Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ingawa Nilikuwa Kipofu, Niliweza Kuona!

Ingawa Nilikuwa Kipofu, Niliweza Kuona!

Simulizi la Maisha

Ingawa Nilikuwa Kipofu, Niliweza Kuona!

LIMESIMULIWA NA EGON HAUSER

Baada ya kuwa kipofu kwa muda wa miezi miwili, nilijifunza kweli za Biblia nilizokuwa nimezipuuza katika maisha yangu yote.

NINAFURAHI sana ninapokumbuka mambo mengi yaliyotukia maishani mwangu miaka zaidi ya sabini iliyopita. Lakini kama kuna jambo ambalo ninajutia ni kutomjua Yehova Mungu mapema maishani.

Nilizaliwa mwaka wa 1927 huko Uruguai, nchi iliyo katikati ya Argentina na Brazili ambayo ina eneo kubwa lenye kuvutia kando ya Pwani ya Atlantiki. Raia wengi wa nchi hii ni wazao wa wahamiaji kutoka nchi za Italia na Hispania. Hata hivyo, wazazi wangu ni wahamiaji kutoka Hungaria, na nilipokuwa mchanga, tuliishi na majirani waliokuwa watu wa kawaida tu na wenye uhusiano wa karibu. Hatukuhitaji makufuli au kufunga madirisha kwa sababu hakukuwa na uhalifu wala ubaguzi wa rangi. Sote tulikuwa marafiki, wageni kwa wenyeji, weusi kwa weupe.

Wazazi wangu walikuwa Wakatoliki wenye bidii, nami nilianza kusaidia kwenye madhabahu ya kanisa nikiwa na umri wa miaka kumi. Nilipokuwa mtu mzima, nilifanya kazi katika parokia ya kwetu na nilikuwa mshiriki wa kikundi cha washauri wa askofu wa dayosisi. Kwa kuwa niliamua kuwa daktari, nilialikwa kushiriki katika semina iliyofanywa Venezuela na ambayo ilipangwa na Kanisa Katoliki. Kwa kuwa kikundi chetu kilikuwa cha madaktari wanaoshughulika na magonjwa ya akina mama, tulipewa mgawo wa kuchunguza dawa za kupanga uzazi zilizokuwa zianze kuuzwa wakati huo.

Maoni Yangu Nilipokuwa Nikisomea Udaktari

Nilipokuwa bado ninasomea udaktari, nikijifunza kuhusu mwili wa kibinadamu, nilivutiwa sana na jinsi mwili ulivyoumbwa kwa hekima. Kwa mfano, nilishangazwa na uwezo wa mwili wa kujiponya na kupata nafuu kutokana na jambo linaloathiri hisia, kama vile jinsi ini au mbavu zinavyokua tena baada ya sehemu fulani kuondolewa.

Wakati huohuo, niliona watu wengi wakifa kutokana na aksidenti mbaya, na nilihuzunika walipokufa kwa sababu ya kutiwa damu. Ningali nakumbuka jinsi ilivyokuwa vigumu kuzungumza na jamaa za wagonjwa waliokufa kutokana na madhara ya kutiwa damu. Mara nyingi, jamaa hao hawakuambiwa kwamba mpendwa wao alikufa kwa sababu ya kutiwa damu. Badala yake, walipewa sababu nyingine. Ingawa miaka mingi imepita, ningali nakumbuka jinsi nilivyosumbuka kuhusu kutia watu damu, na mwishowe nilikata kauli kwamba njia hiyo ina kasoro. Laiti ningalijua wakati huo sheria ya Yehova kuhusu utakatifu wa damu! Ningalielewa kwa nini nilisumbuliwa na zoea la kuwatia watu damu mishipani.—Matendo 15:19, 20.

Naridhika kwa Kuwasaidia Watu

Baada ya muda, nikawa daktari-mpasuaji na msimamizi wa kituo cha afya huko Santa Lucía. Pia nilifanya kazi kwenye taasisi ya National Institute of Biological Science. Nilifurahia sana kazi hiyo. Nilisaidia watu waliokuwa wagonjwa, nikatuliza maumivu yao, nikaokoa uhai mara nyingi, na kuwasaidia akina mama kujifungua. Kwa sababu ya mambo niliyojionea hapo awali kuhusu kuwatia watu damu, nilijiepusha na jambo hilo na kuwafanyia maelfu ya watu upasuaji bila damu. Niliona kupoteza damu nyingi kuwa sawa na pipa linalovuja. Suluhisho pekee ni kuziba mahali panapovuja bali si kuendelea kulijaza pipa maji.

