Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mambo ya Walawi

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mambo ya Walawi

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mambo ya Walawi

BADO mwaka haujapita tangu Waisraeli wakombolewe kutoka utumwani Misri. Sasa wamepangwa kuwa taifa jipya, nao wako njiani kwenda Kanaani. Kusudi la Yehova ni kwamba taifa takatifu lipate kuishi katika nchi hiyo. Hata hivyo, maisha na mazoea ya kidini ya Wakanaani yamepotoka sana. Hivyo, Mungu wa kweli analipa kutaniko la Israeli masharti yanayowatenga kwa ajili ya utumishi wake. Masharti hayo yameandikwa katika kitabu cha Biblia cha Mambo ya Walawi. Kitabu hicho kilichoandikwa na nabii Musa katika nyika ya Sinai yapata mwaka wa 1512 K.W.K., kinazungumzia historia ya muda wa mwezi mmoja tu ya Waisraeli. (Kutoka 40:17; Hesabu 1:1-3) Yehova huwahimiza waabudu wake tena na tena wawe watakatifu.—Mambo ya Walawi 11:44; 19:2; 20:7, 26.

Leo Mashahidi wa Yehova hawako chini ya Sheria ambayo Mungu alitoa kupitia Musa. Kifo cha Yesu Kristo kilifutilia mbali Sheria hiyo. (Waroma 6:14; Waefeso 2:11-16) Hata hivyo, masharti yaliyo katika kitabu cha Mambo ya Walawi yanaweza kutunufaisha na kutufundisha mengi kuhusu ibada ya Mungu wetu Yehova.

MATOLEO MATAKATIFU—YA HIARI NA YA LAZIMA

(Mambo ya Walawi 1:1–7:38)

Baadhi ya dhabihu na matoleo yaliyotolewa kupatana na Sheria yalikuwa ya hiari, lakini mengine yalikuwa ya lazima. Kwa mfano, toleo la kuteketezwa lilikuwa la hiari, nalo lilitolewa kwa Mungu kwa kuteketeza sehemu zote, kama vile Yesu Kristo alivyotoa uhai wake kwa hiari kuwa dhabihu ya fidia. Toleo la hiari la ushirika lilishirikisha wengine. Sehemu moja ilitolewa kwa Mungu kwenye madhabahu, nyingine ikaliwa na kuhani, na bado nyingine ikaliwa na mwenye kutoa. Vivyo hivyo, kwa Wakristo watiwa-mafuta, Ukumbusho wa kifo cha Kristo ni mlo wa ushirika.—1 Wakorintho 10:16-22.

Matoleo ya dhambi na ya hatia yalikuwa ya lazima. Matoleo ya dhambi yalifanya upatanisho kwa ajili ya dhambi zilizotendwa kimakosa, au bila kukusudia. Nayo matoleo ya hatia yalimtuliza Mungu wakati mkosaji alipovunja haki ya mwingine, au kumrudishia mkosaji mwenye kutubu haki fulani—au mambo yote mawili. Pia kulikuwa na matoleo ya nafaka yaliyotolewa ili kumshukuru Yehova kwa maandalizi yake mengi. Mambo hayo yote yanatupendeza kwa sababu dhabibu zilizoamuriwa chini ya agano la Sheria zilielekeza kwa Yesu Kristo na dhabihu yake au kwenye faida za dhabihu hiyo.—Waebrania 8:3-6; 9:9-14; 10:5-10.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:11, 12—Kwa nini asali ‘ikiwa toleo linalotolewa kwa njia ya moto’ haikukubaliwa na Yehova? Asali inayozungumziwa hapa haikuwa ya nyuki. Asali hiyo haikuruhusiwa kutolewa ‘ikiwa toleo linalotolewa kwa njia ya moto,’ lakini ilitolewa pamoja na “mazao ya kwanza ya . . . shamba.” (2 Mambo ya Nyakati 31:5) Yaonekana asali hiyo ilikuwa maji au rojo ya matunda. Kwa kuwa ingeweza kuchacha, haingekubaliwa kutolewa kwenye madhabahu.

