Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Daraka la Kikristo Kuwatunza Walio Wazee

Ni Daraka la Kikristo Kuwatunza Walio Wazee

Ni Daraka la Kikristo Kuwatunza Walio Wazee

“Hata uzeeni mwa mtu mimi ni Yeye yuleyule; na hata wakati wa kichwa chenye mvi cha mtu nitaendelea kubeba.”—ISAYA 46:4.

1, 2. Utunzaji wa Baba yetu wa mbinguni unatofautianaje na ule wa wazazi wa kibinadamu?

WAZAZI wenye kujitoa huwalea watoto tangu utoto hadi miaka yao ya utineja. Hata vijana wanapokuwa watu wazima na kuwa na familia zao, baba na mama zao huendelea kuwatunza na kuwategemeza kwa upendo.

2 Ingawa kuna mipaka kuhusiana na yale ambayo wanadamu wanaweza kuwafanyia watoto wao, sikuzote Baba yetu wa mbinguni anaweza kuwatunza na kuwategemeza kwa upendo watumishi wake. Akizungumza na watu wake wa kale, Yehova alisema: “Hata uzeeni mwa mtu mimi ni Yeye yuleyule; na hata wakati wa kichwa chenye mvi cha mtu nitaendelea kubeba.” (Isaya 46:4) Maneno hayo huwatia moyo sana Wakristo walio wazee. Yehova hawaachi wale wanaoendelea kuwa washikamanifu kwake. Badala yake, yeye anaahidi kuwategemeza, kuwasaidia, na kuwaongoza maishani mwao, hata uzeeni.—Zaburi 48:14.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Tunawezaje kuiga jinsi Yehova anavyowatunza kwa upendo walio wazee? (Waefeso 5:1, 2) Na tuchunguze njia ambazo vijana, wazee wa kutaniko, na Wakristo mmoja-mmoja wanavyoweza kushughulikia mahitaji ya washiriki walio wazee katika undugu wetu wa ulimwenguni pote.

Daraka Letu Tukiwa Watoto

4. Watoto Wakristo wana daraka gani kuelekea wazazi wao?

4 “Mheshimu baba yako na mama yako.” (Waefeso 6:2; Kutoka 20:12) Mtume Paulo alitumia andiko hilo rahisi lakini muhimu ambalo limenukuliwa kutoka katika Maandiko ya Kiebrania, ili kuwakumbusha watoto daraka lao kwa wazazi wao. Lakini maneno hayo yanahusianaje na kuwatunza walio wazee? Ili kujibu swali hilo acheni tufikirie kielelezo chenye kuchangamsha moyo cha kabla ya Ukristo.

5. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yosefu hakuwa amesahau madaraka yake kuelekea wazazi? (b) Inamaanisha nini kuwaheshimu wazazi wetu, naye Yosefu aliweka kielelezo gani kizuri kuhusiana na hilo?

5 Kwa miaka zaidi ya 20, Yosefu hakuwasiliana na Yakobo, babake mzee aliyekuwa mzee wa ukoo. Hata hivyo, ni wazi kwamba bado Yosefu alimpenda babake Yakobo. Kwa kweli, Yosefu alipojitambulisha kwa ndugu zake, aliuliza: “Je, baba yangu angali hai?” (Mwanzo 43:7, 27; 45:3) Wakati huo, nchi ya Kanaani iliathiriwa na njaa kali. Hivyo, Yosefu alituma ujumbe kwa babake, na kusema: “Njoo kwangu. Usikawie. Ukae katika nchi ya Gosheni, uishi karibu nami . . . Nami nitakupa chakula huko.” (Mwanzo 45:9-11; 47:12) Naam, kuwaheshimu wazazi waliozeeka hutia ndani kuwalinda na kuwaandalia mahitaji ya kimwili ikiwa hawawezi kufanya hivyo. (1 Samweli 22:1-4; Yohana 19:25-27) Yosefu alikubali kwa furaha daraka hilo.