Kuwatibu Wagonjwa Mashahidi

Nilikutana na Mashahidi wa Yehova mara ya kwanza katika miaka ya 1960 walipoanza kuja kwenye kliniki yetu ili kufanyiwa upasuaji bila damu. Sitasahau kamwe kisa cha painia (mhudumu wa wakati wote) mmoja aitwaye Mercedes Gonzalez, ambaye alikuwa mgonjwa. Alikuwa amepungukiwa sana na damu hivi kwamba madaktari kwenye chuo kikuu hawakutaka kumfanyia upasuaji, wakiwa na uhakika kwamba angekufa. Ingawa alikuwa akivuja damu, tulimfanyia upasuaji katika kliniki yetu. Upasuaji huo ulifaulu, naye aliendelea kufanya upainia kwa zaidi ya miaka 30 hadi alipokufa hivi karibuni akiwa na umri wa miaka 86.

Sikuzote nilivutiwa na jinsi Mashahidi walivyoonyesha upendo na hangaiko walipowatunza ndugu zao Wakristo waliolazwa hospitalini. Nilipowatembelea wagonjwa, nilifurahi kuwasikiliza wakizungumza kuhusu imani yao, na nilikubali vichapo walivyonipa. Sikufikiri kamwe kwamba baada ya muda mfupi singekuwa tu daktari wao bali pia ndugu yao wa kiroho.

Nilianza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mashahidi nilipomwoa Beatriz, binti ya mgonjwa fulani. Washiriki wengi wa familia ya Beatriz tayari walikuwa wakishirikiana na Mashahidi, na baada ya kuoana, yeye pia akawa Shahidi mwenye bidii. Kwa upande mwingine, mimi nilijishughulisha sana na kazi yangu na nilifurahia umaarufu niliokuwa nao kati ya madaktari. Maisha yalionekana kuwa shwari kabisa. Sikufikiri kwamba baada ya muda mfupi maisha yangu yangebadilika kabisa kwa sababu ya shida fulani.

Napatwa na Shida

Kati ya mambo mabaya zaidi yanayoweza kumpata daktari-mpasuaji ni kutoweza kuona. Nilijikuta katika hali hiyo. Kwa ghafula retina zangu zote mbili zilipasuka, nikawa kipofu na sikujua kama ningepata kuona tena. Baada ya kufanyiwa upasuaji, nililala kitandani huku macho yangu yakiwa yamefungwa bendeji, nami nikashuka moyo. Nilihisi kuwa bure na nilikata tamaa kabisa hivi kwamba niliamua kujiua. Kwa kuwa nilikuwa kwenye orofa ya nne, nilitoka kitandani na kupapasa-papasa ukuta nikitafuta dirisha. Nilitaka kujirusha na kufa. Hata hivyo, niliishia kwenye ukumbi wa hospitali bila kujua, ambako muuguzi mmoja alinirudisha kitandani mwangu.

Sikujaribu kujiua tena. Lakini kwa sababu ya kutoweza kuona chochote, nilizidi kushuka moyo na kuwa mwenye kukasirika upesi. Wakati huo ambapo sikuweza kuona, nilimwahidi Mungu kwamba ikiwa nitaweza kuona tena, nitaisoma Biblia yote. Mwishowe, niliweza kuona tena kwa kadiri fulani na ningeweza kusoma. Lakini singeweza kuendelea na kazi ya udaktari. Hata hivyo, nchini Uruguai, kuna msemo upendwao sana ambao husema “No hay mal que por bien no venga,” ambao unamaanisha, “Baada ya dhiki faraja.” Nilikuwa karibu kushuhudia ukweli wa msemo huo.

