Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Jasiri Kama Yeremia

Uwe Jasiri Kama Yeremia

Uwe Jasiri Kama Yeremia

“Mtumaini Yehova; uwe hodari na moyo wako uwe na nguvu. Naam, mtumaini Yehova.”—ZABURI 27:14.

1. Ni baraka gani nyingi ambazo Mashahidi wa Yehova hufurahia?

MASHAHIDI WA YEHOVA wanaishi katika paradiso ya kiroho. (Isaya 11:6-9) Katikati ya ulimwengu wenye misukosuko mingi, wao hufurahia hali ya kipekee ya kiroho pamoja na Wakristo wenzao, ambao wana amani kati yao na pia pamoja na Yehova Mungu. (Zaburi 29:11; Isaya 54:13) Paradiso yao ya kiroho inaendelea kukua. Wote ‘wanaofanya mapenzi ya Mungu kwa nafsi yote’ wanasaidia kuipanua. (Waefeso 6:6) Jinsi gani? Kwa kuishi kupatana na kanuni za Biblia na kwa kuwafundisha wengine wafanye hivyo, na hivyo kuwaalika wanufaike na baraka nyingi za paradiso hiyo.—Mathayo 28:19, 20; Yohana 15:8.

2, 3. Wakristo wa kweli wanapaswa kuvumilia nini?

2 Hata hivyo, kuishi katika paradiso ya kiroho hakumaanishi kwamba hatutapatwa na majaribu. Sisi bado si wakamilifu na hupatwa na maumivu yanayotokana na magonjwa, uzee, na kifo. Pia, tunaona utimizo wa unabii mbalimbali unaohusu “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Vita, uhalifu, magonjwa, njaa, na hali nyingine ngumu sana huwapata wanadamu wote na hata Mashahidi wa Yehova.—Marko 13:3-10; Luka 21:10, 11.

3 Licha ya hayo yote, tunajua vizuri sana kwamba ingawa tuna usalama katika paradiso yetu ya kiroho bado tunapata upinzani mkali kutoka kwa wale ambao hawamo katika paradiso hiyo. Yesu aliwaonya wafuasi wake hivi: “Sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi. Kumbukeni neno nililowaambia, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yohana 15:18-21) Hali iko hivyo leo. Watu wengi bado hawaelewi wala hawathamini ibada yetu. Baadhi yao hutuchambua, hutudhihaki, au hata—kama vile Yesu alivyoonya—kutuchukia. (Mathayo 10:22) Mara nyingi, wengine hueneza habari za uwongo na propaganda yenye chuki kupitia vyombo vya habari kusudi tueleweke vibaya. (Zaburi 109:1-3) Naam, sote hukabili hali ngumu, na huenda baadhi yetu tukavunjika moyo. Tunawezaje kuvumilia?

4. Sisi hutafuta wapi msaada ili kuendelea kuvumilia?

4 Yehova atatusaidia. Mtunga-zaburi aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Mwadilifu ana misiba mingi, lakini Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo.” (Zaburi 34:19; 1 Wakorintho 10:13) Wengi wetu tunaweza kushuhudia kwamba tunapomtumaini Yehova kabisa, yeye hutuimarisha kuvumilia hali yoyote ngumu. Upendo wetu kwake na shangwe iliyowekwa mbele yetu hutusaidia kukabiliana na woga na kuvunjika moyo. (Waebrania 12:2) Hivyo, tunapokabili magumu, sisi huendelea kusimama imara.

Neno la Mungu Lilimwimarisha Yeremia

5, 6. (a) Tuna mifano gani ya waabudu wa kweli ambao waliweza kuvumilia? (b) Yeremia aliitikiaje alipoitwa kuwa nabii?

