia? La. (Isaya 55:9-11) Lakini yalitokeza masuala yaliyohitaji kutatuliwa: Je, wanadamu wanaweza “kuwa kama Mungu, wakijua mema na mabaya,” kama Shetani alivyodai? Yaani, tukipewa muda wa kutosha, je, tunaweza kuamua kati ya lililo sawa na lililo kosa, lenye kunufaisha na lenye kudhuru, katika sehemu zote za maisha? Je, Mungu anastahili utii kamili kwa sababu njia yake ya kutawala ndiyo bora? Je, tunapaswa kutii kikamili mapenzi yake? Ungejibuje?

Kulikuwa na njia moja tu ya kutatua masuala hayo mbele ya viumbe wote wenye akili: Kuwaruhusu wale waliotaka uhuru wajaribu kuona kama watafanikiwa kuishi bila kumtegemea Mungu. Kuwaua hakungeweza kutatua masuala hayo yaliyotokezwa. Kuwaacha wanadamu waendelee kuishi bila kumtegemea Mungu kwa muda wa kutosha kungetatua masuala hayo kwa kuwa matokeo ya kujitegemea yangekuwa wazi kwa kila mtu. Mungu alionyesha kwamba angeshughulikia mambo kwa njia hiyo alipomwambia mwanamke kwamba angezaa watoto na kutokeza familia ya kibinadamu. Kwa sababu hiyo, tuko hai leo!—Mwanzo 3:16, 20.

Hata hivyo, hilo halikumaanisha kwamba Mungu angewaruhusu wanadamu na mwana huyo wa roho aliyeasi kufanya vyovyote walivyotaka. Mungu hakuacha enzi kuu yake wala kusudi lake. (Zaburi 83:18) Alionyesha wazi jambo hilo kwa kutabiri kwamba mwishowe mwanzilishi wa uasi angepondwa na matokeo mabaya ya uasi huo kufutiliwa mbali. (Mwanzo 3:15) Kwa hiyo, tangu mwanzo, familia ya mwanadamu iliahidiwa kitulizo.

Wakati huohuo, wazazi wetu wa kwanza na wazao wao wa baadaye walijitenga na utawala wa Mungu. Ili Mungu awakinge wasipatwe na matokeo yote mabaya ya uamuzi wao, hiyo ingemaanisha kwamba nyakati zote angewalazimisha kufanya mapenzi yake. Hiyo ingekuwa sawa na kuwazuia kujaribu kuona kama wanaweza kuishi bila kumtegemea.

Bila shaka, watu mmoja-mmoja wangechagua utawala wa Mungu. Wangejifunza mapenzi ya Mungu kwa wanadamu wakati huu na kuyatenda kadiri wawezavyo. (Zaburi 143:10) Hata hivyo, wangeendelea kupatwa na matatizo maadamu suala la wanadamu la kutaka uhuru kamili halingetatuliwa.

Matokeo ya kujifanyia uamuzi yalionekana wazi mapema katika historia ya mwanadamu. Kaini, mtoto wa kwanza wa familia hiyo ya kibinadamu, alimuua Abeli ndugu yake kwa sababu “matendo yake mwenyewe yalikuwa maovu, lakini yale ya ndugu yake yalikuwa ya uadilifu.” (1 Yohana 3:12) Hayo hayakuwa mapenzi ya Mungu kwa kuwa Mungu alikuwa amemwonya Kaini na baadaye akamwadhibu. (Mwanzo 4:3-12) Kaini alichagua uhuru wa kujiamulia mema na mabaya uliotolewa na Shetani; hivyo ‘akatokana na yule mwovu.’ Wengine walifanya vivyo hivyo.

