Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana, Je, Mnajitayarisha kwa Ajili ya Wakati Ujao?

Vijana, Je, Mnajitayarisha kwa Ajili ya Wakati Ujao?

Vijana, Je, Mnajitayarisha kwa Ajili ya Wakati Ujao?

“Mimi najua vema mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi, . . . mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili kuwapa ninyi wakati ujao na tumaini.”—YEREMIA 29:11.

1, 2. Tunaweza kuwa na maoni gani mbalimbali kuhusu miaka ya ujana?

WATU wengi wazima hufikiria ujana kuwa kipindi kizuri sana maishani. Wao hukumbuka nguvu na bidii waliyokuwa nayo wakiwa vijana. Wao hukumbuka kwa shauku wakati walipokuwa na madaraka machache, walipofurahia mambo mengi, nao walikuwa na nafasi ya kutimiza mengi maishani.

2 Yaelekea ninyi vijana mna maoni tofauti. Huenda mkawa na matatizo kukabiliana na mabadiliko ya kihisia na kimwili ya ujanani. Huenda ukawa unakabili mkazo mkali kutoka kwa wanashule wenzako. Huenda ukalazimika kujitahidi sana kukataa dawa za kulevya, kileo, na mambo ya uasherati. Wengi wenu pia hukabili suala la kutokuwamo au masuala mengine yanayohusu imani yenu. Naam, ujana unaweza kuwa wakati mgumu. Lakini, huo ni wakati unapokuwa na nafasi ya kutimiza mengi. Swali ni, Utatumiaje nafasi hizo?

Furahia Ujana Wako

3. Sulemani aliwatolea vijana shauri na onyo gani?

3 Watu wenye umri mkubwa watakuambia kwamba ujana haudumu, na wanasema kweli. Baada ya miaka michache tu, hutakuwa kijana tena. Hivyo, uufurahie sasa! Mfalme Sulemani alitoa shauri hilo alipoandika: “Ewe kijana, shangilia katika ujana wako, na moyo wako ukufanyie mema siku za ujana wako, nawe utembee katika njia za moyo wako na katika mambo ambayo macho yako yameona.” Hata hivyo, Sulemani aliwaonya vijana hivi: “Ondoa masumbuko moyoni mwako, nawe uondolee mbali msiba kutoka katika mwili wako.” Aliongeza kusema: “Ujana na upeo wa maisha ni ubatili.”—Mhubiri 11:9, 10.

4, 5. Kwa nini ni hekima vijana wajitayarishe kwa ajili ya wakati ujao? Toa mfano.

4 Je, unaelewa maneno hayo ya Sulemani? Kwa mfano, fikiria kijana anayepokea zawadi kubwa, labda urithi wa pesa. Atatumiaje pesa hizo? Anaweza kuzitumia zote kujifurahisha sawa na yule mwana mpotevu katika mfano wa Yesu. (Luka 15:11-23) Lakini itakuwaje pesa hizo zikiisha? Bila shaka, atajuta kwamba hakuzitumia vizuri! Kwa upande mwingine, tuseme anatumia pesa hizo kujitayarisha kwa ajili ya wakati ujao, labda kwa kununua kwa hekima kitu kitakachomletea faida. Mwishowe, anapopata faida kutokana na kitu alichonunua, je, unafikiri kwamba atajuta kuwa hakutumia pesa zake zote kwa kujifurahisha alipokuwa kijana? La.

5 Ione miaka yako ya ujana kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Utaitumiaje? Unaweza kutumia vibaya nguvu na bidii hiyo yote kwa kujiingiza katika mambo ya anasa, huku ukijifurahisha bila kufikiria wakati ujao. Lakini ukifanya hivyo, “ujana na upeo wa maisha” yako utakuwa “ubatili.” Ni vema kutumia ujana wako ili kujitayarisha kwa ajili ya wakati ujao.

6. (a) Ni shauri gani la Sulemani linalotoa mwongozo kwa vijana? (b) Yehova angependa kuwafanyia vijana nini, na kijana anawezaje kunufaika na jambo hilo?

