Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafsiri ya Complutensian Polyglot—Ni Kifaa Muhimu Katika Utafsiri

Tafsiri ya Complutensian Polyglot—Ni Kifaa Muhimu Katika Utafsiri

Tafsiri ya Complutensian Polyglot—Ni Kifaa Muhimu Katika Utafsiri

YAPATA mwaka wa 1455, kulikuwa na mabadiliko makubwa katika uchapaji wa Biblia. Johannes Gutenberg alitumia matbaa yenye herufi zilizopangwa ili kuchapisha Biblia ya kwanza kabisa. Mwishowe, kugawanywa kwa Biblia hakukuzuiwa na kutokuwepo kwa nakala za kutosha zilizoandikwa kwa mkono. Hatimaye, Biblia zingeweza kuchapishwa kwa wingi na kwa gharama ndogo zaidi. Muda si muda, Biblia ikawa kitabu kilichogawanywa kwa wingi zaidi duniani.

Biblia ya Gutenberg ilichapishwa katika Kilatini. Lakini baada ya muda wasomi wa Ulaya wakatambua kwamba walihitaji maandishi yenye kutegemeka ya Biblia katika lugha za awali, yaani, Kiebrania na Kigiriki. Kanisa Katoliki lilikubali tu tafsiri ya Kilatini ya Vulgate, ingawa ilikuwa na kasoro mbili kubwa. Katika karne ya 16, watu wengi hawangeweza kuelewa Kilatini. Isitoshe, kwa kipindi cha miaka zaidi ya elfu moja, watu walionakili tafsiri ya Vulgate walikuwa wamefanya makosa mengi sana.

Watafsiri na wasomi walihitaji Biblia katika lugha za awali, na pia tafsiri bora ya Kilatini. Mnamo mwaka wa 1502, kadinali Jiménez de Cisneros, aliyekuwa mshauri wa kisiasa na wa kidini wa malkia Isabella wa Kwanza wa Hispania, aliamua kutimiza uhitaji wao kwa kichapo kimoja tu. Kifaa hicho muhimu katika utafsiri kiliitwa Complutensian Polyglot. Cisneros alikusudia kutokeza Polyglot, au Biblia ya lugha nyingi, yenye maandishi bora ya Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini, pamoja na sehemu kadhaa katika Kiaramu. Uchapaji haukuwa umepiga hatua kubwa, hivyo kuchapwa kwa Biblia hiyo kungekuwa pia hatua muhimu katika uchapishaji.

Cisneros alianza kazi yake ngumu kwa kununua vitabu vya kale vya kukunjwa vya Kiebrania, ambavyo vilipatikana kwa wingi huko Hispania. Pia alikusanya vitabu mbalimbali vya kukunjwa, vya Kigiriki na Kilatini. Vitabu hivyo vingetumiwa ili kuchapisha Polyglot. Cisneros alikipa kikundi cha wasomi alichoanzisha katika Chuo Kikuu kipya cha Alcalá de Henares, Hispania, kazi ya kupanga na kuhariri Polyglot hiyo. Kati ya wasomi walioalikwa kufanya kazi hiyo ni Erasmus wa Rotterdam, lakini mjuzi huyo mashuhuri wa lugha mbalimbali alikataa mwaliko huo.

Iliwachukua wasomi hao miaka kumi kupanga na kuhariri mabuku kadhaa yaliyofanyiza Biblia hiyo kubwa. Kisha ikachukua miaka mingine minne kuichapisha. Kulikuwa na matatizo mengi ya kiufundi kwa kuwa mashine za kuchapa za Hispania hazikuwa na herufi za Kiebrania, Kigiriki, au Kiaramu. Hivyo, Cisneros alitumia mchapishaji mkuu wa Hispania, Arnaldo Guillermo Brocario, kutayarisha herufi za lugha hizo. Mwishowe, uchapaji ulianza mwaka wa 1514. Mabuku hayo sita yalikamilishwa Julai 10, 1517, miezi minne tu kabla ya kadinali huyo kufa. Nakala zipatazo 600 za Biblia hiyo zilichapishwa, wakati harakati za Baraza la Kuhukumu Waasi wa Kidini huko Hispania zilipopamba moto. *

Mpangilio wa Polyglot

Kila ukurasa wa Polyglot ulikuwa na habari nyingi. Katika mabuku manne yenye Maandiko ya Kiebrania, maandishi ya Vulgate yalikuwa katikati ya kila ukurasa, maandishi ya Kiebrania katika safu ya nje, nayo ya Kigiriki yaliyokuwa sambamba na tafsiri yake ya Kilatini, katika safu ya ndani. Pambizoni, kulikuwa na herufi nyingi zinazofanyiza maneno ya Kiebrania. Katika sehemu ya chini ya kila ukurasa katika vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, wahariri pia walitia ndani Targum of Onkelos (ufafanuzi wa Kiaramu wa vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia) pamoja na tafsiri ya Kilatini.