Uhusiano Wangu na Mashahidi Wawa Mbaya Mwanzoni

Nilitaka kununua chapa kubwa ya The Jerusalem Bible, lakini nikapata habari kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa na Biblia ya bei rahisi, ambayo kijana mmoja Shahidi alijitolea kuniletea nyumbani. Asubuhi iliyofuata, alikuwa amesimama mlangoni mwangu akiwa na Biblia hiyo. Mke wangu alimfungulia mlango na kuzungumza naye. Nilipiga kelele kwa ujeuri nikiwa ndani ya nyumba na kusema kwamba ikiwa kijana huyo alikuwa amelipwa pesa za Biblia, aondoke nyumbani mwangu. Aliondoka mara moja. Sikutambua kwamba baada ya muda mfupi kijana huyo angetimiza fungu muhimu katika maisha yangu.

Siku moja nilimwahidi mke wangu jambo ambalo sikuweza kutimiza. Kwa hiyo, ili kulipia deni hilo na kumfurahisha, nilisema kwamba nitaenda naye kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Siku hiyo ilipofika, nilikumbuka ahadi yangu na kuhudhuria Ukumbusho huo pamoja naye. Nilivutiwa na jinsi nilivyopokelewa kwa uchangamfu na kwa fadhili. Msemaji alipoanza hotuba yake, nilishangaa kuona kwamba alikuwa yule kijana niliyemfukuza nyumbani kwangu kwa ukali. Hotuba yake ilinigusa moyo sana, hivi kwamba nilihisi vibaya sana kwa kumtendea kwa njia isiyo ya fadhili. Ningefanya nini ili kurekebisha hali hiyo?

Nilimwomba mke wangu amkaribishe kwa chakula cha jioni, lakini akasema: “Je, huoni kwamba itafaa zaidi ukimkaribisha wewe mwenyewe? Kaa hapa tu, atakuja.” Mke wangu alisema kweli. Kijana huyo alikuja kutusalimu na akakubali mwaliko huo kwa furaha.

Mazungumzo tuliyokuwa nayo jioni aliyokuja kututembelea yalikuwa mwanzo wa mabadiliko mengi maishani mwangu. Alinionyesha kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, * nami nikamwonyesha nakala sita za kitabu hicho. Nilipewa vitabu hivyo na wagonjwa Mashahidi hospitalini, lakini sikuwahi kuvisoma. Wakati wa chakula na baada ya hapo—usiku sana—nilimwuliza maswali mengi ambayo alijibu akitumia Biblia. Tuliendelea na mazungumzo hadi asubuhi na mapema iliyofuata. Kabla ya kuondoka, kijana huyo alikubali kujifunza Biblia pamoja nami, akitumia kitabu Kweli. Tulimaliza kusoma kitabu hicho kwa miezi mitatu na kuendelea na kitabu “Babylon the Great Has Fallen!” God’s Kingdom Rules! * Baada ya hapo, nilijiweka wakfu kwa Yehova Mungu na kubatizwa.

Ninahisi Kuwa Ninafaa Tena

Kwa sababu ya kutoweza kuona kihalisi, ‘macho ya moyo wangu’ yalifunguliwa kuona kweli za Biblia ambazo sikuzithamini hadi wakati huo! (Waefeso 1:18) Maisha yangu yalibadilika kabisa baada ya kumjua Yehova na kusudi lake lenye upendo. Sasa nina furaha na ninahisi kuwa ninafaa tena. Ninawasaidia watu kimwili na kiroho na kuwaonyesha jinsi ya kurefusha maisha yao kwa miaka michache katika mfumo huu na kuishi milele katika mfumo mpya.

Nimejitahidi kupata habari za karibuni zaidi kuhusu tiba, na nimefanya utafiti kuhusu hatari za damu, aina nyingine za tiba, haki za wagonjwa, na elimu-maadili ya kibiolojia. Nimepata nafasi za kuwaeleza madaktari wa hapa mambo hayo ninapoalikwa kuyazungumzia kwenye semina za kitiba. Mnamo 1994, nilihudhuria mkutano wa kwanza kuhusu matibabu yasiyohusisha damu huko Rio de Janeiro, Brazili, na kutoa hotuba kuhusu jinsi ya kushughulikia uvujaji wa damu. Sehemu fulani ya hotuba hiyo ilitiwa ndani ya makala niliyoandika, “Una propuesta: Estrategias para el Tratamiento de las Hemorragias” (“Pendekezo Kuhusu Tiba ya Kuzuia Kuvuja Damu”), iliyochapishwa katika gazeti la kitiba Hemoterapia.