6 Sulemani alitaja kanuni fulani inayoweza kukusaidia kutumia ujana wako vizuri. Alisema: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” (Mhubiri 12:1) Ili ufanikiwe, fuata shauri hilo, yaani, msikilize Yehova na ufanye mapenzi yake. Yehova aliwaambia Waisraeli mambo aliyotaka kuwafanyia: “Mimi najua vema mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi, . . . mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili kuwapa ninyi wakati ujao na tumaini.” (Yeremia 29:11) Yehova angependa pia kukupa “wakati ujao na tumaini.” Ukimkumbuka katika matendo, mawazo, na maamuzi yako, tumaini lako na wakati wako ujao utakuwa mzuri.—Ufunuo 7:16, 17; 21:3, 4.

“Mkaribieni Mungu”

7, 8. Kijana anawezaje kumkaribia Mungu?

7 Yakobo alitutia moyo kumkumbuka Yehova alipotuhimiza: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Yehova ndiye Muumba, Mwenye Enzi Kuu mbinguni, anayestahili ibada na sifa zote. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, tukimkaribia, yeye pia atatukaribia. Je, huchangamshwi moyo na jinsi anavyopendezwa nasi?—Mathayo 22:37.

8 Tunamkaribia Yehova kwa njia nyingi. Kwa mfano, mtume Paulo anasema: “Endeleeni kudumu katika sala, mkikaa macho katika hiyo pamoja na kutoa shukrani.” (Wakolosai 4:2) Yaani, sitawisha zoea la kusali. Usiridhike tu kusema amina baada ya babako au Mkristo mwenzako kutanikoni kukuwakilisha katika sala. Je, umewahi kumweleza Yehova yote yaliyo moyoni mwako na kutaja yale unayofikiria, unayoogopa, na magumu unayokabili? Je, umewahi kumweleza mambo ambayo ungeona aibu kuyazungumza na mtu mwingine yeyote? Sala za unyoofu zinazotoka moyoni zitakuletea amani. (Wafilipi 4:6, 7) Sala hizo hutusaidia kumkaribia Yehova na kuhisi kwamba yeye anatukaribia.

9. Kijana anawezaje kumsikiliza Yehova?

9 Tunaona njia nyingine ya kumkaribia Yehova katika maneno haya yaliyoongozwa na roho yake: “Sikiliza shauri na kukubali nidhamu, ili upate kuwa na hekima katika wakati wako ujao.” (Methali 19:20) Naam, ukimsikiliza Yehova na kumtii, unajitayarisha kwa ajili ya wakati ujao. Unawezaje kuonyesha kwamba unamsikiliza Yehova? Bila shaka, wewe huhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kusikiliza sehemu mbalimbali za programu. Pia, ‘unaheshimu baba yako na mama yako’ kwa kuwepo kwenye funzo la Biblia la familia. (Waefeso 6:1, 2; Waebrania 10:24, 25) Unafanya vema. Lakini, je, ‘unanunua wakati’ ili kujitayarisha kwa ajili ya mikutano, kusoma Biblia kwa ukawaida, na kufanya utafiti? Je, wewe hujitahidi kufuata yale unayosoma, ili uweze kutembea kama ‘mtu mwenye hekima’? (Waefeso 5:15-17; Zaburi 1:1-3) Ukifanya hivyo, unamkaribia Yehova.

10, 11. Vijana hupata baraka zipi kubwa wanapomsikiliza Yehova?

10 Katika maneno ya utangulizi ya kitabu cha Methali, mwandikaji huyo aliyeongozwa na roho ya Mungu anaeleza kusudi la kitabu hicho cha Biblia. Anasema kusudi ni “ili mtu ajue hekima na nidhamu, na kutambua maneno ya uelewaji, apokee nidhamu ambayo humpa mtu ufahamu, uadilifu na haki na unyoofu, kuwapa werevu wale wasio na uzoefu, kumpa kijana ujuzi na uwezo wa kufikiri.” (Methali 1:1-4) Hivyo, unaposoma na kufuata maneno ya kitabu cha Methali, na pia vitabu vingine vya Biblia, utasitawisha uadilifu na unyoofu, naye Yehova atafurahi unapomkaribia. (Zaburi 15:1-5) Ukiendelea kusitawisha haki, werevu, ujuzi, na uwezo wa kufikiri, maamuzi yako yatakuwa mazuri zaidi.

