Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tianeni Nguvu

Tianeni Nguvu

Tianeni Nguvu

“Hawa ndio wamekuwa msaada wenye kunitia nguvu.”—WAKOLOSAI 4:11.

1, 2. Licha ya hatari, kwa nini marafiki wa Paulo walimtembelea gerezani?

INAWEZA kuwa hatari unapokuwa rafiki ya mtu anayeteseka gerezani, hata kama rafiki yako amefungwa isivyo haki. Huenda maofisa wa gereza wakawa na shaka nawe, huku wakichunguza kila jambo unalofanya ili kuhakikisha kwamba hutendi uhalifu. Kwa hiyo, unahitaji kuwa na ujasiri ili kuwasiliana na rafiki yako na kumtembelea gerezani.

2 Lakini marafiki fulani wa Paulo walifanya vivyo hivyo miaka 1,900 iliyopita. Hawakusita kumtembelea Paulo gerezani ili kumfariji, kumtia moyo, na kumwimarisha kiroho. Marafiki hao washikamanifu walikuwa akina nani? Nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na ujasiri, ushikamanifu, na urafiki wao?—Methali 17:17.

‘Msaada Wenye Kutia Nguvu’

3, 4. (a) Marafiki watano wa Paulo ni akina nani, nao walimfanyia nini? (b) ‘Msaada wenye kutia nguvu’ ni nini?

3 Na tufikirie mwaka wa 60 W.K. Mtume Paulo yuko gerezani Roma kwa mashtaka ya uwongo ya uchochezi. (Matendo 24:5; 25:11, 12) Paulo anataja Wakristo watano waliomtegemeza: Tikiko, mjumbe wake binafsi kutoka wilaya ya Asia na ‘mtumwa mwenzake katika Bwana’; Onesimo, ‘ndugu mwaminifu na mpendwa’ kutoka Kolosai; Aristarko, Mmakedonia kutoka Thesalonike ambaye wakati mmoja alikuwa “mateka” pamoja na Paulo; Marko, binamu ya Barnaba aliyeandamana na Paulo katika kazi ya umishonari na ambaye aliandika kitabu cha Injili chenye jina lake; na Yusto, aliyekuwa mmoja wa wale waliofanya kazi pamoja na mtume huyo “kwa ajili ya ufalme wa Mungu.” Akizungumza kuhusu Wakristo hao watano, Paulo anasema: “Hawa ndio wamekuwa msaada wenye kunitia nguvu.”—Wakolosai 4:7-11.

4 Paulo alitoa taarifa yenye nguvu kuhusu msaada aliopata kutoka kwa marafiki wake waaminifu. Alitumia neno la Kigiriki (pa·re·go·riʹa) linalotafsiriwa ‘msaada wenye kutia nguvu,’ ambalo linapatikana tu katika mstari huo wa Biblia. Neno hilo lina maana nyingi na lilitumiwa hasa kuhusiana na madawa. * Linaweza kutafsiriwa kuwa ‘kitulizo, faraja, au nafuu.’ Paulo alihitaji kuimarishwa kwa njia hiyo, nao wanaume hao watano walifanya hivyo.

Kwa Nini Paulo Alihitaji ‘Msaada Wenye Kutia Nguvu’?

5. Ingawa Paulo alikuwa mtume, alihitaji nini, na sote tunahitaji nini pindi kwa pindi?

5 Paulo aliyekuwa mtume alihitaji kuimarishwa, ingawa huenda wengine wakashangazwa na jambo hilo. Ni kweli kwamba Paulo alikuwa na imani yenye nguvu, naye alivumilia kuteswa sana kimwili, “mapigo kwa kuzidi mno,” “kukaribia kufa mara nyingi,” na mambo mengine yenye kuumiza. (2 Wakorintho 11:23-27) Hata hivyo, alikuwa mwanadamu, na pindi kwa pindi wanadamu wote wanahitaji faraja na kusaidiwa na wengine kuimarisha imani yao. Ilikuwa vivyo hivyo kuhusiana na Yesu. Usiku wake wa mwisho malaika alimtokea huko Gethsemane na ‘kumtia nguvu.’—Luka 22:43.