2:13—Kwa nini chumvi ilipaswa kutolewa “pamoja na kila toleo”? Hiyo haikufanywa ili kuboresha ladha ya dhabihu. Chumvi hutumiwa duniani kama kihifadhi. Yaelekea ilitolewa pamoja na matoleo kwa sababu inawakilisha kutoharibika au kutooza.

Mambo Tunayojifunza:

3:17. Kwa kuwa mafuta yalionwa kuwa sehemu iliyo bora zaidi, yaelekea Waisraeli walikatazwa wasiyale ili wapate kuelewa kwamba sehemu iliyo bora ilikuwa ya Yehova. (Mwanzo 45:18) Hiyo inatukumbusha kwamba ni lazima tumpe Yehova kilicho bora zaidi.—Methali 3:9, 10; Wakolosai 3:23, 24.

7:26, 27. Waisraeli hawakupaswa kula damu. Kwa maoni ya Mungu, damu huwakilisha uhai. “Kwa maana nafsi ya mwili iko katika damu,” lasema andiko la Mambo ya Walawi 17:11. Waabudu wa kweli bado wanatakiwa kujiepusha na damu.—Matendo 15:28, 29.

UKUHANI MTAKATIFU WAANZISHWA

(Mambo ya Walawi 8:1–10:20)

Ni nani waliopewa daraka la kushughulikia kazi zilizohusisha dhabihu na matoleo? Makuhani ndio waliopewa kazi hizo. Kama alivyoagizwa na Mungu, Musa aliongoza sherehe ya kumweka Haruni rasmi kuwa kuhani mkuu, na wanawe wanne kuwa makuhani wa cheo cha chini. Yaonekana sherehe hiyo ilichukua muda wa siku saba, nao makuhani hao wakaanza kufanya kazi siku iliyofuata.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

9:9—Ni nini maana ya kumimina damu kwenye msingi wa madhabahu na kuitia juu ya vitu mbalimbali? Hiyo ilionyesha kwamba Yehova alikubali damu kwa ajili ya upatanisho. Mpango mzima wa upatanisho ulitegemea damu. Mtume Paulo aliandika: “Karibu vitu vyote husafishwa kwa damu kulingana na Sheria, na damu isipomwagwa hakuna msamaha unaotokea.”—Waebrania 9:22.

10:1, 2—Huenda ikawa dhambi ya Nadabu na Abihu, wana wa Haruni, ilihusisha nini? Punde baada ya Nadabu na Abihu kutenda isivyofaa katika majukumu yao ya ukuhani, Yehova aliwakataza makuhani kunywa mvinyo au kileo wanapotumikia kwenye maskani. (Mambo ya Walawi 10:9) Hiyo inaonyesha kwamba huenda wana wawili wa Haruni walikuwa wamelewa katika pindi inayotajwa hapa. Hata hivyo, sababu hasa iliyofanya wafe ni kutoa “moto haramu, ambao [Yehova] hakuwa amewaamuru.”

Mambo Tunayojifunza:

10:1, 2. Leo lazima watumishi wa Yehova wenye madaraka wafuate viwango vya Mungu. Pia, hawapaswi kuwa na kimbelembele wanaposhughulikia madaraka yao.

10:9. Hatupaswi kufanya kazi tuliyopewa na Mungu tukiwa tumekunywa kileo.