Kudumisha Uaminifu Licha ya Mkazo

Mwanzoni, shaka niliyokuwa nayo kuhusu kutia watu damu ilitegemea hasa ujuzi wa kisayansi. Hata hivyo, nilipokuwa mgonjwa niliona kwamba si rahisi kukataa damu na kudumisha imani yangu chini ya mkazo mkali kutoka kwa madaktari. Baada ya kushikwa na ugonjwa wa moyo, ilinibidi kumweleza daktari-mpasuaji msimamo wangu kwa muda unaozidi saa mbili. Alikuwa mwana wa marafiki wangu wa karibu sana na alisema kwamba hangeniruhusu nife ikiwa angeona kwamba ningeokoka kwa kutiwa damu. Nilitoa sala ya moyoni kwa Yehova nikimwomba amsaidie daktari huyo kuelewa na kuheshimu msimamo wangu hata kama hakubaliani nao. Mwishowe, alikubali kuheshimu msimamo wangu.

Pindi nyingine, ilibidi uvimbe mkubwa uondolewe kutoka kwenye tezi ya kibofu. Nilipoteza damu nyingi. Kwa mara nyingine tena, nilijikuta nikieleza sababu zilizofanya nikatae kutiwa damu, na ingawa nilipoteza thuluthi mbili za damu, madaktari waliheshimu msimamo wangu.

Badiliko la Maoni

Nikiwa mshiriki wa shirika la International Association of Bioethics, nimefurahi kuona madaktari na wanasheria wakibadili maoni yao kuhusu haki za mgonjwa. Sasa madaktari wameacha kuwa na mtazamo wa kimabavu na badala yake wanaheshimu msimamo wa wagonjwa. Sasa wanawaruhusu wagonjwa wachague aina ya matibabu. Mashahidi wa Yehova hawaonwi tena kuwa washupavu wasiopaswa kutibiwa. Badala yake, wanaonwa kuwa wagonjwa wenye ujuzi ambao haki zao zinapaswa kuheshimiwa. Kwenye semina za kitiba na kwenye vipindi vya televisheni, maprofesa mashuhuri wamesema: “Kwa sababu ya jitihada za Mashahidi wa Yehova, sasa tunaelewa . . . ” “Tumejifunza kutoka kwa Mashahidi . . . ” na “Wametusaidia kufanya maendeleo.”

Imesemekana kwamba uhai ni muhimu kuliko vitu vyote kwa sababu bila huo uhuru na heshima ingekuwa bure. Sasa wengi wana maoni yanayopatana na sheria huku wakitambua kwamba kila mtu ana haki za kibinafsi na yeye ndiye anayepaswa kuamua ni haki gani inayopaswa kutangulizwa chini ya hali fulani. Kwa njia hiyo, heshima, uhuru wa kuchagua, na imani ya kidini zinatangulizwa. Mgonjwa ana haki ya kuamua. Huduma za Habari za Kihospitali zilizoanzishwa na Mashahidi wa Yehova zimewasaidia madaktari wengi kuelewa masuala hayo.

Msaada ninaozidi kupata kutoka kwa familia yangu umeniwezesha kuwa mwenye manufaa katika utumishi wa Yehova na pia kumtumikia nikiwa mzee katika kutaniko la Kikristo. Kama nilivyosema awali, ninajuta kwamba sikumjua Yehova mapema zaidi maishani. Hata hivyo, ninashukuru sana kwamba amenisaidia kujua tumaini zuri la kuishi chini ya Ufalme wake, ambapo “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 24 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 24 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 34 Makala hii ilipokuwa ikitayarishwa, Ndugu Egon Hauser alikufa. Alikufa akiwa mwaminifu, nasi tunafurahi pamoja naye kwamba tumaini lake ni hakika.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa na umri wa miaka 30 na kitu, nikifanya kazi katika hospitali huko Santa Lucía

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na mke wangu Beatriz, mwaka wa 1995