Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walio Wazee Ni Washiriki Wenye Thamani wa Undugu Wetu wa Kikristo

Walio Wazee Ni Washiriki Wenye Thamani wa Undugu Wetu wa Kikristo

Walio Wazee Ni Washiriki Wenye Thamani wa Undugu Wetu wa Kikristo

“Wale ambao wamepandwa katika nyumba ya Yehova . . . watachanuka. Bado wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi.”—ZABURI 92:13, 14.

1. Watu wengi huwaonaje walio wazee?

YEHOVA anawapenda watumishi wake wote waaminifu, kutia ndani wale walio wazee. Hata hivyo, kulingana na kadirio lililofanywa nchini Marekani, kila mwaka karibu wazee nusu milioni hudhulumiwa au kupuuzwa. Ripoti kama hizo kutoka sehemu zote za ulimwengu zinaonyesha kwamba walio wazee hudhulumiwa ulimwenguni pote. Shirika moja linataja sababu kuwa ‘mtazamo wa watu wengi kwamba walio wazee hawana manufaa yoyote, nao huwategemea sana wengine.’

2. (a) Yehova huwaonaje watumishi wake waaminifu walio wazee? (b) Ni ufafanuzi gani mchangamfu tunaopata katika Zaburi 92:12-15?

2 Yehova Mungu anawathamini watumishi wake washikamanifu walio wazee. Yeye huzingatia “mtu tuliye kwa ndani,” yaani, hali yetu ya kiroho, wala si kupungukiwa kwetu kimwili. (2 Wakorintho 4:16) Katika Neno lake, Biblia, tunapata uhakikisho huu mchangamfu: “Mwadilifu atachanua kama mtende; kama mwerezi katika Lebanoni, atakuwa mkubwa. Wale ambao wamepandwa katika nyumba ya Yehova, katika nyua za Mungu wetu, watachanuka. Bado wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi, wataendelea kuwa wanono na wabichi, ili kutangaza kwamba Yehova ni mnyoofu.” (Zaburi 92:12-15) Kwa kuchunguza mistari hiyo tutaona njia mbalimbali ambazo enyi mlio wazee mnaweza kuwa wenye thamani katika undugu wa Kikristo.

“Kusitawi Wakati wa Kuwa na Kichwa Chenye Mvi”

3. (a) Kwa nini waadilifu wanalinganishwa na mitende? (b) Walio wazee wanawezaje “kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi”?

3 Mtunga-zaburi analinganisha waadilifu na mitende ‘iliyopandwa katika nyua za Mungu wetu.’ Wanaendelea “kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi.” Tafsiri nyingine inasema: “Watazaa matunda hadi wakati wa uzee.” (Union Version) Je, hukubali kwamba hilo ni jambo lenye kutia moyo? Nyakati za Biblia ilikuwa kawaida kuona mitende maridadi na iliyonyooka kwenye nyua za nyumba katika Nchi za Mashariki. Mbali na umaridadi wake, mitende pia ilithaminiwa kwa kuzaa matunda mengi. Mitende fulani iliendelea kuzaa matunda kwa miaka zaidi ya mia moja. * Kwa kuendelea kuwa thabiti katika ibada ya kweli, unaweza pia ‘kuendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema.’—Wakolosai 1:10.

4, 5. (a) Wakristo wanapaswa kuzaa matunda gani muhimu? (b) Taja vielelezo katika Biblia vya wazee waliozaa “tunda la midomo.”

4 Yehova hutarajia Wakristo wazae “tunda la midomo,” yaani, wamsifu yeye na makusudi yake. (Waebrania 13:15) Je, unaweza kumsifu ukiwa mzee? Bila shaka.

5 Biblia ina vielelezo vya walio wazee ambao walitoa ushahidi kwa ujasiri kuhusu jina la Yehova na makusudi yake. Musa alikuwa na umri wa zaidi ya “miaka 70” Yehova alipomweka kuwa nabii na mwakilishi wake. (Zaburi 90:10; Kutoka 4:10-17) Uzee haukumzuia nabii Danieli kutoa ushahidi kwa ujasiri kuhusu enzi kuu ya Yehova. Yaelekea Danieli alikuwa na umri wa miaka 90 na kitu Belshaza alipomwita amfasirie mwandiko usioeleweka ukutani. (Danieli, sura ya 5) Namna gani mtume Yohana aliyezeeka? Alipokaribia kumaliza utumishi wake wa muda mrefu, alijikuta gerezani katika kisiwa cha Patmo “kwa sababu ya kusema juu ya Mungu na kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 1:9) Yaelekea unaweza kukumbuka watu wengi katika Biblia ambao walizaa “tunda la midomo” walipokuwa wazee.—1 Samweli 8:1, 10; 12:2; 1 Wafalme 14:4, 5; Luka 1:7, 67-79; 2:22-32.