5 Katika historia yote, watumishi waaminifu wa Yehova wamepata shangwe licha ya hali ngumu. Baadhi yao waliishi wakati Yehova alipotekeleza hukumu kwa kuonyesha hasira yake juu ya watu wasio waaminifu. Kati ya waabudu hao waaminifu kulikuwemo Yeremia na watu wachache wa siku zake, na pia Wakristo wa karne ya kwanza. Habari kuhusu watu hao wa zamani zimeandikwa katika Biblia ili zitutie moyo, na tunaweza kujifunza mengi kwa kuzisoma. (Waroma 15:4) Kwa mfano, fikiria Yeremia.

6 Yeremia alikuwa kijana alipoitwa kutumikia akiwa nabii huko Yuda. Huo ulikuwa mgawo mgumu. Wengi waliabudu miungu ya uwongo. Ingawa Yosia, aliyekuwa mfalme wakati Yeremia alipoanza huduma yake, alikuwa mwaminifu, wafalme wote waliofuata hawakuwa waaminifu, nao wengi wa manabii na makuhani waliokuwa na daraka la kuwafundisha watu, hawakuitetea kweli. (Yeremia 1:1, 2; 6:13; 23:11) Basi, Yeremia alihisije Yehova alipomwita awe nabii? Aliogopa! (Yeremia 1:8, 17) Yeremia alikumbuka jinsi alivyoitikia mara ya kwanza: “Nikasema: ‘Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama, mimi hakika sijui jinsi ya kusema, kwa sababu mimi ni mvulana tu.’”—Yeremia 1:6.

7. Yeremia alipata itikio gani katika eneo lake, naye alitendaje?

7 Wengi katika eneo ambalo Yeremia alihubiri hawakuitikia, na mara nyingi walimpinga vikali. Pindi moja, Pashuri aliyekuwa kuhani alimpiga na kuagiza awekwe katika mikatale. Yeremia alieleza jinsi alivyohisi wakati huo: “Nilisema: ‘Sitamtaja [Yehova] tena, wala sitasema tena katika jina lake.’” Labda wakati mwingine umehisi hivyo, ukataka kuacha kumtumikia Yehova. Ona kilichomsaidia Yeremia avumilie. Alisema: “Moyoni mwangu hali hiyo [neno la Mungu, au ujumbe] ikawa kama moto unaowaka ambao umefungiwa ndani ya mifupa yangu; nami nikachoka kujizuia, nami sikuweza kuivumilia.” (Yeremia 20:9) Je, wewe huhisi hivyo kuhusu maneno ya Mungu?

Watu Waliofanya Kazi Pamoja na Yeremia

8, 9. (a) Nabii Uriya alionyesha udhaifu gani, na ikawaje? (b) Kwa nini Baruku alivunjika moyo, naye alisaidiwaje?

8 Yeremia hakufanya kazi ya unabii akiwa peke yake. Kulikuwa na wengine aliofanya kazi nao, na hapana shaka walimtia moyo. Hata hivyo, wakati mwingine wale aliofanya kazi nao hawakutenda kwa hekima. Kwa mfano, nabii mwenzake aitwaye Uriya alitoa maonyo kwa bidii dhidi ya Yerusalemu na Yuda “sawasawa na maneno yote ya Yeremia.” Lakini Mfalme Yehoyakimu alipoamuru Uriya auawe, nabii huyo aliogopa na kukimbilia Misri. Hiyo haikumwokoa. Wanaume wa mfalme walimfuata, wakamkamata, na kumrudisha Yerusalemu, ambako aliuawa. Bila shaka, Yeremia alishtuka sana.—Yeremia 26:20-23.

9 Mtu mwingine aliyefanya kazi na Yeremia ni mwandishi wake Baruku. Baruku alimsaidia sana Yeremia, lakini pindi moja yeye pia aliacha kuwa na maoni ya kiroho. Alianza kulalamika, akisema: “Ole wangu, sasa, kwa maana Yehova ameongeza huzuni juu ya maumivu yangu! Nimechoka kwa sababu ya kuugua kwangu, nami sikupata mahali pa kupumzika.” Baruku alivunjika moyo na kuanza kupoteza uthamini wa mambo ya kiroho. Hata hivyo, kwa upole, Yehova alimpa Baruku shauri la hekima, naye akarekebisha maoni yake. Hivyo, alihakikishiwa kwamba angeokoka uharibifu wa Yerusalemu. (Yeremia 45:1-5) Yeremia alitiwa moyo kama nini wakati Baruku alipopata tena usawaziko wa kiroho.