6. Yosefu alionyeshaje upendo wa kweli kwa babake, nasi tunawezaje kuiga kielelezo chake?

6 Yosefu alisaidiwa na Yehova kuwa mmoja wa watu tajiri na wenye uwezo mkubwa zaidi nchini Misri. (Mwanzo 41:40) Lakini hakujiona kuwa mtu wa maana sana au mwenye shughuli nyingi sana asiweze kumheshimu babake mwenye umri wa miaka 130. Alipojua kwamba Yakobo (au Israeli) alikuwa anakaribia, ‘Yosefu alitayarisha gari lake, akaenda kumpokea babake Israeli huko Gosheni. Alipomtokea, alimwangukia shingoni mara moja, akalia shingoni pake tena na tena.’ (Mwanzo 46:28, 29) Makaribisho hayo hayakuwa wonyesho wa heshima wa kidesturi tu. Yosefu alimpenda sana babake mzee na hakuaibika kumwonyesha upendo. Ikiwa tuna wazazi wazee, je, sisi pia huwaonyesha upendo mwingi?

7. Kwa nini Yakobo alitaka akazikwe Kanaani?

7 Yakobo aliendelea kujitoa kwa Yehova hadi kifo chake. (Waebrania 11:21) Kwa kuwa aliamini ahadi za Mungu, Yakobo aliomba mwili wake ukazikwe Kanaani. Yosefu alimheshimu babake kwa kukubali ombi lake licha ya gharama na jitihada kubwa zilizohusika.—Mwanzo 47:29-31; 50:7-14.

8. (a) Ni nini hasa hutuchochea kuwatunza wazazi wetu wazee? (b) Mtumishi mmoja wa wakati wote alifanya nini ili kuwatunza wazazi wake wazee? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 17.)

8 Ni nini kilichomchochea Yosefu amtunze babake? Ni tamaa yake kubwa ya kumpendeza Yehova na pia upendo na hisia kwamba alikuwa na deni kwa babake kwa sababu ya kumzaa na kumlea. Tunapaswa kuwa na tamaa hiyohiyo. Paulo aliandika: “Ikiwa mjane yeyote ana watoto au wajukuu, acha hao wajifunze kwanza kuzoea ujitoaji-kimungu nyumbani kwao wenyewe na kuendelea kuwalipa wazazi na wazazi wa wazazi wao malipo yanayowastahili, kwa maana hilo linakubalika machoni pa Mungu.” (1 Timotheo 5:4) Naam, kumpenda Yehova na woga wenye heshima kwake utatuchochea kuwatunza wazazi wetu wazee, bila kujali magumu yanayohusika katika kufanya hivyo. *

Jinsi Ambavyo Wazee Huonyesha Kwamba Wanajali

9. Ni nani ambao Yehova ameweka rasmi ili kulichunga kundi, kutia ndani Wakristo walio wazee?

9 Alipokaribia kufa baada ya kuishi kwa muda mrefu, Yakobo alimrejelea Yehova kuwa “Mungu wa kweli ambaye amekuwa akinichunga maisha yangu yote mpaka leo hii.” (Mwanzo 48:15) Leo, Yehova huwachunga watumishi wake duniani kupitia waangalizi au wazee Wakristo, chini ya uongozi wa Mwanawe Yesu Kristo aliye “mchungaji mkuu.” (1 Petro 5:2-4) Waangalizi wanawezaje kumwiga Yehova wanapowatunza washiriki wa kundi walio wazee?

10. Ni nini ambacho kimefanywa ili kuwasaidia kimwili Wakristo walio wazee? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 19.)

10 Muda mfupi baada ya kutaniko la Kikristo kuanzishwa, mitume waliwaweka rasmi “wanaume saba waliothibitishwa . . . wenye kujaa roho na hekima” ili kusimamia “ugawaji wa kila siku” wa chakula kati ya wajane Wakristo wenye uhitaji. (Matendo 6:1-6) Baadaye, Paulo alimwagiza mwangalizi Timotheo awatie wajane wazee wenye mfano mzuri kwenye orodha ya wale ambao walistahili kupokea msaada wa kimwili. (1 Timotheo 5:3, 9, 10) Leo pia, waangalizi wa kutaniko hupanga na kusimamia kwa hiari msaada unaotolewa kwa ajili ya Wakristo walio wazee inapohitajika. Hata hivyo, mengi zaidi yanahitajiwa katika kuwatunza wazee walio waaminifu.

