Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Tunawezaje kuihuzunisha roho takatifu ya Mungu, kwa kuwa hiyo si mtu?

Mtume Paulo ndiye aliyeandika: “Msiwe mkiihuzunisha roho takatifu ya Mungu.” (Waefeso 4:30) Watu wengine hufikiri kuwa maneno hayo yanamaanisha kwamba roho takatifu ni mtu. Hata hivyo, mara nyingi vichapo vya “msimamizi-nyumba mwaminifu” vimethibitisha Kimaandiko na kihistoria kwamba Wakristo wa mapema hawakuiona roho takatifu kuwa mtu wala mungu aliye sawa na yule Mungu Aliye Juu zaidi, wala hawakuiona kuwa sehemu ya ule uitwao Utatu. * (Luka 12:42) Hivyo, Paulo hakuwa akirejelea roho takatifu ya Mungu kuwa mtu.

Roho takatifu ya Mungu ni nguvu yake ya utendaji isiyoonekana. (Mwanzo 1:2) Yesu alipaswa kubatiza “kwa roho takatifu,” kama vile Yohana alivyobatiza kwa maji. (Luka 3:16) Wakati wa Pentekoste 33 W.K. wanafunzi 120 hivi ‘walijazwa roho takatifu’—hawakujazwa mtu. (Matendo 1:5, 8; 2:4, 33) Wanafunzi hao waliotiwa mafuta walipokea tumaini la kuishi mbinguni, nayo roho ya Mungu ikawaongoza kuishi maisha ya uaminifu. (Waroma 8:14-17; 2 Wakorintho 1:22) Roho hiyo ilitokeza matunda ya kimungu na kuwasaidia kuepuka “matendo ya mwili” yanayoweza kuwafanya wakataliwe na Mungu.—Wagalatia 5:19-25.

Ikiwa sisi ni watumishi wa Mungu wenye tumaini la kuishi duniani, hatujatiwa mafuta kwa roho takatifu. Hata hivyo, tunaweza kuwa na kiasi kilekile cha roho takatifu kama wale walio na tumaini la kuishi mbinguni. Hivyo, sisi pia tunaweza kuihuzunisha roho ya Mungu. Jinsi gani?

Kama tungepuuza shauri la Kimaandiko lililoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu, tungekuwa na tabia ambazo zingefanya tutende dhambi kimakusudi dhidi ya roho, tupoteze kibali cha Yehova, na mwishowe kuharibiwa. (Mathayo 12:31, 32) Huenda tukawa hatufanyi dhambi nzito, lakini tunaweza kuwa na tabia ambazo mwishowe zingefanya tutende kinyume na mwelekezo wa roho hiyo. Chini ya hali kama hizo tungekuwa tukiihuzunisha roho takatifu.

Basi, tunawezaje kuepuka kuihuzunisha roho ya Mungu? Bila shaka, ni lazima tudhibiti mawazo na matendo yetu. Katika barua yake kwa Waefeso, sura ya 4, mtume Paulo alizungumza kuhusu kuepuka maelekeo ya kusema uwongo, kuwa na kinyongo, uzembe, na usemi usiofaa. Iwapo ‘tumevaa utu mpya’ na bado turudie mazoea hayo mabaya, tungekuwa tunafanya nini? Tungekuwa tunapinga shauri la Neno la Mungu, Biblia, lililoongozwa na roho yake. Kwa kufanya hivyo tungekuwa tunaihuzunisha roho takatifu.

Katika Waefeso sura ya 5, tunasoma shauri la Paulo kuhusu kuepuka kuvutiwa na mambo ya uasherati, mwenendo wa aibu, na mizaha michafu. Ikiwa hatutaki kuihuzunisha roho takatifu ya Mungu, lazima tukumbuke mambo hayo tunapochagua vitumbuizo. Hatupaswi kuonyesha kwamba tunavutiwa na mambo hayo kwa kuyazungumzia, kuyasoma, kuyatazama kwenye televisheni, au mahali penginepo.

Bila shaka, tunaweza kuihuzunisha roho kwa njia mbalimbali. Roho ya Yehova husaidia kuwe na umoja kutanikoni, lakini je, hatungekuwa tukipinga mwongozo wa roho kuhusu umoja kama tungeeneza porojo mbaya au kuchochea watu wajitenge katika vikundi-vikundi kutanikoni? Kwa jumla, tungekuwa tukiihuzunisha roho takatifu, kama wale waliosababisha migawanyiko katika kutaniko la Korintho. (1 Wakorintho 1:10; 3:1-4, 16, 17) Tungekuwa pia tunaihuzunisha roho kama tungewavunjia heshima kimakusudi wanaume waliowekwa rasmi kwa roho kutanikoni.—Matendo 20:28; Yuda 8.

Basi, ni wazi kwamba ni jambo la hekima kufikiria mtazamo na matendo yetu kupatana na ule tunaojua kuwa mwongozo wa roho takatifu kama unavyoonyeshwa katika Biblia na kutaniko la Kikristo. Acheni pia tuwe ‘tukisali tukiwa na roho takatifu,’ huku tukikubali mwongozo wake na sikuzote kutenda kupatana na Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (Yuda 20) Na tuazimie kabisa kutoihuzunisha roho, bali ituongoze sikuzote kwa utukufu wa jina takatifu la Yehova.

