Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kumfanya Mungu Ashangilie

Unaweza Kumfanya Mungu Ashangilie

Unaweza Kumfanya Mungu Ashangilie

JE, KWELI tunaweza kugusa hisia za Mungu? Je, Mungu anaweza kushangilia? Wengine hufikiri kwamba Mungu ni nguvu tu. Je, tunaweza kutarajia nguvu isiyo na utu ishangilie? La. Hata hivyo, chunguza yale ambayo Biblia inasema kumhusu Mungu.

Yesu Kristo alisema “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Mtu wa roho ni aina ya uhai ambayo ni tofauti na wanadamu. Ingawa haonekani machoni pa wanadamu, mtu wa roho ana mwili “wa roho.” (1 Wakorintho 15:44; Yohana 1:18) Ikitumia usemi wa mfano, Biblia hata husema kwamba Mungu ana macho, masikio, mikono, na kadhalika. * Pia Mungu ana jina, yaani, Yehova. (Zaburi 83:18) Hivyo, Mungu wa Biblia, ni mtu wa roho. (Waebrania 9:24) “Yeye ndiye Mungu aliye hai na Mfalme mpaka wakati usio na kipimo.”—Yeremia 10:10.

Kwa kuwa Yehova ni mtu halisi anayeishi, yeye anaweza kufikiri na kutenda. Yeye ana sifa na hisia, na pia anaweza kupenda na kuchukia. Kwa kweli, Biblia ina maneno yanayoonyesha mambo yanayompendeza au yasiyompendeza Mungu. Ingawa miungu na sanamu zilizotengenezwa na wanadamu huonyesha tu tabia au sifa za wanadamu waliozifanya, Yehova, Mungu Mweza-Yote, ndiye Chanzo cha hisia alizoweka ndani ya wanadamu.—Mwanzo 1:27; Isaya 44:7-11.

Bila shaka, Yehova ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Yeye hashangilii tu katika kazi zake za uumbaji, bali pia hufurahia kutimiza kusudi lake. Kupitia nabii Isaya, Yehova anasema: “Kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya . . . Mimi nimesema hilo; pia nitalitimiza. Nimelifanyiza, pia nitalitenda.” (Isaya 46:9-11) Mtunga-zaburi aliimba: “Yehova atashangilia kwa kazi zake.” (Zaburi 104:31) Lakini kuna jambo lingine linalomfurahisha Mungu. Anasema: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie.” (Methali 27:11) Fikiria maana ya maneno hayo, kwamba tunaweza kumfanya Mungu ashangilie!

Jinsi Tunavyoweza Kuufanya Moyo wa Mungu Ushangilie

Fikiria jinsi mzee wa ukoo Noa alivyoufanya moyo wa Yehova ushangilie. Noa ‘alipata kibali machoni pa Yehova’ kwa kuwa “alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake.” Tofauti kabisa na watu waovu wa wakati huo, imani na utii wa Noa ulimfurahisha Mungu hivi kwamba ingeweza kusemwa kuwa “Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwanzo 6:6, 8, 9, 22) “Kwa imani Noa . . . alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake.” (Waebrania 11:7) Yehova alipendezwa na Noa naye akambariki yeye na familia yake kwa kuwaokoa katika kipindi hicho chenye msukosuko cha historia ya wanadamu.

Pia mzee wa ukoo Abrahamu alijua sana hisia za Yehova. Kujua kwake maoni ya Mungu kulionekana wazi wakati Yehova alipomjulisha kwamba angeharibu majiji ya Sodoma na Gomora kwa sababu ya upotovu wao wa maadili. Abrahamu alimjua Yehova vya kutosha kuweza kufikia mkataa kwamba lilikuwa jambo lisilowaziwa Mungu kuua mtu mwadilifu pamoja na mwovu. (Mwanzo 18:17-33) Miaka mingi baadaye, ‘ni kana kwamba Abrahamu alimtoa Isaka,’ kwa kutii agizo la Mungu, kwa kuwa ‘alifikia uamuzi kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua hata kutoka kwa wafu.’ (Waebrania 11:17-19; Mwanzo 22:1-18) Abrahamu alijua vizuri hisia za Mungu naye alionyesha utii na imani yenye nguvu hivi kwamba “akaitwa ‘rafiki ya Yehova.’”—Yakobo 2:23.

Mtu mwingine aliyejitahidi kuufurahisha moyo wa Mungu ni Mfalme Daudi, wa Israeli la kale. Yehova alisema hivi kumhusu: “Nimemwona Daudi mwana wa Yese, mtu anayekubalika kwa moyo wangu, atakayefanya mambo yote ambayo ninatamani.” (Matendo 13:22) Kabla ya kulikabili lile jitu Goliathi, Daudi alimtumaini kabisa Mungu, naye akamwambia Mfalme Sauli wa Israeli, hivi: “Yehova, aliyenikomboa kutoka katika makucha ya simba na kutoka katika makucha ya dubu, yeye ndiye atakayenikomboa kutoka mkononi mwa huyu Mfilisti.” Yehova alimbariki Daudi kwa kumtumaini, naye akamwezesha kumuua Goliathi. (1 Samweli 17:37, 45-54) Daudi alitaka si matendo yake tu, bali pia ‘maneno ya kinywa chake na kutafakari kwa moyo kupendeze mbele za Yehova.’—Zaburi 19:14.