6, 7. (a) Ni nani waliomvunja moyo Paulo akiwa Roma, na ni nani waliomtia moyo? (b) Ndugu Wakristo wa Paulo walimsaidiaje akiwa Roma, na hivyo kuthibitika kuwa ‘msaada wenye kutia nguvu’?

6 Paulo pia alihitaji kuimarishwa. Alipofika Roma akiwa mfungwa hakukaribishwa kwa uchangamfu na watu wa jamii yake. Kwa ujumla, Wayahudi hao hawakupendezwa na ujumbe wa Ufalme. Baada ya wakuu wa Wayahudi kumtembelea Paulo kifungoni, masimulizi katika kitabu cha Matendo yanasema: ‘Wengine walianza kuamini mambo yaliyosemwa; wengine hawakuamini. Kwa hiyo, kwa sababu walikosa kukubaliana, wakaanza kuondoka.’ (Matendo 28:17, 24, 25) Bila shaka, Paulo aliumia sana kuona kwamba hawakuthamini fadhili zisizostahiliwa za Yehova! Alionyesha wazi hisia zake kali kuhusu jambo hilo katika barua aliyokuwa ameliandikia kutaniko la Roma miaka michache mapema: “Nina huzuni kubwa na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu. Kwa maana ningetaka mimi mwenyewe nitenganishwe na Kristo, niwe aliyelaaniwa kwa ajili ya ndugu zangu [Wayahudi], jamaa zangu kulingana na mwili.” (Waroma 9:2, 3) Hata hivyo, akiwa Roma alipata waandamani wa kweli na washikamanifu waliomtuliza kwa ujasiri na upendo wao. Walikuwa ndugu zake wa kiroho wa kweli.

7 Ndugu hao watano walikuwaje msaada wenye kutia nguvu? Hawakuona haya kumtembelea Paulo kwa sababu tu alikuwa gerezani. Badala yake, walimsaidia Paulo kwa hiari na kwa upendo, wakimfanyia kazi ambazo hangeweza kufanya kwa sababu alikuwa kifungoni. Kwa mfano, Paulo aliwatuma kupelekea makutaniko mbalimbali barua na maagizo ya mdomo nao wakamletea ripoti zenye kumtia moyo kuhusu hali ya akina ndugu huko Roma na kwingineko. Yaelekea walimletea Paulo vitu alivyohitaji kama vile mavazi ya kujikinga na baridi kali, vitabu vya kukunjwa, na vifaa vya kuandikia. (Waefeso 6:21, 22; 2 Timotheo 4:11-13) Msaada huo wote ulimwimarisha na kumtia moyo mtume huyo aliyekuwa gerezani, ili naye aweze kuwa ‘msaada wenye kutia nguvu’ kwa wengine, na kwa makutaniko mazima.—Waroma 1:11, 12.

Jinsi ya Kuwa ‘Msaada Wenye Kutia Nguvu’

8. Tunaweza kujifunza nini kutokana na unyenyekevu wa Paulo wa kukubali kwamba alihitaji ‘msaada wenye kutia nguvu’?

8 Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi hayo ya Paulo na wafanyakazi wenzake? Na tuchunguze jambo moja hususa tunaloweza kujifunza: Tunahitaji kuwa wajasiri na wenye kujidhabihu ili kuwasaidia wengine wanapopatwa na shida. Isitoshe, tunahitaji kuwa wanyenyekevu kukubali kwamba huenda nyakati nyingine tukahitaji kusaidiwa tunapopatwa na shida. Paulo alikiri kwamba alihitaji msaada na kuukubali kwa upole huku akiwapongeza walioutoa. Hakuona ni udhaifu au ni aibu kukubali msaada kutoka kwa wengine, nasi pia tunapaswa kuwa vivyo hivyo. Tukisema kwamba hatuhitaji msaada wenye kutia nguvu, hiyo itamaanisha tuna nguvu zinazozidi za binadamu. Kumbuka kwamba mfano wa Yesu unaonyesha kuwa huenda wakati mwingine hata mwanadamu mkamilifu akalilia msaada.—Waebrania 5:7.

