Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Msimamo wa Kutokuwamo Huzuia Upendo wa Kikristo?

Je, Msimamo wa Kutokuwamo Huzuia Upendo wa Kikristo?

Je, Msimamo wa Kutokuwamo Huzuia Upendo wa Kikristo?

KUWA Mkristo humaanisha mengi zaidi ya kusoma Biblia, kusali, na kuimba Jumapili. Humaanisha kufanya mambo kwa ajili ya Mungu na wanadamu. Biblia inasema: “Acheni tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yohana 3:18) Yesu aliwajali wengine kikweli, nao Wakristo wanataka kumwiga. Mtume Paulo aliwahimiza waamini wenzake sikuzote wawe “na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 15:58) Lakini kazi ya Bwana ni nini? Je, inatia ndani kujaribu kubadili maongozi ya serikali ili kuwanufaisha maskini na waliokandamizwa? Je, Yesu alifanya hivyo?

Ingawa Yesu alihimizwa kufanya hivyo, yeye alikataa kuingilia mambo ya kisiasa au kuunga mkono upande fulani wa kisiasa. Alikataa wakati Shetani alipomtolea falme zote za ulimwengu, akakataa kuingizwa katika mabishano kuhusu kulipa kodi, naye aliondoka wakati kikundi fulani cha watu maarufu walipotaka kumfanya mfalme. (Mathayo 4:8-10; 22:17-21; Yohana 6:15) Lakini msimamo wake wa kutokuwamo haukumzuia kufanya mambo yaliyowanufaisha wengine.

Yesu alizingatia mambo ambayo yangewaletea watu manufaa ya kudumu. Ingawa kuwalisha watu elfu tano na kuwaponya wagonjwa kuliwaletea watu wachache kitulizo cha muda, mafundisho yake yaliwapa wanadamu wote nafasi ya kupata baraka za milele. Yesu alijulikana kuwa “Mwalimu,” wala si mtu aliyefanya mipango ya kampeni za kutoa misaada. (Mathayo 26:18; Marko 5:35; Yohana 11:28) Alisema: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.”—Yohana 18:37.

Kuhubiri Jambo Lililo Bora Kuliko Siasa

Ukweli ambao Yesu alifundisha haukuwa nadharia ya kisiasa tu. Ulikazia Ufalme ambao yeye mwenyewe angekuwa Mfalme. (Luka 4:43) Ufalme huo ni serikali ya mbinguni, nayo itachukua mahali pa serikali zote za kibinadamu na kuwaletea wanadamu amani ya milele. (Isaya 9:6, 7; 11:9; Danieli 2:44) Kwa hiyo, Ufalme huo ndio tumaini la pekee kwa wanadamu. Tunawaonyesha watu upendo mwingi zaidi tunapowatangazia tumaini hilo hakika badala ya kuwahimiza wawatumaini wanadamu walete wakati ujao ulio salama. Biblia inasema: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote. Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea. Mwenye furaha ni yule ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake, ambaye tumaini lake liko katika Yehova Mungu wake.” (Zaburi 146:3-5) Hivyo, badala ya kuwatuma wanafunzi wake wakahubiri njia bora ya kuunda serikali, Yesu aliwafundisha wahubiri “habari njema ya ufalme.”—Mathayo 10:6, 7; 24:14.

Basi, hiyo ndiyo “kazi ya Bwana” ambayo wahubiri Wakristo wameagizwa wafanye. Kwa kuwa raia za Ufalme wa Mungu wanatakiwa kupendana, Ufalme utafanikiwa kuondoa umaskini kwa kugawanya mali za wanadamu kwa njia ifaayo. (Zaburi 72:8, 12, 13) Hizo ni habari njema ambazo tunapaswa kuhubiri.

Leo, Mashahidi wa Yehova wamepangwa kwa ajili ya ‘kazi hiyo ya Bwana’ katika nchi 235. Kupatana na amri ya Yesu, wao huheshimu serikali zote. (Mathayo 22:21) Lakini wao pia hutii maneno haya ambayo Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni.”—Yohana 15:19.

