Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuiga Imani ya Abrahamu na Sara!

Unaweza Kuiga Imani ya Abrahamu na Sara!

Unaweza Kuiga Imani ya Abrahamu na Sara!

ANAITWA “baba ya wale wote walio na imani.” (Waroma 4:11) Pia mke wake mpendwa alikuwa na sifa hiyo. (Waebrania 11:11) Watu hao ni Abrahamu, mzee wa ukoo, na Sara mke wake, ambao walimwogopa Mungu. Kwa nini walikuwa vielelezo vizuri vya imani? Walivumilia majaribu gani? Masimulizi ya maisha yao yanatunufaishaje?

Abrahamu alionyesha imani Mungu alipomwamuru aondoke kwao. Yehova alimwambia: “Nenda zako kutoka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na kutoka kwa nyumba ya baba yako mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.” (Mwanzo 12:1) Mzee huyo wa ukoo mwaminifu alitii, kwa kuwa tunaambiwa: “Kwa imani Abrahamu, alipoitwa, alitii kwa kutoka akaenda na kuingia mahali alipokusudiwa kupokea kuwa urithi; naye akatoka, ijapokuwa hakujua mahali alipokuwa akienda.” (Waebrania 11:8) Wazia ilimaanisha nini kuhama.

Abrahamu aliishi Uru, katika eneo ambalo liko kusini mwa Iraki. Uru lilikuwa jiji lenye ufanisi la Mesopotamia ambalo lilikuwa kituo cha biashara kati yake na nchi za Ghuba ya Uajemi, na yaelekea hata Bonde la Indus. Bwana Leonard Woolley, ambaye aliongoza uchimbuaji wa hatua kwa hatua wa jiji hilo, anasema kwamba siku za Abrahamu nyumba nyingi zilijengwa kwa matofali, nazo kuta zilipigwa plasta na kupakwa chokaa. Kwa mfano, raia mmoja tajiri alikuwa na nyumba yenye orofa mbili ambayo ilikuwa na ua wa katikati wenye sakafu iliyotengenezwa kwa mawe. Nyumba za chini zilitumiwa na watumishi wa nyumbani na wageni. Kwenye orofa ya kwanza, kulikuwa na ukuta uliozungukwa na roshani ya mbao, na hivyo watu wa familia wangeweza kuingia katika vyumba walivyotengewa. Nyumba hizo zilizokuwa na vyumba 10 hadi 20, zilikuwa “na nafasi kubwa nazo ziliwawezesha watu kuishi maisha mazuri ya starehe, na kulingana na viwango vya Mashariki, maisha ya anasa,” asema Woolley. Nyumba hizo zilikuwa “hasa makao ya watu waliostaarabika na zilitosheleza mahitaji ya wakaaji wa mjini walioishi maisha ya hali ya juu.” Ikiwa Abrahamu na Sara waliacha makao kama hayo na kwenda kuishi katika mahema, basi walijidhabihu sana ili kumtii Yehova.

Kwanza, Abrahamu na familia yake walihamia Harani, jiji lililo kaskazini mwa Mesopotamia, kisha wakaenda Kanaani. Huo ulikuwa umbali wa kilometa 1,600—mwendo mrefu kwa wenzi hao wazee! Walipoondoka Harani, Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 75, naye Sara 65.—Mwanzo 12:4.

Sara alihisije Abrahamu alipomwambia kwamba walikuwa waondoke Uru? Labda alikuwa na wasiwasi kuacha nyumba nzuri, yenye usalama, na kukubali kwenda kuishi maisha ya hali ya chini katika nchi asiyoijua, ambayo ingeweza kuwa yenye uadui. Hata hivyo, Sara alijitiisha, akimwona Abrahamu kuwa “bwana” wake. (1 Petro 3:5, 6) Wasomi fulani huona jambo hilo kuwa wonyesho wa kwamba ‘kwa kawaida Sara alikuwa mwenye heshima kumwelekea,’ jambo linalodhihirisha “maoni na hisia zake za kweli.” Lakini zaidi ya yote, Sara alimtumaini Yehova. Ujitiisho na imani yake ni kielelezo kizuri kwa wake Wakristo.

Ni kweli kwamba si lazima tuache makao yetu ili kumtii Mungu, ingawa waeneza-injili fulani wa wakati wote wameacha nchi zao kwenda kuhubiri habari njema katika nchi nyingine. Hata iwe tunamtumikia Mungu tukiwa wapi, atatimiza mahitaji yetu mradi tu tunatanguliza mambo ya kiroho maishani.—Mathayo 6:25-33.

Sara na Abrahamu hawakujuta kwa sababu ya uamuzi waliofanya. Mtume Paulo anasema: “Kama kwa kweli wangeendelea kukumbuka mahali pale walipokuwa wametoka, wangepata nafasi ya kurudi.” Lakini hawakurudi. Waliamini ahadi za Yehova kwa kuwa walikuwa na uhakika kwamba yeye “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” Tunapaswa kufanya vivyo hivyo ikiwa tutaendelea kujitoa kwa Yehova kwa moyo wote.—Waebrania 11:6, 15, 16.