Buku la tano la Polyglot lilikuwa na Maandiko ya Kigiriki katika safu mbili. Safu moja ilikuwa na maandishi ya Kigiriki, na ile nyingine ilikuwa na maandishi hayohayo katika lugha ya Kilatini kutoka katika tafsiri ya Vulgate. Herufi ndogo kwenye kila neno katika safu zote mbili zilimsaidia msomaji kutambua maneno yaliyolingana katika lugha hizo mbili. Maandishi ya Kigiriki ya Polyglot ndiyo maandishi ya kwanza kamili ya “Agano Jipya” kuchapishwa, ambayo muda mfupi baadaye yalifuatwa na Maandiko ya Kigiriki yaliyotayarishwa na Erasmus.

Wasomi hao walikuwa makini sana katika usahihishaji wa maandishi hayo hivi kwamba kulikuwa na makosa 50 tu ya uchapishaji. Kwa sababu wasomi hao walikuwa makini, wachambuzi wa siku hizi wamesema kwamba buku hilo lilikuwa bora kuliko yale maandishi maarufu ya Kigiriki ya Erasmus. Herufi za Kigiriki zilivutia kama zile za maandishi ya awali. Katika kitabu chake The Printing of Greek in the Fifteenth Century, R. Proctor anasema: “Hispania inapaswa kusifiwa kwa kutokeza herufi za kwanza za Kigiriki ambazo bila shaka ndizo bora zaidi kuwahi kutokezwa.”

Buku la sita la Polyglot lilikuwa na vifaa mbalimbali vya kujifunzia Biblia: kamusi ya Kiebrania na Kiaramu, fasiri ya majina ya Kigiriki, Kiebrania, na Kiaramu, sarufi ya Kiebrania, na fahirisi ya Kilatini kwa ajili ya kamusi hiyo. Haishangazi kwamba Complutensian Polyglot imetambuliwa kuwa ‘kazi bora ya usanii wa maandishi na ustadi wa kupanga Maandiko.’

Cisneros alikusudia Biblia hiyo “iwachochee watu waanze kusoma maandiko tena.” Hata hivyo, hakutaka Biblia hiyo ipatikane kwa watu wa kawaida. Alifikiri kwamba “Neno la Mungu lilipaswa kufichwa kwa busara ili lisieleweke kwa watu wa kawaida.” Pia aliamini kwamba “Maandiko yanapaswa kupatikana tu katika zile lugha tatu za kale ambazo Mungu aliruhusu zitumiwe katika maandishi yaliyokuwa juu ya kichwa cha Mwana wake aliyesulubishwa.” * Kwa sababu hiyo, Complutensian Polyglot haikutia ndani tafsiri yoyote ya Kihispania.

Kulinganisha Vulgate na Lugha za Awali

Muundo wa Polyglot ulisababisha hali ya kutoelewana kati ya wasomi waliohusika. Msomi maarufu Mhispania, Antonio de Nebrija, * alipewa daraka la kusahihisha maandishi ya Vulgate ambayo yangekuwa katika Biblia ya Polyglot. Ingawa Kanisa Katoliki liliiona tafsiri ya Jerome ya Vulgate kuwa ndiyo tafsiri rasmi pekee, Nebrija aliona uhitaji wa kuilinganisha na maandishi ya awali ya Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki. Alitaka kusahihisha yale yaliyoonekana kuwa makosa ambayo yalikuwa katika nakala za Vulgate zilizokuwako.

Ili kutatua tofauti kati ya tafsiri ya Vulgate na lugha za awali, Nebrija alimsihi Cisneros hivi: “Tumia tena lugha ya Kiebrania na ya Kigiriki kuelewesha watu dini yetu. Wathawabishe wale wanaojitoa kufanya kazi hiyo.” Pia alitoa dokezo hili: “Kila wakati kasoro inapopatikana katika maandishi ya Agano Jipya la Kilatini, tunapaswa kuyalinganisha na maandishi ya Kigiriki. Kila mara kunapokuwa na tofauti kati ya maandishi mbalimbali ya Kilatini au kati ya maandishi ya Kilatini na Kigiriki ya Agano la Kale, tunapaswa kuthibitisha usahihi wake kwa kuchunguza maandishi ya Kiebrania ambayo ni sahihi.”

Cisneros aliitikiaje? Alitaja maoni yake waziwazi katika utangulizi wake wa Biblia ya Polyglot. “Tumeiweka tafsiri ya Kilatini ya mtakatifu Jerome katikati ya tafsiri ya Sinagogi [maandishi ya Kiebrania] na ya Kanisa la Mashariki [maandishi ya Kigiriki], kama vile tu wale wezi walivyotundikwa mmoja kwenye kila upande wa Yesu, ambaye huwakilisha Kanisa la Roma, au la Kilatini.” Hivyo, Cisneros hakumruhusu Nebrija aisahihishe tafsiri ya Kilatini ya Vulgate akitumia maandishi ya lugha za awali. Mwishowe, Nebrija aliamua kuacha kazi hiyo badala ya jina lake kuhusianishwa na tafsiri iliyosahihishwa lakini yenye kasoro.

