Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Hali Zako Hutawala Maisha Yako?

Je, Hali Zako Hutawala Maisha Yako?

Je, Hali Zako Hutawala Maisha Yako?

MATATIZO na hali zenye kutaabisha ni mambo ya kawaida katika ‘nyakati hizi za hatari.’ (2 Timotheo 3:1) Huenda matatizo fulani yakawa ni ya muda tu na hivyo mwishowe yatakoma. Mengine yanadumu kwa miezi au hata miaka. Kwa sababu hiyo, wengi huhisi kama alivyohisi mtunga-zaburi Daudi, ambaye alimlilia Yehova hivi: “Taabu za moyo wangu zimeongezeka; uniondoe katika mikazo iliyo juu yangu.”—Zaburi 25:17.

Je, unajitahidi kukabiliana na matatizo makubwa? Ikiwa ndivyo, unaweza kupata msaada na kitia moyo katika Biblia. Na tuchunguze maisha ya watumishi waaminifu wawili wa Yehova, Yosefu na Daudi, ambao walifanikiwa kukabiliana na magumu. Kwa kuchunguza jinsi walivyokabiliana na magumu, tunaweza kujifunza mambo muhimu yatakayotusaidia kukabili magumu kama hayo leo.

Walikabili Magumu Makali

Alipofikia umri wa miaka 17, Yosefu alikuwa na tatizo kubwa katika familia yake. Ndugu zake wakubwa walitambua kwamba Yakobo, baba yao, “alimpenda [Yosefu] kuliko ndugu zake wote.” Hivyo, “wakaanza kumchukia, nao hawakusema naye kwa amani.” (Mwanzo 37:4) Tunaweza kuwazia jinsi hali hiyo ilivyomletea Yosefu hangaiko na mkazo. Mwishowe, chuki ya ndugu zake iliongezeka sana hivi kwamba wakamuuza utumwani.—Mwanzo 37:26-33.

Alipokuwa mtumwa huko Misri, Yosefu alikataa kutongozwa na mke wa bwana wake. Akiwa amekasirika kwa kukataliwa, mwanamke huyo alimshtaki Yosefu kwa uwongo kwamba alijaribu kumlala kinguvu. Alitiwa “katika nyumba ya gereza,” ambapo ‘walitesa miguu yake kwa pingu na nafsi yake ikaingia katika vyuma.’ (Mwanzo 39:7-20; Zaburi 105:17, 18) Hilo lilikuwa jaribu lililoje! Kwa miaka 13 hivi, Yosefu alikuwa ama mtumwa au mfungwa kwa sababu ya kutendewa na wengine isivyo haki, kutia ndani washiriki wa familia yake mwenyewe.—Mwanzo 37:2; 41:46.

Akiwa kijana, Daudi wa Israeli la kale alikabili majaribu pia. Kwa muda wa miaka mingi, alilazimika kuishi kama mtoro, akiwindwa kama mnyama na Mfalme Sauli. Maisha ya Daudi yalikuwa hatarini sikuzote. Wakati mmoja, alienda kwa kuhani Ahimeleki ili kuomba chakula. (1 Samweli 21:1-7) Sauli aliposikia kwamba Ahimeleki alikuwa amemsaidia Daudi, aliagiza Ahimeleki, makuhani wote, na familia zao, wauawe. (1 Samweli 22:12-19) Je, unaweza kuwazia uchungu ambao Daudi alihisi moyoni kwa kusababisha kwa njia isiyo ya moja kwa moja msiba huo?

Fikiria jinsi Yosefu na Daudi walivyovumilia magumu na kutendewa vibaya kwa miaka mingi. Kwa kuchunguza yale waliyofanya ili kushinda au kuvumilia hali ngumu, tunaweza kujifunza mambo muhimu. Na tuchunguze njia tatu ambazo tunastahili kuwaiga wanaume hao.

Acha Kinyongo na Uchungu

Kwanza, wanaume hao waaminifu walijiepusha na uchungu na kinyongo. Alipokuwa gerezani, Yosefu angeweza kwa urahisi kuwafungia ndugu zake kinyongo kwa kumsaliti, labda kwa kufikiria jinsi ambavyo angeweza kulipiza kisasi ikiwa angewaona tena. Tunajuaje kwamba Yosefu aliyapinga mawazo hayo mabaya? Ona jinsi alivyotenda alipopata nafasi ya kulipiza kisasi juu ya ndugu zake ambao walikuja Misri kununua chakula. Masimulizi yanasema: “[Yosefu] akajitenga nao, akaanza kulia. . . . Baada ya hayo Yosefu akatoa amri, nao [watumishi wake] wakavijaza kabisa vyombo vya [ndugu zake] nafaka. Pia, walipaswa kurudisha pesa za watu hao kwenye gunia la kila mmoja wao na kuwapa vyakula kwa ajili ya safari.” Baadaye, alipowatuma ndugu zake wamlete baba yao Misri, Yosefu aliwatia moyo kwa maneno haya: “Msigombane njiani.” Kwa maneno na matendo, Yosefu alionyesha kwamba hakuacha uchungu na kinyongo vitawale maisha yake.—Mwanzo 42:24, 25; 45:24.