Utajiri wa Kiroho na wa Kimwili

Abrahamu alipofika Kanaani, Mungu alimwambia: “Nitaupa uzao wako nchi hii.” Abrahamu aliitikia kwa kumjengea Yehova madhabahu na kwa “kuliitia jina la Yehova.” (Mwanzo 12:7, 8) Yehova alimtajirisha Abrahamu, na watu waliokuwa katika kambi yake walikuwa wengi sana. Imedokezwa kwamba “watu waliokuwa kambini mwake walikuwa zaidi ya elfu moja,” kwa kuwa wakati mmoja alikusanya wanaume 318 waliozoezwa ambao walikuwa watumwa waliozaliwa katika nyumba yake. Vyovyote vile, watu walimwona kuwa ‘mkuu, mtu wa Mungu.’—Mwanzo 13:2; 14:14; 23:6.

Abrahamu aliongoza katika ibada na kuwafundisha watu wa nyumbani mwake “washike njia ya Yehova ili kutenda uadilifu na haki.” (Mwanzo 18:19) Leo, vichwa vya familia walio Wakristo wanaweza kutiwa moyo na kielelezo cha Abrahamu aliyefanikiwa kufundisha washiriki wa nyumba yake kumtegemea Yehova na kutenda kwa uadilifu. Hivyo, haishangazi kwamba Hagari Mmisri, aliyekuwa kijakazi wa Sara, na yule mtu aliyekuwa mtumishi wa zamani zaidi wa Abrahamu, na pia Isaka, mwana wa Abrahamu, walimtegemea Yehova Mungu.—Mwanzo 16:5, 13; 24:10-14; 25:21.

Abrahamu Alitafuta Amani

Mambo yaliyotukia katika maisha ya Abrahamu yanaonyesha kwamba alikuwa mtu wa kimungu. Badala ya kuruhusu ugomvi uendelee kati ya wachungaji wake na wale wa Loti, mpwa wake wa kiume, Abrahamu alipendekeza watengane, naye akamwomba Loti achague eneo alilopendelea. Abrahamu alikuwa mfanya-amani.—Mwanzo 13:5-13.

Ikiwa siku moja tutalazimika kuchagua kati ya kudai haki zetu au kupata hasara ili kudumisha amani, ni vizuri kuona kwamba Yehova hakuruhusu Abrahamu ateseke kwa sababu ya kumfikiria Loti. Kinyume cha hilo, baadaye Mungu alimwahidi Abrahamu na uzao wake nchi yote iliyomzunguka. (Mwanzo 13:14-17) Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani, kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’”—Mathayo 5:9.

Ni Nani Angekuwa Mrithi wa Abrahamu?

Licha ya ahadi za kupata uzao, Sara alibaki tasa. Abrahamu alisali kwa Mungu kuhusu hali hiyo. Je, Eliezeri, mtumishi wake, ndiye angerithi mali yake yote? La, kwa kuwa Yehova alisema: “Mtu huyu hatakuwa mrithi wako, lakini yule atakayetoka katika viuno vyako mwenyewe ndiye atakayekuwa mrithi wako.”—Mwanzo 15:1-4.

Hata hivyo, Abrahamu na Sara hawakupata mtoto, naye Sara aliyekuwa na umri wa miaka 75 akawa hana tumaini lolote la kupata mimba. Hivyo, akamwambia Abrahamu: “Yehova amenifunga nisizae watoto. Tafadhali, lala na mjakazi wangu. Labda ninaweza kupata watoto kutokana naye.” Ndipo Abrahamu akamchukua Hagari kuwa mke wa pili, akalala naye, naye akapata mimba. Mara tu Hagari alipojua ana mimba, akaanza kumdharau bimkubwa wake. Sara alimlalamikia Abrahamu kwa uchungu na kumfedhehesha Hagari, na hivyo akamfanya akimbie.—Mwanzo 16:1-6.

Abrahamu na Sara walitenda hivyo kwa nia nzuri, nao walifuata desturi ambayo ilikubaliwa katika siku zao. Hata hivyo, Yehova hangetokeza uzao wa Abrahamu kupitia njia hiyo. Huenda utamaduni wetu ukaonyesha kwamba matendo fulani yanaruhusiwa chini ya hali mbalimbali, lakini hiyo haimaanishi kwamba Yehova anakubaliana na jambo hilo. Huenda akawa na maoni tofauti kabisa kuhusu hali yetu. Hivyo, tunahitaji kutafuta mwongozo wa Mungu na kusali ili atuonyeshe jinsi anavyotaka tutende.—Zaburi 25:4, 5; 143:8, 10.