IBADA TAKATIFU HUTAKA USAFI

(Mambo ya Walawi 11:1–15:33)

Masharti kuhusu wanyama safi na wasio safi yaliwanufaisha Waisraeli katika njia mbili. Yaliwakinga wasiambukizwe maradhi na vijidudu hatari, nayo yaliimarisha mpaka kati yao na mataifa yaliyowazunguka. Masharti mengine yalihusu uchafu uliotokana na mizoga, kutakaswa kwa wanawake baada ya kuzaa, hatua zilizopaswa kuchukuliwa kuhusiana na ukoma, na uchafu uliotokana na umajimaji unaotoka kwenye viungo vya uzazi vya wanaume na wanawake. Makuhani walipaswa kushughulikia watu ambao hawakuwa safi.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

12:2, 5—Kwa nini kuzaa kulimfanya mwanamke awe “asiye safi”? Viungo vya uzazi vilikusudiwa kupitisha uhai mkamilifu wa kibinadamu. Lakini, kwa sababu ya matokeo ya dhambi iliyorithiwa, uhai usio mkamilifu na wenye dhambi ulipitishwa kwa watoto. Vipindi vifupi vya ‘kutokuwa safi’ vilivyohusiana na kuzaa, na pia mambo mengine kama vile hedhi na kutokwa na shahawa, viliwakumbusha Waisraeli dhambi waliyorithi. (Mambo ya Walawi 15:16-24; Zaburi 51:5; Waroma 5:12) Masharti ya kutakaswa yaliyowekwa yangewasaidia Waisraeli waelewe kwa nini dhabihu ya fidia ilihitajiwa ili kufunika hali yenye dhambi ya mwanadamu na kumrudishia ukamilifu. Hivyo, Sheria ikawa ‘mtunzaji wao kuwaongoza kwa Kristo.’—Wagalatia 3:24.

15:16-18—‘Kutokwa na shahawa’ kunakotajwa katika mistari hii ni nini? Yaonekana kunarejelea kule kutokwa na shahawa usiku na pia wakati wa ngono kati ya mume na mke.

Mambo Tunayojifunza:

11:45. Yehova Mungu ni mtakatifu naye hutaka wale wanaomtolea utumishi mtakatifu wawe watakatifu pia. Lazima waendelee kuwa watakatifu, wakidumisha usafi wa kimwili na wa kiroho.—2 Wakorintho 7:1; 1 Petro 1:15, 16.

12:8. Yehova aliwaruhusu maskini watoe ndege kama toleo la dhambi badala ya kondoo aliyekuwa ghali zaidi. Yeye huwajali maskini.

LAZIMA UTAKATIFU UDUMISHWE

(Mambo ya Walawi 16:1–27:34)

Dhabihu muhimu zaidi kwa ajili ya dhambi zilitolewa kila mwaka katika Siku ya Upatanisho. Ng’ombe-dume alitolewa kwa ajili ya makuhani na kabila la Lawi. Mbuzi alitolewa kwa ajili ya makabila ya Israeli ambayo hayakuwa makuhani. Mbuzi mwingine alipelekwa nyikani akiwa hai baada ya dhambi za watu kutangazwa juu yake. Mbuzi hao wawili walihesabiwa kuwa toleo moja la dhambi. Hayo yote yalionyesha kwamba Yesu Kristo angetolewa akiwa dhabihu na pia angechukua dhambi za watu.

Masharti kuhusu kula nyama na kuhusu mambo mengine hukazia uhitaji wa kuwa watakatifu tunapomwabudu Yehova. Kwa kufaa, makuhani walipaswa kuendelea kuwa watakatifu. Sherehe tatu zilizofanywa kila mwaka zilikuwa pindi za kushangilia na kumshukuru Muumba. Yehova pia aliwapa watu masharti kuhusu kutumia vibaya jina lake takatifu, kushika Sabato na Yubile, na jinsi ya kuwatendea maskini na watumwa. Baraka ambazo zingetokana na kumtii Mungu zinatofautishwa na laana ambazo zingetokana na kutotii. Pia kuna masharti juu ya matoleo yaliyohusiana na nadhiri na makadirio, mzaliwa wa kwanza wa wanyama, na kutolewa kwa fungu la kumi kama ‘kitu kitakatifu kwa Yehova.’