11. Yesu alisema nini kuhusu mjane maskini aliyetoa mchango mdogo?

11 Alipokaribia kumaliza huduma yake duniani, Yesu aliketi hekaluni na “kuanza kuangalia jinsi umati ulivyokuwa ukitumbukiza pesa ndani ya masanduku.” Ndipo akavutiwa na mtu fulani. Masimulizi hayo yanasema: “Mjane fulani maskini akaja, akatumbukiza ndani sarafu mbili ndogo, zenye thamani ndogo sana.” Yesu aliwaita wanafunzi wake na kuwaambia: “Kwa kweli ninawaambia kwamba mjane huyu maskini ametumbukiza nyingi kuliko wote waliokuwa wakitumbukiza pesa ndani ya masanduku ya hazina; kwa sababu wote walitumbukiza ndani kutokana na ziada yao, lakini yeye, kutokana na uhitaji wake, alitumbukiza ndani vyote alivyokuwa navyo, riziki yake yote.” (Marko 12:41-44) Mjane huyo alitoa mchango wenye thamani ndogo, lakini Yesu alijua jinsi Babake wa mbinguni anavyothamini ujitoaji kama huo wa nafsi yote. Yesu hakupuuza jambo ambalo mjane huyo maskini alifanya licha ya umri wake.

12. Wazee wanaweza kuonyeshaje uthamini kwa yale yanayofanywa na Wakristo walio wazee?

12 Kama Yesu, waangalizi Wakristo hawapuuzi yale ambayo wazee wanaweza kufanya ili kuendeleza ibada ya kweli. Wazee wanapaswa kuwapongeza walio wazee kwa yale wanayofanya katika huduma, kwa kushiriki katika mikutano, kwa uvutano wao wenye kujenga kutanikoni, na kwa uvumilivu wao. Neno lenye kutia moyo linalotoka moyoni, linaweza kuwasaidia walio wazee wapate “sababu ya kufurahi” katika utumishi wao mtakatifu, na hivyo kuepuka kuvunjika moyo kwa kujilinganisha na Wakristo wengine au kulinganisha yale wanayoweza kutimiza sasa na yale waliyotimiza zamani.—Wagalatia 6:4.

13. Wazee wanaweza kutumiaje uwezo na ujuzi mbalimbali wa walio wazee?

13 Wazee wanaweza kuonyesha uthamini kwa msaada wenye thamani wa Wakristo walio wazee kwa kutumia ujuzi na uwezo mbalimbali wa Wakristo hao. Pindi kwa pindi, Wakristo walio wazee wenye mfano mzuri wanaweza kutumiwa katika maonyesho au mahojiano. Mzee mmoja anasema, “Wasikilizaji husikiliza kwa makini ninapomhoji ndugu au dada mzee ambaye amewalea watoto wake katika kweli.” Wazee katika kutaniko lingine wanasema kwamba dada mmoja painia mwenye umri wa miaka 71 amefanikiwa kuwasaidia wahubiri wa Ufalme kuwa wa kawaida katika utumishi wa shambani. Yeye pia huwatia moyo wafanye “mambo ya msingi,” kama vile kusoma Biblia na andiko la siku, kisha kutafakari wanayosoma.

14. Baraza moja la wazee lilionyeshaje uthamini kwa mwangalizi mwenzao mwenye umri mkubwa?

14 Wazee pia huthamini msaada kutoka kwa waangalizi wenzao wenye umri mkubwa. Hivi karibuni, José, mwenye umri wa miaka 70 na kitu na ambaye amekuwa mzee kwa miaka mingi, alifanyiwa upasuaji mkubwa. Kwa kuwa ingemchukua muda mrefu kupona, alifikiria kuacha pendeleo la kutumikia akiwa mwangalizi-msimamizi. “Itikio la wazee wengine lilinishangaza,” asema José. “Badala ya kukubali pendekezo langu, waliniuliza nilihitaji msaada gani ili kuendelea na madaraka yangu.” Kwa msaada wa mzee mmoja kijana, José aliendelea kutumikia kwa furaha akiwa mwangalizi-msimamizi, na hilo limelinufaisha kutaniko. Mzee mwenzake anasema: “Kutaniko linathamini sana kazi ambayo José anafanya akiwa mzee. Wanampenda na kumheshimu kwa sababu ya ujuzi na kielelezo chake katika imani. Yeye analinufaisha kutaniko letu.”

Kutunzana

15. Kwa nini Wakristo wote wanapaswa kuhangaikia hali njema ya walio wazee kati yao?

15 Si watoto walio na wazazi wazee na watumishi waliowekwa rasmi tu wanaopaswa kuwahangaikia walio wazee. Akilinganisha kutaniko la Kikristo na mwili wa binadamu, Paulo aliandika: “Mungu aliuungamanisha mwili, akiipa heshima iliyo nyingi zaidi sehemu iliyokuwa na upungufu, ili kusiwe na mgawanyiko katika mwili, bali ili viungo vyake vitunzane kwa njia ileile.” (1 Wakorintho 12:24, 25) Ili kutaniko la Kikristo lifanye kazi kwa upatano, kila mshiriki anapaswa kuhangaikia hali njema ya waamini wenzake, kutia ndani walio wazee.—Wagalatia 6:2.

16. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunawahangaikia walio wazee tunapohudhuria mikutano ya Kikristo?

16 Mikutano ya Kikristo hutupa nafasi nzuri ya kuonyesha hangaiko letu kwa walio wazee. (Wafilipi 2:4; Waebrania 10:24, 25) Je, sisi huzungumza nao kwenye mikutano? Ingawa huenda ikafaa kuwajulia hali, je, tunaweza ‘kuwapa sehemu ya zawadi ya kiroho,’ labda kwa kuwaeleza jambo fulani lenye kujenga lililoonwa au wazo fulani la Biblia? Kwa kuwa baadhi ya walio wazee hawawezi kutembea kwa urahisi, lingekuwa jambo la fadhili kwenda mahali walipo badala ya kutarajia wao waje. Ikiwa wana tatizo la kusikia, huenda tukahitaji kuzungumza polepole na kutamka maneno waziwazi. Ili kuwa na “ubadilishanaji wa kitia-moyo” wa kweli, tunapaswa kusikiliza kwa makini yale ambayo mtu aliye mzee anasema.—Waroma 1:11, 12.

17. Tunawezaje kuonyesha tunawajali Wakristo walio wazee ambao hawawezi kutoka nyumbani?

17 Namna gani ikiwa baadhi ya walio wazee hawawezi kuhudhuria mikutano ya Kikristo? Andiko la Yakobo 1:27 linaonyesha kwamba tuna daraka la “kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao.” Maana moja ya kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa ‘kutunza’ ni “kutembelea.” (Matendo 15:36) Walio wazee huthamini kama nini tunapowatembelea! Alipokuwa gerezani huko Roma, yapata mwaka wa 65 W.K., “mwanamume mzee” Paulo alijikuta peke yake. Alitamani sana kumwona Timotheo, mfanyakazi mwenzake, naye akaandika: “Fanya kabisa yote unayoweza ili uje kwangu upesi.” (Filemoni 9; 2 Timotheo 1:3, 4; 4:9) Ingawa wao si wafungwa, baadhi ya walio wazee hawawezi kutoka nyumbani kwa sababu ya matatizo ya afya. Kwa kweli, huenda wakawa wanasema, ‘Tafadhali jitahidi uwezavyo kunitembelea karibuni.’ Je, tunaitikia miito hiyo?

18. Unaweza kupata manufaa gani kwa kuwatembelea walio wazee?

18 Usipuuze manufaa ya kumtembelea ndugu au dada wa kiroho aliye mzee. Mkristo aitwaye Onesiforo alipokuwa Roma, alimtafuta Paulo kwa bidii, akampata, na baadaye ‘akamletea kiburudisho mara nyingi.’ (2 Timotheo 1:16, 17) “Mimi napenda kutumia wakati pamoja na vijana,” asema dada mmoja aliye mzee. “Jambo ambalo hunipendeza zaidi ni kwamba wao hunitendea kama mshiriki wa familia yao. Hilo hunitia moyo sana.” Mkristo mwingine aliye mzee anasema: “Mimi huthamini sana mtu anaponitumia kadi, kunipigia simu kwa dakika chache, au kunitembelea kwa muda mfupi. Hiyo inaburudisha sana.”

Yehova Huwathawabisha Wale Wanaojali

19. Ni baraka gani zinazotokana na kuwatunza walio wazee?

19 Kuna baraka nyingi zinazotokana na kuwatunza walio wazee. Ni pendeleo kushirikiana na walio wazee na kutumia ujuzi na uzoefu wao. Wale ambao huwatunza wengine hupata furaha kubwa inayotokana na kutoa, na mbali na kuhisi kwamba wametimiza jambo fulani, wao pia hupata amani ya akili inayotokana na kutimiza daraka lao la Kimaandiko. (Matendo 20:35) Isitoshe, wale wanaowatunza walio wazee hawapaswi kuogopa kwamba wao wenyewe hawatatunzwa watakapokuwa wazee. Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Nafsi yenye ukarimu hiyo yenyewe itanoneshwa, naye anayenywesha wengine kwa ukarimu yeye mwenyewe pia atanyweshwa kwa ukarimu.”—Methali 11:25.