11 Je, ni jambo lisilo la akili kutarajia kijana atende kwa hekima katika njia hiyo? La, kwa kuwa vijana wengi Wakristo wanatenda hivyo. Kwa hiyo, wengine huwaheshimu na ‘hawaudharau ujana wao.’ (1 Timotheo 4:12) Kwa kufaa, wazazi wao hujivunia vijana hao, naye Yehova husema kwamba wao humfurahisha moyo. (Methali 27:11) Ingawa hao ni vijana, wanaweza kuwa na hakika kwamba maneno haya yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanawahusu: “Mwangalie mtu asiye na lawama na uendelee kumwangalia mnyoofu, kwa maana wakati ujao wa mtu huyo utakuwa wenye amani.”—Zaburi 37:37.

Fanya Maamuzi Mazuri

12. Ni nini mojawapo ya maamuzi muhimu ambayo vijana hufanya, na kwa nini uamuzi huo unaweza kuathiri maisha yako kwa miaka mingi?

12 Miaka ya ujana ni kipindi cha kufanya maamuzi. Baadhi ya maamuzi unayofanya sasa yatakuathiri kwa miaka mingi ijayo. Maamuzi ya hekima hufanya ufanikiwe na kuwa mwenye furaha maishani. Maamuzi yasiyo ya hekima yanaweza kuharibu maisha yako yote. Fikiria jinsi maamuzi haya mawili unayopaswa kufanya yanavyoweza kukuathiri. Kwanza: Wewe huchagua kushirikiana na nani? Kwa nini hilo ni muhimu? Methali iliyoongozwa na roho ya Mungu inasema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Yaani, mwishowe tutakuwa kama wale tunaoshirikiana nao—wenye hekima au wajinga. Ungependa kuwa mtu wa aina gani?

13, 14. (a) Licha ya kushirikiana moja kwa moja na watu, mashirika yanatia ndani nini? (b) Vijana wanapaswa kuepuka kosa gani?

13 Unapofikiria mashirika, yaelekea unafikiria kuwa pamoja na watu. Hiyo ni kweli, lakini mengi zaidi yanahusika. Unapotazama kipindi cha televisheni, kusikiliza muziki, kusoma hadithi, kwenda kwenye sinema, au kutumia vituo fulani katika Intaneti, unashirikiana na watu. Ikiwa ushirika huo unakusudiwa kutosheleza tamaa za kijeuri na kingono au unakutia moyo utumie dawa za kulevya, kunywa kupita kiasi, au kufanya jambo lingine lolote linalovunja kanuni za Biblia, unashirikiana na mtu “asiye na akili,” anayetenda kana kwamba Yehova hayuko.—Zaburi 14:1.

14 Labda unahisi kwamba kwa kuwa unahudhuria mikutano ya Kikristo na u mwenye bidii kutanikoni, una nguvu za kutosha usiweze kuathiriwa na sinema yenye jeuri au muziki wenye mdundo mtamu lakini wenye maneno yasiyofaa. Pengine unahisi kwamba hutapatwa na madhara yoyote kwa kutupia jicho kituo fulani cha ponografia kwenye Intaneti. Mtume Paulo anakwambia kwamba umekosea! Anasema: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Inasikitisha kwamba tabia za vijana wengi Wakristo wenye kutegemeka zimeharibiwa kwa kuchagua mashirika yasiyofaa. Kwa hiyo, azimia kuepuka mashirika hayo. Ukifanya hivyo, utakuwa ukifuata shauri hili la Paulo: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Waroma 12:2.

15. Ni uamuzi gani wa pili ambao vijana wanapaswa kufanya, na nyakati nyingine wanakabili mikazo gani kuhusiana na jambo hilo?