Yehova Alimtegemeza Nabii Wake

10. Yehova alimpa Yeremia ahadi zipi za kumtegemeza?

10 Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba Yehova hakumwacha Yeremia. Alielewa hisia za nabii wake, naye akampa nguvu na msaada aliohitaji. Kwa mfano, mwanzoni mwa huduma yake, wakati Yeremia alipotilia shaka uwezo wake, Yehova alimwambia hivi: “Usiogope kwa sababu ya nyuso zao, kwa maana ‘mimi niko pamoja nawe ili kukukomboa,’ asema Yehova.” Kisha, baada ya kumjulisha Yeremia mgawo wake, Yehova akasema: “Hakika watapigana nawe, lakini hawatakushinda, kwa maana ‘Mimi niko pamoja nawe,’ asema Yehova, ‘ili nikukomboe.’” (Yeremia 1:8, 19) Ahadi hiyo ilimfariji kama nini! Naye Yehova aliitimiza.

11. Tunajuaje kwamba Yehova alitimiza ahadi yake ya kumtegemeza Yeremia?

11 Hivyo, baada ya Yeremia kutiwa katika mikatale na kudhihakiwa hadharani, alisema hivi kwa uhakika: “Yehova alikuwa pamoja nami kama mwenye nguvu anayetisha. Ndiyo sababu wale wanaonitesa watajikwaa nao hawatashinda. Hakika watapatwa na aibu kabisa.” (Yeremia 20:11) Katika miaka ya baadaye, wakati majaribio ya kumuua yalipofanywa, Yehova aliendelea kuwa pamoja naye, na kama Baruku, Yeremia aliokoka uharibifu wa Yerusalemu akiwa mtu huru. Lakini watu waliomtesa na wale waliopuuza maonyo yake walikufa au wakachukuliwa mateka kwenda Babiloni.

12. Ingawa kuna mambo mbalimbali yenye kuvunja moyo, tunapaswa kukumbuka nini?

12 Leo Mashahidi wengi wa Yehova huvumilia mateso kama Yeremia. Kama ilivyotajwa awali, baadhi ya mateso hayo hutokana na hali yetu ya kutokamilika, mengine hutokana na machafuko katika ulimwengu wa leo, nayo mengine hutokana na wale wanaoipinga kazi yetu. Mateso hayo yanaweza kuvunja moyo. Kama Yeremia, huenda tukaanza kuona kama hatutaweza kuendelea na utumishi wetu. Naam, tunaweza kutarajia kuvunjika moyo pindi kwa pindi. Kuvunjika moyo hujaribu kina cha upendo wetu kwa Yehova. Hivyo, na tusiruhusu kamwe kuvunjika moyo kufanye tuache utumishi wa Yehova kama Uriya. Badala yake, na tumwige Yeremia na kuwa na hakika kwamba Yehova atatutegemeza.