Comma Johanneum

Ingawa kuchapishwa kwa Biblia ya Polyglot ya Alcalá de Henares kulikuwa hatua kubwa katika kutolewa kwa maandishi bora katika lugha za awali za Biblia, mara kwa mara mapokeo yalipewa umuhimu mkubwa kuliko usomi. Tafsiri ya Vulgate iliheshimiwa sana hivi kwamba mara nyingi wahariri walihisi wana wajibu wa kusahihisha maandishi ya Kigiriki ya “Agano Jipya” ili kuhakikisha kwamba yalilingana na ya Kilatini badala ya maandishi ya awali ya Kigiriki. Mmojawapo wa mifano hiyo ni yale maandishi maarufu na bandia ya comma Johanneum. * Maneno hayo hayakuwa katika maandishi yoyote ya awali ya Kigiriki, ambayo yaonekana yaliingizwa karne kadhaa baada ya Yohana kuandika barua yake; wala hayakuwako katika maandishi ya awali ya Kilatini ya tafsiri ya Vulgate. Kwa hiyo, Erasmus hakutia ndani maneno hayo yanayobadili maana katika tafsiri yake ya “Agano Jipya” ya Kigiriki.

Wahariri wa Polyglot hawakutaka kuondoa mstari ambao ulikuwa sehemu ya tafsiri ya zamani ya Vulgate kwa karne nyingi. Hivyo, hawakuuondoa mstari huo bandia katika Kilatini bali waliamua kuutafsiri na kuuweka katika maandishi ya Kigiriki ili safu hizo mbili zipatane.

Yatumiwa Katika Kutafsiri Biblia Nyingine

Thamani ya tafsiri ya Complutensian Polyglot haitegemei tu uhakika kwamba ilikuwa na chapa ya kwanza kamili ya Maandiko ya Kigiriki pamoja na yale ya Septuagint. Kama vile tafsiri ya “Agano Jipya” ya Kigiriki ya Erasmus (ilivyotumiwa kutafsiri Biblia nyingi katika lugha nyingine), maandishi ya Kiebrania ya Polyglot yalitumiwa kutafsiri Maandiko ya Kiebrania na Kiaramu. * William Tyndale alitumia tafsiri ya Polyglot ya Kiebrania kutafsiri Biblia katika Kiingereza.

Hivyo, kazi iliyofanywa na kikundi cha wasomi ya kutokeza tafsiri ya Complutensian Polyglot ilichangia sana katika utafiti wa Maandiko. Tafsiri hiyo ilichapishwa wakati ambapo tafsiri katika lugha ya kawaida ilianza kuhitajika kwa sababu hesabu ya watu waliopendezwa na Biblia ilizidi kuongezeka huko Ulaya. Tafsiri ya Polyglot ilikuwa mojawapo ya tafsiri zilizochangia kuboreshwa na kuhifadhiwa kwa maandishi ya Kigiriki na Kiebrania. Jitihada zote hizo zinaambatana na kusudi la Mungu kwamba ‘neno la Yehova limetakaswa,’ ‘neno la Mungu wetu, litadumu mpaka wakati usio na kipimo.’—Zaburi 18:30; Isaya 40:8; 1 Petro 1:25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Nakala 600 zilichapishwa kwenye karatasi, na 6 kwenye ngozi. Mnamo 1984 nakala ya kisasa inayofanana na ya awali ilichapishwa.

^ fu. 12 Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini.—Yohana 19:20.

^ fu. 14 Nebrija anadhaniwa kuwa wa kwanza kati ya wanafunzi wa Hispania wa elimu ya ubinadamu (wasomi wenye mawazo huru). Mnamo 1492 alichapisha kitabu cha kwanza cha Gramática castellana (Sarufi ya Lugha ya Castilia). Miaka mitatu baadaye, aliamua kutumia maisha yake yote kuchunguza Maandiko Matakatifu.

^ fu. 18 Maneno bandia yanayopatikana katika tafsiri fulani za Biblia kwenye 1 Yohana 5:7 yanasomeka, “huko mbinguni, Baba, Neno, na Roho Mtakatifu: nao watatu hao ni mmoja.”

^ fu. 21 Ili kupata habari zaidi kuhusu tafsiri ya Erasmus, ona gazeti Mnara wa Mlinzi, Septemba 15, 1982, ukurasa wa 8-11, la Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kadinali Jiménez de Cisneros

[Hisani]

Biblioteca Histórica. Universidad Complutense de Madrid

[Picha katika ukurasa wa 30]

Antonio de Nebrija

[Hisani]

Biblioteca Histórica. Universidad Complutense de Madrid

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 30]

Biblioteca Histórica. Universidad Complutense de Madrid