Watu fulani waliohubiri siasa walibadilika baada ya kujifunza Biblia kwa makini. Mwanasiasa mmoja Mwitaliano aliyekuwa mshiriki wa Harakati ya Katoliki, kikundi kinachosimamiwa na kanisa, alisema: “Nilijiunga na siasa nikifikiri kwamba mtu anapaswa kuchangia ukuzi wa kisiasa na wa kijamii.” Baada ya kujiuzulu kama meya wa jiji ili kuhubiri Ufalme wa Mungu akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, yeye alieleza ni kwa nini jitihada za wanasiasa wanyoofu hushindwa. “Ulimwengu uko jinsi ulivyo kwa sababu jitihada za watu wachache wenye mioyo mieupe zimeshindwa na matendo maovu ya walio wengi, wala si kwa sababu watu walio wanyoofu hawajitahidi kuboresha hali katika jamii.”

Kujiepusha na siasa ili kuhubiri tumaini pekee kwa wanadamu hakuwazuii Wakristo wa kweli kuwasaidia wengine. Wale ambao Wakristo hao husaidia wawe raia za Ufalme wa Mungu hujifunza kubadili mitazamo isiyofaa, kuheshimu mamlaka, kuboresha maisha yao ya familia, na kuwa na maoni yanayofaa kuhusu mali. Jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba Mashahidi wa Yehova huwasaidia watu wawe na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.

Wahubiri wa Ufalme wa Mungu hunufaisha watu katika jamii wanakoishi. Isitoshe, wao huwaelekeza watu watumaini serikali ambayo ni halisi na ambayo itawaletea wote wanaompenda Mungu amani ya kudumu. Kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo, Wakristo hao wako huru kutoa msaada wenye kudumu unaopatikana leo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Aliacha Siasa na Kuwa Mhubiri wa Ufalme wa Mungu

Alipokuwa mvulana, Átila alijifunza kuhusu harakati za ukombozi kutoka kwa kasisi wa parokia yake huko Belém, Brazili. Alifurahi kusikia kwamba mwishowe wanadamu watawekwa huru kutokana na ukandamizaji, hivyo akajiunga na kikundi kimoja cha kuhamasisha watu, naye akajifunza kupanga maandamano ya kuteta na kampeni za kuchochea maasi.

Lakini Átila pia alifurahia kuwafundisha watoto wa wafuasi wa kikundi hicho, akitumia kitabu alichopewa, Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. * Kitabu hicho kilizungumzia mwenendo mzuri na kuwatii wenye mamlaka. Jambo hilo lilimfanya Átila ashangae ni kwa nini wale waliounga mkono harakati za ukombozi hawakufuata maadili bora ya Yesu, na kwa nini wengine wanapopata mamlaka huwasahau watu waliokandamizwa. Aliacha kikundi hicho. Baadaye, Mashahidi wa Yehova walimtembelea na kuzungumza naye kuhusu Ufalme wa Mungu. Muda si muda, akaanza kujifunza Biblia na kujua kitulizo cha kweli kwa wanadamu wanaokandamizwa.

Wakati huo, Átila alihudhuria mkutano wa Wakatoliki kuhusu dini na siasa. Waliohutubu walisema, “Hakuna tofauti kati ya Dini na Siasa.” Pia alihudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Aliona tofauti iliyoje! Kwanza kabisa, hakuna mtu aliyevuta sigareti, kunywa pombe, au kufanya mizaha michafu. Aliamua kujiunga na Mashahidi katika kazi yao ya kuhubiri, na muda si muda akabatizwa. Sasa anaweza kuona ni kwa nini harakati za ukombozi si suluhisho kamili la matatizo ya walio maskini.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Msimamo wa kutokuwamo wa wahudumu Wakristo hauwazuii kuwasaidia wengine