20, 21. Yehova huwaonaje wale wanaowatunza walio wazee, nasi tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Yehova huwathawabisha watoto, waangalizi, na Wakristo wengine wenye kumwogopa ambao hushughulikia bila ubinafsi mahitaji ya waamini wenzao walio wazee. Roho hiyo inapatana na methali hii: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” (Methali 19:17) Tukichochewa na upendo kuwaonyesha maskini kibali na watu wa hali ya chini, Mungu huona kama tunamkopesha naye hulipa kwa kutubariki. Yeye pia hutulipa kwa kuwatunza kwa upendo waabudu wenzetu walio wazee, ambao wengi wao ni ‘maskini kwa habari ya ulimwengu lakini matajiri katika imani.’—Yakobo 2:5.

21 Mungu hutulipa kwa ukarimu kama nini! Malipo yake hutia ndani uzima wa milele. Kwa walio wengi kati ya watumishi wa Yehova, malipo hayo yatakuwa uzima wa milele katika dunia paradiso, ambako madhara ya dhambi tuliyorithi yataondolewa, nao walio wazee ambao ni waaminifu watafurahi kurudishiwa nguvu zao za ujana. (Ufunuo 21:3-5) Tunapongojea wakati huo wenye baraka, na tuendelee kutimiza daraka letu la Kikristo la kuwatunza walio wazee.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ili kupata madokezo yafaayo kuhusu jinsi ya kuwatunza wazazi wazee, ona Amkeni!, Februari 8, 1994, ukurasa wa 3-10.

Unajibuje?

• Watoto wanawezaje kuwaheshimu wazazi wao walio wazee?

• Wazee huonyeshaje uthamini kwa washiriki wa kundi walio wazee?

• Wakristo mmoja-mmoja wanaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba wanawahangaikia kikweli walio wazee?

• Ni baraka gani zinazotokana na kuwatunza Wakristo walio wazee?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

Wazazi Wake Walipohitaji Msaada

Philip alikuwa mjenzi wa kujitolea huko Liberia mwaka wa 1999 wakati alipopata habari kwamba babake alikuwa mgonjwa sana. Akiwa na uhakika kwamba mamake hangeweza kushughulikia hali hiyo akiwa peke yake, aliamua kurudi nyumbani ili kufanya mipango ya matibabu kwa ajili ya babake.

“Haikuwa rahisi kurudi nyumbani,” akumbuka Philip, “lakini nilihisi kwamba daraka langu la kwanza ni kwa wazazi wangu.” Katika miaka mitatu iliyofuata, aliwahamisha wazazi wake kwenda katika nyumba nzuri zaidi na kwa msaada wa Wakristo wenzake, alirekebisha nyumba hiyo ili ifae kwa mahitaji ya pekee ya babake.

Sasa mama ya Philip anaweza kukabiliana ifaavyo na matatizo mabaya ya afya ya babake. Hivi karibuni, Philip alikubali mwaliko wa kuwa mfanyakazi wa kujitolea katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Makedonia.

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

Hawajapuuza Mahitaji Yake

Wakati Ada, dada Mkristo mwenye umri wa miaka 85 huko Australia alipolazimika kukaa nyumbani kwa sababu ya afya mbaya, wazee wa kutaniko walifanya mpango ili kumsaidia. Walipanga kikundi cha waamini ambao wangeweza kumsaidia. Ndugu na dada hao walifurahia kazi kama vile kusafisha, kufua, kupika, na kutumwa.

Mipango hiyo ya kumsaidia ilianzishwa karibu miaka kumi iliyopita. Kufikia sasa, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 30 wamesaidia kumtunza Ada. Wanaendelea kumtembelea, kumsomea vichapo vinavyozungumzia Biblia, kumweleza maendeleo ya kiroho ya washiriki wa kutaniko, na kusali kwa ukawaida pamoja naye.

Mzee mmoja Mkristo mwenyeji alisema hivi: “Wale wanaomtunza Ada wanafurahia kazi hiyo. Wengi wamechochewa na utumishi wa uaminifu na wa miaka mingi wa dada huyo, nao hawawezi kamwe kupuuza mahitaji yake.”

[Picha katika ukurasa wa 16]

Je, sisi huwaonyesha upendo mwingi wazazi walio wazee?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wote kutanikoni wanaweza kuwaonyesha upendo waamini wenzao walio wazee