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

16:29—Ni katika njia gani Waisraeli ‘wangezitesa nafsi zao’? Hatua hiyo, iliyofuata Siku ya Upatanisho, inahusiana na kutafuta msamaha wa dhambi. Yaonekana kufunga wakati huo kulihusianishwa na kukubali kwamba wao ni wenye dhambi. Hivyo, yaelekea ‘kutesa nafsi’ kulimaanisha kufunga.

19:27—Ni nini kinachomaanishwa na amri ya ‘kutokata ndevu ziwe fupi kuzunguka pande zote,’ au ‘kuharibu ncha’ ya ndevu? Yaonekana sheria hiyo ilitolewa kuwazuia Wayahudi wasikate ndevu au nywele kwa kuiga mazoea fulani ya wapagani. (Yeremia 9:25, 26; 25:23; 49:32) Hata hivyo, amri ya Mungu haikumaanisha kwamba Wayahudi hawangeweza kukata hata kidogo ndevu au nywele za uso.—2 Samweli 19:24.

25:35-37—Je, sikuzote ilikuwa makosa kwa Waisraeli kutoza riba? Ikiwa pesa zilikopeshwa kwa sababu za kibiashara, mkopeshaji angezitoza riba. Hata hivyo, Sheria ilikataza kuitoza riba mikopo iliyotolewa kusaidia maskini. Ilikuwa kosa kujifaidi kutokana na matatizo ya kiuchumi ya jirani yako.—Kutoka 22:25.

26:19—‘Mbingu zinawezaje kuwa kama chuma na nchi kama shaba’? Kwa sababu ya ukosefu wa mvua, mbingu zilizotanda juu ya nchi ya Kanaani zingefanana na chuma kigumu kisichopenya maji. Bila mvua, rangi ya nchi ingekuwa kama ya shaba yenye kumetameta.

26:26—Ni nini kinachomaanishwa na ‘wanawake kumi kuoka mkate katika jiko moja’? Kwa kawaida, kila mwanamke angehitaji jiko tofauti kwa ajili ya uokaji wake wote. Lakini maneno hayo yanaonyesha kungekuwa na uhaba mkubwa wa chakula hivi kwamba wanawake kumi wangetumia jiko moja tu kuokea. Hilo ni mojawapo ya matokeo yaliyotabiriwa ya kushindwa kudumisha utakatifu.

Mambo Tunayojifunza:

20:9. Roho ya chuki na ya ukatili ilikuwa sawa na mauaji machoni pa Yehova. Kwa hiyo, aliamuru kuwe na adhabu moja kwa yule anayewalaani wazazi wake au kuwaua. Hilo linapaswa kutuchochea tuwapende waamini wenzetu.—1 Yohana 3:14, 15.

22:32; 24:10-16, 23. Jina la Yehova halipaswi kudhihakiwa. Badala yake, tunapaswa kulitukuza na kusali ili litakaswe.—Zaburi 7:17; Mathayo 6:9.

JINSI KITABU CHA WALAWI KINAVYOATHIRI IBADA YETU

Leo Mashahidi wa Yehova hawako chini ya Sheria. (Wagalatia 3:23-25) Yale yanayosemwa katika kitabu cha Mambo ya Walawi hutusaidia kuelewa maoni ya Yehova kuhusu mambo mbalimbali, na pia yanaweza kuathiri ibada yetu.

Unapofanya usomaji wa Biblia wa kila juma ili kujitayarisha kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, bila shaka utavutiwa na uhakika wa kwamba Mungu wetu hutaka watumishi wake wawe watakatifu. Kitabu hiki cha Biblia kinaweza pia kukuchochea umtolee Aliye Juu Zaidi kilicho bora zaidi, sikuzote ukidumisha utakatifu na hivyo kumtukuza.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Dhabihu zilizotolewa chini ya Sheria zilielekeza kwa Yesu Kristo na dhabihu yake

[Picha katika ukurasa wa 22]

Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu ilikuwa tukio lenye shangwe sana

[Picha katika ukurasa wa 23]

Sherehe zilizofanywa kila mwaka, kama vile Sherehe ya Vibanda, zilikuwa pindi za kumshukuru Yehova