Hakuna Jambo Lililo “Kubwa Mno Isivyo Kawaida kwa Yehova”

Hatimaye, Hagari alimzalia Abrahamu mwana aliyeitwa Ishmaeli. Lakini hakuwa ule Uzao ulioahidiwa. Sara mwenyewe ndiye angezaa mrithi huyo, licha ya umri wake mkubwa.—Mwanzo 17:15, 16.

Mungu aliposema kwamba Sara angemzalia mume wake mwana, ‘Abrahamu alianguka kifudifudi, akaanza kucheka na kusema moyoni mwake: “Je, mtu wa umri wa miaka 100 atazaa mtoto, na je, Sara, ndiyo, je, mwanamke wa umri wa miaka 90 atazaa?”’ (Mwanzo 17:17) Malaika huyo aliporudia ujumbe huo naye Sara akamsikia, yeye ‘alicheka ndani yake.’ Lakini hakuna jambo lililo “kubwa mno isivyo kawaida kwa Yehova.” Tunaweza kuwa na imani kwamba anaweza kufanya lolote atakalo.—Mwanzo 18:12-14.

‘Kwa imani Sara mwenyewe alipokea nguvu ili kuchukua mimba ya uzao, hata alipokuwa amepita mpaka wa umri, kwa kuwa alimwona kuwa mwaminifu yeye aliyekuwa ameahidi.’ (Waebrania 11:11) Mwishowe, Sara alimzaa Isaka, ambaye jina lake linamaanisha “Kicheko.”

Kutumaini Kabisa Ahadi za Mungu

Yehova alimtaja Isaka kuwa mrithi aliyengojewa kwa muda mrefu. (Mwanzo 21:12) Hivyo, lazima Abrahamu awe alishtuka sana Mungu alipomwagiza amdhabihu mwanaye. Lakini Abrahamu alikuwa na sababu nzuri za kumtumaini Mungu kabisa. Yehova angeweza kumfufua Isaka. (Waebrania 11:17-19) Isitoshe, Mungu alikuwa amethibitisha kwamba ana nguvu kwa kuwarudishia Abrahamu na Sara nguvu za kuzaa ili wamzae Isaka. Abrahamu alikuwa tayari kumtii Mungu kwa kuwa alikuwa na hakika kwamba Mungu ana uwezo wa kutimiza ahadi zake. Ni kweli kwamba alizuiwa kumwua mwanaye. (Mwanzo 22:1-14) Lakini, fungu ambalo Abrahamu alitimiza kuhusiana na jambo hilo hutusaidia kuona jinsi ilivyokuwa vigumu kwa Yehova Mungu ‘kumtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’—Yohana 3:16; Mathayo 20:28.

Kwa kuwa Abrahamu alimwamini Mungu alijua kwamba mrithi wa ahadi za Yehova hangeweza kuoa mwabudu wa uwongo kutoka nchi ya Kanaani. Akiwa mzazi mwenye kumwogopa Mungu, hangekubali mtoto wake aoe mwanamke asiyemtumikia Yehova. Hivyo, akamtafutia Isaka mke afaaye kutoka kati ya jamaa zake walioishi Mesopotamia, umbali wa zaidi ya kilometa 800. Mungu alibariki jitihada hizo kwa kuonyesha kwamba alimchagua Rebeka aolewe na Isaka na awe nyanya wa Masihi. Naam, Yehova ‘alimbariki Abrahamu katika kila jambo.’—Mwanzo 24:1-67; Mathayo 1:1, 2.

Baraka kwa Mataifa Yote

Abrahamu na Sara waliweka kielelezo kizuri katika kuvumilia majaribu na kuonyesha imani katika ahadi za Mungu. Kutimizwa kwa ahadi hizo kunahusiana na matarajio ya milele ya mwanadamu, kwa kuwa Yehova alimhakikishia Abrahamu hivi: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.

Bila shaka, Abrahamu na Sara hawakuwa wakamilifu, kama vile sisi tusivyo wakamilifu. Hata hivyo, walipotambua mapenzi ya Mungu, walitii mara moja, bila kujali gharama iliyohusika. Hivyo, Abrahamu anakumbukwa kuwa “rafiki ya Yehova” naye Sara kuwa ‘mwanamke mtakatifu aliyemtumaini Mungu.’ (Yakobo 2:23; 1 Petro 3:5) Kwa kujitahidi kuiga imani ya Abrahamu na Sara, sisi pia tunaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Pia, tunaweza kunufaika na ahadi nzuri ambazo Yehova alimtolea Abrahamu.—Mwanzo 17:7.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwa sababu ya imani yao, Yehova aliwabariki Abrahamu na Sara kwa kuwapa mwana wakiwa wazee

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kielelezo cha Abrahamu hutusaidia kuelewa jinsi Yehova alivyohisi kumruhusu Mwana wake mzaliwa-pekee afe