Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Rebeka—Mwanamke Mwenye Bidii Aliyemwogopa Mungu

Rebeka—Mwanamke Mwenye Bidii Aliyemwogopa Mungu

Rebeka—Mwanamke Mwenye Bidii Aliyemwogopa Mungu

TUSEME kwamba ungeweza kumchagulia mwana wako mke. Ungemchagulia mke wa aina gani? Angehitaji kuwa na sifa gani? Je, ungetafuta mwanamke mrembo, mwenye akili, fadhili, na mwenye bidii? Au kuna sifa nyingine ambazo ungetaka awe nazo?

Abrahamu alikabili tatizo hilo. Yehova alikuwa ameahidi kwamba wazao wake wangebarikiwa kupitia mwanaye Isaka. Tunapoanza kuchunguza masimulizi hayo, Abrahamu sasa ni mzee, lakini mwanaye bado ni mseja. (Mwanzo 12:1-3, 7; 17:19; 22:17, 18; 24:1) Kwa kuwa Isaka atabarikiwa pamoja na mwanamke atakayekuwa mke wake na watoto wowote ambao huenda wakazaa, Abrahamu anapanga kumtafutia Isaka mke anayefaa. Kwanza kabisa, lazima awe mtumishi wa Yehova. Na kwa kuwa Abrahamu hawezi kupata mwanamke wa aina hiyo huko Kanaani, ambako anaishi, inambidi atafute kwingineko. Mwishowe, Rebeka ndiye anayechaguliwa. Abrahamu anampataje? Je, yeye ni mwanamke wa kiroho? Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza kielelezo chake?

Kumtafuta Mwanamke Anayestahili

Abrahamu anamtuma mtumishi wake mwenye umri mkubwa zaidi, labda Eliezeri, katika nchi ya mbali ya Mesopotamia ili akamchagulie Isaka mke kati ya jamaa za Abrahamu ambao ni waabudu wa Yehova. Jambo hilo ni zito sana hivi kwamba Eliezeri anaapishwa asimchukulie Isaka mke Mkanaani. Kule kusisitiza kwa Abrahamu kwamba mwanamke huyo hapaswi kuwa Mkaanani, ni jambo muhimu.—Mwanzo 24:2-10.

Baada ya kusafiri hadi jiji la jamaa za Abrahamu, Eliezeri anawapeleka ngamia zake kumi kwenye kisima. Wazia hilo! Ni jioni-jioni, naye anasali hivi: “Hapa nimesimama kwenye chemchemi ya maji, na binti za watu wa jiji wanatoka nje kuteka maji. Litakalotokea ni kwamba mwanamke kijana ambaye nitamwambia, ‘Tafadhali, shusha mtungi wako wa maji ili ninywe,’ na ambaye kwa kweli atasema, ‘Kunywa, na pia nitanywesha ngamia zako,’ huyo ndiye utakayemchagulia mtumishi wako, Isaka.”—Mwanzo 24:11-14.

Yaelekea kila mwanamke wa eneo hilo anajua kwamba ngamia mwenye kiu anaweza kunywa maji mengi sana, (karibu lita 100). Kwa hiyo, mwanamke aliyejitolea kunywesha ngamia kumi alipaswa kuwa tayari kwa kazi ngumu. Kama angewanywesha peke yake huku wengine wakimtazama tu bila kumsaidia, ingethibitisha kabisa kwamba ana nguvu, subira, unyenyekevu, na ana fadhili kuelekea mwanadamu na mnyama.

Inakuwaje? ‘Kabla hajamaliza kusema, tazama, Rebeka, aliyezaliwa na Bethueli mwana wa Milka mke wa Nahori, ndugu ya Abrahamu, akatoka nje na mtungi wake wa maji ukiwa begani mwake. Sasa huyo mwanamke kijana alikuwa mwenye sura ya kuvutia sana, bikira, naye akateremka kuja kwenye chemchemi, akaanza kujaza mtungi wake wa maji kisha akapanda. Mara moja yule mtumishi akakimbia akutane naye na kusema: “Tafadhali, nipe maji kidogo katika mtungi wako.” Naye akasema: “Kunywa, bwana wangu.” Kisha akashusha upesi mtungi wake mkononi mwake, akamnywesha.’—Mwanzo 24:15-18.