Jinsi ya Kukabiliana na Kuvunjika Moyo

13. Tunawezaje kuiga vielelezo vya Yeremia na Daudi?

13 Yeremia aliwasiliana kwa ukawaida na Yehova Mungu, na kumweleza hisia zake za ndani kabisa na kumwomba amwimarishe. Huo ni mfano mzuri wa kuigwa. Daudi wa kale ambaye pia alitegemea nguvu kutoka kwa Yehova, aliandika: “Kwa maneno yangu utege sikio, Ee Yehova; uelewe kuugua kwangu. Sikiliza kwa makini sauti ya kilio changu kwa ajili ya msaada, Ee Mfalme wangu na Mungu wangu, kwa maana kwako wewe ninasali.” (Zaburi 5:1, 2) Masimulizi kuhusu maisha ya Daudi ambayo yameongozwa na roho ya Mungu, yanaonyesha kwamba Yehova alijibu tena na tena sala za Daudi za kumwomba msaada. (Zaburi 18:1, 2; 21:1-5) Katika njia hiyohiyo, tunapopatwa na mikazo mikali au matatizo yetu yanapoonekana kama hayawezi kutatulika, inafariji sana kusali kwa Yehova na kumweleza yote yaliyo moyoni. (Wafilipi 4:6, 7; 1 Wathesalonike 5:16-18) Yehova hakatai kutusikiliza, bali hutuhakikishia kwamba ‘yeye anatujali sisi.’ (1 Petro 5:6, 7) Hata hivyo, halingekuwa jambo la akili kusali kwa Yehova na kutosikiliza anayosema.

14. Maneno ya Yehova yalimwathirije Yeremia?

14 Yehova huzungumzaje nasi? Fikiria jinsi Yehova alivyowasiliana na Yeremia. Kwa kuwa Yeremia alikuwa nabii, Yehova aliwasiliana naye moja kwa moja. Yeremia anaeleza jinsi maneno ya Mungu yalivyouathiri moyo wake: “Maneno yako yalipatikana, nami nikayala; na neno lako linakuwa kwangu furaha na kushangilia kwa moyo wangu; kwa maana jina lako limeitwa juu yangu, Ee Yehova Mungu wa majeshi.” (Yeremia 15:16) Naam, Yeremia alifurahi kwamba alihusianishwa na jina la Mungu, nayo maneno Yake yalikuwa yenye thamani kwake. Hivyo, kama mtume Paulo, Yeremia alitamani kutangaza ujumbe aliopewa.—Waroma 1:15, 16.

15. Tunawezaje kuyatia maneno ya Yehova katika mioyo yetu, na ni kwa kutafakari mambo gani kutafanya tusinyamaze?

15 Leo Yehova hawasiliani moja kwa moja na mtu yeyote tu. Hata hivyo, tunapata maneno ya Mungu katika Biblia. Hivyo, ikiwa tunajifunza Biblia kwa bidii na kutafakari kwa uzito mambo tunayojifunza, maneno ya Mungu yatakuwa “furaha na kushangilia” katika moyo wetu pia. Na tunaweza kufurahi kwamba tunawasilisha jina la Yehova tunapoenda kuwaeleza wengine maneno hayo. Na tusisahau kamwe kwamba leo hakuna watu wengine duniani wanaolitangaza jina la Yehova. Ni Mashahidi wake tu wanaotangaza habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu uliosimamishwa na kuwafundisha wapole kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. (Mathayo 28:19, 20) Tumebarikiwa kama nini! Tunapofikiria pendeleo kubwa ambalo kwa upendo Yehova ametupa, hatuwezi kunyamaza.

Na Tujihadhari na Mashirika Yetu

16, 17. Yeremia alikuwa na maoni gani kuhusu mashirika, nasi tunawezaje kumwiga?

16 Yeremia anataja jambo lingine lililomsaidia awe jasiri. Alisema: “Sikuketi katika kikundi cha rafiki wanaofanya utani na kuanza kufurahi. Kwa sababu ya mkono wako nimeketi mimi peke yangu, kwa maana wewe umenijaza shutuma.” (Yeremia 15:17) Yeremia aliona ni afadhali kuwa peke yake kuliko kupotoshwa na mashirika mabaya. Leo sisi tuna maoni hayohayo. Hatusahau kamwe onyo la mtume Paulo kwamba “mashirika mabaya huharibu tabia nzuri,” hata tabia nzuri ambazo tumekuwa nazo kwa miaka mingi.—1 Wakorintho 15:33.