Yesu Kristo alisema ni vigumu kwa tajiri kuingia katika Ufalme kama vile ilivyo vigumu kwa ngamia kupita katika tundu la sindano. Je, Yesu alikuwa anarejelea ngamia na sindano halisi?

Maandiko mawili kati ya matatu yanayozungumzia jambo hilo yanafanana. Kulingana na masimulizi ya Mathayo, Yesu alisema: “Ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Mathayo 19:24) Pia, andiko la Marko 10:25 linasema: “Ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.”

Vitabu fulani vya marejeo vinasema kwamba “tundu la sindano” lilikuwa lango dogo kwenye mojawapo ya malango makubwa ya Yerusalemu. Lango kubwa lilipofungwa usiku, lile dogo lilifunguliwa. Inaaminika kwamba ngamia angeweza kupitia lango hilo dogo. Je, Yesu alikuwa anarejelea lango hilo?

Yaonekana hakuwa anarejelea lango hilo. Yaelekea Yesu alikuwa anarejelea sindano ya kushona. Kwa kuwa sindano za zamani za mifupa na chuma zimepatikana katika eneo hilo, bila shaka zilitumiwa sana nyumbani wakati huo. Andiko la Luka 18:25 linaondoa shaka yoyote kuhusu maneno ya Yesu, kwa kuwa linamnukuu kuwa alisema: “Kwa kweli, ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano ya kushonea kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.”

Watungaji kadhaa wa kamusi hukubaliana na tafsiri “sindano ya kushonea” kama ilivyo katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Neno la Kigiriki (rha·phisʹ) linalotafsiriwa kuwa ‘sindano’ kwenye Mathayo 19:24 na Marko 10:25, linatokana na kitenzi kinachomaanisha “shona.” Nalo neno la Kigiriki (be·loʹne) kwenye Luka 18:25, linatumiwa kurejelea sindano halisi inayotumiwa katika upasuaji. Kichapo Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words kinasema: “Wazo kwamba ‘tundu la sindano’ linarejelea malango madogo ni la karibuni; hakuna uthibitisho unaoonyesha kwamba ‘tundu la sindano’ lilitumiwa katika maana hiyo. Lengo la Bwana katika maneno hayo ni kuonyesha jinsi ilivyo vigumu kwa tajiri kuingia katika Ufalme, na hakuna haja ya kuonyesha kwamba jambo hilo ni rahisi kwa kusema hiyo si sindano halisi.”—1981, Buku la 3, ukurasa wa 106.

Wengine hudokeza kwamba katika mistari hiyo, neno “ngamia” linapaswa kutafsiriwa “kamba.” Neno la Kigiriki (kaʹmi·los) linalotafsiriwa kuwa kamba linafanana na neno (kaʹme·los) linalotafsiriwa kuwa ngamia. Hata hivyo, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ngamia,” wala si lile linalotafsiriwa “kamba,” ndilo limetumiwa kwenye Mathayo 19:24 katika maandishi ya zamani ya Kigiriki ya Injili ya Mathayo yaliyopo leo (Maandishi ya Biblia ya Sinaitic, Vatican Na. 1209, na ya Alexandrine). Yasemekana kwamba mwanzoni Mathayo aliandika Injili yake katika Kiebrania na huenda yeye mwenyewe aliitafsiri katika Kigiriki. Alijua hasa yale Yesu aliyosema, hivyo akatumia neno lifaalo.

Hivyo basi, Yesu alimaanisha sindano na ngamia halisi. Alitumia mifano hiyo ili kukazia jambo fulani lisilowezekana. Lakini, je, Yesu alimaanisha kwamba hakuna tajiri anayeweza kwa vyovyote kuingia katika Ufalme? La, kwa kuwa maneno ya Yesu hayakupaswa kuchukuliwa kihalisi. Yesu alitumia usemi uliotiwa chumvi ili kuonyesha kwamba kama vile ngamia halisi asivyoweza kupita katika tundu la sindano halisi, ndivyo tajiri asivyoweza kupita katika Ufalme ikiwa ataendelea kushikamana na mali zake na kutotanguliza Yehova maishani mwake.—Luka 13:24; 1 Timotheo 6:17-19.

Yesu alitamka maneno hayo punde baada ya mtawala mmoja kijana, aliyekuwa tajiri, kukataa pendeleo tukufu la kuwa mfuasi wake. (Luka 18:18-24) Mtu tajiri anayependa mali zake zaidi ya mambo ya kiroho hawezi kutarajia kupata uzima wa milele katika mpango wa Ufalme. Hata hivyo, matajiri fulani walipata kuwa wanafunzi wa Yesu. (Mathayo 27:57; Luka 19:2, 9) Hivyo, tajiri ambaye anatambua uhitaji wake wa kiroho na anayetafuta msaada wa Mungu anaweza kupata wokovu kutoka kwa Mungu.—Mathayo 5:3; 19:16-26.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona broshua Je! Uamini Utatu? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.