Je, Rebeka Ana Sifa Zinazohitajiwa?

Rebeka ni mjukuu wa ndugu ya Abrahamu. Yeye haogopi kuongea na mtu asiyemjua, wala si mwenye urafiki kupita kiasi. Anakubali kumpatia Eliezeri maji anapomwomba. Ingetazamiwa afanye hivyo kwa kuwa hilo ni tendo la heshima. Namna gani sehemu ya pili ya jaribu hilo?

Rebeka anasema: “Kunywa, bwana wangu.” Lakini si hayo tu, bali anaongeza hivi: “Nitateka maji pia kwa ajili ya ngamia zako mpaka wamalize kunywa.” Anajitolea kufanya mengi zaidi ya yale ambayo kwa kawaida angetazamiwa kufanya. Kwa haraka, ‘anamimina upesi maji ya mtungi wake ndani ya chombo cha kunyweshea wanyama na kukimbia tena na tena kisimani ili kuteka maji, naye anaendelea kuteka kwa ajili ya ngamia zake wote.’ Anafanya kazi hiyo kwa bidii sana. Masimulizi hayo yanasema, ‘Wakati huo wote yule mwanamume anamkazia macho kwa kustaajabu.’—Mwanzo 24:19-21.

Anapotambua kwamba mwanamke huyo kijana ni wa jamaa ya Abrahamu, Eliezeri anasujudu kwa kumshukuru Yehova. Anamuuliza Rebeka kama yeye na watu anaoandamana nao wanaweza kupata nafasi ya kulala usiku nyumbani kwa baba yake. Rebeka anamwambia kuna nafasi kisha anakimbia nyumbani kuwapasha habari kuhusu wageni hao.—Mwanzo 24:22-28.

Baada ya kumsikiliza Eliezeri, Labani, ndugu ya Rebeka, na baba yake, Bethueli, wanatambua kwamba Mungu ndiye anayeongoza mambo. Hakika Rebeka amechaguliwa awe mke wa Isaka. Wanasema, “Mchukue uende, na awe mke wa mwana wa bwana wako, kama vile ambavyo Yehova amesema.” Rebeka anahisije? Anapoulizwa kama ataondoka mara moja, yeye anajibu kwa neno moja tu la Kiebrania linalomaanisha: “Mimi niko tayari kwenda.” Yeye halazimishwi kukubali aolewe na Isaka. Abrahamu alikuwa amemwambia Eliezeri waziwazi kwamba angekuwa amewekwa huru kutoka kwenye kiapo chake ‘ikiwa huyo mwanamke hatataka’ kuondoka. Lakini Rebeka pia anatambua kwamba Mungu ndiye anayeongoza mambo. Hivyo, anaacha familia yake mara moja na kwenda kuolewa na mwanamume ambaye hamjui. Uamuzi huo wa ujasiri ni wonyesho wa kipekee wa imani. Bila shaka, yeye ndiye anayefaa kuwa mke wa Isaka!—Mwanzo 24:29-59.

Anapokutana na Isaka, Rebeka anajifunika uso kama ishara ya ujitiisho. Isaka anamchukua awe mke wake, na bila shaka anaanza kumpenda kwa sababu ya sifa zake bora.—Mwanzo 24:62-67.

Wana Walio Mapacha

Rebeka anabaki bila mtoto kwa miaka 19 hivi. Mwishowe, anapata mimba ya mapacha, lakini mimba hiyo ina matatizo, kwa kuwa watoto hao wanapambana tumboni mwake, wakifanya Rebeka amlilie Mungu. Huenda sisi pia tukamlilia Mungu tunapopatwa na matatizo makubwa maishani. Yehova anamsikiliza Rebeka na kumtia moyo. Atakuwa mama ya mataifa mawili, na “mkubwa atamtumikia mdogo.”—Mwanzo 25:20-26.