Namna gani sisi? Tunawezaje kumpendeza Yehova? Kadiri tunavyozidi kujifunza hisia za Mungu, ndivyo tutakavyokuwa na ujuzi zaidi kuhusu yale tunayoweza kufanya ili kuufanya moyo wake ushangilie. Hivyo, tunaposoma Biblia, ni muhimu tujitahidi kujua jinsi Mungu anavyohisi kusudi ‘tujazwe ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na utambuzi wa kiroho, ili tutembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili.’ (Wakolosai 1:9, 10) Ujuzi tunaopata hutusaidia kusitawisha imani yetu. Hilo ni muhimu kwa kuwa “bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema.” (Waebrania 11:6) Naam, kwa kujitahidi kusitawisha imani yenye nguvu na kwa kuishi kupatana na mapenzi ya Yehova, tunaweza kuufurahisha moyo wake. Wakati huohuo, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusiumize moyo wa Yehova.

Usiumize Moyo wa Mungu

Mfano mmoja wa jinsi Yehova anavyoweza kuumia moyoni unapatikana katika masimulizi kuhusu siku za Noa. Wakati huo, ‘dunia ilijaa jeuri. Basi Mungu akaiona dunia na, tazama! ilikuwa imeharibika, kwa sababu kila mwenye mwili alikuwa amejiharibia njia yake duniani.’ Mungu alihisije alipoona upotovu wa maadili na jeuri? Biblia inasema: ‘Yehova alijuta kwamba amewafanya wanadamu duniani, naye akaumia moyoni mwake.’ (Mwanzo 6:5, 6, 11, 12) Mungu alijuta katika maana ya kwamba mwenendo wa wanadamu ulikuwa mwovu sana hivi kwamba alibadili mtazamo kuelekea kizazi hicho kiovu cha kabla ya Gharika. Kwa sababu ya kuchukizwa na uovu wao, Mungu aliacha mtazamo wake wa kuwa Muumba wa wanadamu, na akawa mwangamizi wao.

Pia Yehova alihuzunika wakati watu wake mwenyewe, taifa la kale la Israeli, walipoendelea kupuuza hisia na mwongozo wake wenye upendo. Mtunga-zaburi alisema kwa huzuni hivi: “Jinsi walivyomwasi mara nyingi nyikani, wakamhuzunisha jangwani! Nao wakawa wakimjaribu Mungu tena na tena, nao wakamtia uchungu Mtakatifu wa Israeli.” Hata hivyo, “alikuwa mwenye rehema; akawa akilifunika kosa wala hakuharibu. Na mara nyingi akageuzia mbali hasira yake.” (Zaburi 78:38-41) Hata ingawa Waisraeli waasi walipatwa kwa haki na matokeo mabaya ya dhambi zao, Biblia hutuambia kwamba “wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha [Mungu].”—Isaya 63:9.

Licha ya uthibitisho mwingi kwamba Mungu alikuwa na hisia nyororo kuwaelekea, Waisraeli “waliendelea kuwadhihaki wale wajumbe wa Mungu wa kweli na kuyadharau maneno yake na kuwafanyia mzaha manabii wake, mpaka ghadhabu ya Yehova ikapanda juu ya watu wake, mpaka kukawa hakuna kuponywa.” (2 Mambo ya Nyakati 36:16) Mwishowe, uasi wao wenye kiburi ‘uliihuzunisha roho yake takatifu’ kiasi kwamba walipoteza kibali cha Yehova. (Isaya 63:10) Ikawaje? Kwa haki, Mungu aliondoa ulinzi wake, nao wakapatwa na msiba wakati Wababiloni walipoteka Yuda na kuharibu Yerusalemu. (2 Mambo ya Nyakati 36:17-21) Ni huzuni kama nini watu wanapochagua kuishi maisha ya dhambi ambayo yanamchukiza na kumhuzunisha Muumba wao!

Biblia hutueleza wazi kwamba Mungu huumizwa sana na mwenendo wa ukosefu wa maadili. (Zaburi 78:41) Kati ya mambo yanayomchukiza Mungu ni kiburi, uwongo, mauaji, mazoea ya uchawi, uaguzi, kuabudu mababu wa kale, ukosefu wa maadili, ngono kati ya watu wa jinsia moja, kukosa uaminifu katika ndoa, ngono na mtu wa familia, na kukandamiza maskini.—Mambo ya Walawi 18:9-29; 19:29; Kumbukumbu la Torati 18:9-12; Methali 6:16-19; Yeremia 7:5-7; Malaki 2:14-16.