15 Kuna uamuzi wa pili unaokabili. Wakati utafika ambapo itakubidi uamue unalotaka kufanya baada ya kumaliza shule. Ikiwa unaishi katika nchi ambako ni vigumu kupata kazi, huenda ukalazimika kufanya kazi yoyote inayopatikana. Ikiwa unaishi katika nchi tajiri, huenda kukawa na nafasi nyingi za kazi ambazo baadhi yake ni zenye kushawishi sana. Wakiwa na nia nzuri, walimu au wazazi wako wanaweza kukuhimiza ufuatie kazi yenye kutegemeka kifedha au hata ufuatie mali. Hata hivyo, huenda kujizoeza kwa ajili ya kazi hiyo kukapunguza sana wakati unaoweza kutumia kumtumikia Yehova.

16, 17. Eleza jinsi maandiko mbalimbali yanavyoweza kumsaidia kijana awe na maoni yenye usawaziko kuhusu kazi.

16 Kabla ya kufanya uamuzi, kumbuka kuchunguza Biblia. Biblia hututia moyo tufanye kazi ili kujipatia riziki, ikionyesha kwamba tuna daraka la kujitegemeza. (2 Wathesalonike 3:10-12) Hata hivyo, kuna mambo mengine yanayohusika. Tunakutia moyo usome maandiko yafuatayo na ufikirie jinsi yanavyoweza kumsaidia kijana awe na usawaziko katika kuchagua kazi: Methali 30:8, 9; Mhubiri 7:11, 12; Mathayo 6:33; 1 Wakorintho 7:31; 1 Timotheo 6:9, 10. Baada ya kusoma mistari hiyo, je, unaona Yehova ana maoni gani kuhusu jambo hilo?

17 Kazi haipaswi kamwe kuwa muhimu sana kuliko utumishi wetu kwa Yehova. Ikiwa cheti cha shule ya sekondari kinaweza kukusaidia kupata kazi inayofaa, ni vema. Ikiwa unahitaji mazoezi zaidi baada ya shule ya sekondari, unaweza kuzungumzia jambo hilo na wazazi wako. Hata hivyo, usisahau kamwe “mambo yaliyo ya maana zaidi,” yaani, mambo ya kiroho. (Wafilipi 1:9, 10) Usifanye kosa kama la Baruku, mwandishi wa Yeremia. Aliacha kuthamini pendeleo lake la utumishi na kuanza “kujitafutia makuu.” (Yeremia 45:5) Kwa muda fulani, alisahau kwamba hakuna ‘jambo kuu’ katika ulimwengu huu ambalo lingemsaidia kumkaribia Yehova au kuokoka uharibifu wa Yerusalemu. Tunaweza kujikuta katika hali kama hiyo leo.

Thamini Mambo ya Kiroho

18, 19. (a) Wengi wa majirani wako wanateseka kutokana na nini, nawe unapaswa uhisije kuwaelekea? (b) Kwa nini wengi hawahisi njaa ya kiroho?

18 Je, umeona picha katika vyombo vya habari za watoto katika nchi zenye njaa? Ikiwa umeziona, bila shaka uliwahurumia sana. Je, unawahurumia vivyo hivyo majirani wako? Kwa nini uwahurumie? Kwa sababu wengi wao wana njaa pia. Wanateseka kwa njaa iliyotabiriwa na Amosi: “‘Siku zinakuja,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘nami nitaleta njaa katika nchi, wala si njaa ya mkate, nami nitaleta kiu, wala si kiu ya maji, bali ya kuyasikia maneno ya Yehova.’”—Amosi 8:11.

19 Ni kweli kwamba wengi wa wale wanaoteseka kwa njaa ya kiroho ‘hawatambui uhitaji wao wa kiroho.’ (Mathayo 5:3) Wengi hawahisi njaa ya kiroho. Huenda wengine hata wakafikiri kwamba wanalishwa vizuri. Lakini ikiwa wanafikiri hivyo, hiyo ni kwa sababu wanalishwa “hekima ya ulimwengu” isiyofaa ambayo inatia ndani ufuatiaji wa vitu vya kimwili, udadisi wa kisayansi, maoni kuhusu maadili, na kadhalika. Wengine huhisi kwamba “hekima” hiyo ya kisasa hufanya mafundisho ya Biblia yaonekane kuwa ya kizamani. Hata hivyo, “ulimwengu kupitia hekima yake haukuja kumjua Mungu.” Hekima ya ulimwengu haitakusaidia kumkaribia Mungu. Hiyo ni “upumbavu kwa Mungu.”—1 Wakorintho 1:20, 21; 3:19.