Si maneno hayo tu yanayomfanya Rebeka ampende zaidi mwana wake mdogo, Yakobo. Wavulana hao ni tofauti. Yakobo ‘hana lawama,’ lakini Esau anadharau sana mambo ya kiroho hivi kwamba kwa mlo mmoja anamuuzia Yakobo haki yake ya kuzaliwa, ambayo ingemwezesha kurithi ahadi za Mungu. Kwa kuoa wanawake wawili Wahiti, Esau anaonyesha hajali, hata anadharau mambo ya kiroho, jambo linalofanya wazazi wake wahuzunike sana.—Mwanzo 25:27-34; 26:34, 35.

Ajitahidi Kuona Yakobo Anabarikiwa

Biblia haisemi kama Isaka anajua kwamba Esau anapaswa kumtumikia Yakobo. Vyovyote vile, Rebeka na Yakobo wanajua kwamba Yakobo ndiye anayepaswa kubarikiwa. Rebeka anachukua hatua mara moja anaposikia kwamba Isaka anataka kumbariki Esau wakati Esau atakapomletea chakula cha nyama ya mawindo. Bado Rebeka ana bidii na uwezo wa kuamua mambo aliokuwa nao alipokuwa msichana. ‘Anamwamuru’ Yakobo amletee wana-mbuzi wawili. Atatayarisha chakula ambacho mume wake anapenda. Kisha Yakobo anapaswa kujifanya kuwa Esau ili abarikiwe. Yakobo anakataa, akisema kwamba lazima baba yake atatambua ujanja wake na kumlaani! Rebeka anasisitiza afanye hivyo akisema, “Laana uliyokusudiwa wewe na iwe juu yangu, mwanangu.” Ndipo anatayarisha chakula, anamfanya Yakobo afanane na Esau, kisha anamtuma kwa mume wake.—Mwanzo 27:1-17.

Biblia haitaji ni kwa nini Rebeka anatenda hivyo. Wengi humshutumu kwa tendo lake, lakini Biblia haifanyi hivyo. Isaka pia hamshutumu anapotambua kwamba alimbariki Yakobo. Badala yake, Isaka anambariki Yakobo zaidi. (Mwanzo 27:29; 28:3, 4) Rebeka anajua yale ambayo Yehova alitabiri kuhusu wanawe. Hivyo, anachukua hatua ya kuhakikisha kwamba Yakobo anapata baraka ambazo ni haki yake. Ni wazi kwamba jambo hilo linapatana na mapenzi ya Yehova.—Waroma 9:6-13.

Yakobo Atumwa Harani

Sasa Rebeka anavuruga mipango ya Esau kwa kumhimiza Yakobo akimbie hadi hasira ya ndugu yake ipoe. Anamwomba Isaka ruhusa ili Yakobo aende Harani, lakini kwa fadhili anaepuka kutaja hasira ya Esau. Badala yake, kwa busara anamsihi mume wake akisema kwamba ana wasiwasi kwamba huenda Yakobo akaoa Mkaanani. Wazo hilo linatosha kumshawishi Isaka amwamuru Yakobo asioe Mkaanani na kumtuma kwa familia ya Rebeka akatafute mke anayemwogopa Mungu. Biblia haionyeshi kwamba Rebeka alimwona Yakobo tena, lakini matendo yake yanathawabisha sana taifa la baadaye la Israeli.—Mwanzo 27:43–28:2.

Mambo tunayojua kumhusu Rebeka hufanya tuvutiwe naye. Alikuwa mrembo sana, lakini urembo wake halisi ulihusiana na ujitoaji wake kimungu. Hiyo ndiyo sifa ambayo Abrahamu alitaka binti-mkwe wake awe nayo. Yaelekea alikuwa na sifa nyingine nyingi tena nzuri kuliko vile Abrahamu alivyotazamia. Imani na ujasiri wake katika kufuata mwongozo wa Mungu, pamoja na bidii, kiasi, na ukarimu wake, ni sifa ambazo wanawake wote Wakristo wanapaswa kuiga. Hizo ndizo sifa ambazo Yehova mwenyewe hutafuta katika mwanamke ambaye kwa kweli ni kielelezo kizuri.