17 Mashirika mabaya yanaweza kufanya roho ya ulimwengu ichafue mawazo yetu. (1 Wakorintho 2:12; Waefeso 2:2; Yakobo 4:4) Basi na tuzoeze nguvu zetu za ufahamu ili kutambua mashirika mabaya na kuyaepuka kabisa. (Waebrania 5:14) Kama Paulo angekuwa hai duniani leo, unafikiri angemwambiaje Mkristo anayetazama sinema zinazoonyesha mambo ya uasherati au michezo yenye jeuri? Angemshaurije ndugu anayeshirikiana na watu asiowajua kabisa katika Intaneti? Angemwonaje Mkristo anayetumia wakati mwingi kucheza michezo ya video au kutazama televisheni, lakini ambaye hana mazoea mazuri ya funzo la kibinafsi?—2 Wakorintho 6:14b; Waefeso 5:3-5, 15, 16.

Kudumu Katika Paradiso ya Kiroho

18. Ni nini kitakachotusaidia kudumu tukiwa imara kiroho?

18 Tunathamini sana paradiso yetu ya kiroho. Haiwezi kulinganishwa na chochote ulimwenguni leo. Hata watu wasioamini husifu upendo, ufikirio, na fadhili ambazo Wakristo huonyeshana. (Waefeso 4:31, 32) Hata hivyo, huu ndio wakati hasa tunapohitaji kupambana na kuvunjika moyo. Mashirika mazuri, sala, na mazoea mazuri ya kujifunza yanaweza kutusaidia kudumu tukiwa imara kiroho. Mambo hayo yatatuimarisha kukabiliana na jaribu lolote lile kwa kumtumaini Yehova kabisa.—2 Wakorintho 4:7, 8.

19, 20. (a) Ni nini kitakachotusaidia kuvumilia? (b) Makala inayofuata inaelekezwa kwa nani, nayo itawapendeza nani pia?

19 Na tusiwaruhusu kamwe wale wanaouchukia ujumbe wa Biblia watuogopeshe na kudhoofisha imani yetu. Kama maadui waliomtesa Yeremia, wale wanaotupinga wanampinga Mungu. Hawatashinda. Yehova, ambaye ana nguvu zaidi kuliko wapinzani wetu, anatuambia: “Mtumaini Yehova; uwe hodari na moyo wako uwe na nguvu. Naam, mtumaini Yehova.” (Zaburi 27:14) Kwa kumtumaini kabisa Yehova kwa moyo wetu, na tuazimie kuendelea kufanya yaliyo mema. Na tuwe na hakika kwamba, kama Yeremia na Baruku, tutavuna tusipochoka kabisa.—Wagalatia 6:9.

20 Wakristo wengi hupambana daima na hali ya kuvunjika moyo. Hata hivyo, vijana hukabili matatizo ya kipekee. Lakini wao pia wana nafasi nzuri za kufanya maendeleo. Makala inayofuata inaelekezwa moja kwa moja kwa vijana walio kati yetu. Itawapendeza pia wazazi na watu wote wazima waliojiweka wakfu kutanikoni ambao kwa maneno, mwenendo, na kwa kutoa utegemezo wa moja kwa moja wanaweza kuwasaidia vijana kutanikoni.

Ungejibuje?

• Kwa nini tunaweza kutarajia hali zenye kuvunja moyo, nasi tutatafuta msaada kwa nani?

• Yeremia alishindaje hali ya kuvunjika moyo ingawa alikuwa na mgawo mgumu?

• Ni nini kitakachofanya mioyo yetu ‘ifurahi na kushangilia’ hata tunapokuwa na matatizo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yeremia alifikiri kwamba alikuwa kijana sana na hakuwa na uzoefu wa kuwa nabii

[Picha katika ukurasa wa 10]

Hata alipoteswa, Yeremia alijua kwamba Yehova alikuwa pamoja naye “kama mwenye nguvu anayetisha”