9, 10. Kunaweza kuwa na matokeo gani mazuri mtu akikubali kwamba anahitaji msaada, na jambo hilo linaweza kuathirije washiriki wengine katika familia na kutanikoni?

9 Matokeo yanaweza kuwa mazuri iwapo ndugu wenye madaraka watakubali kwamba wamepungukiwa na kwamba wanategemea msaada wa wengine. (Yakobo 3:2) Kufanya hivyo huimarisha uhusiano kati ya wale walio na madaraka na wale walio chini yao, na hivyo kukuza mawasiliano yenye uchangamfu na ya kirafiki. Unyenyekevu wa wale wanaokubali msaada unakuwa mfano halisi kwa wale walio katika hali kama hiyo. Hiyo huonyesha kwamba wenye kuongoza ni wanadamu wanaoweza kufikika.—Mhubiri 7:20.

10 Kwa mfano, huenda watoto wakaona ni rahisi zaidi kukubali msaada wa wazazi wao ili kushughulikia matatizo na vishawishi, iwapo wanajua kwamba wazazi wao pia walipatwa na matatizo hayohayo walipokuwa watoto. (Wakolosai 3:21) Hivyo, kunaweza kuwa na mawasiliano mazuri kati ya mzazi na mtoto. Masuluhisho kutoka katika Maandiko yanaweza kuzungumziwa kwa matokeo zaidi na kukubaliwa kwa urahisi zaidi. (Waefeso 6:4) Vivyo hivyo, washiriki wa kutaniko watakuwa tayari zaidi kukubali msaada kutoka kwa wazee wanapotambua kwamba wazee pia hukabili matatizo, hofu, na mambo yenye kutatanisha. (Waroma 12:3; 1 Petro 5:3) Pia, kunaweza kuwa na mawasiliano mazuri, mashauri kutoka katika Maandiko yanaweza kuzungumziwa, na imani inaweza kuimarishwa. Kumbuka kwamba ndugu na dada zetu wanahitaji kuimarishwa hasa wakati huu.—2 Timotheo 3:1.

11. Kwa nini leo watu wengi wanahitaji ‘msaada wenye kutia nguvu’?

11 Hata tuwe tunaishi wapi, tuwe nani, au tuwe na umri gani, wakati mwingine sote tutakabili matatizo maishani. Hayo ni mambo ya kawaida ulimwenguni leo. (Ufunuo 12:12) Hali hizo zinazosumbua kimwili au kihisia hujaribu imani yetu. Huenda majaribu yakatokea kazini, shuleni, katika familia, au kutanikoni. Hali hiyo inaweza kusababishwa na ugonjwa mbaya au jambo lililotukia zamani linaloathiri hisia. Inaweza kuburudisha kama nini ikiwa kwa fadhili mwenzi wa ndoa, mzee, au rafiki anakutia moyo kwa kukusaidia na kwa maneno yenye ufikirio! Kwani, ni kama marhamu juu ya ngozi inayowasha! Hivyo, ukiona mmoja wa ndugu zako akiwa katika hali kama hiyo, na uwe msaada wenye kutia nguvu kwake. Au ikiwa unalemewa na tatizo fulani, waombe watu wanaostahili kiroho wakusaidie.—Yakobo 5:14, 15.