20. Kwa nini si jambo la akili kutaka kuwaiga watu wasiomwabudu Yehova?

20 Unapotazama picha hizo za watoto wenye njaa, je, ungependa kwa vyovyote kuwa kama wao? La. Hata hivyo, vijana fulani katika familia za Kikristo wameonyesha tamaa ya kuwa kama watu wanaowazunguka ambao wana njaa ya kiroho. Yaelekea vijana hao wanafikiri kwamba vijana wa ulimwengu hawasumbuliwi na lolote, wanafurahia maisha. Wanasahau kwamba vijana hao wametengwa na Yehova. (Waefeso 4:17, 18) Wanasahau pia matokeo mabaya ya njaa ya kiroho. Matokeo hayo yanatia ndani mimba za matineja zisizotakiwa na madhara ya kimwili na kihisia yanayotokana na uasherati, kuvuta sigara, kunywa kupita kiasi, na kutumia dawa za kulevya. Njaa ya kiroho husababisha roho ya uasi, kukosa matumaini na mwongozo maishani.

21. Tunawezaje kujilinda tusifuate mitazamo mibaya ya watu wasiomwabudu Yehova?

21 Kwa hiyo, unapokuwa shuleni pamoja na vijana wengine ambao si waabudu wa Yehova, usishawishiwe kufuata mitazamo yao. (2 Wakorintho 4:18) Wengine watadharau mambo ya kiroho. Vyombo vya habari pia vitaeneza propaganda kwa ujanja, vikidokeza kwamba ni jambo la kawaida kufanya uasherati, kulewa au kutumia lugha chafu. Pinga ushawishi huo. Endelea kushirikiana kwa ukawaida na watu ambao ‘hushika imani na dhamiri njema,’ sikuzote ukiwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Timotheo 1:19; 1 Wakorintho 15:58) Uwe na mengi ya kufanya kwenye Jumba la Ufalme na katika utumishi wa shambani. Unapokuwa shuleni, fanya upainia msaidizi mara kwa mara. Imarisha hali yako ya kiroho kwa njia hiyo, nawe hutapoteza usawaziko.—2 Timotheo 4:5.

22, 23. (a) Kwa nini mara nyingi kijana Mkristo atafanya maamuzi ambayo wengine hawatayaelewa? (b) Vijana wanatiwa moyo kufanya nini?

22 Yaelekea kwamba kuona mambo kwa njia ya kiroho kutakusaidia kufanya maamuzi ambayo wengine hawatayaelewa. Kwa mfano, kijana mmoja Mkristo alikuwa na kipawa cha uimbaji naye alifanya vizuri sana katika kila somo shuleni. Alipomaliza shule, alijiunga na baba yake katika kazi ya kusafisha madirisha ili aweze kuwa mweneza-injili wa wakati wote au painia. Walimu hawakuelewa kamwe kwa nini alifanya uamuzi huo, lakini kama wewe umemkaribia Yehova, tuna hakika kwamba unaelewa.

23 Unapofikiria jinsi ya kutumia uwezo wako ukiwa kijana ‘jiwekee mwenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili uushike imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Timotheo 6:19) Azimia ‘kumkumbuka Muumba wako Mkuu’ ukiwa kijana na katika maisha yako yote. Hiyo ndiyo njia pekee ya kuwa na wakati ujao wenye mafanikio, ambao hautakoma.

Umefikia Mkataa Gani?

• Ni shauri gani lililoongozwa na roho ya Mungu ambalo huwasaidia vijana wanapojitayarisha kwa ajili ya wakati ujao?

• Kijana anaweza ‘kumkaribia Mungu’ katika njia zipi?

• Ni maamuzi gani ambayo kijana hufanya ambayo yataathiri wakati wake ujao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, utatumia nguvu na bidii yako yote ya ujana kufuatia mambo ya kibinafsi?

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Vijana Wakristo wenye hekima hudumisha uwezo wao wa kuona vizuri kiroho