6. Yehova amewatumiaje “wazee” kutoa unabii siku hizi za mwisho?

6 Akimnukuu nabii Mwebrania Yoeli, mtume Petro alisema hivi: “‘Katika siku za mwisho,’ Mungu asema, ‘Nitaimimina sehemu ya roho yangu juu ya kila namna ya mwili, [kutia ndani “wazee”], . . . nao watatoa unabii.’” (Matendo 2:17, 18; Yoeli 2:28) Vivyo hivyo, katika siku hizi za mwisho, Yehova ametumia washiriki wa jamii ya watiwa-mafuta ambao wamezeeka na “kondoo wengine” kutangaza makusudi yake. (Yohana 10:16) Baadhi yao wamekuwa wakizaa matunda ya Ufalme kwa uaminifu kwa miaka mingi.

7. Eleza jinsi walio wazee wanavyoendelea kuzaa matunda ya Ufalme licha ya kupungukiwa kimwili.

7 Fikiria Sonia ambaye alipata kuwa mhubiri wa wakati wote wa Ufalme mwaka wa 1941. Licha ya kupambana na ugonjwa usiopona kwa muda mrefu, aliongoza mafunzo ya Biblia nyumbani kwake kwa ukawaida. “Kuhubiri habari njema ni sehemu ya maisha yangu, siwezi kuacha kuhubiri,” akaeleza Sonia. Muda mfupi uliopita, Sonia na dadake Olive, walimweleza Janet ujumbe wa Biblia wenye tumaini. Walikutana na Janet, aliyekuwa na ugonjwa usiotibika, kwenye sebule ya hospitali. Mama ya Janet, Mkatoliki mwenye bidii, alivutiwa sana na upendezi ambao binti yake alionyeshwa hivi kwamba alikubali kuwa na funzo la Biblia la nyumbani na sasa anaendelea vizuri. Je, unaweza kutumia nafasi kama hizo kuzaa matunda ya Ufalme?

8. Kalebu aliyekuwa amezeeka alionyeshaje kwamba alimtumaini Yehova, nao Wakristo walio wazee wanawezaje kuiga kielelezo chake?

8 Kwa kuendelea kwa ujasiri katika kazi ya kuhubiri Ufalme licha ya kupungukiwa kwa sababu ya uzee, Wakristo walio wazee wanaiga kielelezo cha Kalebu, Mwisraeli mwaminifu, aliyeandamana na Musa nyikani kwa miaka 40. Kalebu alikuwa na umri wa miaka 79 alipovuka Mto Yordani na kuingia katika Nchi ya Ahadi. Baada ya kupigana katika jeshi lenye kushinda la Israeli kwa miaka sita, angeweza kupumzika tu. Lakini hakufanya hivyo, bali kwa ujasiri aliomba mgawo mgumu wa kuteka “majiji makubwa yenye ngome” katika eneo lenye milima la Yuda, ambako Waanaki, watu wakubwa isivyo kawaida, waliishi. Kwa msaada wa Yehova, Kalebu ‘aliwanyang’anya nchi na kuwafukuza, kama vile Yehova alivyoahidi.’ (Yoshua 14:9-14; 15:13, 14) Unapoendelea kuzaa matunda ya Ufalme uzeeni, uwe na hakika kwamba Yehova yuko pamoja nawe kama alivyokuwa pamoja na Kalebu. Na ukiendelea kuwa mwaminifu, Yehova atakuruhusu uishi katika ulimwengu wake mpya ambao ameahidi.—Isaya 40:29-31; 2 Petro 3:13.

“Wataendelea Kuwa Wanono na Wabichi”

9, 10. Wakristo walio wazee huendeleaje kuwa wenye afya katika imani na kudumisha nguvu za kiroho? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 13.)

9 Akikazia jinsi watumishi wa Yehova walio wazee wanavyozaa matunda, mtunga-zaburi aliimba: “Mwadilifu atachanua kama mtende; kama mwerezi katika Lebanoni, atakuwa mkubwa. Bado wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi, wataendelea kuwa wanono na wabichi.”—Zaburi 92:12, 14.