Vivyo hivyo, Daudi hakumfungia kinyongo Mfalme Sauli. Daudi alipata nafasi mbili za kumuua Sauli. Hata hivyo, wanaume wake walipomhimiza amuue, Daudi alisema: “Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba nimfanyie bwana wangu jambo hili, mtiwa-mafuta wa Yehova, kwa kunyoosha mkono wangu juu yake, kwa kuwa yeye ni mtiwa-mafuta wa Yehova.” Daudi aliacha Yehova asuluhishe mambo, kwa kuwaambia wanaume wake hivi: “Kama Yehova anavyoishi, Yehova mwenyewe atampiga; au siku yake itakuja naye atakufa, au ataanguka vitani, na kufagiliwa mbali.” Baadaye, Daudi hata alitunga wimbo wa maombolezo kwa ajili ya Sauli na mwanaye Yonathani. Kama vile Yosefu, Daudi hakujiacha ashindwe na kinyongo.—1 Samweli 24:3-6; 26:7-13; 2 Samweli 1:17-27.

Je, tunakuwa wenye kinyongo na uchungu tunapoumizwa na matendo fulani ya ukosefu wa haki? Hali hiyo inaweza kutokea kwa urahisi. Tukiruhusu hisia zetu zitutawale, huenda hali hiyo ikatuathiri vibaya zaidi kuliko tendo la ukosefu wa haki ambalo tumetendewa. (Waefeso 4:26, 27) Hata ingawa huenda hatuwezi kuzuia yale ambayo wengine hutenda, tunaweza kudhibiti matendo yetu. Ni rahisi zaidi kushinda kinyongo na uchungu tunapoamini kwamba Yehova atarekebisha mambo kwa wakati wake.—Waroma 12:17-19.

Jitahidi Kadiri Uwezavyo Kulingana na Hali Yako

Jambo la pili tunaloweza kujifunza ni kutoacha hali zetu zituzuie kufanya mambo ambayo tungefanya chini ya hali za kawaida. Huenda tukahangaikia sana mambo tusiyoweza kufanya hivi kwamba tunasahau yale tunayoweza kufanya. Hivyo, hali zetu huanza kututawala. Hilo lingetokea kwa Yosefu. Badala yake, alijitahidi kadiri alivyoweza kulingana na hali yake. Alipokuwa mtumwa, Yosefu ‘alizidi kupata kibali machoni pa bwana wake naye akamtumikia siku zote hata akamweka juu ya nyumba yake.’ Yosefu alikuwa na mtazamo huohuo alipokuwa gerezani. Kwa sababu ya baraka za Yehova na bidii ya Yosefu, ‘ofisa mkuu wa nyumba ya gereza aliwatia mkononi mwa Yosefu wafungwa wote waliokuwa katika nyumba hiyo ya gereza; na yote waliyokuwa wakifanya humo yeye ndiye aliyekuwa akiagiza yafanywe.’—Mwanzo 39:4, 21-23.

Katika miaka ambayo Daudi aliishi kama mtoro, yeye pia alijitahidi kadiri alivyoweza kulingana na hali zake. Walipokuwa wakiishi katika nyika ya Parani, yeye na wanaume wake walilinda mifugo ya Nabali isiporwe na vikundi vya waporaji. “Walikuwa ukuta kutuzunguka wakati wa usiku na wakati wa mchana,” akasema mmoja wa wachungaji wa Nabali. (1 Samweli 25:16) Baadaye, wakati alipokuwa Ziklagi, Daudi alivamia miji iliyokaliwa na maadui wa Israeli upande wa kusini, hivyo mipaka ya Yuda ikawa salama.—1 Samweli 27:8; 1 Mambo ya Nyakati 12:20-22.

Je, tunahitaji kujitahidi kadiri tuwezavyo kulingana na hali zetu? Ingawa inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo, tunaweza kufanikiwa. Akifikiria maisha yake, mtume Paulo aliandika: “Nimejifunza kuwa mwenye kujitosheleza katika hali zozote nilizo nazo. . . . Katika mambo yote na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kupatwa na uhitaji.” Paulo alikuzaje mtazamo huo wa maisha? Kwa kuendelea kumtegemea Yehova. Alikiri hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:11-13.