Jinsi Kutaniko Linavyoweza Kusaidia

12. Kila mmoja kutanikoni anaweza kufanya nini ili kuwaimarisha ndugu zake?

12 Wote kutanikoni, kutia ndani vijana, wanaweza kufanya jambo fulani ili kuwaimarisha wengine. Kwa mfano, unapohudhuria mikutano na kuhubiri kwa ukawaida unaimarisha sana imani ya wengine. (Waebrania 10:24, 25) Unapokuwa imara katika utumishi mtakatifu unathibitisha ushikamanifu wako kwa Yehova na kuonyesha kwamba unaendelea kuwa macho kiroho ingawa huenda ikawa unakabili magumu. (Waefeso 6:18) Uimara huo unaweza kuwaimarisha wengine.—Yakobo 2:18.

13. Kwa nini huenda wengine wakawa wahubiri wasiotenda, na ni nini kinachoweza kufanywa ili kuwasaidia?

13 Mara kwa mara, mikazo ya maisha na matatizo mengine yanaweza kufanya wengine wapunguze mwendo au wawe wahubiri wasiotenda. (Marko 4:18, 19) Huenda tusiwaone kwenye mikutano ya kutaniko. Lakini huenda wakawa bado wanampenda Mungu moyoni mwao. Ni nini kinachoweza kufanywa ili kuimarisha imani yao? Kwa fadhili wazee wanaweza kuwasaidia kwa kuwatembelea. (Matendo 20:35) Pia washiriki wengine wa kutaniko wanaweza kuombwa wasaidie. Huenda ziara hizo zenye upendo ndizo tu zinazohitajiwa ili kuimarisha imani ya ndugu hao walio dhaifu.

14, 15. Paulo anatoa shauri gani kuhusu kuwaimarisha wengine? Toa mfano wa kutaniko moja lililofuata shauri hilo.

14 Biblia hutuhimiza ‘kusema kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika, kutegemeza walio dhaifu.’ (1 Wathesalonike 5:14) Labda ‘nafsi hizo zilizohuzunika’ wanatambua kwamba ujasiri wao unadidimia na kwamba bila msaada hawawezi kushinda matatizo wanayokabili. Je, unaweza kuwasaidia? Maneno ‘kutegemeza walio dhaifu’ yametafsiriwa “kushika sana” au “kushikamana na” walio dhaifu. Yehova anawathamini na kuwapenda kondoo zake wote. Hawaoni kuwa duni, na hangependa yeyote apeperuke. Je, unaweza kulisaidia kutaniko ‘lishike sana’ wale walio dhaifu kiroho hadi wapate nguvu?—Waebrania 2:1.

15 Mzee mmoja alitembelea mume na mke ambao walikuwa wahubiri wasiotenda kwa miaka sita. Mzee huyo anaandika: “Hangaiko lenye upendo na fadhili ambazo kutaniko zima liliwaonyesha liliwachochea sana hivi kwamba walirudi kwenye kundi.” Dada huyo asiyetenda alihisije kuhusu ziara za washiriki wa kutaniko? Sasa anasema: “Kilichotusaidia kuanza kutenda tena ni kwamba ndugu waliotutembelea pamoja na dada walioandamana nao, hawakutulaumu wala kutushutumu. Badala yake, walikuwa wenye huruma, nao walitutia moyo kwa kutumia Maandiko.”

16. Ni nani ambaye yuko tayari sikuzote kuwasaidia wale wanaohitaji kuimarishwa?

16 Naam, Mkristo mnyoofu hufurahia kuwa msaada wenye kutia nguvu kwa wengine. Nazo hali zinapobadilika katika maisha yetu, huenda sisi pia tukahitaji kuimarishwa na ndugu zetu. Kwa kweli, tunahitaji kuelewa kwamba huenda ndugu zetu wasipatikane wakati tunapohitaji msaada. Hata hivyo, kuna mmoja aliye Chanzo cha nguvu ambaye hupatikana sikuzote, naye huwa tayari kutusaidia sikuzote—Yehova Mungu.—Zaburi 27:10.

Yehova Ndiye Chanzo Kikuu Zaidi cha Nguvu

17, 18. Yehova alimwimarisha Mwanawe Yesu Kristo katika njia zipi?