10 Unawezaje kudumisha nguvu zako za kiroho licha ya kuzeeka? Mtende utadumisha umaridadi wake tu iwapo utapata maji ya kutosha. Vivyo hivyo, unaweza kutegemezwa na maji ya kweli za Biblia kwa kujifunza Neno la Mungu na kwa kushirikiana na tengenezo lake. (Zaburi 1:1-3; Yeremia 17:7, 8) Unakuwa mwenye thamani kwa waabudu wenzako unapokuwa na nguvu za kiroho. Fikiria jinsi jambo hilo linavyothibitishwa na kielelezo cha Kuhani Mkuu Yehoyada aliyekuwa mzee.

11, 12. (a) Yehoyada alitimiza fungu gani muhimu katika historia ya ufalme wa Yuda? (b) Yehoyada alitumiaje mamlaka yake kuendeleza ibada ya kweli?

11 Labda Yehoyada alikuwa na umri wa miaka zaidi ya mia moja wakati Malkia Athalia mwenye kutaka makuu alipoanza kutawala Yuda baada ya kuwaua wajukuu wake. Mzee Yehoyada angefanya nini? Kwa miaka sita, yeye na mke wake walimficha hekaluni Yehoashi, mrithi pekee wa kiti cha ufalme aliyeokoka. Kisha, katika hatua ya kushangaza, Yehoyada akamtangaza Yehoashi mwenye umri wa miaka saba kuwa mfalme na kuagiza Athalia auawe.—2 Mambo ya Nyakati 22:10-12; 23:1-3, 15, 21.

12 Akiwa mlinzi wa mfalme, Yehoyada alitumia mamlaka yake kuendeleza ibada ya kweli. ‘Alifanya agano kati yake na watu wote na mfalme kwamba wao wataendelea kuwa watu wa Yehova.’ Yehoyada aliwaagiza watu wabomoe nyumba ya mungu wa uwongo Baali, waondoe madhabahu yake, sanamu, na kuhani wake. Pia Yehoashi alirudisha huduma za hekalu na kulifanyia ukarabati uliohitajiwa sana chini ya mwongozo wa Yehoyada. ‘Yehoashi aliendelea kufanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova siku zake zote ambazo Yehoyada kuhani alimfundisha.’ (2 Mambo ya Nyakati 23:11, 16-19; 24:11-14; 2 Wafalme 12:2) Yehoyada alipokufa akiwa na umri wa miaka 130, alipewa heshima ya kipekee kwa kuzikwa pamoja na wafalme kwa sababu “alikuwa ametenda mema katika Israeli na kwa Mungu wa kweli na kwa nyumba Yake.”—2 Mambo ya Nyakati 24:15, 16.

13. Wakristo walio wazee wanawezaje ‘kutenda mema kwa Mungu wa kweli na kwa nyumba yake’?

13 Labda afya mbaya au hali nyingine zinapunguza yale unayoweza kufanya ili kuendeleza ibada ya kweli. Hata kama hali yako iko hivyo, bado unaweza ‘kutenda mema kwa Mungu wa kweli na kwa nyumba yake.’ Unaweza kuwa mwenye bidii kwa ajili ya nyumba ya Yehova kwa kuhudhuria na kutoa maelezo katika mikutano ya kutaniko na kwa kushiriki katika huduma ya shambani inapowezekana. Kuwa tayari kukubali shauri la Biblia na kumuunga mkono kwa ushikamanifu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na kutaniko pia, kutawaimarisha ndugu zako Wakristo. (Mathayo 24:45-47) Pia unaweza kuwachochea waabudu wenzako “katika upendo na matendo mazuri.” (Waebrania 10:24, 25; Filemoni 8, 9) Nawe utawanufaisha wengine ukifuata shauri hili la mtume Paulo: “Wanaume wenye umri mkubwa wawe na kiasi katika mazoea, wenye kuchukua mambo kwa uzito, wenye utimamu wa akili, wenye afya katika imani, katika upendo, katika uvumilivu. Vivyo hivyo wanawake wenye umri mkubwa wawe wenye tabia ya kumhofu Mungu, si wachongezi, wala si watumwa wa divai nyingi sana, wawe walimu wa yaliyo mema.”—Tito 2:2-4.

14. Waangalizi Wakristo ambao wametumikia kwa muda mrefu wanaweza kufanya nini ili kuendeleza ibada ya kweli?

14 Je, umetumikia ukiwa mzee wa kutaniko kwa miaka mingi? “Tumia hekima ambayo umejipatia kwa miaka mingi bila ubinafsi,” ndivyo anavyoshauri mzee mmoja wa kutaniko ambaye ametumikia kwa muda mrefu. “Wakabidhi wengine madaraka, na kushiriki ujuzi wako pamoja na wale walio tayari kujifunza . . . Tambua uwezo wa wengine. Uongeze na kuukuza uwezo huo. Jitayarishe kwa ajili ya wakati ujao.” (Kumbukumbu la Torati 3:27, 28) Ikiwa unapendezwa kikweli na kazi ya kuhubiri Ufalme inayozidi kupanuka, utawanufaisha sana wengine katika undugu wetu wa Kikristo.