Mngojee Yehova

Jambo la tatu la kujifunza ni kwamba badala ya kutumia njia zisizo za kimaandiko ili kurekebisha hali zetu, tunapaswa kumngojea Yehova. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili muwe kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yakobo 1:4) Tunapaswa kuacha uvumilivu “ukamilishe kazi yake” kwa kuvumilia majaribu hadi mwisho bila kutumia njia zisizo za kimaandiko ili kuyakomesha upesi. Hivyo, imani yetu itajaribiwa na kusafishwa, na itafunuliwa kama imani yetu ina nguvu ya kututegemeza. Yosefu na Daudi walikuwa na uvumilivu wa aina hiyo. Hawakujaribu kutafuta suluhisho ambalo lingeweza kumkasirisha Yehova. Badala yake, walijitahidi kadiri walivyoweza kulingana na hali zao. Waliendelea kumngojea Yehova, nao wakapokea baraka nyingi sana kwa kufanya hivyo. Wote wawili walitumiwa na Yehova kuokoa na kuongoza watu wake.—Mwanzo 41:39-41; 45:5; 2 Samweli 5:4, 5.

Sisi pia tunaweza kukabili hali ambazo zitatushawishi kutumia njia zisizo za kimaandiko. Kwa mfano, je, unavunjika moyo kwa sababu hujapata mwenzi wa ndoa anayefaa? Ikiwa ndivyo, epuka kishawishi chochote cha kutotii amri ya Yehova ya kuoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Je, una matatizo katika ndoa yako? Badala ya kuathiriwa na roho ya ulimwengu inayochochea mtengano na talaka, jitahidi kushirikiana na mwenzi wako kusuluhisha matatizo. (Malaki 2:16; Waefeso 5:21-33) Je, una magumu ya kutunza familia yako kwa sababu ya hali za kiuchumi? Kumngojea Yehova hutia ndani kuepuka kufanya mambo yanayotiliwa shaka au yasiyo halali ili kujaribu kupata pesa. (Zaburi 37:25; Waebrania 13:18) Kwa kweli, sote tunapaswa kujitahidi kadiri tuwezavyo kulingana na hali zetu na kuacha Yehova atuthawabishe. Tunapofanya hivyo, na tuazimie kumngojea Yehova ili atoe suluhisho lifaalo.—Mika 7:7.

Yehova Atakutegemeza

Tunaweza kunufaika kwa kutafakari jinsi watu wanaotajwa na Biblia, kama vile Yosefu na Daudi, walivyofanikiwa kushughulika na hali ngumu na zenye kukatisha tamaa. Ingawa habari kuwahusu zinaelezwa katika kurasa chache tu za Biblia, majaribu yao yalidumu kwa miaka mingi. Jiulize hivi: ‘Watumishi hao wa Mungu walijifunzaje kukabili hali zao? Walidumishaje shangwe yao? Walipaswa kukuza sifa gani?’

Pia, tunapaswa kufikiria uvumilivu wa watumishi wa Yehova wa kisasa. (1 Petro 5:9) Kila mwaka magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yana masimulizi mengi kuhusu maisha ya watu. Je, wewe husoma na kutafakari vielelezo hivyo vya Wakristo waaminifu? Isitoshe, katika makutaniko yetu kuna wale ambao wanavumilia kwa uaminifu hali zisizopendeza. Je, unashirikiana nao kwa ukawaida na kujifunza kutoka kwao kwenye mikutano ya kutaniko?—Waebrania 10:24, 25.

Unapokabili hali ngumu, uwe na hakika kwamba Yehova anakujali na kwamba atakutegemeza. (1 Petro 5:6-10) Jitahidi kutoruhusu hali zako zitawale maisha yako. Fuata kielelezo cha Yosefu, Daudi, na wengine kwa kuacha kinyongo, kwa kujitahidi kadiri uwezavyo kulingana na hali yako, na kwa kumngojea Yehova ili atoe suluhisho lifaalo. Mkaribie kupitia sala na utendaji mbalimbali wa kiroho. Katika njia hiyo, wewe pia utakuwa mwenye shangwe na furaha hata katika nyakati ngumu.—Zaburi 34:8.

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Yosefu alijitahidi kadiri alivyoweza kulingana na hali zake

[Picha katika ukurasa wa 23]

Daudi aliendelea kumngojea Yehova ili asuluhishe matatizo yake