Miaka zaidi ya 1,500 baada ya kuumbwa kwa mwanadamu, “dunia ikaharibika machoni pa Mungu wa kweli, dunia ikajaa jeuri.” (Mwanzo 6:11) Hatua thabiti ilihitaji kuchukuliwa ili kuhifadhi dunia isiharibiwe. Mungu alichukua hatua kwa kuleta gharika ya ulimwengu wote na kuiokoa familia moja yenye uadilifu—Noa, mke wake, wana wake, na wake zao. (Mwanzo 7:1) Sote ni wazao wao.

Katika historia ya mwanadamu tangu wakati wa Noa, Mungu ametoa mwongozo kwa wale wanaotaka kikweli kujua mapenzi yake. Aliwaongoza kwa roho yake wanaume washikamanifu ili waandike ujumbe wake kwa ajili ya yeyote anayetafuta mwongozo wake. Ujumbe huo umeandikwa katika Biblia. (2 Timotheo 3:16) Kwa upendo, aliwaruhusu wanadamu waaminifu wawe na uhusiano pamoja naye, hata kuwa marafiki wake. (Isaya 41:8) Naye aliwapa nguvu walizohitaji ili kuvumilia magumu ambayo yamewapata wanadamu katika muda wa maelfu ya miaka ya kujitegemea. (Zaburi 46:1; Wafilipi 4:13) Tunashukuru kama nini kwa msaada huo wote!

‘Mapenzi Yako Yafanywe’ Kikamili

Yale ambayo Mungu amefanya hadi sasa si utimizo kamili wa mapenzi yake kwa wanadamu. Mtume Mkristo Petro aliandika: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Usemi huo wa mfano unarejelea serikali mpya itakayotawala wanadamu na jamii mpya ya wanadamu chini ya serikali hiyo.

Akitumia maneno yaliyo wazi, nabii Danieli aliandika hivi: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. . . . Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Unabii huo unatabiri mwisho wa mfumo wa leo wa mambo usioweza kurekebishwa na mahali pake kuchukuliwa na Ufalme, au serikali ya Mungu. Hizo ni habari njema kama nini! Ubinafsi na mizozo ambayo imejaza jeuri katika ulimwengu wa leo na ambao unatisha kuiharibu dunia tena, utatoweka kabisa siku moja.

Mambo hayo yatatukia lini? Wanafunzi wa Yesu walimwuliza: “Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Kwa sehemu, Yesu alijibu: “Na hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:3, 14.

Inajulikana wazi kwamba kazi hii ya kuhubiri inafanywa sasa katika dunia yote. Labda umeona ikifanywa katika ujirani wako. Katika kitabu chake, These Also Believe, Profesa Charles S. Braden anaandika: “Mashahidi wa Yehova wamehubiri katika dunia yote. . . . Hakuna dini nyingine duniani ambayo imejitahidi kueneza habari njema ya Ufalme kwa bidii na kwa kuendelea kama Mashahidi wa Yehova.” Mashahidi wanahubiri kwa bidii habari hii njema katika nchi zaidi ya 230 na katika lugha 400 hivi. Kazi hii iliyotabiriwa haijawahi kufanywa kwa kiwango ambacho imefanywa leo duniani pote. Kazi hiyo ni mojawapo ya uthibitisho mwingi kwamba sasa wakati unakaribia Ufalme huo uchukue mahali pa serikali za wanadamu.

Ufalme ambao Yesu alisema ungehubiriwa ndio uleule ambao alitufundisha tusali uje katika sala yake ya kielelezo: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Naam, Ufalme huo ndio chombo ambacho Mungu atatumia kutimiza kusudi lake, mapenzi yake kuelekea wanadamu na dunia.

Hiyo inamaanisha nini? Andiko la Ufunuo 21:3, 4 linajibu: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’” Kisha mapenzi ya Mungu yatafanywa kikamili duniani na mbinguni. * Je, ungependa kuwapo wakati mapenzi hayo yatatimizwa?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 26 Iwapo ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au uandike barua kwa kutumia mojawapo ya anwani zilizoonyeshwa kwenye ukurasa wa 2 wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kukataa kufanya mapenzi ya Mungu kulileta msiba