‘Tangaza Kwamba Yehova Ni Mnyoofu’

15. Wakristo walio wazee ‘hutangazaje kwamba Yehova ni mnyoofu’?

15 Watumishi wa Mungu walio wazee hutimiza kwa furaha daraka lao la “kutangaza kwamba Yehova ni mnyoofu.” Ikiwa wewe ni Mkristo aliyezeeka, maneno na matendo yako yanaweza kuwaonyesha wengine kwamba ‘Yehova ni Mwamba wako, ambaye ndani yake hamna ukosefu wowote wa uadilifu.’ (Zaburi 92:15) Mtende hutoa ushahidi kimya-kimya kuhusu sifa bora za Muumba wake. Lakini Yehova amekupa pendeleo la kutoa ushuhuda kumhusu kwa wale ambao sasa wanaikubali ibada ya kweli. (Kumbukumbu la Torati 32:7; Zaburi 71:17, 18; Yoeli 1:2, 3) Kwa nini hilo ni muhimu?

16. Ni kielelezo gani cha Biblia kinachoonyesha umuhimu wa “kutangaza kwamba Yehova ni mnyoofu”?

16 Yoshua, kiongozi wa Waisraeli alipokuwa “mzee na mwenye siku nyingi,” yeye ‘aliita Israeli wote, wanaume wao wazee na wakuu wao na waamuzi wao na maofisa wao,’ na kuwakumbusha matendo manyoofu ya Mungu. Alisema: “Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu.” (Yoshua 23:1, 2, 14) Kwa muda fulani, maneno hayo yaliimarisha azimio la Waisraeli la kubaki wakiwa waaminifu. Hata hivyo, baada ya Yoshua kufa, ‘kizazi kingine kikaanza kutokea ambacho hakikumjua Yehova wala ile kazi ambayo alikuwa amewafanyia Israeli. Na wana wa Israeli wakaanza kufanya yaliyo mabaya machoni pa Yehova, wakatumikia Mabaali.’—Waamuzi 2:8-11.

17. Yehova ameshughulikaje na watu wake leo?

17 Utimilifu wa kutaniko la Kikristo leo hautegemei ushuhuda wa mdomo wa watumishi wa Mungu walio wazee. Hata hivyo, imani yetu katika Yehova na ahadi zake huimarika wengine wanapotueleza moja kwa moja ‘kazi kubwa’ ambazo Yehova amewafanyia watu wake siku hizi za mwisho. (Waamuzi 2:7; 2 Petro 1:16-19) Ikiwa umeshirikiana na tengenezo la Yehova kwa miaka mingi, huenda ukakumbuka wakati ambapo wahubiri wa Ufalme walikuwa wachache katika eneo au nchi yako, au wakati ambapo kazi ya kuhubiri ilipingwa vikali. Mwishowe, umeona Yehova akiondoa vizuizi fulani na ‘kuharakisha’ ukuzi wa Ufalme. (Isaya 54:17; 60:22) Umeona jinsi ambavyo kweli za Biblia zimefafanuliwa na kushuhudia marekebisho ya hatua kwa hatua ya tengenezo la Mungu linaloonekana. (Methali 4:18; Isaya 60:17) Je, unajitahidi kuwatia moyo wengine kwa kuwaeleza mambo ambayo umejionea kuhusiana na matendo ya unyoofu ya Yehova? Jambo hilo linaweza kuchochea na kuimarisha sana undugu wa Kikristo.

18. (a) Onyesha matokeo ya muda mrefu ya ‘kuwatangazia wengine kwamba Yehova ni mwadilifu.’ (b) Wewe mwenyewe umejionea uadilifu wa Yehova jinsi gani?