Yehova huhisije kuhusu ibada ya sanamu? Kitabu cha Kutoka 20:4, 5 kinasema: “Usijifanyie sanamu ya kuchongwa wala umbo lililo kama kitu chochote kilicho juu mbinguni wala kilicho chini duniani wala kilicho ndani ya maji chini ya dunia. Usiviinamie wala kushawishiwa kuvitumikia.” Kwa nini? Kwa sababu sanamu “ni chukizo kwa Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 7:25, 26) Mtume Yohana alionya hivi: “Watoto wadogo, jilindeni na sanamu.” (1 Yohana 5:21) Naye mtume Paulo aliandika: “Wapendwa wangu, ikimbieni ibada ya sanamu.”—1 Wakorintho 10:14.

Tafuta Kibali cha Mungu

Mungu hufanya ‘urafiki pamoja na watu wanyoofu.’ Nao wale “wasio na lawama katika njia yao ni furaha kwake.” (Methali 3:32; 11:20) Kwa upande mwingine, wale wanaoendelea kwa ukaidi kumchukiza Mungu kwa kupuuza au kuasi maoni yake ya uadilifu, wataharibiwa karibuni. (2 Wathesalonike 1:6-10) Kwa kweli, hivi karibuni atakomesha uovu wote ambao umeenea sana leo.—Zaburi 37:9-11; Sefania 2:2, 3.

Hata hivyo, Biblia huonyesha wazi kwamba Yehova “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Angependelea zaidi kuonyesha upendo wake kwa watu waadilifu wanaompenda lakini kudhihirisha hasira yake kwa wale wasiotaka kubadilika. Yehova hapendezwi “na kifo cha mwovu, bali kwamba mtu mwovu ageuke na kuiacha njia yake na kwa kweli aendelee kuishi.”—Ezekieli 33:11.

Si lazima kila mtu apatwe na hasira ya Yehova. “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) Ukiwa na hakika kabisa kwamba hayo ndiyo maoni ya Mungu, unaweza ‘kutupa mahangaiko yako yote juu yake, kwa sababu yeye anakujali wewe.’ (1 Petro 5:7) Uwe na hakika kwamba wale wanaofanya moyo wa Mungu ushangilie wana tarajio zuri ajabu la kupata kibali chake na kuwa rafiki zake. Hivyo, huu ndio wakati muhimu zaidi ‘kuendelea kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.’—Waefeso 5:10.

Ni jambo zuri kama nini kwamba Mungu katika fadhili zake zisizostahiliwa alifunua maoni na sifa zake tukufu! Nawe unaweza kufanya moyo wake ushangilie. Ikiwa ungependa kufanya hivyo, tunakuhimiza uwasiliane na Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu. Watafurahi kukuonyesha mambo ambayo wameona yanafaa na yanayowezekana katika jitihada zao za kumpendeza Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona sanduku lenye kichwa “Kwa Nini Biblia Hutumia Maneno ya Kibinadamu Kumfafanua Mungu?”

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Kwa Nini Biblia Hutumia Maneno ya Kibinadamu Kumfafanua Mungu?

Kwa kuwa “Mungu ni Roho,” hatuwezi kumuona kwa macho halisi. (Yohana 4:24) Hivyo, ili kutusaidia kuelewa uwezo, ukuu, na kazi za Mungu, Biblia hutumia semi za mfano, kama vile maneno ya ufananisho, na yale yanayompa Mungu sifa za kibinadamu. Hivyo, hata ingawa hatujui jinsi mwili wa roho wa Mungu unavyofanana, Biblia husema kwamba Mungu ana macho, masikio, mikono, vidole, miguu, na moyo.—Mwanzo 8:21; Kutoka 3:20; 31:18; Ayubu 40:9; Zaburi 18:9; 34:15.

Maneno hayo yanayomfafanua Mungu hayamaanishi kwamba mwili wake wa roho una viungo kama vya mwili wa kibinadamu. Maneno yanayompa Mungu sifa za kibinadamu hayapaswi kuchukuliwa kihalisi. Yanawasaidia tu wanadamu wapate kumwelewa Mungu vizuri zaidi. Bila semi hizo za mfano, ingekuwa vigumu, au hata haingewezekana kwa wanadamu duni kuelewa ufafanuzi wowote kumhusu Mungu. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba wanadamu ndio waliobuni sifa za Yehova Mungu. Biblia inaeleza wazi kwamba mtu aliumbwa kwa mfano wa Mungu, wala si Mungu kwa mfano wa mtu. (Mwanzo 1:27) Kwa kuwa waandikaji wa Biblia ‘waliongozwa na roho ya Mungu,’ kwa wazi maelezo yao kuhusu utu wa Mungu ni maelezo ya Mungu mwenyewe kuhusu sifa zake—sifa ambazo ameweka kwa viwango tofauti-tofauti ndani ya viumbe wake wa kibinadamu. (2 Timotheo 3:16, 17) Badala ya sifa za mwanadamu kuwa ndani ya Mungu, kwa kweli mwanadamu ndiye ana sifa za Mungu ndani yake.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Courtesy of Anglo-Australian Observatory, photograph by David Malin

[Picha katika ukurasa wa 4]

Noa alipata kibali machoni pa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 5]

Abrahamu alijua vizuri hisia za Mungu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Daudi alimtumaini kabisa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 7]

Unaposoma Biblia, unaweza kujua jinsi ya kumfanya Mungu ashangilie