17 Alipokuwa amepigiliwa misumari kwenye mti wa mateso, Yesu alilia kwa sauti kubwa hivi: “Baba, ninaikabidhi roho yangu mikononi mwako.” (Luka 23:46) Kisha akafa. Muda mfupi kabla ya hapo, alikuwa amekamatwa na marafiki wake wa karibu wakamwacha na kukimbia kwa woga. (Mathayo 26:56) Baada ya marafiki wake kumwacha, Yesu alibaki na Chanzo kimoja tu cha nguvu, yaani, Babake wa mbinguni. Hata hivyo, hakumtumaini Yehova bure. Kwa kuwa Yesu alikuwa mshikamanifu, Babake alimthawabisha kwa kumtegemeza kwa ushikamanifu.—Zaburi 18:25; Waebrania 7:26.

18 Wakati wa huduma ya Yesu duniani, Yehova alimwandalia Mwanawe yale aliyohitaji ili kudumisha utimilifu wake hadi kifo. Kwa mfano, punde baada ya Yesu kubatizwa ili kuanza huduma yake, alisikia sauti ya Babake ikisema kwamba anamkubali na kumhakikishia kwamba anampenda. Yesu alipohitaji msaada, Yehova aliwatuma malaika ili kumwimarisha. Yesu alipokabili jaribu kubwa zaidi mwishoni mwa maisha yake duniani, Yehova alisikia na kukubali dua na maombi yake. Bila shaka, mambo hayo yote yalikuwa msaada uliomtia Yesu nguvu.—Marko 1:11, 13; Luka 22:43.

19, 20. Tunawezaje kuwa na hakika kwamba Yehova atatuimarisha wakati tunapokuwa na uhitaji?

19 Yehova anataka pia awe Chanzo chetu kikuu cha nguvu. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Yehova anaweza kuwa msaada wenye kututia nguvu wakati tunapokuwa na uhitaji kwa kuwa yeye ndiye Chanzo cha kweli cha nguvu zote zenye msukumo, naye ni hodari katika nguvu. (Isaya 40:26) Tunaweza kukabili mkazo mkubwa sana kutokana na vita, umaskini, ugonjwa, kifo, au hali yetu ya kutokamilika. Majaribu ya maisha yanapoonekana kuwa makubwa sana kama ‘adui mwenye nguvu,’ Yehova anaweza kuwa nguvu na uwezo wetu. (Zaburi 18:17; Kutoka 15:2) Yeye hutusaidia kupitia roho yake takatifu iliyo na nguvu nyingi. Kupitia roho hiyo, Yehova anaweza kumpa “nguvu mtu aliyechoka” ili aweze ‘kuruka juu kwa mabawa kama tai.’—Isaya 40:29, 31.

20 Roho ya Mungu ndiyo nguvu kuu zaidi katika ulimwengu wote. Paulo alisema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” Naam, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anaweza kutupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili tuvumilie matatizo yote yenye kuumiza hadi atakapofanya “vitu vyote kuwa vipya” katika Paradiso aliyoahidi ambayo inakaribia sana.—Wafilipi 4:13; 2 Wakorintho 4:7; Ufunuo 21:4, 5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kichapo Vine’s Complete Expository Dictionary of Old and New Testament Words, cha W. E. Vine, kinasema: “Kitenzi cha neno [pa·re·go·riʹa] hurejelea dawa ambazo hutuliza mwasho.”

Je, Unakumbuka?

• Akina ndugu huko Roma walikuwaje ‘msaada wenye kutia nguvu’ kwa Paulo?

• Ni katika njia zipi tunaweza kuwa ‘msaada wenye kutia nguvu’ kutanikoni?

• Yehova ni Chanzo chetu kikuu zaidi cha nguvu jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Akina ndugu walikuwa ‘msaada wenye kutia nguvu’ kwa Paulo kwa kumtegemeza kwa ushikamanifu, kumtia moyo, na kumsaidia

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wazee huwa mstari wa mbele katika kuimarisha kundi