18 Namna gani pindi ambazo umejionea upendo na mwongozo wa Yehova maishani mwako? (Zaburi 37:25; Mathayo 6:33; 1 Petro 5:7) Dada mmoja mzee aitwaye Martha alikuwa akiwatia moyo wengine kwa kuwaambia: “Hata iweje, usimwache Yehova kamwe. Atakutegemeza.” Shauri hilo lilikuwa na matokeo mazuri sana kwa Tolmina, mmoja wa wanafunzi wa Biblia wa Martha, ambaye alibatizwa mapema miaka ya 1960. Tolmina anasema, “Mume wangu alipokufa, nilivunjika moyo sana, lakini maneno hayo yalifanya niazimie kutokosa mkutano hata mmoja. Kwa kweli, Yehova aliniimarisha niendelee.” Tolmina amewapa shauri hilohilo wengi wa wanafunzi wake wa Biblia. Naam, kwa kuwatia wengine moyo na kusimulia matendo manyoofu ya Yehova, unaweza kuimarisha sana imani ya waamini wenzako.

Yehova Huwathamini Wazee Walio Waaminifu

19, 20. (a) Yehova huonaje matendo ya watumishi wake walio wazee? (b) Makala inayofuata itazungumzia nini?

19 Ulimwengu wa leo usio na shukrani hauwajali wazee. (2 Timotheo 3:1, 2) Mara nyingi wanakumbukwa kwa sababu ya mafanikio yao ya zamani—yale waliyofanya wala si kwa yale wanayofanya sasa. Kinyume cha hilo, Biblia inasema: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.” (Waebrania 6:10) Bila shaka, Yehova Mungu hukumbuka matendo yako ya uaminifu ya zamani. Lakini yeye pia anakuthamini kwa yale unayoendelea kufanya katika utumishi wake. Naam, yeye huwaona watumishi waaminifu walio wazee kuwa Wakristo wenye kuzaa matunda, wenye afya kiroho, na wenye bidii, ambao maisha yao huthibitisha kwamba ana uwezo.—Wafilipi 4:13.

20 Je, wewe huwaona Wakristo walio wazee katika undugu wetu wa Kikristo kama Yehova awaonavyo? Ikiwa ndivyo, utachochewa kuwapenda. (1 Yohana 3:18) Makala inayofuata itazungumzia njia ambazo unaweza kuonyesha upendo huo unaposhughulikia mahitaji yao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kila kishada cha tende kinaweza kuwa na tende elfu moja na uzito wa kilogramu nane au zaidi. Mwandishi mmoja anakadiria kwamba “kila [mtende] unaozaa matunda utakuwa umewanufaisha wamiliki wake kwa tani mbili au tatu za tende kabla ya kuacha kuzaa.”

Unajibuje?

• Wazee ‘huzaa matunda’ jinsi gani?

• Kwa nini nguvu za kiroho za Wakristo walio wazee zina thamani?

• Walio wazee wanawezaje “kutangaza kwamba Yehova ni mnyoofu”?

• Kwa nini Yehova huwathamini watumishi wake ambao wamemtumikia kwa muda mrefu?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

Jinsi Ambavyo Wamedumisha Afya Katika Imani

Ni nini ambacho kimewasaidia Wakristo wa muda mrefu waendelee kuwa na afya katika imani na kudumisha nguvu za kiroho? Baadhi yao wamesema hivi:

“Ni muhimu sana kusoma maandiko yanayokazia uhusiano wetu pamoja na Yehova. Mara nyingi usiku, mimi hukariri Zaburi ya 23 na 91.”—Olive, aliyebatizwa mwaka wa 1930.

“Nimehakikisha kwamba ninahudhuria kila hotuba ya ubatizo na kusikiliza kwa makini, kana kwamba mimi ndiye ninayebatizwa. Kuendelea kufikiria ubatizo wangu kumenisaidia kubaki mwaminifu.”—Harry, aliyebatizwa mwaka wa 1946.

“Ni muhimu kusali kila siku—sikuzote tukiomba msaada, ulinzi, na baraka za Yehova, ‘tukimtambua katika njia zetu zote.’” (Methali 3:5, 6)—Antônio, aliyebatizwa mwaka wa 1951.

“Kusikiliza mambo yaliyoonwa kutoka kwa wale ambao bado wanamtumikia Yehova kwa uaminifu baada ya miaka mingi, hufanya niazimie kudumisha uaminifu na ushikamanifu wangu kwake.”—Joan, aliyebatizwa mwaka wa 1954.

“Si vizuri kujifikiria kupita kiasi. Kila kitu tulicho nacho kinatokana na fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Kuwa na maoni hayo hutusaidia tutafute chakula cha kiroho mahali panapofaa ili kuvumilia hadi mwisho.”—Arlene, aliyebatizwa mwaka wa 1954.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Walio wazee huzaa matunda ya Ufalme yenye thamani

[Picha katika ukurasa wa 14]

Nguvu za kiroho za walio wazee zina thamani